Hekaya Za Kisasa Kuhusu Vita Ya Kiroho – Sehemu Ya 1

Sura Ya Thelathini

 

Mada ya vita ya kiroho imezidi kupendwa sana katika kanisa la siku hizi. Kwa bahati mbaya sana, mengi yanayofundishwa kuhusu jambo hili yanapingana na Maandiko. Matokeo ni kwamba duniani kote, watumishi wengi wanafundisha na kutenda aina ya vita ya kiroho ambayo Biblia haisemi. Kwa kweli – kuna vita ya kiroho kimaandiko, na hiyo ndiyo itakiwayo kufanywa.

Katika sura hii na inayofuata, tutatazama baadhi ya mawazo ya makosa ambayo yamezoeleka sana kuhusu Shetani na vita ya kiroho. Sura hizi ni ufupisho wa kitabu kizima kuhusu jambo hili, kiitwacho Mawazo Ya Kisasa Juu Ya Vita Ya Kiroho.

Hekaya Ya Kwanza: “Katika milele iliyopita, Mungu na Shetani walipigana vita kubwa. Siku hizi, bado kuna mapambano kati yao.”

Hekaya hii inakwenda kinyume na kweli moja thabiti na ya msingi sana kuhusu Mungu, inayofunuliwa katika Maandiko – kwamba Yeye ana nguvu zote.

Yesu alituambia kwamba yote yanawezekana kwa Mungu (ona Mathayo 19:26). Yeremia alithibitisha kwamba hakuna kilicho kigumu kwa Mungu (ona Yeremia 32:17). Hakuna mtu wala nguvu viwezavyo kumzuia kufanya mapenzi Yake (ona 2Nyakati 20:6; Ayubu 41:10; 42:2). Mungu anauliza hivi kupitia kwa Yeremia, “Ni nani aliye kama Mimi … awezaye kusimama kinyume changu?” (Yeremia 50:44). Jibu ni kwamba, hakuna, hata Shetani hawezi.

Kama Mungu kweli ana nguvu zote kama inavyosemekana katika Maandiko yote hapo juu, basi kusema kwamba Mungu na Shetani walikuwa katika vita au wako katika vita ni kudai kwamba hana nguvu zote. Kama Mungu aliwahi kushindwa hata mara moja, au alishindwa kidogo tu na Shetani, au kama ilimbidi kukabiliana naye na kupambana hata kwa muda mfupi, basi Yeye hana nguvu zote kama anavyojitangaza.

Maelezo Ya Kristo Kuhusu Nguvu Za Shetani

Wakati mmoja Yesu alisema kitu kuhusu kuanguka kwa Shetani kutoka mbinguni kitakachotusaidia kuelewa nguvu alizo nazo, ukimlinganisha na Mungu wetu.

Ndipo wale sabini waliporudi kwa furaha wakisema, ‘Bwana! Hata pepo wanatutii kwa jina lako.’ Akawaambia, ‘Nilimwona Shetani akianguka kutoka mbinguni kama umeme’ (Luka 10:17, 18).

Wakati Mungu mwenye nguvu zote alipoagiza Shetani afukuzwe mbinguni, Shetani hakuwa na uwezo wowote wa kupinga. Yesu alichagua lugha ya mfano ili kueleza jinsi Shetani alivyoanguka haraka – kama umeme. Yaani, alianguka kutoka huko juu haraka sana. Sekunde moja alikuwa mbinguni, na iliyofuata – PWAA! – amekwisha ondoka!

Kama Mungu anaweza kumfukuza Shetani mwenyewe haraka hivyo na kirahisi hivyo, haipaswi kuwa kitu cha ajabu kwamba watumishi Wake aliowapa agizo wanaweza kuwafukuza mapepo haraka sana na kwa urahisi sana. Shida ni kwamba, kama wanafunzi wa kwanza wa Kristo, wengi katika Wakristo wanaheshimu sana nguvu ya Shetani na bado hawajatambua kwamba nguvu za Mungu ni kubwa sana, sana, sana. Mungu ndiye Mwumbaji – Shetani ni kiumbe tu. Shetani hamwezi Mungu.

Vita Ambayo Haikuwepo

Ingawa itasikika kama kitu cha ajabu masikioni kwetu, tunahitaji kuelewa kwamba Mungu na Shetani hawako katika vita, wala hawajawahi kuwepo, na hawatakuwa katika vita. Ni kweli kwamba wana makusudi na malengo tofauti, na ni kweli kusema kwambva wanapingana. Lakini, watu wawili wanapopingana, na mmoja awe na nguvu zaidi sana kuliko mwingine, upinzani wao hauwezi kuitwa vita. Je, mdudu anaweza kupigana na tembo? Shetani – sawa na mdudu – alifanya juhudi za kinyonge sana kumpinga Yule mwenye nguvu sana sana. Upinzani wake ulishughulikiwa haraka sana, naye alifukuzwa kutoka mbinguni “kama umeme”. Hapakuwa na vita hapo – ni mtu alifukuzwa.

Kama Mungu ana nguvu zote, Shetani hana nafasi hata ndogo tu ya kumzuia Mungu kufanya anachotaka. Na kama Mungu anamruhusu Shetani kufanya kitu, mwisho wake kitu hicho ni kwa ajili ya kutimiza mapenzi Yake kama Mungu. Kweli hii itawekwa wazi zaidi tunapoendelea kuchunguza Maandiko kuhusu mada hii.

Kufungwa Kwa Shetani Katika Siku Zijazo

Mamlaka makuu ya Mungu juu ya Shetani hayakuonyeshwa katika umilele uliopita tu, bali pia yataonyeshwa katika siku za baadaye. Tunasoma katika Ufunuo kwamba malaika mmoja tu atamshika Shetani na kumfunga kwa miaka elfu moja (ona Ufunuo 20:1-3). Tukio hilo la wakati ujao haliwezi kusemekana ni vita kati ya Mungu na Shetani. Ona pia kwamba Shetani hatakuwa na nguvu za kutoka gerezani humo, bali atafunguliwa wakati Mungu atakapotaka, na itakapokuwa sawa katika mapenzi Yake (ona Ufunuo 20:7-9).

Vipi Kuhusu “Vita Mbinguni” Ya Siku Zijazo?

Kama ni kweli kwamba Mungu na Shetani hawako vitani, na hawajawahi kuwepo, na hawatakuwa wakati wowote, mbona katika kitabu cha Ufunuo tunasoma kuhusu vita mbinguni hapo baadaye, ambayo Shetani anahusika (ona Ufunuo 12:7-9)? Hilo ni swali zuri, na ni rahisi kulijibu.

Ona kwamba vita hii itakuwa kati ya Mikaeli na malaika zake, na Shetani na malaika zake. Mungu hatajwi kuhusika katika vita hii. Kama angehusika, isingeitwa vita kwa sababu, Mungu, akiwa na nguvu zote, angeweza kufinya upinzani wa aina yoyote kwa muda mfupi sana tu, kama alivyothibitisha tayari.

Malaika – pamoja na Mikaeli – hawana nguvu zote, na ndiyo sababu vita yao na Shetani na malaika zake inaitwa vita kwa sababu kutakuwepo na mapambano kwa muda fulani. Lakini – kwa kuwa wao wana nguvu zaidi, watamshinda Shetani na majeshi yake.

Mbona Mungu asijihusishe na vita hii, na badala yake anawaachia malaika zake? Jibu si rahisi. Bila shaka, Mungu, akijua kila kitu, alijua kwamba malaika Zake wangeshinda vita hiyo, na pengine ndiyo maana aliona hakuna haja Yeye ajihusishe.

Bila shaka Mungu angewamaliza wale Wakanaani waovu upesi na kwa urahisi kabisa katika siku za Yoshua, lakini aliamua kuwapa Waisraeli kazi hio. Kitu ambacho Mungu angefanya bila shida yoyote kwa nukta chache, aliamua kuwaachia wafanye kwa muda mrefu, tena kwa juhudi nyingi sana. Pengine hilo lilikuwa linampendeza Mungu zaidi kwa sababu lilidai imani kwa Waisraeli. Pengine ndiyo sababu hatahusika katika ile vita ya wakati ujao huko mbinguni. Labda. Ila, Biblia haisemi.

Sasa – kwa kuwa itakuwepo vita mbinguni huko baadaye kati ya Mikaeli na malaika zake na Shetani na malaika zake, hiyo isiwe sababu ya kudhani kwamba Mungu hana nguvu zote – sawa tu na jinsi ambavyo vita za Israeli huko Kanaani zisiwe sababu ya kutufanya kufikiri kwamba Mungu hana nguvu zote.

Je, Shetani Hakushindwa Na Yesu Pale Msalabani?

Mwisho – kwa habari ya hii mada ya kwanza kwamba Mungu na Shetani wanapigana vita, tuhitimishe kwa kutazama usemi huu uliozoeleka sana: Yesu alimshinda Shetani pale msalabani. Maandiko hayasemi kwamba Yesu alimshinda Shetani msalabani.

Tunaposema kwamba Yesu alimshinda Shetani, ni kana kwamba Shetani na Yesu walikuwa katika vita, na hilo linaonyesha kwamba Mungu hana nguvu zote, na kwamba Shetani hayuko chini ya mamlaka ya Mungu tayari. Kuna njia za KiBiblia za kueleza mambo yaliyompata Shetani wakati Yesu alipotoa maisha Yake pale Kalvari. Kwa mfano: Maandiko yanatuambia kwamba kwa njia ya kifo Chake, Yesu “alimdhoofisha yeye aliyekuwa na nguvu za mauti” (ona Waebrania 2:14, 15).

Je, Yesu alimdhoofisha Shetani kwa kiwango gani? Ni wazi kwamba Shetani ana nguvu, vinginevyo mtume Yohana asingeandika hivi: “Dunia yote iko katika nguvu za yule mwovu” (1Yohana 5:19. Maneno mepesi kukazia). Kulingana na Waebrania 2:14, 15, Shetani alidhoofishwa kwa habari ya “nguvu za mauti”. Nini maana yake?

Maandiko yanataja aina tatu za mauti: mauti ya kiroho, mauti ya mwili, na mauti ya pili.

Kama tulivyokwisha jifunza mapema, mauti ya pili (au, kifo cha milele) inatajwa katika Ufunuo 2:22; 20:6, 14; 21:8, nayo huelezwa kwamba ni wakati ambapo waamini watatupwa katika ziwa la moto.

Mauti ya mwili hutokea wakati roho ya mtu inapotoka katika mwili wake, na mwili wake unaacha kufanya kazi.

Mauti ya kiroho hueleza hali ya roho ya mwanadamu ambaye hajazaliwa mara ya pili kwa njia ya Roho Mtakatifu. Mtu aliyekufa kiroho ana roho ambayo imetengwa na Mungu, roho yenye asili ya dhambi, roho ambayo, kwa kiwango fulani, imeungana na Shetani. Katika Waefeso 2:1-3 kuna picha kwa ajili yetu, ya mtu aliyekufa kiroho.

Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi; ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine.

Paulo aliandika kwamba Wakristo wa Efeso walikuwa wafu katika makosa na dhambi zao. Hakuwa anasema juu ya mauti ya mwili kwa sababu alikuwa anawaandikia watu walio hai. Basi, alikuwa anasema kwamba wamekufa, kwa jinsi ya kiroho.

Nini kilichowaua kiroho? Ni “makosa na dhambi zao”. Kumbuka Mungu alikuwa amemwambia Adamukwamba siku atakayoacha kutii, angekufa (ona Mwanzo 2:17). Mungu hakuwa anasema juu ya kifo cha kimwili bali cha kiroho, kwa sababu Adamu hakufa kimwili siku alipokula lile tunda alilokatazwa. Ila, alikufa kiroho siku hiyo, na hakufa kimwili mpaka miaka mia nyingi baadaye.

Paulo akaendelea kusema kwamba Waefeso hao, kama wafu kiroho, walikuwa wakienenda kulingana na makosa hayo na dhambi hizo, wakifuata “mtindo wa dunia” (yaani, wakifanya yote yaliyokuwa yanafanywa na kila mtu) na kumfuata “mfalme wa uwezo wa anga”.

Huyo “mfalme wa uwezo wa anga” ni nani? Ni Shetani, anayetawala ufalme wake wa giza kama amiri jeshi mkuu anayesimamia majeshi ya pepo wabaya wanaokaa angani. Hizo pepo chafu zinaorodheshwa kulingana na vyeo katika sura mojawapo ya Waefeso (ona Waefeso 6:12).

Paulo akasema kwamba huyo mfalme wa giza ni “roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi”. Maneno “wana wa kuasi” ni jina lingine tu la wasioamini wote, lenye kukazia kwamba asili yao ni ya dhambi. Baadaye Paulo anawataja kwamba “kwa tabia ni watoto wa hasira” (Waefeso 2:3. Maneno mepesi kukazia). Tena akaongezea na kusema kwamba Shetani alikuwa anafanya kazi ndani yao.

Shetani Kama Baba

Kama watu ambao hawajaokoka wanajua au hawajui, ni kwamba wao wanamfuata Shetani, na ni watu wake katika ufalme wa giza. Wana asili yake ovu na ya kibinafsi ndani ya roho zao zilizokwisha kufa. Ukweli ni kwamba Shetani ni bwana wao kiroho, na baba yao. Ndiyo sababu wakati mmoja Yesu aliwaambia viongozi wa dini ambao hawajaokoka, hivi: “Ninyi ni wa baba yenu Ibilisi, ndiyo maana mnataka kufanya mapenzi yake” (Yohana 8:44).

Hiyo ndiyo picha mbaya ya mtu ambaye hajazaliwa mara ya pili! Anaishi akiwa amekufa kiroho, akiwa amejawa na asili ya Shetani, akiwa anakwenda kwenye mauti ya mwili isiyoepukika anayoiogopa sana, na, atambue au asitambue, siku moja atapatikana na mauti mbaya zaidi sana – mauti ya milele – atakapotupwa katika ziwa la moto.

Ni muhimu sana tuelewe kwamba mauti ya kiroho, kimwili na milele ni madhihirisho ya hasira ya Mungu juu ya mwanadamu mwenye dhambi, na kwamba Shetani anahusika katika kila moja. Shetani ameruhusiwa na Mungu atawale ufalme wa giza na wote wenye “kulipenda giza” (Yohana 3:19). Yaani, ni kama Mungu alimwambia Shetani hivi: “Wewe watawale kwa nguvu zako wale wote ambao hawaninyenyekei mimi.” Shetani akawa chombo cha ghadhabu ya Mungu juu ya wanadamu waasi. Kwa kuwa wote wamefanya dhambi, wote wako chini ya nguvu za Shetani, wakijaa asili yake katika roho zao na kushikwa mateka ili kufanya mapenzi yake (ona 2Timo. 2:26).

Malipo Kwa Ajili Ya Kutekwa Kwetu

Lakini, tunaweza kumshukuru Mungu kwamba alikuwa na rehema juu ya binadamu, na kwa sababu ya huruma Zake, hakuna anayetakiwa kubaki katika hali hiyo mbaya. Kwa kuwa kifo cha Yesu badala yetu kilitosheleza madai ya haki ya Mungu, wale wote wanaomwamini Kristo wanaweza kuepukana na kifo cha kiroho na uteka wa Shetani kwa sababu hawako tena chini ya hasira ya Mungu. Tunapomwamini Yesu Kristo, Roho Mtakatifu huingia katika roho zetu na kufutilia mbali asili ya Shetani, na kuifanya roho zetu kuzaliwa mara ya pili (ona Yohana 3:1-16) na kuturuhusu kuwa washiriki wa asili ya Mungu (ona 2Petro 1:4).

Turudie swali tuliloanza nalo. Wakati mwandishi wa Waebrania anaposema kwamba Yesu, kwa njia ya kifo Chake, “alimdhoofisha yeye aliyekuwa na nguvu ya mauti, yaani Shetani” maana yake ni kwamba nguvu ya mauti ya kiroho, ambayo Shetani anayo juu ya kila mtu asiyeokoka, imevunjwa kwa wote walio “katika Kristo”. Sisi tunahuishwa kiroho kwa sababu ya Kristo; amekwisha lipa adhabu kwa ajili ya dhambi zetu.

Tena – kwa kuwa sisi hatujafa kiroho tena na hatuko tena chini ya utawala wa Shetani, hatuna haja ya kuogopa mauti ya mwili, kwa sababu tunajua kinachotungojea mbele – urithi wa utukufu mwingi, wa milele.

Mwisho – kwa sababu ya Yesu, tumekombolewa na mauti ya pili, yaani, kutupwa katika ziwa la moto.

Je, Yesu alimshinda Shetani pale msalabani? Hapana, kwa sababu hapakuwepo vita kati ya Yesu na Shetani. Ila, yesu alimdhoofisha Shetani kwa habari ya nguvu zake juu ya mauti ya kiroho, ambayo kwa hiyo anawashikilia wasio-okoka katika utumwa wa dhambi. Shetani bado ana nguvu za mauti ya kiroho juu ya watu ambao hawajaokoka, ila kwa habari ya wale walio katika Kristo, hana nguvu zozote juu yao!

Kuvuliwa Kwa Enzi Na Mamlaka

Hili pia linatusaidia kuelewa maana ya maneno ya Paulo, kwamba “enzi na mamlaka zilivuliwa uwezo wake” katika Wakolosai 2:13-15.

Na ninyi mliokuwa mmekufa [kiroho] kwa sababu ya makosa yenu …. Aliwafanya hai pamoja naye, akiisha kutusamehe makosa yote; akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; akisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo (maneno mepesi kukazia).

Paulo anatumia lugha ya mfano, yenye kueleweka kirahisi, katika fungu hili. Katika sehemu ya kwanza, analinganisha hatia yetu na “hati ya madai”. Kile ambacho sisi hatukuweza kulipa tulilipiwa na Kristo, aliyechukua deni letu la dhambi mpaka msalabani.

Katika sehemu ya pili, kama ambavyo wafalme wa kale walivyokuwa wanawavua silaha wale waliokuwa wamewashinda vitani na kuwatembeza kwa ushindi katika mitaa ya miji yao, kifo cha Kristo kilikuwa ushindi juu ya “falme, enzi na mamlaka,” yaani, majeshi ya mapepo wa ngazi za chini ambao hutawala wanadamu waasi, na kuwashika mateka.

Sasa – kutokana na fungu hili, hatuwezi kusema kwamba Kristo alimshinda Shetani? Labda, lakini kwa kuongeza maelezo. Inatupasa kukumbuka kwamba, katika fungu hili, Paulo alikuwa anaandika kwa lugha ya mfano. Na kila mfano una mahali ambapo mlinganisho hubadilika na kupingana, kama tulivyojifunza katika sura juu ya kutafsiri maandiko.

Katika kutafsiri mifano ya Paulo katika Wakolosai 2:13-15, lazima tuwe makini. Ni wazi kwamba hapakuwepo na “hati ya mashtaka” iliyokuwa imeandikwa dhambi zetu zote, iliyogongomewa pale msalabani. Ila, ni mfano wa yale ambayo Yesu alifanikisha.

Vivyo hivyo, mapepo waliotawala wanadamu ambao hawajaokoka hawakunyang’anywa panga zao na ngao zao na kutembezwa na Yesu hadharani barabarani. Lugha anayotumia Paulo ni ya mfano tu kuonyesha kile ambacho Yesu alifanikisha kwa ajili yetu. Tulikuwa mateka wa pepo hizo. Lakini, kwa kufa kwa ajili ya dhambi zetu, Yesu alitufungua kutoka uteka wetu. Si kwamba alipambana ana kwa ana na hao pepo wabaya, wala hawakuwa vitani Naye. Wao, kwa kuruhusiwa na haki ya Mungu, walikuwa ametutawala kwa nguvu zao maisha yetu yote. “Silaha” zao hazikuwa zime-elekezwa kwa Kristo, bali kwetu. Lakini, Yesu “aliwanyang’anya silaha” zao. Hawana uwezo wa kutushika mateka tena.

Tusije tukafikiri kwamba kulikuwepo na vita ya miaka na miaka kati ya Yesu na mapepo wa Shetani, na hatimaye Yesu akashinda vita hiyo pale msalabani. Tukisema kwamba Yesu alimshinda Shetani, ni vizuri tuelewe kwamba alimshind Shetani kwa ajili yetu, si kwa ajili Yake Mwenyewe.

Wakati fulani nilifukuza mbwa mdogo aliyekuwa anamtishia binti yangu. Naweza kusema kwamba nilimshinda huyo mbwa, lakini usidhani kwamba huyo mbwa alikuwa kitisho kwangu. Alikuwa anamtishia binti yangu. Ndivyo ilivyokuwa kwa Yesu na Shetani. Yesu alimfukuza mbwa aliyekuwa anatutishia sisi, si Yeye.

Alimfukuzaje huyo Shetani mbwa? Alifanya hivyo kwa kuchukua adhabu za dhambi zetu, na kwa njia hiyo kutuweka huru kutokana na hatia yetu mbele za Mungu. Kwa kufanya hivyo, alituweka huru kutokana na hasira ya Mungu, na hivyo, wale pepo wachafu ambao Mungu anawaruhusu kwa haki kabisa kuwatawala wanadamu waasi hawakuwa na haki tena ya kututawala sisi. Mungu asifiwe kwa hilo!

Tunafikia mahali panapofaa, kutazama hekaya ya pili.

Hekaya Ya Pili: “Zipo vita zinazoendelea katika ulimwengu wa roho, kati ya malaika wa Mungu na wa Shetani. Matokeo ya vita hizo hutegemeana na jinsi sisi tunavyopigana vita kiroho.”

Tayari tumejifunza kutoka kitabu cha Ufunuo kwamba siku moja itakuwepo vita mbinguni kati ya Mikaeli na malaika zake, na Shetani na malaika zake. Zaidi ya hapo, kuna vita nyingine moja kati ya malaika inayotajwa katika Maandiko, katika Danieli sura ya kumi.[1]

Danieli anatuambia alikuwa akiomboleza kwa majuma matatu katika mwaka wa tatu wa utawala wake Koreshi, mfalme wa Uajemi. Mara malaika akamtokea kando ya Mto Tigris. Kusudi la safari ya malaika lilikuwa kumpa yeye ufahamu juu ya wakati ujao wa taifa la Israeli, na tayari tumetazama kwa kifupi yale ambayo Danieli aliambiwa kuhusu Unyakuo na Nyakati za Mwisho katika sura iliyotangulia. Katika mazungumzo yao, malaika huyo ambaye hatajwi jina alimwambia Danieli hivi:

Usiogope, Danieli; kwa maana tangu siku ile ya kwanza ulipotia moyo wako ufahamu, na kujinyenyekeza mbele za Mungu wako, maneno yako yalisikiwa; nami nimekuja kwa ajili ya maneno yako. Lakini mkuu wa ufalme wa Uajemi alinipinga siku ishirini na moja; bali, tazama, huyo Mikaeli, mmoja wa hao wakuu wa mbele, akaja kunisaidia; nami nikamwacha huko pamoja na wafalme wa Uajemi (Danieli 10:12, 13. Maneno mepesi kukazia).

Danieli akajua kwamba maombi yake yalikwisha sikiwa majuma matatu kabla ya kukutana na huyo malaika, lakini pia akajua kwamba malaika mwenyewe ametumia majuma matatu kumfikia. Sababu ya kuchelewa kwa malaika ni kwamba, “mkuu wa ufalme wa Uajemi” alimpinga. Ila, alifanikiwa kupenya wakati Mikaeli, “mmoja wa hao wakuu wa mbele” alipofika kumsaidia.

Alipokaribia kuondoka, malaika alimwambia Danieli hivi:

Na sasa nitarudi ili nipigane na mkuu wa Uajemi; nami nitakapotoka huku, tazama, mkuu wa Uyunani atakuja. Lakini nitakuambia yaliyoandikwa katika maandiko ya kweli; wala hapana anisaidiaye juu ya hao ila huyo Mikaeli, mkuu wenu (Danieli 10:20, 21).

Zipo kweli kadhaa za kusisimua zipatikanazo katika fungu hili. Hapa tena tunaona kwamba malaika wa Mungu hawana nguvu zote, na wanaweza kuingia katika mapigano na malaika waovu.

Pili tunajifunza kwamba malaika wengine (kama vile Mikaeli) wana nguvu zaidi kuliko wengine (kama huyo aliyezungumza na Danieli).

Maswali Tusiyokuwa Na Majibu Yake

Tunaweza kuuliza hivi: “Kwa nini Mungu hakumtuma Mikaeli kupeleka huo ujumbe kwa Danieli moja kwa moja, ili kusiwe na kuchelewa kwa majuma matatu?” Ukweli ni kwamba Biblia haituambii sababu za Mungu kumtuma malaika ambaye alijua kabisa asingeweza kumpita “mkuu wa ufalme wa Uajemi” bila kusaidiwa na Mikaeli. Ukweli ni kwamba hatujui ni kwa nini Mungu atumie malaika yeyote ili kupeleka ujumbe kwa mtu! Mbona hakwenda Mwenyewe, au kusema na Danieli kwa sauti, au kumfikisha Danieli mbinguni kwa muda tu ili amwambie? Hatujui!

Sasa je! Maandiko haya yanathibitisha kwamba kuna vita za mara kwa mara katika ulimwengu wa roho kati ya malaika wa Mungu na wa Shetani? Hapana. Maandiko haya yanathibitisha tu kwamba, miaka elfu kadhaa iliyopita, kulikuwa na mapambano ya majuma matatu kati ya malaika moja dhaifu wa Mungu, na malaika mmoja mwenye nguvu wa Shetani, aitwaye “mkuu wa ufalme wa Uajemi.” Vita hiyo, kama Mungu angetaka, isingetokea kamwe. Vita nyingine ya malaika inayotajwa katika Biblia ni ile ya wakati ujao huko mbinguni, iliyoandikwa katika Kitabu cha Ufunuo. Basi. Pengine zimekuwepo vita zingine za malaika zilizotokea, lakini tukiamua hivyo tutakuwa tunakisia tu – hatuna ushahidi.

Hekaya Iliyojengwa Juu Ya Hekaya

Je, hii habari ya Danieli na mkuu wa ufalme wa Uajemi inathibitisha kwamba vita yetu ya kiroho inaweza kuamua matokeo ya vita za malaika? Hapa tena, wazo hili linadhania (kutokana na maandiko machache sana) kwamba zipo vita mara kwa mara kati ya malaika. Hebu tukisie tu na kukubali kwamba ndiyo, zipo vita za malaika mara kwa mara. Je, habari hii kuhusu Danieli inathibitisha kwamba vita yetu ya kiroho inaweza kuamua matokeo ya vita za malaika ambazo pengine zinakuwepo?

Mara nyingi, watu wenye kusambaza mawazo haya huuliza swali hili: “Ingekuwaje kama Danieli angekata tamaa baada ya siku moja?” Swali hilo halina jibu kutoka kwa yeyote, maana Danieli hakuacha kumtafuta Mungu katika maombi mpaka huyo malaika asiyejulikana alipofika. Ila, sababu ya kuliuliza ni kutushawishi tuamini kwamba, Danieli, kwa kuendelea katika vita ya kiroho, alikuwa funguo ya ushindi katika vita ya huyo malaika asiyetajwa jina. Kama Danieli angekata tamaa na kuacha kupambana kiroho, inadaiwa kwmaba huyo malaika asingempita yule mkuu wa ufalme wa Uajemi. Wanataka tuamini kwamba hata sisi, kama Danieli, lazima tudumu katika vita ya kiroho, la sivyo malaika fulani mwovu atawashinda malaika wema wa Mungu.

Sawa, lakini – Ni vizuri kwanza tujue kwamba Danieli hakuwa “kwenye vita ya kiroho” – yeye alikuwa anamwomba Mungu. Hatusomi popote kwamba alisema kitu kinyume cha mapepo, au kwamba aliwafunga, au kwamba “alipigana” nao. Ukweli ni kwamba, Danieli hakujua kwamba kulikuwa na vita baina ya malaika mpaka baada ya majuma matatu kupita, na yule malaika asiyetajwa jina kumtokea. Yeye alitumia majuma hayo matatu katika kufunga na kumtafuta Mungu.

Basi tuliseme swali hilo kwa namna nyingine: Kama Danieli angeacha kuomba na kumtafuta Mungu baada ya siku moja au mbili, je, huyo malaika asiyetajwa jina angeshindwa kumfikishia ujumbe wa Mungu? Hatujui, ila ni vizuri kusema kwamba yule malaika asiyetajwa jina hakumwambia Danieli hivi: “Ni vizuri uliendelea kuomba maana kama si hivyo, nisingefanikiwa.” Hapana! Malaika alimsifu Mikaeli kwa kufanikiwa kwake. Bila shaka Mungu ndiye aliyemtuma malaika huyo asiyetajwa jina, pamoja na Mikaeli, Naye aliwatuma kama itikio la maombi ya Danieli kutaka kuelewa mambo ambayo yangetokea katika siku zijazo za Israeli.

Ni mawazo tu kudhani kwamba kama Danieli angeacha kufunga au kumtafuta Mungu, Mungu angesema hivi: “Haya! Ninyi malaika wawili, Danieli ameacha kufunga na kuomba. Kwa hiyo, ingawa nilimtuma mmoja wenu kumpelekea ujumbe siku ile ya kwanza alipoanza maombi, achaneni na huo ujumbe. Kitabu chake hakitakuwa na sura ya kumi na moja wala ya kumi na mbili.”

Hakika Danieli alidumu katika maombi (si katika “vita ya kiroho”), na Mungu alimwitikia kwa kutuma malaika. Sisi nasi tunapaswa kudumu katika kumwomba Mungu, na kama Mungu atapenda, jibu letu linaweza kuja kwa njia ya malaika. Lakini usisahau kwamba kuna mifano mingi sana ya malaika kupeleka jumbe muhimu sana kwa watu katika Biblia, ambapo hapataji hata sala moja ya mtu yeyote, licha ya kuomba majuma matatu.[2] Tuwe na msimamo. Tena, kuna mifano mingi sana ya malaika kuwapa watu jumbe, na katika mifano hiyo hakuna kutajwa kwamba ilibidi wapambane na mapepo walipokuwa wanatoka mbinguni. Labda hao malaika walipambana na mapepo ili kuweza kufikisha jumbe zao, lakini kama ilikuwa hivyo, hatuna habari, maana Biblia haisemi.

Tunafikia kwenye hekaya ya tatu, inayoaminika sana.

Hekaya Ya Tatu: “Adamu Alipoanguka, Shetani Alipata Haki Ya Adamu Kutawala Ulimwengu.”

Je, ni kitu gani kilichotokea kwa Shetani wakati binadamu walipoanguka? Kuna

wanaodhani kwamba Shetani alipata cheo kikubwa sana Adamu alipoanguka. Wanasema mwanzoni Adamu alikuwa ndiye “mungu wa dunia hii,” lakini alipoanguka, Shetani akapata cheo hicho na kuwa na haki ya kufanya chochote alichotaka hapa duniani. Hata Mungu hakuweza kumzuia kuanzia wakati huo na kuendelea, kwa sababu Adamu alikuwa na ”haki kisheria” kumpa Shetani cheo chake na nafasi yake, na Mungu ilibidi aheshimu makubaliano kati Yake na Adamu, ambayo sasa yalikuwa kwa Shetani. Inasemekana kwamba sasa hivi Shetani ndiye mwenye “hati miliki ya Adamu”, na Mungu hawezi kumzuia kitu Shetani mpaka “hati miliki ya Adamu itakapofikia mwisho wake”.

Tunauliza hivi: Je, nadharia hiyo ni kweli? Je, Shetani alipata “hati miliki ya Adamu” wakati binadamu walipoanguka? Jibu ni HAPANA KABISA! Shetani hakupata chochote wakati binadamu walipoanguka isipokuwa laana kutoka kwa Mungu, na ahadi kuhusu kuangamizwa kwake kabisa.

Ukweli ni kwamba Biblia haisemi kwamba Adamu alikuwa ndiye “mungu wa dunia hii”. Tena, Biblia haisemi kwamba Adamu alikuwa na haki kisheria ya kumpa mtu mwingine mamlaka anayodhaniwa kuwa nayo juu ya dunia. Tena, Biblia haisemi kwamba Adamu alikuwa na hati miliki ambayo siku moja ingefikia mwisho. Mawazo hayo yote si ya KiBiblia.

Sasa basi: Adamu alikuwa na mamlaka gani? Tunasoma katika Mwanzo kwamba Mungu alimwambia Adamu na Hawa hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi” (Mwanzo 1:28. Maneno mepesi kukazia).

Mungu hakusema chochote kwa Adamu juu ya kuwa “mungu” duniani, au kwamba angeweza kutawala kila kitu, kama vile hali ya hewa na watu wote ambao wangezaliwa baadaye na kadhalika. Yeye alimpa Adamu na Hawa kama binadamu wa kwanza, utawala juu ya samaki, ndege na wanyama, na kuwaagiza waijaze dunia na kuitiisha.

Wakati Mungu alipotamka hukumu kwa mwanadamu, hakusema chochote kuhusu Adamu kupoteza inayodhaniwa kuwa nafasi yake kama “mungu wa dunia hii.” Tena, hakusema chochote kwa Adamu na Hawa kuhusu wao kutokuwa na mamlaka tena juu ya samaki, ndege na wanyama. Ni dhahiri kwamba bado binadamu wanatawala juu ya samaki na ndege na “kila kiendacho juu ya nchi”. Binadamu bado wanaijaza dunia na kuitiisha. Wakati wa kuanguka binadamu, Adamu hakupoteza mamlaka yake aliyopewa na Mungu.

Je, Shetani Si “Mungu Wa Dunia Hii”?

Lakini, mbona Paulo anamtaja Shetani kuwa “mungu wa dunia hii,” na Yesu kumtaja kuwa “mkuu wa dunia hii”? Ndiyo, lakini hakuna aliyesema kwamba Adamu aliwahi kuwa “mungu wa dunia hii” au kwamba Shetani alipata cheo hicho kutoka kwa Adamu, alipoanguka.

Tena, jina hilo la Shetani kwamba ni “mungu wa dunia hii” halithibitishi kwamba Shetani anaweza kufanya chochote atakacho hapa duniani, au kwamba Mungu hana uwezo wa kumzuia. Yesu alisema hivi: “Nimepwa mamlaka yote mbinguni na duniani” (Mathayo 28:18. Maneno mepesi kukazia). Kama Yesu ana mamlaka yote duniani, ni kwamba Shetani anaweza kutenda kazi kwa ruhusa Yake tu.

Nani aliyempa Yesu mamlaka yote mbinguni na duniani? Bila shaka ni Mungu Baba, ambaye alikuwa nayo Mwenyewe, ili ampe Yesu. Ndiyo sababu Yesu alisema juu ya Baba yake kwamba ni “Bwana wa mbingu na dunia” (Mathayo 11:25; Luka 10:21. Maneno mepesi kukazia). Mungu amekuwa na mamlaka yote duniani tangu alipoiumba. Alitoa mamlaka kidogo kwa binadamu mwanzoni, na hawajawahi kupoteza kile alichokitoa Mungu.

Biblia inaposema juu ya Shetani kuwa mungu au mtawala au mkuu wa dunia hii, maana yake hasa ni kwamba watu wa dunia (yaani, ambao hawajazaliwa mara ya pili) wanamfuata Shetani. Yeye ndiye wanayemtumikia, wajue au wasijue. Yeye ni mungu wao.

Je, Shetani Alifanya Toleo Lolote?

Nadharia hiyo ya Shetani kupata utawala imejengwa kwenye hadithi ya kujaribiwa kwa Yesu huko nyikani na Shetani, kama ilivyoandikwa katika Mathayo na Luka. Hebu tuchunguze maelezo atoayo Luka ili tuone tunachoweza kujifunza.

[Shetani] Akampandisha juu, akamwonyesha miliko zote za ulimwengu kwa dakika moja. Ibilisi akamwambia, ‘Nitakupa wewe enzi hii yote, na fahari yake, kwa kuwa imo mikononi mwangu, nami humpa yeyote kama nipendavyo. Basi, wewe ukisujudu mbele yangu yote yatakuwa yako.’ Yesu akajibu akamwambia, ‘Imeandikwa: Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake’ (Luka 4:5-8).

Je, tukio hili linathibitisha kwamba Shetani ana mamlaka juu ya kila kitu duniani, au kwamba Adamu alimpa kila kitu, au kwamba Mungu hana uwezo wa kumzuia? Hapana, na sababu zinafuata.

Kwanza: Tuwe makini sana kuhusu kujenga itikadi juu ya tamko lililofanywa na mtu ambaye Yesu anamwita “baba wa uongo” (Yohana 8:44). Wakati mwingine Shetani husema ukweli, lakini kat ika swala hili, tunapaswa kuwa macho kwa sababu kile alichosema Shetani kinapingana na kitu ambacho kilikwisha semwa na Mungu.

Katika sura ya nne ya kitabu cha Danieli, tunapata hadithi ya kunyenyekezwa kwa mfalme Nebukadneza. Huyu mfalme, akiwa amejaa kiburi juu ya cheo chake na nafasi yake na mafanikio yake, aliambiwa na nabii Danieli kwamba angepewa akili ya mnyama mpaka atakapotambua kwamba “Aliye juu ndiye anayemiliki katika ufalme wa wanadamu, naye humpa yeye amtakaye, awaye yote” (Danieli 4:25. Maneno mepesi kukazia). Tamko hilo linatolewa mara nne katika habari hii, kutilia mkazo umuhimu wake (tazama 4:17, 25, 32; 5:21).

Ona kwamba Danieli alisema hivi: “Aliye juu ndiye anayemiliki katika ufalme wa wanadamu.” Hiyo inaonyesha kwamba Mungu ana mamlaka kiasi fulani juu ya dunia, sivyo?

Ona vile vile kwamba anachosema Danieli ni kinyume kabisa na kile ambacho Shetani alimwambia Yesu. Danieli anasema “naye humpa yeye amtakaye, awaye yote”. Shetani akasema, “nami humpa yeyote, kama nipendavyo” (Luka 4:6).

Sasa, wewe utamwamini nani? Mimi nimeamua kumwamini Danieli.

Lakini – kuna uwezekano kwamba Shetani alikuwa anasema ukweli – tukitazama alichosema kutoka upande mwingine.

Shetani ni “mungu wa dunia hii” kama tulivyokwisha ona. Maana yake ni kwamba anatawala ufalme wa giza, ambao ni pamoja na watu katika kila taifa waliomwasi Mungu. Biblia inasema hivi: “Dunia yote pia hukaa katika yule mwovu” (1Yohana 5:19). Wakati Shetani alipodai kwamba angeweza kumpa yeyote apendaye mamlaka juu ya falme za dunia, yawezekana alikuwa anazungumza juu ya enzi yake mwenyewe, yaani ufalme wa giza, ambayo inaundwa na falme ndogo ndogo ambazo zinakubaliana kwa sehemu na falme za duniani kijiografia. Tunajulishwa na Maandiko kwamba Shetani ana ngazi kadhaa za vyeo miongoni mwa pepo wake wabaya, ambazo kupitia hizo anatawala ufalme wake (ona Waefeso 6:12), na ni sawa tukikisia kwamba yeye ndiye mwenye kuwapandisha au kuwashusha vyeo hao pepo katika ngazi zao, maana ndiye mkuu. Kwa hali hiyo, Shetani alikuwa anampa Yesu kihalali kabisa nafasi ya kuwa pepo msaidizi, ili amsaidie kutawala katika ufalme wake wa giza. Kitu alichopaswa kufanya Yesu ni kumsujudia Shetani na kumwabudu. Shukuru kwa sababu Yesu hakukubaliana na nafasi hiyo ya “kupanda cheo”!

Nani Aliyempa Shetani Cheo Chake?

Sasa: Vipi kuhusu madai ya Shetani kwamba mamlaka juu ya falme hizo amepewa yeye?

Hapa tena lazima tujue kuna uwezekano mkubwa tu kwamba alikuwa anadanganya. Lakini hebu tuseme alikuwa anasema ukweli, tuone.

Ona kwamba Shetani hakusema Adamu ndiye alimpa mamlaka hayo. Kama tulivyokwisha ona mapema, Adamu asingeweza kuwa alimpa Shetani kwa sababu hakuwa na kitu cha kutoa. Adamu alitawala samaki, ndege na wanyama, si falme. (Ukweli ni kwamba wakati Adamu anaanguka, hakukuwepo falme za watu za kutawala.) Tena, kama Shetani alikuwa anampa Yesu utawala juu ya ufalme wa giza, ambao ni mapepo wote na watu ambao hawajaokoka, isingewezekana kabisa kwamba Adamu ndiye alimpa Shetani ufalme huo. Shetani alikuwa anatawala malaika walioanguka kabla Adamu hajaumbwa.

Yawezekana Shetani alimaanisha kwamba watu wote wa duniani walimpa yeye mamlaka juu yao, maana hawakujitolea kwa Mungu na kwa njia hiyo, kwa kujua au pasipo kujua, walikuwa wamejitolea kwake yeye.

Uwezekano bora zaidi ni kwamba Mungu ndiye alimpa mamlaka hayo. Inawezekana kabisa, kutokana na Maandiko, kwamba Mungu alimwambia Shetani, “Wewe na pepo wako waovu mna ruhusa Yangu kutawala juu ya kila mtu ambaye hajajitolea kwangu.” Unaweza kushindwa kulipokea hilo, lakini baadaye utaona kwamba pengine hayo ndiyo maelezo bora zaidi ya madai aliyotoa Shetani. Kama kweli Mungu ni “mtawala juu ya wanadamu wote” (Danieli 4:25), basi mamlaka yoyote ambayo Shetani anayo lazima awe alipewa na Mungu.

Shetani anatawala ufalme wa giza tu, ambao pia unaweza kuitwa “ufalme wa uasi.” Yeye alikuwa anatawala ufalme huo tangu siku ile alipofukuzwa mbinguni, kitu kilichotokea kabla ya kuanguka kwa Adamu. Mpaka wakati Adamu alipoanguka, ufalme wa giza ulikuwa na malaika waasi tu. Lakini wakati Adamu alipotenda dhambi, yeye naye akajiunga katika kundi la waasi, na ufalme wa Shetani tangu hapo ukawa na binadamu waasi, pamoja na malaika waasi.

Shetani alikuwa anatawala juu ya ufalme wake wa giza kabla hata Adamu hajaumbwa. Basi, tusije tukafikiri kwamba Adamu alipoanguka, Shetani alipata kitu ambacho Adamu alikuwa nacho. Hapana. Wakati Adamu alipotenda dhambi, alijiunga ufalme wa uasi ambao ulikuwepo kwa muda mrefu tu – ufalme uliotawaliwa na Shetani.

Je, Mungu Alishtushwa Na Anguko?

Hitilafu nyingine katika nadharia kwamba “Shetani Alifaidika” ni kwamba, inamfanya Mungu aonekane mpumbavu, kana kwamba alishtukizwa na matukio ya anguko, na kwa sababu hiyo, akajikuta katika hali ya kusikitisha. Je, Mungu hakujua kwamba Shetani angewajaribu Adamu na Hawa na kwamba binadamu wangeanguka kwa sababu hiyo? Ikiwa Mungu anajua yote – na ni kweli anajua yote – basi alikuwa anajua yatakayotokea. Ndiyo sababu Biblia inatuambia kwamba alifanya mipango ya kukomboa wanadamu hata kabla ya kuwaumba (ona Mathayo 25:34; Matendo 2:2-23; 4:27, 28; 1Wakor. 2:7,8; Waefeso 3:8-11; 2Timo. 1:8-10; Ufunuo 13:8).

Mungualimwumba Shetani akijua ataanguka, na alimwumba Adamu na Hawa akijua wataanguka. Hakuna jinsi ambavyo Shetani angeweza kumdanganya Mungu na kupata kitu ambacho Mungu hakutaka awe nacho.

Je, maana yake ni kwamba Mungu anataka Shetani awe “mungu wa dunia hii?” Ndiyo, kwa muda wote ambao itatimiza makusudi Yake. Kama Mungu asingemtaka

Shetani afanye kazi, angemzuia tu mara moja kama atakavyofanya wakati mmoja, katika Ufunuo 20:1, 2.

Lakini, si kwamba Mungu anataka yeyote abaki chini ya utawala wa Shetani. Mungu anamtaka kila mmoja aokolewe na kuepukana na utawala wa Shetani (Matendo 26:18; Wakolosai 1:13; 1Timo. 2:3, 4; 2Petro 3:9). Lakini Mungu anamruhusu Shetani kutawala kila mtu anayependa giza (ona Yohana 3:19) – yaani, wale wote wanaoendelea kuwa kinyume Chake.

Je, hakuna chochote tunachoweza kufanya ili kuwasaidia watu waepukane na ufalme wa Shetani wa giza? Kipo. Tunaweza kuwaombea na kuwaita watubu na kuiamini Injili (kama tulivyoagizwa na Yesu). Wakifanya hivyo, watawekwa huru kutoka mamlaka ya Shetani. Lakini kudhani kwamba tunaweza “kuangusha” pepo wabaya wanaowashikilia watu ni makosa. Kama watu wanataka kukaa gizani, Mungu atawaruhusu. Yesu aliwaambia wanafunzi Wake kwamba kama watu katika miji fulani wasingepokea ujumbe wao, wakung’ute mavumbi ya miguu yao na kwenda mji mwingine (Mathayo 10:14). Hakuwaambia wakae na kuangusha ngome juu ya mji huo ili watu waweze kupokea zaidi. Mungu huruhusu pepo wabaya kuwafunga watu wanaokataa kutubu na kumrudia Yeye.

Ushahidi Zaidi Kuhusu Mamlaka Ya Mungu Juu Ya Shetani

Yapo maandiko mengine mengi yenye kuthibitisha vizuri sana kwamba Mungu hakupoteza mamlaka yoyote juu ya Shetani wakati mwanadamu alipoanguka. Biblia mara kwa mara inatuambia kwamba Mungu siku zote ana mamlaka juu ya Shetani, na atakuwa nayo. Shetani anaweza kufanya kile anachoruhusiwa kufanya na Mungu tu. Hebu tutazame kwanza mifano kadhaa kutoka Agano la Kale juu ya jambo hili.

Sura mbili za kwanza za kitabu cha Ayubu zinaeleza mfano wa mamlaka ya Mungu juu ya Shetani. Hapo tunasoma kuhusu Shetani mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, akimshtaki Ayubu. Ayubu alikuwa mtiifu kwa Mungu kuliko mtu mwingine yeyote duniani wakati huo. Basi, Shetani akamtafuta sana. Mungu alijua kwamba Shetani “ameweka moyo wake” juu ya Ayubu (1:8). Basi, alimsikiliza Shetani alipomshtaki kwa kumtumikia Mungu tu kwa sababu ya baraka zote ambazo alikuwa anazifurahia (ona Ayubu 1:9-12).

Shetani alisema Mungu alikuwa ameweka uzio kumzunguka Ayubu, na akamwomba aondoe baraka za Ayubu. Basi, Mungu alimruhusu Shetani kumtesa Ayubu kwa kiwango fulani. Mwanzoni, hakuruhusiwa kugusa mwili wa Ayubu, ila baadaye, Mungu alimruhusu Shetani kuutesa mwili wake. Lakini alimkataza kumwua (Ayubu 2:5, 6).

Fungu hili moja la Maandiko hakika linathibitisha kwamba Shetani hawezi kufanya chochote anachotaka. Hakuweza kugusa mali za Ayubu mpaka Mungu alipomruhusu. Hakuweza kuiba afya ya Ayubu mpaka Mungu alipomruhusu. Na hakuweza kumwua Ayubu kwa sababu Mungu alimkataza.[3] Ni hivi: Mungu anamtawala Shetani kikamilifu, hata tangu wakati wa anguko la Adamu.

Roho Mbaya Ya Sauli, “Kutoka Kwa Bwana”

Kuna mifano mingi ya Mungu akiwatumia pepo wabaya wa Shetani kama mawakala wa ghadhabu Yake katika Agano la Kale. Tunasoma hivi katika 1Samweli 16:14 – “Basi roho ya BWANA ilikuwa imemwacha Sauli, na roho mbaya kutoka kwa BWANA ikamsumbua.” Hali hii bila shaka ilitokea kwa sababu ya adhabu ya Mungu juu ya Sauli mfalme, aliyeacha kumtii Mungu.

Swali kubwa ni hili: Nini maana ya maneno yale, “roho mbaya kutoka kwa BWANA”? Je, maana yake ni kwamba Mungu alituma pepo anayekaa Naye huko mbinguni, au maana yake ni kwamba Mungu aliruhusu pepo mmoja mwovu wa Shetani kumsumbua Sauli? Nadhani Wakristo wengi watakubaliana na maana ya pili, kutokana na mengine yanayofundishwa na Biblia. Sababu ya Maandiko kusema kwamba huyo pepo alitoka “kwa BWANA” ni kutokana na ukweli kwamba kazi yake ya kumsumbua Sauli ilitokana na adhabu ya Mungu juu yake. Basi, tunaona kwamba hata pepo wako chini ya utawala wa enzi ya Mungu.

Tunasoma pia katika Waamuzi 9:23 hivi: “Kisha Mungu akapeleka roho mbaya kati ya Abimeleki na watu wa Shekemu”, ili hukumu ya Mungu iwajie kwa sababu ya matendo yao maovu. Hapo tena, huyu pepo hakutoka mbinguni kwa Mungu bali katika ufalme wa Shetani, na aliruhusiwa na Mungu kutekeleza mambo maovu dhidi ya watu fulani, waliostahili hayo. Pepo hawawezi kufanikiwa kutimiza mipango yao miovu dhidi ya mtu awaye yote bila ya ruhusa ya Mungu. Kama si hivyo, basi Mungu hana nguvu zote. Kwa hiyo, tunaweza kuhitimisha kwa kusema kwamba, wakati Adamu alipoanguka, Shetani hakupata mamlaka yaliyozidi mipaka aliyoweka Mungu.

Mifano Ya Agano Jipya Kuhusu Nguvu Za Mungu Juu Ya Shetani

Agano Jipya linatoa ushahidi wa ziada wenye kupingana na hoja kwamba Shetani alifaidika kutokana na Anguko la Adamu.

Kwa mfano: Tunasoma katika Luka 9:1 kwamba Yesu aliwapa wanafunzi wake kumi na mbili “mamlaka juu ya pepo wote”. Tena katika Luka 10:19, Yesu aliwaambia hivi: “Tazama, nimewapa mamlaka ya kukanyaga nyoka na nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu chochote kitakachowadhuru” (maneno mepesi kukazia).

Kama Yesu aliwapa wao mamlaka juu ya nguvu zote za Shetani, ni kwamba Yeye alikuwa na hayo mamlaka. Shetani yuko chini ya mamlaka ya Mungu.

Baadaye katika Injili ya Luka tunasoma habari za Yesu akimwambia Petro hivi: “Simoni! Simoni! Tazama, Shetani ameomba ruhusa ili akupepete kama ngano” (Luka 22:33, TLR). Maandiko yanaonyeshakwamba asingeweza kumpepeta Petro bila ya kupata ruhusa kutoka kwa Mungu kwanza. Hapo tena, Shetani anaonyesha kuwa chini ya mamlaka ya Mungu.[4]

Kifungo Cha Shetani Cha Miaka Elfu Moja

Tunaposoma habari za kufungwa kwa Shetani na malaika mmoja tu katika Ufunuo 20, Adamu hatajwi hapo kwamba milki yake imefikia mwisho. Sababu itoleayo hapo ni kwamba, “ili asiwadanganye tena mataifa” (Ufunuo 20:3).

Ajabu ni hii: Baada ya Shetani kufungwa miaka elfu moja, atafunguliwa, “naye atatoka ili kuwadanganya mataifa, walio katika pembe nne za dunia” (Ufunuo 20:8). Hayo mataifa yatakayodanganywa yataandaa majeshi yao ili kushambulia Yerusalemu, mahali ambapo Yesu atakuwepo akitawala. Baada ya kuuzunguka mji, moto utatoka mbinguni na “kuwateketeza” (Ufunuo 20:9).

Je, kuna anayeweza kuwa mjinga kiasi cha kusema kwamba haki ya kumiliki ya Adamu ilihusu kipindi kifupi tu cha muda baada ya miaka elfu moja, na ndiyo maana Mungu ilibidi amwachie Shetani kwa sababu hiyo? Wazo kama hilo ni la kipuuzi!

Hapana! Tunachojifunza kwa mara nyingine tena kutoka fungu hili la Maandiko ni kwamba Mungu ana mamlaka kamili juu ya Shetani, na humruhusu afanye udanganyifu wake ili kutimiza makusudi Yake tu.

Katika ule utawala wa Yesu hapo baadaye wa miaka elfu moja, Shetani hatakuwa katika utendaji – atashindwa kumdanganya mtu yeyote. Ila, watakuwepo watu duniani watakaokuwa watiifu kwa utawala wa Kristo kwa nje tu, ambao ndani watapenda kumwona aking’olewa madarakani. Lakini hawatajaribu kufanya mapinduzi kwa sababu wanajua hawawezi kumpindua mtu “atakayetawala kwa fimbo ya chuma” (Ufunuo 19:15).

Lakini Shetani atakapofunguliwa, ataweza kuwadanganya wale ambao wanamchukia Kristo mioyoni mwao, nao watajaribu kufanya yasiyowezekana, kwa sababu ya upumbavu. Naye Shetani atakaporuhusiwa kuwadanganya waasi waliojificha, hali halisi ya mioyo yao itafunuliwa, ndipo Mungu kwa haki kabisa atakapowahukumu wale ambao hawastahili kuishi katika ufalme Wake.

Hiyo ndiyo sababu moja ya Mungu kumruhusu Shetani kuwadanganya watu siku hizi. Baadaye tutachunguza makusudi kamili ya Mungu kwa ajili ya Shetani, lakini kwa sasa yatosha tu kusema kwamba Mungu hataki mtu yeyote abaki amedanganywa. Ila, anataka kujua kilichomo mioyoni mwa watu. Shetani hawezi kuwadanganya wale wanaojua na kuamini kweli. Lakini Mungu anamruhusu Shetani kuwadanganya wale ambao, kwa sababu ya mioyo yao migumu, wanakataa ukweli.

Paulo anasema juu ya kipindi cha utawala wa mpingakristo, kama ifuatavyo:

Hapo ndipo atakapofunuliwa yule asi, ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, na kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake; yule ambaye kuja kwake ni kwa mfano wa kutenda kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za uongo; na katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa. Kwa hiyo Mungu awaletea nguvu ya upotevu, wauamini uongo; ili wahukumiwe wote ambao hawakuiamini kweli, bali walikuwa wakijifurahisha katika udhalimu (2Wathes. 2:8-12. Maneno mepesi kukazia).

Ona kwamba anayetajwa kwamba atatuma “nguvu ya upotevu, wauamini uongo” ni Mungu. Lakini pia ona kwamba watu hao watakaodanganywa ni watu ambao “hawakuiamini kweli,” kuonyesha kwamba wao walipata nafasi, lakini bado walikataa Injili. Mungu atamruhusu Shetani kumtia nguvu mpingakristo kwa uwezo wa kufanya ishara za uongo na maajabu, ili wanaomkataa Kristo wadanganyike, na kusudi la Mungu hatimaye ni kwamba “wote wahukumiwe.” Kwa sababu hiyo hiyo, Mungu anamruhusu Shetani kuwadanganya watu siku hizi.

Kama Mungu hakuwa na sababu ya kumruhusu Shetani kufanya kazi hapa duniani, angekwisha mfukuza aende mahali pengine, wakati alipoanguka. Tunaambiwa katika 2Petro 2:4 kwamba kuna malaika fulani waliotenda dhambi ambao tayari Mungu amekwisha watupa kuzimu, na kuwafunga katika “vifungo vya giza, wakisubiri hukumu.” Mungu wetu mwenye nguvu zote angeweza kufanya hivyo hivyo kwa Shetani na kwa yeyote katika malaika zake kama ingefaa mapenzi Yake makamilifu. Lakini, kwa muda kidogo zaidi, Mungu ana sababu nzuri tu za kumruhusu Shetani na malaika zake kufanya kazi hapa duniani.

Hofu Ya Mapepo Kuteswa

Tunapomalizia mafunzo yetu kuhusu hekaya hii, tutazame mfano mmoja kutoka Maandiko, unaohusu watu wawili kutoka Gerasi, waliokuwa na pepo.

Naye [Yesu] alipofika ng’ambo katika nchi ya Wagerasi, watu wawili wenye pepo walikutana naye, wanatoka makaburini, wakali mno, hata mtu asiweze kuipitia njia ile. Na tazama, wakapiga kelele wakisema, ‘Tuna nini nawe, Mwana wa Mungu? Je! Umekuja kututesa kabla ya muhula wetu?’ (Mathayo 8:28, 29. Maneno mepesi kukazia).

Mara nyingi habari hii hutumiwa na wale wenye kufundisha kwamba Shetani Alifaidika ili kuunga mkono mawazo yao. Wanasema hivi: “Unaona! Pepo walimwomba Yesu awatendee haki. Walijua hakuwa na haki ya kuwatesa kabla ya wakati wa kumalizika kwa haki ya umiliki nchi aliyokuwa nayo Adamu, yaani, wakati ambapo wao na Shetani wangetupwa katika ziwa la moto ili wateswe humo mchana na usiku hata milele.”

Ukweli ni tofauti kabisa. Wao walijua kwamba Yesu alikuwa na uwezo na haki zote kuwatesa wakati wowote aliotaka. Ndiyo sababu walimwomba awahurumie. Waliogopa san asana kwamba Mwana wa Mungu angewatuma wakateswe mapema zaidi. Luka anatuambia kwamba walimsihi “asiwaagize waende shimoni” (Luka 8:31). Kama Yesu hakuwa na haki hiyo kwa sababu ya haki fulani ambayo Shetani anadaiwa alikuwa nayo, wasingejali hata kidogo.

Hao pepo walitambua kwamba walikuwa wakitegemea rehema zsa Yesu kabisa, kama inavyo-onekana kwa wao kumwomba asiwatume nje ya nchi (Marko 5:10), na kumwomba awaruhusu kuwaingia kundi la nguruwe lililokuwepo (Marko 5:12), wao kumsihi wasitupwe “shimoni” (Luka 8:31), na kumwomba Kristo wasiteswe “kabla ya wakati”.

Tutazame hekaya nyingine inayoaminiwa sana, kuhusu Shetani.

Hekaya Ya Nne: “Shetani Kama ‘mungu wa dunia hii’ Anatawala Kila Kitu Duniani – Serikali Za Wanadamu, Majanga, Na Hali Ya Hewa.”

Katika Maandiko, Shetani anatajwa na mtume Paulo kwamba ni “mungu wa

dunia hii” (2Wakor. 4:4) na kuitwa na Yesu “mkuu wa dunia hii” (Yohana 12:31; 14:30; 16:11). Kutokana na majina haya ya Shetani, wengi wamedhani kwamba anatawala kikamilifu kabisa dunia. Japo tumekwisha tazama maandiko ya kutosha kuweka wazi kosa la hekaya hii, itatusaidia kujifunza zaidi ili tuwe na ufahamu kamili kuhusu jinsi ambavyo nguvu za Shetani zilivyo na mipaka. Ni lazima tuwe makini kwamba ufahamu wetu kuhusu Shetani usiwe umejengwa kwenye maandiko manne tu yenye kumtaja kwamba ni mungu, au mkuu wa dunia hii.

Tunapochunguza Biblia zaidi tunaona kwamba zaidi ya Yesu kumtaja Shetani kwamba ni “mkuu wa dunia hii” alimtaja Baba Yake wa mbinguni kwamba ni “Bwana wa mbingu na nchi” (Mathayo 11:25; Luka 10:21. Maneno mepesi kukazia). Tena, mtume Paulo hakumwita Shetani kuwa ni “mungu wa dunia hii” tu, bali pia aliongeza, kama Yesu, akamtaja Mungu kuwa ni “Bwana wa mbingu na nchi” (Matendo 17:24. Maneno mepesi kukazia). Hii hututhibitishia sisi kwamba Yesu wala Paulo hawataki tudhani kwamba Shetani ana mamlaka kamili juu ya nchi. Lazima mamlaka ya Shetani yawe na mipaka.

Tofauti muhimu sana kati ya maandiko hayo yanayotofautiana inapatikana katika maneno mawili: dunia na nchi. Japo tunayatumia kwa pamoja, katika Kiyunani hayo mawili hayafanani. Tukiisha elewa jinsi yanavyotofautiana, ufahamu wetu kuhusu mamlaka ya Mungu na ya Shetani hapa duniani yanaongezeka sana.

Yesu alimwita Mungu Baba kuwa ni Bwana wa nchi. Neno la Kiyunani linalotafsiriwa nchi ni ge. Hili linamaanisha sayari hii tunayoishi, na neno la Kiingereza geography (au, jiografia) limetokana nalo.

Kinyume chake, Yesu alisema kwamba Shetani ni mtawala wa dunia hii. Neno la Kiyunani linalotafsiriwa dunia ni kosmos, ambalo kikawaida husema juu ya mpango au utaratibu. Linazungumzia watu badala ya sayari yenyewe. Ndiyo sababu Wakristo mara nyingi wanasema juu ya Shetani kama “mungu anayetawala taratibu za dunia hii.”

Kwa sasa hivi, Mungu hana mamlaka yote juu ya dunia kwa sababu hajawatawala watu wote wa dunia. Sababu yake ni kwamba, amewapa watu wote uchaguzi kuhusu nani awe bwana katika maisha yao, na wengi wamechagua kumpa Shetani nafasi hiyo. Tusisahau kwamba hiari ya mwanadamu ni sehemu ya mpango wa Mungu.

Paulo alitumia neno tofuati la Kiyunani kusema juu ya dunia, alipoandika juu ya mungu wa dunia hii. Ni neno aion, ambalo mara nyingi hutafsiriwa kama kipindi, majira, nyakati, yaani, wakati maalum uliopangwa au kuwekwa. Shetani ni mungu wa kipindi au wakati huu wa sasa.

Nini basi maana ya yote hayo? Nchi ni sayari tunayokaa. Dunia ni watu ambao wanakaa kwa sasa duniani, n asana sana wale ambao hawamfuati Yesu. Wao wanamfuata Shetani, na wamenaswa katika utaratibu wake uliopotoka, wa dhambi. Sisi kama Wakristo tunasemekana “tupo duniani” lakini si “wa dunia” (Yohana 17:11, 14). Tunakaa miongoni mwa raia wa ufalme wa giza, lakini ukweli ni kwamba tuko katika ufalme wa nuru – ufalme wa Mungu.

Basi, sasa tunalo jibu. Kwa ufupi tu ni hivi: Mungu anatawala dunia nzima kimamlaka. Ila, kwa ruhusa ya Mungu, Shetani anatawala “taratibu za dunia” tu, yaani, anawatawala wale raia wa ufalme wake wa giza. Kwa sababu hii, mtume Yohana aliandika kwamba “dunia nzima (sio nchi nzima) iko katika nguvu za yule mwovu” (1Yohana 5:19).

Hii haimaanishi kwamba Mungu hana mamlaka juu ya dunia au mipangilio ya dunia, au watu katika dunia hii. Kama Danieli alivyosema, Yeye ni “anatawala katika falme za wanadamu, naye humpa yule amtakaye” (Danieli 4:25). Bado anaweza kumwinua au kumshusha mtu yeyote amtakaye. Ila, kama “mtawala” mkuu “juu ya falme za wanadamu” amemruhusu Shetani kuwatawala wanadamu wote walio kinyume Chake, yaani, waasi.

Tutazame Toleo La Shetani

Hii tofauti kati ya dunia na nchi itatusaidia pia kuelewa jaribu la Yesu pale nyikani. Huko, Shetani alimwonyesha Yesu “falme zote za dunia kwa dakika moja.” Shetani asingempa Yesu nafasi ya kisiasa juu ya serikali za wanadamu duniani – yaani, kitu tunachoita urais au uwaziri mkuu. Si Shetani anayewainua na kuwashusha wanadamu wakuu wa dunia – ni Mungu.

Badala yake – Shetani bila shaka alimwonyesha Yesu falme zote ndogo ndogo katika ufalme wake wa giza duniani kote. Alimwonyesha Yesu mpangilio wa utawala wa kipepo, ambao, katika maeneo yao, wanatawala juu ya ufalme wa giza, pamoja na wale binadamu waasi ambao ni raia wao. Shetani akampa Yesu mamlaka juu ya utawala wake – kama Yesu angejiunga na uasi wa Shetani dhidi ya Mungu. Hapo, Yesu angekuwa makamu wake katika ufalme wa giza.

Utawala Wa Mungu Juu Ya Serikali Za Binadamu, Duniani

Hebu tuonyeshe vizuri zaidi mipaka ya mamlaka ya Shetani kwa kutazama maandiko kwanza, yenye kuthibitisha mamlaka ya Mungu juu ya serikali za duniani za wanadamu. Shetani anayo mamlaka kiasi katika serikali za duniani za wanadamu kwa sababu ana mamlaka juu ya watu ambao hawajaokoka, na serikali mara nyingi hutawaliwa na watu ambao hawajaokoka. Lakini, Mungu ndiye mwenye mamlaka yote juu ya serikali za wanadamu, na Shetani anaweza kuzitumia kwa kiwango ambacho Mungu ataruhusu tu.

Tayari tumekwisha tazama maneno ya Danieli kwa mfalme Nebukadneza, lakini kwa sababu ni kitu kinachosaidia, hebu tuyatazame tena.

Mfalme mkuu Nebukadneza alikuwa ameinuka sana kwa kiburi kutokana na uwezo wake na mafanikio yake makubwa. Basi, Mungu akatangaza kwamba atashushwa mpaka chini kabisa ili aweze kujifunza kwamba “Aliye Juu anatawala katika falme za wanadamu, naye humpa yeyote amtakaye” (Danieli 4:17). Ni dhahiri kwamba Mungu ndiye anahusika na kupanda kwa Nebukadneza kufikia ukuu kisiasa. Ndivyo ilivyo kwa kila kiongozi wa kidunia. Mtume Paulo, akisema juu ya watawala wa duniani, alitangaza kwamba “kila mamlaka hutoka kwa Mungu, na zilizoko zimewekwa na Mungu” (Warumi 13:1).

Mungu ndiye mamlaka kuu katika ulimwengu wote. Kama kuna mwenye mamlaka mwingine, ni kwa sababu Mungu amempa kidogo, au amemruhusu mwingine kuwa nayo kidogo.

Vipi basi kuhusu watawala waovu? Je, Paulo anamaanisha kwamba hata wao wanawekwa na Mungu? Ndiyo. Mapema kidogo katika barua hiyo hiyo, Paulo aliandika hivi: “Kwa maana maandiko yasema juu ya Farao ya kwamba, ‘Nilikusimamisha kwa kusudi hili, ili nionyeshe nguvu zangu kwako, Jina langu likatangazwe katika nchi yote’.” (Warumi 9:17). Mungu alimwinua Farao – mwenye moyo mgumu – kwa kusudi la kujitukuza Mwenyewe. Mungu angeonyesha nguvu Zake kuu kupitia miujiza Yake ya ukombozi – nafasi iliyopatikana kwa kuwepo mtu jeuri ambaye Yeye Mwenyewe alimwinua.

Kwani, jambo hili haliko wazi katika mazungumzo ya Yesu na Pilato? Pilato, akishangazwa na jinsi ambavyo Yesu hakumjibu maswali yake, alisema hivi: “Mbona huzungumzi nami? Hujui kwamba nina mamlaka ya kukuachia huru, na mamlaka ya kukusulubisha?” (Yohana 19:10).

Yesu akamjibu hivi: “Wewe usingekuwa na mamlaka juu Yangu, kama usingepewa kutoka juu” (Yohana 19:11. Maneno mepesi kukazia). Akijua tabia ya Pilato ya uoga, Mungu alimwinua ili mpango Wake kwa Yesu kufa msalabani uweze kufanikiwa.

Ukisoma vitabu vya historia katika Agano la Kale kwa haraka haraka, utaona kwamba wakati mwingine Mungu huwatumia watawala wanadamu ambao ni waovu kama mawakala wa hasira Yake juu ya watu wanaostahili hukumu. Nebukadneza alitumiwa na Mungu kuleta hukumu Yake juu ya mataifa mengi katika Agano la Kale.

Ipo mifano mingi sana ya watawala ambao Mungu aliwainua au kuwashusha katika Biblia. Kwa mfano: Katika Agano Jipya tunasoma juu ya Herode ambaye hakumpa Mungu utukufu wakati baadhi ya raia wake walipopiga kelele mbele zake na kusema, “Hiyo ni sauti ya mungu, si ya mwanadamu!” (Matendo 12:22).

Ikawaje? “Mara, malaika wa Bwana akampiga … naye akaliwa na funza, akafa” (Matendo 12:23).

Kumbuka hivi: Herode alikuwa raia katika ufalme wa Shetani, lakini hakuwa nje ya mamlaka ya Mungu. Basi, Mungu anaweza kumwangusha kiongozi yeyote wa duniani hata sasa, kama akitaka.[5]

Ushuhuda Binafsi Wa Mungu

Kwa kumalizia, hebu tusome kile ambacho Mungu Mwenyewe aliwahi kusema kupitia nabii Yeremia, kwa habari ya enzi na ukuu Wake juu ya falme za wanadamu, hapa duniani.

Ee nyumba ya Israeli, je! Siwezi mimi kuwatendea ninyi vile vile kama mfinyanzi huyu alivyotenda? Asema Bwana. Angalieni, kama udongo ulvyo katika mkono wa mfinyanzi, ndivyo mlivyo ninyi katika mkono wangu, Ee nyumba ya Israeli. Wakati wowote nitakapotoa habari za taifa, na habari za ufalme, kuung’oa, na kuuvunja, na kuuangamiza; ikiwa taifa lile nililolitaja litageuka, na kuacha maovu yake, nitaghairi, nisitende mabaya yale niliyoazimia kuwatenda. Na wakati wowote nitakapotoa habari za taifa na habari za ufalme, kuujenga na kuupanda, ikiwa watatenda maovu mbele za macho yangu, wasiitii sauti yangu, basi nitaghairi, nisitende mema yale niliyoazimia kuwatendea (Yeremia 18:6-10).

Je, unaona sasa kwamba hakuna jinsi ambayo Shetani angeweza kumpa Yesu utawala halali juu ya falme za duniani za wanadamu za kisiasa, wakati alipokuwa anamjaribu pale nyikani? Kama alikuwa anamwambia kweli (kama ambavyo anafanya wakati mwingine), basi alichokuwa anampa Yesu ni utawala juu ya ufalme wake wa giza.

Lakini je, Shetani ana ushawishi katika serikali za wanadamu? Ndiyo, lakini ni kwa sababu yeye ndiye bwana wa kiroho juu ya watu ambao hawajaokoka, na watu ambao hawajaokoka wamo katika serikali za wanadamu. Ila, ana mamlaka kiasi cha ruhusa anayopewa na Mungu kuwa nayo, na Mungu anaweza kuvuruga mipango ya Shetani wakati wowote anaotaka. Mtume Yohana aliandika juu ya Yesu kwamba ni “mtawala wa wafalme wa dunia” (Ufunuo 1:5).

Je, Shetani Huleta Majanga Na Hali Mbaya Ya Hewa?

Kwa kuwa Shetani ni “mungu wa dunia hii,” wengi wamedhani kwamba

anatawala hali ya hewa, na ndiye mwenye kuleta majanga yote kama vile ukame, mafuriko, vimbunga, matetemeko, na kadhalika. Lakini je, hivyo ndivyo Maandiko yanavyotufundisha? Hapa tena inabidi tuwe makini kutokujenga itikadi yetu kuhusu Shetani kutokana na andiko moja tu linalosema hivi: “Mwivi haji isipokuwa aibe, kuua na kuharibu” (Yohana 10:10). Mara nyingi sana watu wametumia mstari huu kuthibitisha kwamba kila kitu kinachoiba, kuua au kuharibu hutoka kwa Shetani. Lakini, tukitazama Biblia zaidi tunajifunza kwamba Mungu Mwenyewe wakati mwingine huua na kuharibu. Hebu tazama mafungu haya matatu, kutoka katika mifano mingi tu iliyopo.

Mtoa sheria na mwenye kuhukumu ni mmoja tu, ndiye awezaye kuokoa na kuangamiza (Yakobo 4:12. Maneno mepesi kukazia).

Lakini nitawaonya mtakayemwogopa; mwogopeni yule ambaye akiisha kumwua mtu ana uweza wa kumtupa katika Jehanum; naam, nawaambia, Mwogopeni huyo! (Luka 12:5. Maneno mepesi kukazia).

Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum (Mathayo 10:28. Maneno mepesi kukazia).

Tukisema kwamba kila kitu kinachohusisha kuua au kuharibu ni kazi ya Shetani, tunakosea. Kuna mifano mingi sana ya Mungu kuua na kuharibu katika Biblia.

Tujiulize hivi: Wakati Mungu aliposema juu ya mwizi anayekuja kuua, kuiba na kuharibu, alikuwa anasema juu ya Shetani, au mwingine? Hapo tena, tunachohitaji ni kusoma maneno Yake katika mantiki yake. Mstari mmoja kabla hajasema aliyosema juu ya mwizi kuja kuiba, kuua na kuharibu, Yesu alisema hivi: “Wote walionitangulia ni wezi na wanyang’anyi, na kondoo hawakuwasikia” (Yohana 10:8). Tunaposoma maelezo yote ya Yesu katika Yohana 10:1-15 akisema Yeye ni Mchungaji mwema, inakuwa wazi zaidi kwamba maneno aliyotumia – mwizi na wezi – yanawahusu waalimu wa uongo na viongozi bandia wa dini.

Maoni Mbalimbali Kuhusu Hali Mbaya Ya Hewa Na Majanga

Kimbunga au tetemeko linapotokea, swali la kitheolojia hutokea katika akili za watu wanaomwamini Mungu. Ni hili: “Nani amesababisha hili?” Kwa Wakristo wanaoamini Biblia, ni mawili: Aidha ni Mungu, au ni Shetani.

Wengine wanaweza kupinga hivi: “Hapana! Mungu hahusiki! Watu ndiyo wanahusika. Mungu anawahukumu kwa ajili ya dhambi zao.”

Kama Mungu analeta kimbunga na matetemeko kwa sababu ya hukumu Yake juu ya dhambi, basi kweli tunaweza kuwalaumu binadamu waasi badala ya Mungu, lakini hata hivyo, Mungu bado anawajibika, kwa sababu majanga kama hayo yasingetokea bila ya agizo Lake.

Au kama ni kweli kwamba Mungu humruhusu Shetani kutuma vimbunga na matetemeko ili kuleta hukumu Yake juu ya wenye dhambi, basi tunaweza kusema ni Shetani anayesababisha, lakini bado Mungu anawajibika. Sababu ni kwamba, Yeye ndiye aliyemruhusu Shetani kusababisha uharibifu huo, na ni kwa sababu majanga hayo yanatokea kama itikio Lake kwa dhambi.

Kuna wanaosema si Mungu wala Shetani wanaohusika katika vimbunga na matetemeko, bali ni “matukio ya kawaida ya kiasili katika dunia yetu ya dhambi.” Hata hao wanajaribu kwa mbali kuweka lawama juu ya binadamu kwa majanga ya kiasili, lakini nao wanapotea. Maelezo hayo hayamwondoi Mungu katika picha. Kama vimbunga ni “tukio la kawaida kiasili katika dunia yetu ya dhambi”, nani aliyeamua iwe hivyo? Ni dhahiri kwamba vimbunga havitengenezwi na mwanadamu. Yaani, havitokei kwa sababu kiasi fulani cha uongo kimejaa katika anga. Matetemeko hayatokei wakati kiasi fulani cha watu wanapozini.

Hapana. Ni hivi: Kama kuna mahusiano kati ya kimbunga na dhambi, basi Mungu anahusika, kwa sababu vimbunga ni madhihirisho ya hukumu Yake juu ya dhambi. Hata kama vinatokea bila mpangilio, ni lazima iwe kwa amri ya Mungu, na kwa hali hiyo, anahusika.

Hata kama hakuna mahusiano yoyote kati ya dhambi na majanga, na iwe kwamba Mungu alikosa alipoitengeneza dunia na kusababisha udhaifu katika umbo la dunia mpaka kuna nyakati linasogea, na iwe kwamba taratibu za hali ya hewa mara kwa mara huondoka kwenye mpango, bado Mungu angebeba wajibu kwa ajili ya matetemeko na vimbunga, kwa sababu Yeye ndiye Mwumbaji, na makosa Yake yanawadhuru watu.

Hakuna Kitu Kinachoitwa “Asili Mama”

Basi, tuna majibu mawili yanayoweza kutolewa kuhusu swala la majanga. Aidha Mungu au Shetani wanahusika. Kabla hatujatazama Maandiko fulani ili kuamua jibu sahihi, hebu tufikiri zaidi majibu hayo mawili.

Kama Shetani ndiye mwenye kuleta majanga, basi Mungu anaweza au hawezi kumzuia. Kama Mungu anaweza kumzuia Shetani asilete majanga na hamzuii, basi hapo tena anawajibika. Janga lisingetokea bila ruhusa Yake.

Twende upande wa pili. Hebu tudhani kwamba Mungu hawezi kumzuia Shetani, lakini angetaka. Je, kitu kama hicho kipo?

Ikiwa Mungu hawezi kumzuia Shetani asilete janga, basi ni kwamba Shetani ana nguvu zaidi ya Mungu, au Shetani ni mjanja kuliko Mungu. Kimsingi, hicho ndicho kinachosemwa na wale wanaosema kwamba “Shetani alipata utawala wa dunia wakati Adamu alipoanguka.” Wanadai kwamba Shetani ana haki kisheria kufanya chochote anachotaka hapa duniani kwa sababu yeye aliiba hati miliki ya Adamu. Sasa – tuseme kwamba Mungu angependa kumzuia Shetani lakini hawezi kwa sababu inabidi aheshimu hati miliki ya Adamu ambaye sasa iko mikononi mwa Shetani. Maana yake ni kwamba, Mungu alikuwa mjinga kiasi cha kutoweza kuona mambo ambayo yangetokea wakati wa anguko la mwanadamu, lakini Shetani, kwa sababu ana akili kuliko Mungu, sasa amepata zile nguvu ambazo Mungu alitaka asiwe nazo. Haiwezekani kuwa hivyo. Shetani hana akili kuliko Mungu!

Kama nadharia kwamba “Shetani Alifaidika” ni ya kweli, tungetaka kujua ni kwa nini Shetani hasababishi matetemeko na vimbunga zaidi kuliko vlivyoko sasa, na kwa nini halengi idadi kubwa ya Wakristo. (Ukisema “ni kwa sababu Mungu ha tamruhusu alenge idadi kubwa ya Wakristo”, tayari umekubali kwamba Shetani hawezi kutenda chochote bila ruhusa ya Mungu.)

Tukifupisha mambo, majibu mawili tu yanayowezekana ni haya: Aidha (1) Mungu husababisha matetemeko na vimbunga, au (2) Shetani hufanya hivyo kwa ruhusa ya Mungu.

Ona hapo kwamba bila ya kujali jibu gani ni sahihi, Mungu bado ndiye mwenye kuwajibika? Watu wanaposema, “Mungu hakutuma kimbunga hicho – ni Shetani aliyefanya kwa ruhusa ya Mungu,” hawamwondolei Mungu wajibu kama wanavyodhani. Kama Mungu angeweza kumzuia Shetani asisababishe kimbunga, bila ya kujali kama alitaka au hakutaka, bado anawajibika. Binadamu waasi wanaweza kuwa wa kulaumiwa kwa sababu ya dhambi zao (ikiwa kimbunga kilitumwa na Mungu au kuruhusiwa na Mungu kama hukumu), lakini bado itakuwa upuuzi kusema Mungu hahusiki kwa njia yoyote ile, au hawajibiki.

Ushuhuda wa Maandiko

Je, Maandiko yanasema nini hasa kuhusu “majanga”? Je, Biblia inasema kwamba yanaletwa na Mungu au na Shetani? Tuanze kwa kutazama matetemeko kwa sababu Biblia inataja mengi.

Kulingana na Maandiko, matetemeko yanaweza kutokea kama hukumu ya Mungu juu ya wenye dhambi wanaostahili. Tunasoma hivi katika Yeremia: “Mbele ya ghadhabu yake [Mungu] nchi yatetemeka, wala mataifa hawawezi kustahimili hasira yake” (Yeremia 10:10. Maneno mepesi kukazia).

Isaya anatoa onyo lifuatalo:

Naye atajiliwa na BWANA wa majeshi kwa ngurumo, na tetemeko la nchi, na sauti kuu, na chamchela, na tufani, na mwali wa moto uteketezao (Isaya 29:6. Maneno mepesi kukazia).

Utakumbuka bila shaka katika siku za Musa kwamba nchi ilifunuka na kuwameza akina Kora na wafuasi wake waasi (ona Hesabu 16:23-34). Hili lilikuwa tendo la hukumu ya Mungu kabisa. Mifano mingine ya hukumu ya Mungu kwa matetemeko inapatkana katika Ezekieli 38:19; Zaburi 18:7; 77:18; Hagai 2:6; Luka 21:11; Ufunuo 6:12; 8:5; 11:13; 16:18.

Matetemeko mengine yanayotajwa katika Maandiko si matendo ya hukumu ya Mungu, ila yalisababishwa na Mungu. Kwa mfano: Kulingana na injili ya Mathayo, kulikuwa na tetemeko wakati Yesu alipokufa (Mathayo 27:51, 54) na lingine wakati alipofufuka (Mathayo 28:2). Je, Shetani alisababisha hayo?

Wakati Paulo na Sila walipokuwa wanaimba sifa kwa Mungu usiku wa manane katika gereza huko Filipi, “mara kukatokea tetemeko kubwa la nchi, misingi ya gereza ikatikiswa, na mara ile ile milango yote ikafunguliwa, na minyororo ya kila mmoja ikalegezwa” (Matendo 16:26. Maneno mepesi kukazia). Je, Shetani ndiye alisababisha tetemeko hilo? Hapana. Hata mkuu wa gereza aliokoka baada ya kuona nguvu za Mungu. Na hilo si tetemeko la pekee lililosababishwa na Mungu katika kitabu cha Matendo (ona Matendo 4:31).

Hivi karibuni nilisikia kuhusu Mkristo mwenye nia njema tu, ambaye, baada ya kusikia juu ya uwezekano wa kutokea kwa tetemeko katika sehemu fulani, alisafiri hadi hapo kwenda kufanya “vita ya kiroho” dhidi ya Shetani. Unaona kosa katika dhana hiyo? Ingekuwa sawa kimaandiko kwake kumwomba Mungu awarehemu hao watu walioishi katika eneo hilo. Na kama angefanya hivyo, asingekuwa na haja ya kupoteza muda wake na fedha kwenda kwenye eneo lenyewe – Mungu angeombwa pale pale nyumbani kwake. Ila, kufanya vita na Shetani ili kuzuia tetemeko si kitu kinachoungwa mkono na maandiko.

Vipi Kuhusu Vimbunga?

Neno kimbunga halipo katika Maandiko, lakini tunaweza kupata mifano ya upepo mkali. Kwa mfano:

Washukao baharini katika merikebu, wafanyao kazi yao katika maji mengi, hao huziona kazi za BWANA, na maajabu yake vilindini. Maana husema, akavumisha upepo wa dhoruba, ukayainua juu mawimbi yake (Zaburi 107:23-25. Maneno mepesi kukazia).

Lakini BWANA alituma upepo mkuu baharini, ikawa tufani kubwa baharini, hata merikebu ikawa karibu na kuvunjika (Yona 1:4. Maneno mepesi kukazia).

Baada ya hayo nikaona malaika wanne wamesimama katika pembe nne za nchi, wakizizuia pepo nne za nchi, upepo usivume juu ya nchi, wala juu ya bahari, wala juu ya mti wowote (Ufunuo 7:1).

Ni dhahiri kwamba Mungu anaweza kuanzisha dhoruba za upepo mkali, na kuzizuia.[6]

Katika Biblia nzima, kuna mstari mmoja tu unaotaja kwamba Shetani alituma upepo. Ni katika majaribu ya Ayubu. Mjumbe alimletea taarifa hivi: “Upepo mkali ulikuja kutoka nyikani, ukaipiga nyumba pande zote, nayo ikawaangukia vijana, nao wamekufa” (Ayubu 1:19).

Kutokana na kusoma sura ya kwanza ya kitabu cha Ayubu tunajua kwmaba Shetani ndiye aliyesababisha matatizo kwa Ayubu. Lakini, tusisahau kwamba asingeweza kufanya chochote kumdhuru Ayubu au watoto wake bila ya ruhusa ya Mungu. Basi, hapo tena tunaona kwamba Mungu anatawala upepo.

Tufani Ya Galilaya

Vipi kuhusu ile “tufani kali” iliyowavamia Yesu na wanafunzi Wake wakati fulani walipokuwa wanavuka Bahari ya Galilaya? Bila shaka ilisababishwa na Shetani, maana Mungu asingeweza kutuma upepo ambao ungepindua mtumbwi wenye Mwana Wake! “Ufalme ukifitinika juu yake wenyewe utaanguka.” Basi, kwa nini Mungu atume upepo ambao ungeweza kumdhuru Yesu na wanafunzi Wake kumi na wawili?

Hizo ni hoja nzuri, lakini hebu tufikiri kidogo. Kama Mungu hakutuma upepo, na iwe ni Shetani, basi lazima tukubali bado kwamba Mungu alimruhusu Shetani autume. Hivyo, swali lile lile bado linahitaji kujibiwa: Kwa nini Mungu amruhusu Shetani kutuma tufani ambayo ingeweza kumdhuru Yesu na wale kumi na wawili?

Je, kuna jibu? Pengine Mungu alikuwa anawafundisha wanafunzi kuhusu imani. Pengine alikuwa anawapima. Pengine alikuwa anampima Yesu, ambaye ilibidi “ajaribiwe katika mambo yote kama sisi, ila yeye hakutenda dhambi” (Waebrania 4:15). Ili aweze kujaribiwa kikamilifu, Yesu ilibidi apitie katika tukio la kumfanya ahofu. Pengine Mungu alitaka kumtukuza Yesu. Pengine alitaka kufanya hayo yote yaliyotajwa hapo juu.

Mungu aliwaongoza wana wa Israeli ukingoni mwa Bahari ya Shamu akijua kabisa kwamba walikuwa wamenaswa na jeshi la Farao lililowafuatia. Lakini je, hakuwa anawakomboa Waisraeli? Kama ndivyo, mbona alikuwa anajipinga kwa kuwaongoza kwenye sehemu ambapo wangeuawa kabisa? Je, huo si mfano wa “ufalme kufitinika juu yake wenyewe”?

Hapana kwa sababu, Mungu hakukusudia kuwaachia Waisraeli waangamizwe. Naye hakukusudia kuwaacha Yesu na wanafunzi Wake kuzama, wakati alipotuma au alipomruhusu Shetani kusababisha tufani katika Bahari ya Galilaya.

Pamoja na hayo – Biblia haisemi kwamba Shetani alituma tufani hiyo katika Bahari ya Galilaya, wala haisemi Mungu ndiye alituma. Kuna wanaosema kwamba ni Shetani kwa sababu Yesu aliikemea ikatulia. Sawa, lakini si hoja yenye nguvu. Yesu hakumkemea Mungu – Yeye alikemea upepo. Mungu Baba angeweza kufanya vivyo hivyo. Yaani, angeweza kusababisha tufani kwa neno, kisha akautuliza kwa kuukemea. Kwa kuwa Yesu alikemea tufani si uthibitisho kwamba Shetani ndiye aliyeileta.

Hapa tena tusijenge theolojia yetu juu ya mstari mmoja ambao hauthibitishi kitu chochote. Tayari tumetaja maandiko mengi yenye kuthibitisha kwamba Mungu ndiye anayetawala upepo, na mara nyingi inasemekana kwamba Yeye ndiye aliyeutuma. Hoja ni kwamba, Shetani, hata ingawa ndiye “mungu wa dunia hii,” hana mamlaka huru juu ya upepo, wala hana haki ya kusababisha tufani au kimbunga wakati wowote au mahali popote anapotaka.

Basi – wakati vimbunga vinapotokea, tusione kana kwamba ni kitu ambacho kiko nje ya uwezo wa Mungu – kitu ambacho angependa kukizuia lakini hawezi. Yesu alipokemea ule upepo na tufani katika Bahari ya Galilaya ni ushahidi tosha kwamba Mungu anaweza kusimamisha tufani akitaka.

Na kama Mungu anatuma (au anaruhusu) tufani, basi lazima awe na sababu fulani, na jibu linalofaa zaidi kwa habari ya kutuma au kuruhusu tufani yenye kuleta uharibifu mkubwa kabisa ni kwamba, anawaonya na kuwahukumu watu wasiotii.

“Lakini, Wakati Mwingine Vimbunga Hudhuru Wakristo”

Ila sasa – vipi kuhusu Wakristo ambao wanaathiriwa na majanga ya kawaida? Kimbunga kinapopiga mahali, hakibomoi nyumba za wasiokuwa Wakristo tu. Je, Wakristo hawaepushwi na ghadhabu ya Mungu kutokana na kifo cha Yesu kama dhabihu kwa ajili yao? Tunawezanje basi kusema kwamba Mungu ndiye anayehusika na majanga, wakati yanaweza kuwadhuru watoto Wake Mwenyewe?

Kwa kweli hayo ni maswali magumu. Ila, tunapaswa kutambua kwamba majibu yake hayatakuwa rahisi kama tutayajenga kwenye dhana potofu kwamba Shetani husababisha majanga. Kama Shetani anasababisha majanga yote, inakuwaje Mungu amruhusu kufanya mambo yatakayodhuru watoto wa Mungu Mwenyewe? Bado tatizo ni lile lile.

Lakini Biblia inasema wazi kabisa kwamba walio katika Kristo “si watoto wa ghadhabu” (1Wathes. 5:9). Pia, inasema kwamba “ghadhabu ya Mungu inawakalia” wale wasiomtii Yesu (Yohana 3:36). Sasa – ghadhabu ya Mungu inawezaje kukaa juu ya wasiookoka bila ya kuwaathiri walio-okoka, na huku wote wanaishi pamoja? Jibu ni kwamba, wakati mwingine haiwezekani, na huo ndiyo ukweli.

Siku zile za Waisraeli kutoka Misri, Waisraeli wote walikuwa wanakaa mahali pamoja, na mapigo ambayo Mungu alituma juu ya Wamisri kama hukumu hayakuwa-athiri (ona Kutoka 8:22, 23; 9:3-7; 24-26; 12:23). Lakini kwa habari yetu, tunaishi na kufanya kazi pamoja na “Wamisri”. Kama Mungu atawahukumu kwa njia ya janga, tutaepukaje?

Kuepuka ndiyo neno muhimu hapa, katika kuelewa jibu la swali letu. Ingawa Nuhu aliepuka ghadhabu ya Mungu wakati gharika ilipofunika dunia, bado aliathirika, maana ilimbidi afanye kazi kujenga safina, kisha alikaa mwaka mzima na wanyama wengi tu katika safina. (Tusisahau: Agano la Kale pamoja na Agano Jipya humtaja Mungu kuwa ndiye aliyeleta gharika ya Nuhu, si Shetani. Ona Mwanzo 6:17; 2Petro 2:5).

Lutu pia aliponya maisha yake wakati hukumu ya Mungu ilipokuja juu ya Sodoma na Gomora, lakini alipoteza kila kitu katika moto ulioshuka. Hukumu ya Mungu juu ya waovu ilimwathiri mtu mwenye haki.

Miaka ya baadaye tunaona Yesu akiwaonya waamini waliokuwa Yerusalemu kwamba wakimbie watakapoona mji wao umezungukwa na majeshi, maana hizo zitakuwa siku “za ghadhabu” (Luka 21:22, 23) – kuonyesha wazi kabisa makusudi ya ghadhabu ya Mungu kwa kuruhusu Warumi kuuzingira Yerusalemu mwaka wa 70 B.K. Sifa kwa Mungu kwa Wakristo waliojali maonyo ya Kristo, maana waliponya maisha yao, lakini bado walipoteza kila kitu walichotakiwa kuacha Yerusalemu.

Katika hiyo mifano yote mitato, tunaona kwamba watu wa Mungu wanaweza kuteseka kiasi fulani, wakati hukumu ya Mungu inaposhuka juu ya waovu. Basi, hatuwezi kuamua tu kwamba kwa kuwa wakati mwingine Wakristo huathirika na majanga, Mungu hahusiki kuyaleta.

Sasa – Tufanye Nini?

Tunaishi katika dunia iliyolaaniwa na Mungu – ambayo inakumbwa na ghadhabu ya Mungu wakati wote. Paulo aliandika hivi: “Ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa [ sio “itadhihirishwa”] kutoka mbinguni dhidi ya uovu wote na uasi wa wanadamu” (Warumi 1:18). Kama wanaoishi katika dunia ovu, iliyolaaniwa na Mungu, hatuwezi kuepuka kabisa matokeo ya ghadhabu ya Mungu juu yake, hata ingawa hiyo ghadhabu haielekezwi kwetu.

Tukijua hayo, tufanyeje? Kwanza: Tumwamini Mungu. Yeremia anaandika hivi:

Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea BWANA, ambaye BWANA ni tumaini lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, uenezao mizizi yake karibu na mto; hautaona hofu wakati wa hari ujapo, bali jani lake litakuwa bishi; wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, wala hautaaacha kuzaa matunda (Yeremia 17:7, 8).

Angalia – Yeremia hakusema kwamba mtu anayemtegemea Bwana hatakabiliwa na hari. Hapana. Wakati hari na mwaka wa uchache wa mvua vinapokuja, yule mtu anayemtegemea Bwana ni sawa na mti wenye kueneza mizizi yake pembeni ya kijito. Yeye anakuwa na mahali pengine pa kupatia, wakati dunia inayomzunguka inahangaika. Habari za Eliya kulishwa na kunguru wakati wa njaa huko Israeli ni mfano mmoja (ona 1Wafalme 17:1-6). Daudi aliandika hivi kuhusu wenye haki: “Katika siku za njaa watajazwa na vingi” (Zaburi 37:19).

Lakini – njaa haziletwi na Shetani? Hapana – Maandiko hayasemi hivyo. Kwenye hilo, Mungu anawajibika, na njaa mara nyingi husemwa kwamba ni matokeo ya ghadhabu Yake kwa watu wanaostahili. Kwa mfano:

Kwa sababu hiyo BWANA wa majeshi asema hivi, ‘Tazama, nitawaadhibu watu hawa; vijana watakufa kwa upanga; wana wao na binti zao watakufa kwa njaa’ (Yeremia 11:22. Maneno mepesi kukazia).

BWANA wa majeshi asema hivi, ‘Tazama, nitaleta juu yao upanga, na njaa, na tauni, nami nitawafanya kuwa kama tini mbovu zisizoweza kuliwa, kwa kuwa ni mbovu’ (Yeremia 29:17).

Mwanadamu! Nchi itakapofanya dhambi na kuniasi kwa kukosa, nikaunyosha mkono wangu juu yake na kulivunja tegemeo la chakula chake, na kuipelekea njaa, na kukatilia mbali mwanadamu na mnyama … (Ezekieli 14:13. Maneno mepesi kukazia).

Mlitazamia vingi, kumbe vikatokea vichache; tena mlipovileta nyumbani nikavipeperusha. Ni kwa sababu gani? Asema BWANA wa majeshi. Ni kwa sababu ya nyumba yangu inayokaa hali ya kuharibika, wakati ambapo ninyi mnakimbilia kila mtu nyumbani kwake. Basi, kwa ajili yenu mbingu zimezuiliwa zisitoe umande, nayo nchi imezuiliwa isitoe matunda yake. Nami nikaita wakati wa joto uje juu ya nchi, na juu ya milima, na juu ya nafaka, na juu ya divai mpya, na juu ya mafuta, na juu ya kila kitu itoacho nchi, na juu ya wanadamu, na juu ya wanyama, na juu ya kazi zote za mikono (Hagai 1:9-11. Maneno mepesi kukazia).

Katika mfano huu wa mwisho, tunasoma kwamba Waisraeli walilaumiwa kwa sababu ya ukame uliotokana na dhambi yao, lakini bado, Mungu anasema Yeye ndiye ameutuma.[7]

Mungu anapotuma njaa kwa watu waovu, nasi tuwe tunakaa katikati yao, tunachopaswa kufanya ni kuamini kwamba atatupa mahitaji yetu. Paulo alithibitisha kwamba njaa haiwezi kututenga na upendo wa Kristo! “Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je, ni dhiki, au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga?” (Warumi 8:35. Maneno mepesi kukazia). Ona kwamba Paulo hakusema Wakristo hawatakabiliwa na njaa kamwe. Anaonyesha kwamba wanaweza, japo yeye, kama mwanafunzi wa Maandiko, alijua kwmaba njaa inaweza kutumwa na Mungu kuwahukumu waovu.

Utii Na Hekima

Pili – Tunapaswa kuwa watii na kutumia hekima ya Mungu kuepuka kunaswa katika tukio lolote la ghadhabu ya Mungu linalolengwa duniani. Nuhu alijenga safina yake, Lutu alielekea vilimani, Wakristo wa Yerusalemu walitoroka mji wao; wote hao ilibidi kumtii Mungu ili kuepuka kunaswa katika hukumu Yake juu ya waovu.

Kama ningekuwa naishi katika eneo linalokumbwa na vimbunga, ningejenga nyumba yenye nguvu ambayo haiwezi kubomolewa, au nyumba ya bei rahisi ambayo ni rahisi kuijenga tena! Kisha, ningeomba. Kila Mkristo anapaswa kuomba na kuwa msikivu kwa Yule ambaye Yesu aliahidi kwamba “atawajulisha mambo yatakayokuja” (Yohana 16:13), ili aweze kuepuka ghadhabu ya Mungu juu ya dunia.

Tunasoma katika Matendo 11 kuhusu nabii Agabo ambaye alionya juu ya njaa kubwa ambayo ingewaathiri Wakristo waliokaa Uyahudi. Matokeo ni kwamba Paulo na Barnaba walianza kukusanya sadaka ili kuwasaidia (ona Matendo 11:28-30).

Je, mambo kama hayo yanaweza kutokea leo? Hakika, maana Roho Mtakatifu hajabadilika, wala upendo wa Mungu haujapungua. Ila, ni bahati mbaya sana kwamba baadhi ya watu katika mwili wa Kristo siku hizi hawako wazi kwa karama na madhihirisho ya aina hiyo ya Roho Mtakatifu, na kwa sababu hiyo, “wanamzimisha Roho” (1Wathes. 5:19) na kukosa mambo bora ya Mungu.

Katika kitabu kuhusu maisha yake, Marehemu Demos Shakarian, mkuu na mwanzilishi wa huduma ya Full Gospel Businessmen, anaeleza jinsi ambavyo Mungu alizungumza na Wakristo waliokaa nchi ya Armenia mwishoni mwa miaka ya 1800, kwa kupitia nabii mvulana aliyekuwa hajui kusoma wala kuandika. Aliwaonya juu ya mauaji makubwa yanayokuja, na matokeo ni kwamba, Wakristo Wapentekoste ambao waliamini mambo ya namna hiyo walikimbia nchi, pamoja na babu zake Shakarian. Muda mfupi baadaye, Waturuki walivamia Armenia, na WaArmenia zaidi ya milioni moja waliuawa, ikiwa ni pamoja na wale Wakristo waliokataa kusikia maonyo ya Mungu.

Tutakuwa na busara sana tukidumu kuwa wasikivu kwa Roho Mtakatifu na kumtii Mungu, la sivyo tutajikuta tunapitia katika ghadhabu ya Mungu ambayo Yeye hakutaka tuipitie. Kuna wakati Elisha alimwambia mwanamke mmoja hivi: “Ondoka, ukaende wewe na jamaa yako, ukae hali ya kigeni utakakoweza kukaa; kwa sababu BWANA ameiita njaa; nayo itakuja juu ya nchi hii muda wa miaka saba” (2Wafalme 8:1). Ingekuwaje kama huyo mwanamke angepuuzia ushauri wa nabii?

Tunasoma katika kitabu cha Ufunuo onyo la ajabu sana kwa watu wa Mungu, kwamba watoke “Babeli” wasije wakanaswa katika hukumu ya Mungu juu yake.

Kisha nikasikia sauti nyingine kutoka mbinguni ikisema, ‘Tokeni kwake [Babeli] enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake … Kwa sababu hiyo mapigo yake yatakuja katika siku moja, mauti na huzuni na njaa, naye atateketezwa kabisa kwa moto. Kwa maana Bwana Mungu aliyemhukumu ni mwenye nguvu (Ufunuo 18:4, 5, 8. Maneno mepesi kukazia).

Tunapohitimisha, tuseme hivi: Mungu ni mwenyezi – anatawala hali ya hewa na majanga. Amejithibitisha Mwenyewe kama Bwana juu ya nguvu za asili katika Biblia – kuanzia kusababisha mvua siku arobaini wakati wa Nuhu, hadi aliponyesha mvua yam awe pamoja na kutuma mapigo mengine juu ya adui za Israeli, hadi kusababisha kwake upepo mkali dhidi ya merikebu ya Yona, hadi kukemea Kwake ile tufani katika Bahari ya Galilaya. Kama Yesu alivyosema, Yeye ni “Bwana wa mbingu na nchi” (Mat hayo 11:25). Ukitaka ushahidi zaidi wa Maandiko kuhusu mamlaka na ukuu wa Mungu juu ya nguvu za asili, angalia katika Yoshua 10:11; Ayubu 38:22-38; Yeremia 5:24; 10:13; 31:35; Zaburi 78:45-49; 105:16; 107:33-37; 135:6, 7; 147:7, 8, 15-18; Mathayo 5:45; Matendo 14:17.

Majibu Kwa Maswali Machache

Kama Mungu anawahukumu watu kwa njia ya njaa, gharika na matetemeko, je, ni makosa kwetu sisi kama wawakilishi wa Mungu, kusaidia na kupunguza makali ya mateso ya wale watu ambao Mungu anawahukumu?

Hapana, kamwe. Tunapaswa kutambua kwamba Mungu anampenda kila mtu, pamoja na wale watu anaowahukumu. Japo litashangaza masikio yetu, hukumu Yake kwa njia ya majanga ni onyesho la upendo Wake. Inawezekanaje? Ni hivi: Kupitia matatizo na magumu ambayo yanaletwa na majanga, Mungu anawaonya watu anaowapenda kwamba Yeye ni mtakatifu na mwenye kuhukumu, na kwamba kuna malipo kwa ajili ya dhambi. Mungu anaruhusu mateso ya muda ili kuweza kuwasaidia watu waamke na kuona hitaji lao la Mwokozi – ili waepuke ziwa la moto. Huo ni upendo!

Muda wote ambapo watu wanapumua, Mungu bado anawaonyesha rehema wasiyostahili, na unakuwepo bado wakati wao kutubu. Kupitia huruma yetu na msaada, tunaweza kuonyesha upendo wa Mungu kwa watu wanaopitia ghadhabu Yake ya muda, lakini ambao wanaweza kuokoka na ghadhabu Yake ya milele. Majanga ni nafasi nzuri tu za kuwafikia watu wa dunia ambao Yesu aliwafia.

Je! Kitu muhimu kuliko vyote maishani si kuwafikishia watu ujumbe wa Injili? Tunapokuwa na mtazamo wa milele, mateso ya wale walionaswa katika majanga si kitu ukilinganisha na mateso ya wale watakaotupwa katika ziwa la moto.

Ni kweli pia kwamba watu huwa wasikivu kwa Injili wanapokuwa katika mateso. Kuna mifano mingi sana katika Biblia kuhusu ajabu hii, kuanzia toba ya Israeli wakati wa mateso kutoka kwa mataifa jirani, mpaka habari ya Yesu kuhusu mwana mpotevu. Wakristo wanapaswa kutazama majanga kama nyakati ambapo mavuno yamekwisha kuiva, tayari kuvunwa.

Hebu Tuseme Ukweli

Sasa – ujumbe wetu uweje, kwa watu wanaojaribu kurejelea hali ya kawaida kimaisha baada ya kimbunga au tetemeko? Tutawajibuje kama watataka jibu la kitheolojia kuhusu yaliyowapata? Hebu tuseme kweli inayofundishwa na Biblia, na kuwaambia watu kwamba Mungu ni mtakatifu na kwamba dhambi yao ina malipo. Tuwaambie kwamba ile kelele kubwa sana ya kimbunga ni mfano mdogo tu wa nguvu ambazo Mwenyezi Mungu anazo, na hofu waliyosikia wakati nyumba yao ilipotikiswa si kitu ukilinganisha na hofu itakayowashika watakapotupwa jehanamu. Na, tuwaambie kwamba, ingawa sisi sote tunastahili kutupwa jehanamu, Mungu anaturehemu na kutupa sisi muda wa kutubu na kumwamini Yesu, ambaye kwa njia Yake tutaokolewa na ghadhabu ya Mungu.

Wengine watasema, “Tusiwatishe watu kuhusu Mungu.” Jibu linatoka katika Maandiko, hivi: “Kumcha Bwana ni mwanzo wa maarifa” (Mithali 1:7). Watu wasipomcha (au kumwogopa, kumheshimu) Mungu, hawajui kitu chochote.

Itakuwaje Kama Watu Watamkasirikia Mungu?

Je, watu hawatamkasirikia Mungu kwa sababu ya mateso yao? Labda, lakini tunahitaji kuwasaidia waone kiburi chao, kwa upole. Hakuna mwenye haki ya kumlalamikia Mungu kwa mambo anayomtendea, kwa sababu sote tunastahili kutupwa katika ziwa la moto tangu zamani. Badala ya kumlaani Mungu kwa yanayowapata, watu wanatakiwa kumsifu kwa kuwapenda kiasi hicho, cha kuwaonya. Mungu ana kila haki ya kumpuuza kila mtu, na kuwaacha wote wafuate njia zao wenyewe kuelekea jehanamu. Lakini Mungu anawapenda watu, Naye anawaita kila siku. Anawaita kimya kimya kwa maua yanayochanua kwenye miti ya matunda, kwa nyimbo za ndege, kwa ukuu wa milima, na kwa kung’aa kwa nyota nyingi kila siku. Anawaita kupitia dhamiri zao, kupitia mwili Wake yaani Kanisa, na kwa njia ya Roho Mtakatifu. Lakini, wanapuuza mwito Wake.

Kwa hakika si mapenzi ya Mungu kwa watu kuteseka, lakini wanapoendelea kumpuuza, anawapenda kiasi cha kutosha kutumia njia zingine kali zaidi ili kuwafanya wamsikilize. Vimbunga, matetemeko, gharika, na njaa ni baadhi ya njia zingine kali. Mungu hutazamia kwamba majanga kama hayo yatashusha viburi vya watu na kuwafikisha mahali pa kuwa na akili ya kuelewa.

Je, Mungu Anakuwa Hajatenda Haki?

Tunapomtazama Mungu na dunia yetu kwa mtazamo wa KiBiblia, hapo ndipo tunapokuwa tukifanya sahihi. Mtazamo wa KiBiblia ni kwamba kila mtu anastahili ghadhabu ya Mungu, ila, Yeye ni mwenye rehema. Wakati watu wanaoteseka wanaposema kwamba wanatazamia kutendewa vizuri zaidi na Mungu kuliko inavyokuwa wakati huo, Mungu hujisikia vibaya. Ni kwamba kila mtu anapokea rehema nyingi zaidi sana kuliko anavyostahili.

Katika kufafanua zaidi jambo hili, Yesu wakati mmoja alisema kitu kuhusu majanga mawili yaliyotokea katika siku Zake. Tunasoma hivi katika Injili ya Luka:-

Na wakati uo huo walikuwapo watu waliompasha habari ya Wagalilaya wale ambao Pilato alichanganya damu yao na dhabihu zao. Akawajibu akawaambia, ‘Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? Nawaambia, Sivyo. Lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo. Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu? Nawaambia, Sivyo. Lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo’ (Luka 13:1-5).

Ni hivi: Wagalilaya waliokufa kwa mkono wa Pilato wasingeweza kusema, “Mungu hajatutendea haki, maana hajatuokoa na Pilato!” Hapana. Wao walikuwa wenye dhambi waliostahili kufa. Tena, kulingana na Yesu, wale Wagalilaya waliopona wangekosea sana kama wangefikia uamuzi kwamba wao hawana dhambi nyingi sana kama jirani zao waliouawa. Hawakuwa wamefanya kazi ili kupata upendeleo mkubwa kutoka kwa Mungu – ni kwamba walipewa rehema zaidi.

Ujumbe wa Kristo ulikuwa wazi kabisa: “Ninyi nyote ni wenye dhambi. Dhambi ina matokeo yake. Kwa sasa, mnaishi kutokana na rehema za Mungu. Basi, tubuni kabla muda haujawaishia na ninyi.”

Akamalizia maelezo Yake kuhusu majanga hayo kwa kutoa mfano juu ya rehema za Mungu, kama ifuatavyo:

Akanena mfano huu: Mtu mmoja alikuwa na mtini umepandwa katika shamba lake la mizabibu; akaenda akitafuta matunda juu yake, asipate. Akamwambia mtunzaji wa shamba la mizabibu, ‘Tazama, miaka mitatu hii naja nikitafuta matunda juu ya mtini huu, nisipate kitu. Uukate, mbona hata nchi unaiharibu?’ Akajibu akamwambia, ‘Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda baadaye, vema! La usipozaa, ndipo uukate’ (Luka 13:6-9).

Hapa, haki na rehema za Mungu vinaonekana. Haki ya Mungu inasema, “Ukate mti usio na faida!” Lakini rehema Zake zinasema, “Hapana! Upe muda zaidi wa kuzaa matunda.” Kila mtu asiye na Kristo ni kama mti huo.

Je, Tunaweza Kukemea Vimbunga Na Gharika?

Swali moja la mwisho kuhusu majanga. Hivi, tukiwa na imani ya kutosha, hatuwezi kukemea na kuzuia majanga kutokea?

Kuna na imani maana yake kuamini mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa. Basi, imani lazima ijengwe juu ya Neno la Mungu. Bila hivyo inakuwa si imani, bali ni tumaini au tarajio tu. Katika Biblia, hatupati mahali penye kutuahudi kwamba tunaweza kukemea na kutuliza vimbunga. Basi, hakuna jinsi mtu anavyoweza kuwa na imani ya kufanya hivyo (isipokuwa kama Mungu atampa imani hiyo kwa enzi Yake na mamlaka Yake).

Tufafanue zaidi. Njia ya pekee ya mtu kuwa na imani ya kukemea kimbunga ni kama ana uhakika kwamba Mungu hatai kimbunga hicho kipige eneo fulani. Kama tulivyojifunza katika Maandiko, Mungu ndiye mwenye kutawala upepo, Naye anahusika kabisa na vimbunga. Basi, ni kitu kisichowezekana kwa mtu kuwa na imani thabiti kwamba anaweza kuzuia kimbunga wakati Mungu Mwenyewe ameagiza kiwepo. Labda tofauti kwa hilo ni kama Mungu angebadilisha mpango Wake juu ya kimbunga hicho, ambayo inawezekana kama itikio Lake kuhusu maombi ya mtu kwamba awe na rehema, au itikio Lake kwa t oba ya watu wale ambao alikuwa anataka kuwahukumu (habari za Ninawi katika siku za Yona ni mfano rahisi). Lakini, hata kama Mungu angebadilisha mawzo Yake, bado si rahisi mtu awe na imani ya kukemea na kutuliza kimbunga bila mtu huyo kujua kwamba Mungu kabadilisha mawazo Yake na pia kwamba Mungu alitaka yeye akemee na kuzuia kimbunga hicho.

Mtu pekee aliyekemea na kuzuia upepo mkali alikuwa Yesu. Njia ya pekee kwetu sisi kufanya hivyo ni kama Mungu angetupa “karama ya imani” (au karama ya “imani maalum” kama inavyoitwa wakati mwingine), ambayo ni mojawapo katika zile karama tisa za Roho zinazotajwa katika 1Wakorintho 12:7-11. Sawa na karama zingine zote za kiroho, karama ya imani hutenda kazi kama Roho apendavyo, si kama sisi tupendavyo (ona 1Wakor. 12:11). Basi, Mungu asipokupa wewe imani maalum ya kukemea kimbunga kinachokuja, usisimame katika njia yake, ukijifanya kwamba unatenda hivyo kwa imani. Ondoka njiani – kipishe kabisa! Pia, omba ulinzi wa Mungu na umwombe awe na rehema kwa watu wale wanaohukumiwa, ukimwomba aponye maisha yao ili wapate muda zaidi wa kutubu.

Tazama: Wakati Paulo alipokuwa amefungwa kwenye merikebu kuelekea Rumi, na merikebu hiyo ikasukumwa na tufani kali baharini kwa majuma mawili, hakukemea ili bahari itulie (Matendo 27:14-44). Ni kwa sababu asingeweza. Ona pia kwamba Mungu aliwahurumia watu wote waliokuwa merikebuni, maana wote 276 waliokoka baada ya merikebu kuvunjika (ona Matendo 27:24, 34, 44). Ni dhahiri kwamba Mungu aliwahurumia kwa sababu Paulo alimwomba awahurumie.


[1] Hoja mbili pinzani zinajibiwa hivi: (1) Yuda anataja mashindano kati ya Mikaeli na Shetani juu ya mwili wa Musa, lakini hakuna vita inayotajwa. Tunachoambiwa na Yuda ni kwamba Mikaeli “hakuthubutu hata kumshtaki kwa kumlaumu [Shetani], bali alisema, ‘Bwana na akukemee’ “ (Yuda ms. 9). (2) Wakati Elisha na mtumishi wake walipozungukwa na jeshi la Shamu katika mji wa Dothani, Elisha alimwomba Mungu afungue macho ya mtumishi wake (2Wafalme 6:15-17). Basi, mtumishi wake akaona “farasi na magari ya moto” ambayo ni sawa tukisema yalikuwa yamepandwa na kuongozwa na jeshi la malaika katika ulimwengu wa roho. Lakini, huo si ushahidi kwamba walikuwa wamejiandaa kupambana na majeshi ya pepo. Wakati mwingine malaika hutumiwa na Mungu kutekeleza hasira Yake dhidi ya binadamu waovu, kama ilivyoandikwa katika 2Wafalme 19:35, ambapo malaika mmoja tu aliua askari 185,000 wa Ashuri.

[2] Baadhi ya mifano hiyo ni Mathayo 1:20; 2:13, 19; 4:11; Luka 1:11-20, 26-38.

[3] Fungu hili zima pia ni ushahidi kwamba Ayubu “hakumfungulia Shetani mlango kwa sababu ya hofu yake,” kitu kinachoaminiwa na wengine. Mungu Mwenyewe alimwambia Shetani hivi kuhusu Ayubu, katika 2:3 – “Naye [Ayubu] hata sasa anashikamana na utimilifu wake, ujapokuwa ulinichochea juu yake, ili nimwangamize pasipokuwa na sababu” (maneno mepesi kukazia).

[4] Ona pia 1Wakorintho 10:13, mahali panapo-onyesha kwamba Mungu huweka mipaka ya kujaribiwa kwetu. Hiyo inamaanisha kwamba humwekea mipaka mwenye kutujaribu pia!

[5] Je, maana yake ni kwamba tusiwaombee viongozi wa kiserikali, au tusipige kura kwa kuwa tunajua Mungu humwinua yeyote amtakaye kuwa juu yetu? Hapana. Katika demokrasia, hasira ya Mungu iko ndani kwa ndani. Tunampata tunayemchagua, na watu waovu kwa kawaida huchagua waovu wenzao. Kwa sababu hii, wenye haki wanapaswa kupiga kura. Tena, katika Agano la Kale na Jipya, tunashauriwa kuwaombea viongozi wetu wa kiserikali (Yeremia 29:7; 1Timo. 2:1-4). Maana yake ni kwamba tunaweza kumshawishi Mungu anapofanya maamuzi Yake juu ya nani atawale. Kwa kuwa hukumu ya Mungu wakati mwingine huja kwa kupitia viongozi waovu wa serikali, na kwa sababu mataifa mengi yanastahili hukumu hata hivyo, tunaweza kuomba na kupata reheme Zake, ili nchi yetu isipatikane na kila kitu inachostahili kupata.

[6] Maandiko mengine yenye kuthibitisha kwamba Mungu anatawala upepo ni haya: Mwanzo 8:11; Kutoka 10:13, 19; 14:21; 15:10; Hesabu 11:31; Zaburi 48:7; 78:76; 135:7; 147:18; 148:8; Isaya 11:15; 27:8; Yeremia 10:13; 51:16; Ezekieli 13:11, 13; Amosi 4:9, 13; Yona 4:8; Hagai 2:17. Katika hiyo mifano mingi, Mungu alitumia upepo kama kifaa cha kuhukumu.

[7] Ukitaka kusoma zaidi kuhusu Mungu kuleta njaa, angalia Kumbu. 32:23, 24; 2Samweli 21:1; 24:12, 13; 2Wafalme 8:1; Zaburi 105:16; Isaya 14:30; Yeremia 14:12, 15, 15; 16:3, 4; 24:10; 27:8; 34:17; 42:17; 44:12, 13; Ezekieli 5:12, 16, 17; 6:12; 12:16; 14:21; 36:29; Ufunuo 6:8; 18:8). Yesu Mwenyewe alisema kwamba Mungu “hunyesha mvua juu ya wenye haki na waovu” (Mathayo 5:45). Mungu anatawala mvua!

Unyakuo Wa Kanisa Na Nyakati Za Mwisho

Sura Ya Ishirini Na Tisa

 

Yesu alipotembea hapa duniani katika mwili wa mwanadamu, aliwaambia wanafunzi Wake waziwzi kabisa kwamba angeondoka kisha angerudi kuwachukua sikumoja. Wakati wa kurudi, angekwenda nao mbinguni. Kitu hiki siku hizi kinatiwa “Unyakuo.” Kwa mfano: Usiku ule kabla hajasulubiwa, Yesu aliwaambia hivi mitume Wake waaminifu kumi na moja:

Msifadhaike mioyoni mwenu. Mnamwamini Mungu, niaminini na mimi. Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi. Kama sivyo, ningaliwaambia, maana naenda kuwaandalia mahali. Basi, mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo. (Yohana 14:1-3. Maneno mepesi kukazia).

Kilicho wazi katika maneno ya Yesu ni uwezekano wa kurudi Kwake wakati wale mitume wakiwa bado hai. Ukweli ni kwamba, baada ya kusikia maneno ya Yesu, wangeweza kudhani tu kwamba atarudi kuwachukua wakiwa bado hai.

Tena, Yesu aliwaonya wanafunzi Wake mara nyingi sana kwamba wawe tayari kwa ajili ya kurudi Kwake. Hapo tena, uwezekano wa Yeye kurudi wakiwa hai ulikuwepo (ona mfano katika Mathayo 24:42-44).

Kurudi Kwa Yesu Upesi Katika Nyaraka

Mitume walioandika zile barua za Agano Jipya walithibitisha imani yao kwamba Yesu angeweza kurudi wakati wa maisha ya wasomaji wa barua zao. Kwa mfano: Yakobo aliandika hivi:

Kwa hiyo ndugu, vumilieni hata kuja kwake Bwana. Tazama, mkulima hungoja mazao ya nchi yaliyo ya thamani. Huvumilia kwa ajili yake hata yatakapopata mvua ya kwanza na ya mwisho. Nanyi vumilieni, mthibitishe mioyo yenu, kwa maana kuja kwake Bwana kunakaribia (Yakobo 5:7, 8. Maneno mepesi kukazia).

Yakobo asingekuwa na haja ya kuwashauri wasomaji wake kuvumilia kuhusu kitu ambacho kisingetokea maishani mwao. Yeye aliamini kwamba kuja kwa Bwana “kunakaribia.” Kimantiki, Yakobo aliandika barua yake wakati kanisa lilipokuwa linapitia mateso makali (ona Yakobo 1:2-4), wakati ambapo waamini wangetamani sana kurudi kwa Bwana wao.

Paulo vile vile aliamini kwamba Yesu angeweza kurudi wakati wa maisha ya wenzake. Anaandika hivi:

Lakini ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini. Maana ikiwa twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye. Kwa kuwa twaambieni haya kwa neno la Bwana, kwamba sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti. Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele. Basi farijianeni kwa maneno hayo (1Wathes. 4:13-18. Maneno mepesi kukazia).[1]

Kutokana na hayo tunajifunza pia kwamba wakati Yesu atakaporudi kutoka mbinguni, miili ya waamini waliokufa itafufuliwa, kisha, pamoja na waamini walio hai wakati wa kuja Kwake, “kunyakuliwa ili kumlaki Bwana hewani” (Unyakuo). Kwa kuwa Paulo naye alitaja kwamba Yesu angewaleta wale waliokufa “ndani Yake” kutoka mbinguni, tunachoweza kusema ni kwamba wakati wa Unyakuo, roho za waamini walioko mbinguni zitaunganishwa na miili yao iliyofufuliwa punde tu.

Petro naye aliamini kwamba kuja kwa Kristo kulikuwa karibu sana, alipoandika barua yake ya kwanza kabisa.

Kwa hiyo vifungeni viuno vya nia zenu na kuwa na kiasi; mkiitumainia kwa utimilifu ile neema mtakayoletewa katika ufunuo wake Yesu Kristo. …Lakini mwisho wa mambo yote umekaribia, basi iweni na akili, mkeshe katika sala. … Lakini kama mnavyoyashiriki mateso ya Kristo, furahini; ili na katika ufunuo wa utukufu wake mfurahi kwa shangwe (1Petro 1:13; 4:7, 13. Maneno mepesi kukazia).[2]

Na Yohana naye, alipoandika barua zake kwa makanisa, aliamini kwamba mwisho ulikuwa karibu, na kwamba wasomaji wa siku zake wangeona kurudi kwa Yesu.

Watoto, ni wakati wa mwisho; na kama vile mlivyosikia kwamba mpinga Kristo yuaja, hata sasa wapinga Kristo wengi wamekwisha kuwapo. Kwa sababu hiyo twajua ya kuwa ni wakati wa mwisho. … Na sasa watoto wadogo, kaeni ndani yake, ili kusudi atakapofunuliwa, mwe na ujasiri, wala msiaibike mbele zake katika kuja kwake. … Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo. Na kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu (1Yohana 2:18, 28; 3:2, 3. Maneno mepesi kukazia).

Kukawia Kwake

Tukitazama nyuma miaka elfu mbili, tunatambua kwamba Yesu hakurudi mapema kama mitume Wake walivyotazamia. Hata katika siku zao, kuna waliokuwa wameanza kuwa na mashaka kama Yesu angerudi, kutokana na muda ulivyokuwa umepita tangu aondoke. Kwa mfano: Maisha ya Petro hapa duniani yalipokaribia kumalizika (ona 2Petro 1:13, 14), Yesu alikuwa hajarudi bado. Basi, Petro aliwaandikia waliokuwa na mawazo ya mashaka hivi, katika barua yake ya mwisho:

Mkijua kwanza neno hili ya kwamba katika sikuza mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, na kusema, ‘Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? Kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.’ Maana hufumba macho yao wasione neno hili yakuwa zilikuwako mbingu tangu zamani, na nchi pia imefanyizwa kutoka katika maji, na ndani ya maji kwa neno la Mungu. Kwa hayo dunia ile ya wakati ule ioligharikishwa na maji, ikaangamia. Lakini mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu. Lakini wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa Bwana siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja. Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu yeyote apotee, bali wote wafikilie toba. Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea” (2Petro 3:3-10).

Petro anathibitisha kwamba kukawia kurudi kwa Yesu ni kwa sababu ya upendo na rehema na huruma Zake – anataka kutoa nafasi zaidi watu watubu. Lakini anasema pia kwamba hakuna mashaka yoyote – Yesu atarudi. Na atakaporudi, atakuja akiwa na ghadhabu kubwa.

Vile vile Maandiko yako wazi kabisa – kama tutakavyo-ona – kwamba kurudi kwa Kristo kwa ghadhabu kutatanguliwa na miaka ya dhiki isiyo na kifani ya dunia nzima, na kumwagwa kwa hasira ya Mungu juu ya waovu. Sehemu kubwa ya Kitabu cha Ufunuo inasema kuhusu kipindi hicho kinachokuja. Kama tutakavyoona baadaye katika mafunzo yetu, Maandiko yanaonyesha kwamba itakuwepo miaka saba ya dhiki, hapo baadaye. Hakuna shaka yoyote kwamba Unyakuo wa kanisa utafanyika wakati fulani katika hiyo miaka saba, au karibu na hiyo miaka saba.

Je, Unyakuo Ni Lini Hasa?

Swali ambalo mara nyingi linawagawa Wakristo ni wakati hasa wa Unyakuo. Kuna wanaosema kwamba Unyakuo utatokea kabla ya ile miaka saba ya dhiki. Kwa maana hiyo, unaweza kutokea wakati wowote. Wengine wanasema utatokea katikati ya ile miaka saba ya dhiki. Na wengine tena wanasema utatokea punde tu baada ya dhiki ya miaka saba kufika katikati. Na kuna wengine nao wanaosema kwamba Unyakuo utatokea wakati wa Yesu kurudi na ghadhabu nyingi, mwishoni mwa kipindi cha Dhiki.

Hilo si swala la kugawanyikia, na makundi yote manne yanapaswa kukumbuka kwamba yote yanakubali kwamba Unyakuo utatokea wakati fulani katika kipindi hicho cha baadaye cha dhiki ya miaka saba, au karibu nacho. Hilo ni dirisha dogo sana katika upana wa miaka maelfu ya historia. Hivyo, badala ya kugawanyika kutokana na kutokubaliana kwetu, ni afadhali tufurahie makubaliano yetu! Tena, si kitu tunaamini nini maana haitabadilisha kitakachotokea.

Baada ya kusema hayo, sina budi kusema kwamba, kwa miaka ishirini na mitano ya kwanza katika maisha yangu ya Kikristo, niliamini kwamba Unyakuo utatokea kabla ya Dhiki ile ya miaka saba. Niliamini hivyo kwa sababu ndivyo nilivyofundishwa, na pia kwa sababu sikutaka kupitia mambo ninayosoma habari zake katika Kitabu cha Ufunuo! Ila, nilipoendelea kujifunza Maandiko, nilianza kupata mtazamo tofauti. Hebu kwa pamoja tutazame Biblia inavyosema, na tuone tutafikia maamuzi gani. Hata kama sitafanikiwa kukushawishi ujiunge na upande wangu, hebu tuendelee kupendana!

Mafundisho Pale Mlima Wa Mizeituni

Hebu tuanze kwa kutazama sura ya 24 ya Injili ya Mathayo, sehemu ya Maandiko ambayo ni ya msingi sana kwa habari ya matukio ya nyakati za mwisho na kurudi kwa Yesu. Pamoja na sura ya 25, sehemu hiyo huitwa Mafundisho Pale Mlima Wa Mizeituni, kwa sababu sura hizo mbili ni taarifa ya mahubiri ambayo Yesu alitoa kwa baadhi ya wanafunzi Wake wa karibu sana[3] hapo mlimani. Tunaposoma mafundisho hayo, tutajifunza kuhusu matukio mengi ya nyakati za mwisho, nasi tutaona uwezekano wa wanafunzi wa Yesu kufikiri muda wa Unyakuo ni upi, waliposikia mafundisho yenyewe.

Yesu akaenda zake, akatoka hekaluni. Wanafunzi wake wakamwendea ili kumwonyesha majengo ya hekalu. Naye akajibu akawaambia, ‘Hamyaoni haya yote? Amin nawaambieni, halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa.’Hata alipokuwa ameketi katika mlima wa Mizeituni, wanafunzi wake wakamwendea kwa faragha wakisema, ‘Tuambie! Mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini dalili ya kuja kwako, na ya mwisho wa dunia?’ (Mathayo 24:1-3).

Wanafunzi wa Yesu walitaka kujua habari za wakati ujao. Sana sana walitaka kujua majengo ya hekalu yangebomolewa lini (kama Yesu alivyokuwa ametabiri) na ishara gani ingeonyesha wakati wa kurudi Kwake na mwisho wa wakati.

Ukilitazama hivyo, tunajua kwamba majengo ya hekalu yalibomolewa kabisa mwaka wa 70 B.K. na jemadari Tito, akiongoza majeshi ya Kirumi. Pia tunajua kwamba Yesu bado hajarudi kujichukulia kanisa Lake, kwa hiyo, hayo matukio mawili hayafuatani, wala hayatokei wakati mmoja.

Yesu Ajibu Maswali Yao

Inaonekana kwamba Mathayo hakuandika jibu la Yesu ka swali la kwanza, kuhusu kuharibiwa kwa majengo ya hekalu baadaye. Ila, Luka alifanya hivyo katika Injili yake (ona Luka 21:12-24). Katika Injili ya Mathayo, Yesu alianza moja kwa moja kuzungumza kuhusu ishara ambazo zingetangulia kurudi Kwake mwisho wa wakati.

Yesu akajibu akawaambia, ‘Angalieni mtu asiwadanganye [ninyi]. Kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu wakisema, Mimi ni Kristo; nao watadanganya wengi. Nanyi mtasikia habari za vita na matetesi ya vita; angalieni [ninyi] msitishwe; maana hayo hayana budi kutukia; lakini ule mwisho bado. Kwa maana taifa litaondoka kupigana na taifal na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na njaa na matetemeko ya nchi mahali mahali. Hayo yote ndiyo mwanzo wa utungu.’ (Mathayo 24:4-8. Maneno mepesi kukazia).

Kutokana na jinsi mahubiri hayo yalivyoanza, ni dhahiri kwamba Yesu aliamini kwamba hao wanafunzi Wake wa karne ya kwanza wangekuwa hai wakati ishara hizo zinazotangulia kurudi Kwake zinapotendeka. Ona anasema nao moja kwa moja, kibinafsi. Katika sura hii ya 24, Yesu anasema na wanafunzi Wkae moja kw amoja zaidi ya mara ishirini. Basi, wasikilizaji Wake wote wangeamini kwamba wataishi na kuona hayo yote ambayo Yesu ametabiri.

Lakini ni kweli kwamba wanafunzi wote waliomsikiliza Yesu siku hiyo wamekufa siku nyingi sana. Ila, tusidhani kwamba Yesu alikuwa anawadanganya. Yeye Mwenyewe hakujua wakati atakaporudi (ona Mathayo 24:36). Kweli ilikuwa inawezekana kwa wale waliosikiliza mafundisho Yake pale Mlima wa Mizeituni kuwa hai wakati wa kurudi Kwake.

Kilichokuwa cha msingi kabisa kwa Yesu ni kwamba wanafunzi Wake wasidanganywe na makristo wa uongo, kama itakavyokuwa katika siku za mwisho. Tunajua kwamba Mpinga Kristo mwenyewe atakuwa kristo wa uongo, na atadanganya dunia kwa sehemu kubwa. Watuw atamhesabu kuwa mwokozi mzuri sana.

Yesu alisema zitakuwepo vita, njaa na matetemeko, lakini pia alionyesha kwamba hayo matukio si ishara za kurudi Kwake bali ni “mwanzo wa utungu” tu. Ni salama kusema kwamba matukio hayo yamekuwepo kwa miaka zaidi ya elfu mbili iliyopita. Ila, anachosema Yesu baada ya hapo ni kitu ambacho hakijatokea.

Dhiki Inaaza Katika Dunia Nzima

Wakati huo watawasaliti ninyi mpate dhiki, nao watawaua; nanyi mtakuwa watu wa kuchukuwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu. Ndipo wengi watakapojikwaa, nao watasalitiana na kuchukiana. Na manabii wengi wa uongo watatokea, na kudanganya wengi. Na kwa sababu ya kuongezeka maasi, upendo wa wengi utapoa. Lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka. Tena habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja (Mathayo 24:9-14. Maneno mepesi kukazia).

Hapa tena – kama ungewauliza wale waliomsikiliza Yesu siku hiyo swali hili: “Je, mnatazamia kuwa hai ili kuona kutimia kwa mambo hayo?” bila shaka wangejibu ndiyo kwa uhakika sana, maana Yesu alisema nao moja kwa moja.

Kama tulivyosoma – mara tu baada ya “utungu” kuna tukio ambalo kweli halijatokea, la wakati wa Wakristo duniani kote kuteswa. Tutachukiwa na “mataifa yote”. Yesu alikuwa anazungumza juu ya wakati fulani ambapo hayo yangetokea – si kipindi cha jumla cha miaka mia nyingi, maana alisema hivi baada ya hayo, “Ndipo wengi watakapojikwaa,nao watasalitiana na kuchukiana.”

Bila shaka anachosema hapo kinahusu kurudi nyuma kwa waamini Wakristo ambao baada ya hapo watawachukia waamini wengine, maana wasioamini hawawezi “kuanguka,” tena, wanachukiana tayari. Basi, mateso ya dunia nzima yatakapoanza, kutakuwa na kurudi nyuma kwa watu wengi wanaodai kwamba ni wafuasi wa Kristo. Kama ni wakweli au ni waamini bandia – yaani kondoo au mbuzi – wengi sana wataanguka, nao watafichua majina ya waamini wengine kwa watesaji, wakiwachukia wale waliodai kuwapenda. Matokeo ni kwamba kanisa duniani kote litasafishwa.

Halafu tena kutakuwa na ongezeko la manabii wa uongo, na mmoja anatajwa sana katika kitabu cha Ufunuo kuwa mwenzake mpinga Kristo (ona Ufunuo 13:11-18; 19:20; 20:10). Maasi yataongezeka na kufikia mahali pa kumaliza kabisa upendo kidogo utakaokuwa umesalia mioyoni mwa watu, na wenye dhambi watakuwa wabaya kukithiri.

Wafia Dini Na Watakaosalia

Ingawa Yesu alitabiri kwamba waamini watapoteza maisha yao (ktk 24:9), si wote, maana aliahidi kwamba wale watakaovumilia mpaka mwisho wataokolewa (ona 24:13). Yaani, kama hawataruhusu wadanganywe na wale makristo wa uongo au manabii wa uongo, na kama watashinda jaribu la kuacha imani yao na kuanguka, wao wataokolewa na Kristo wakati anaporudi ili kuwakusanya mawinguni. Huu wakati wa dhiki baadaye pamoja na ukombozi wake ulifunuliwa kidogo kwa nabii Danieli pia. Yeye aliambiwa hivi

Na kutakuwa wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo; na watu wako wataokolewa; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile. Tena, wengi wa hao walalao katika mavumbi ya nchi wataamka, wengine wapate uzima wa milele, wengine aibu na kudharauliwa milele (Danieli 12:1, 2).

Wokovu bado utatolewa kwa neema hata katika siku hizo, maana Yesu aliahidi kwamba Injili itahubiriwa kwa mataifa yote, kutoa nafasi moja ya mwisho ya kutubu, ndipo mwisho utakapokuja.[4] Tunasoma kitu katika Kitabu cha Ufunuo ambacho kinaweza kuwa kutimizwa kwa ahadi ya Yesu.

Kisha nikaona malaika mwingine akiruka katikati ya mbingu, mwenye Injli ya milele, awahubiri hao wakaao juu ya nchi, na kila taifa na kabila na lugha na jamaa. Akasema kwa sauti kuu, ‘Mcheni Mungu na kumtukuza, kwa maana saa ya hukumu yake imekuja. Msujudieni yeye aliyezifanya mbingu na nchi na bahari na chemchemi za maji’. (Ufunuo 14:6, 7. Maneno mepesi kukazia).

Kuna wanaodhani kwamba sababu ya malaika kuhubiri Injili wakati huo ni kwamba, kufikia hapo katika kipindi cha dhiki ya miaka saba, Unyakuo utakuwa umetokea na waamini wote watakuwa wameondoka. Lakini, hayo ni mawazo tu.

Mpinga Kristo

Nabii Danieli alifunua kwamba mpingakristo atakuwa na nafasi katika hekalu la Yerusalemu litakalojengwa upya, katikati ya ile miaka saba ya dhiki, na kujitangaza kwamba ni Mungu (ona Danieli 9:27 – tutajifunza baadaye). Tukio hili ndilo Yesu anazungumzia alipoendelea kufundisha pale Mlima wa Mizeituni, kama ifuatavyo:

Basi, hapo mtakapoliona chukizo la uharibifu, lile lililonenwa na nabii Danieli, limesimama katika patakatifu (asomaye na afahamu), ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani; naye aliye juu ya dari asishuke kuvichukua vitu vilivyomo nyumbani mwake; wala aliye shambani asirudi nyuma kuchukua nguo yake. Ole wao wenye mimba na wanyonyeshao siku hizo! Ombeni ili kukimbia kwenu kusiwe wakati wa baridi, wala siku ya sabato. Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.[5] Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu yeyote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo (Mathayo 24:15-22).

Hayo ni maelezo yaliyo dhahiri zaidi kuhusu dhiki ambayo Yesu alizungumzia mapema (ktk 24:9). Wakati mpingakristo atakapotangaza kwamba yeye ni Mungu kutoka hekalu la Yerusalemu, mateso yasiyofikirika yatatokea dhidi ya wanaomwamini Yesu. Kwa kujitangaza kwamba yeye ni Mungu, mpingakristo atatazamia kilamtu kutambua uungu wake. Basi, wafuasi wote wa kweli wa Kristo watakuwa maadui wa taifa, watu wa kusakwa na kuuawa. Ndiyo sababu Yesu aliwaambia waamini wa Uyahudi wakimbilie milimani bila kukawia, wakiomba kwamba kutoroka kwao kusizuiwe na sababu yoyote ile.

Wazo langu ni kwamba ingekuwa vizuri kwa waamini wote duniani kukimbilia maeneo yaliyofichika wakati huo, maana tukio hilo litatangazwa duniani kote kwa njia ya televisheni. Maandiko yanatuambia kwamba dunia nzima itadanganywa na mpingakristo na kudhani yeye ndiye Kristo wao, nao watampa mamlaka na heshima zote. Atakapojitangaza kwamba ni Mungu, watamwamini na kumwabudu. Atakaponena makufuru dhidi ya Mungu wa kweli – Mungu wa Wakristo – atashawishi dunia yote iliyodanganyika ili kuwachukia wale wanaokataa kumwabudu (ona Ufunuo 13:1-8).

Yesu aliahidi ukombozi kwa ajili ya watu Wake mwenyewe kwa “kukatisha” hizo siku za dhiki, vinginevyo, “asingeokoka mtu yeyote” (24:22). Huko “kukatizwa” siku hizo Naye “kwa ajili ya wateule” bila shaka ni kitu kinachohusu Yeye kuwakomboa wakati atakapoonekana na kuwakusanya mawinguni. Yesu hata hivyo hatuambii hapa kwamba ukombozi huo utatokea muda gani baada ya mpingakristo kujitangazia uungu.

Vyovyote vile – tunarudia kusema hapa tena kwamba Yesu aliwaacha wasikilizaji Wake siku hiyo wakiwa wanajua kwamba wangeishi na kumwona mpingakristo akitangaza uungu wake, na kupigana vita na Wakristo. Hili linapingana kabisa na wazo la wale wanaosemakwamba waamini watanyakuliwa kabla ya tukio hilo. Kama ungemwuliza Petro, Yakobo au hata Yohana kwamba Yesu angerudi kuwaokoa kabla ya tamko la mpingakristo kwamba ni Mungu, wangekujibu, “Si hivyo”.

Vita Dhidi Ya Watakatifu

Katika sehemu zingine, Maandiko yanatabiri juu ya mateso ya mpingakristo kwa waamini. Kwa mfano: Yohana alifunuliwa, naye akaandika hivi katika kitabu cha Ufunuo:

Naye [mpingakristo] akapewa kinywa cha kunena maneno makuu, ya makufuru. Akapewa uwezo wa kufanya kazi yake miezi arobaini na miwili. Akafunua kinywa chake amtukane Mungu, na kulitukana jina lake, na maskani yake, nao wakaao mbinguni. Tena akapewa kufanya vita na watakatifu na kuwashinda, akapewa uwezo juu ya kila kabila na jamaa na lugha na taifa (Ufunuo 13:5-7. Maneno mepesi kukazia).

Ona hapo kwamba mpingakristo atapewa “uwezo wa kufanya kazi yake” kwa miezi arobaini na mbili, au, miaka mitatu na nusu kamili. Huu ndiyo wakati unaoitwa nusu ya wakati wa kipindi cha Dhiki ya miaka saba. Ni sawa kabisa kufikiri kwamba ni ile miezi arobaini na mbili ya mwisho ya Dhiki, ndipo mpingakristo atakapopewa “uwezo wa kufanya kazi yake,” kwa sababu mamlaka yake yataondolewa kabisa wakati Kristo atakaporudi kufanya vita naye na majeshi yake wakati wa kumalizika kwa Dhiki.

Ni dhahiri kwamba “uwezo wak ufanya kzi yake” kwa miezi arobaini na mbili maan ayake ni mamlaka maalum, maana mpingakristo atapewa mamlaka kiasi fulani na Mungu katika wakati wake wa kumiliki. Haya “mamlaka maalum ya kufanya kazi” yanaweza kuwa ni muda atakaopewa wa kuwashinda watakatifu, maana, tunasoma hivi katika kitabu cha Danieli:

Nikatazama, na pembe iyo hiyo [mpingakristo] ilifanya vita na watakatifu, ikawashinda; hata akaja huyo mzee wa siku [Mungu], nao watakatifu wake Aliye Juu wakapewa hukumu; na majira yakawadia watakatifu waumiliki ufalme. … Naye [mpingakristo] atanena maneno kinyume chake Aliye Juu, naye atawadhoofisha watakatifu wake Aliye Juu; naye ataazimu kubadili majira na sheria; nao watatiwa mikononi mwake kwa wakati, na nyakati mbili, na nusu wakati (Danieli 7:21, 22; 25. Maneno mepesi kukazia).

Danieli alitabiri kwamba watakatifu wangetiwa mikononi mwa mpingakristo kwa “wakati, nyakati, na nusu wakati.” Maneno hayo yaeleweke kwamba ni miaka mitatu na nusu, kama utafananisha na Ufunuo 12:6 na 14. Tunaambiwa katika Ufunuo 12:6 kwamba mwanamke fulani ambaye ni mfano, atapewa mahali pa kujificha nyikani ili “atunzwe na kulishwa” huko kwa muda wa siku 1,260, ambazo ni sawa na miaka mitatu na nusu kwa mwaka wenye siku 360. Kisha, mistari nane baadaye, anatajwa tena, na wakati huo inasemekana atapewa mahali nyikani ili “atunzwe na kulishwa” kwa “wakati, nyakati, na nusu ya wakati.” Basi, “wakati, nyakati, na nusu ya wakati” ni sawa na zile siku 1,260, au miaka mitatu na nusu.

Kumbe katika mantiki hii, neno “wakati” maana yake mwaka, na “nyakati” maana yake miaka miwili, na “nusu ya wakati” maana yake nusu mwaka. Lugha hii ya ajabu inayopatikana katika Ufunuo 12:14 bila shaka ina maana kama katika Danieli 7:21. Basi, sasa tunajua kamba watakatifu watatiwa mikononi mwa mpingakristo kwa miaka mitatu na nusu, ambao ndiyo muwa ule ule tunaoambiwa katika Ufunuo 13:5 kwamba mpingakristo atapewa “uwezo wa kufanya kazi yake.”

Mimi nadhani vipindi hivyo viwili vya miezi arobaini na mbili vinafanana. Kama vitaanza wakati wa mpingakristo kujitangaza kwamba ni Mungu katikati ya ile Dhiki ya miaka saba, basi ni kwamba watakatifu watatiwa mikononi mwake kwa miaka mitatu na nusu inayofuata, na Yesu atawakomboa atakapotokea mawinguni na kuwakusanya waende Naye wakati huo, au karibu na mwisho wa hiyo Dhiki. Lakini, kama hiyo miezi arobaini na mbili inaanza wakati mwingine katika kipindi cha Dhiki ya miaka saba, basi inatubidi tukubali kwamba Unyakuo utatokea wakati fulani kabla ya mwisho wa Dhiki ya miaka saba.

Tatizo la hoja hiyo ya mwisho ni kwamba inabidi watakatifu watiwe mikononi mwa mpingakristo kabla ya kuingia hatarini na kuhitaji kukimbilia milimani wakati anapojitangaza kuwa Mungu. Hilo ni gumu.

Tatizo la hoja ile ya kwanza ni kwamba watakatifu watakuwepo duniani bado wakati Mungu atakapokuwa anamimina hukumu duniani, tunazosoma katika kitabu cha Ufunuo. Tutatazama ugumu huo baadaye. Tuendelee na Mafundisho ya Mlima wa Mizeituni.

Masiya Wa Uongo

Ndipo Yesu akafafanua zaidi kwa wanafunzi Wake umuhimu wa kutodanganywa na habari kuhusu maKristo wa uongo.

Wakati huo mtu akiwaambia, ‘Tazama, Kristo yupo hapa, au yuko kule msisadiki. Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu, wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio wateule. Tazama, nimekwisha kuwaonya mbele. Basi wakiwaambia, Yuko jangwani, msitoke; yumo nyumbani, msisadiki. Kwa maana kama vile umeme utokavyo mashariki ukaonekana hata magharibi, hivyo ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. Kwa kuwa popote ulipo mzoga, ndipo watakapokusanyika tai (Mathayo 24:23-28).

Ona tena hapa jinsi Yesu anavyosema na wanafunzi moja kwa moja. Wasikilizaji Wake pale Mlima wa Mizeituni wangetazamia kuishi mpaka waone kutokea kwa makristo wa uongo na manabii wa uongo ambao wangetenda miujiza mikubwa. Na bila shaka wangetazamia kumwona Yesu akirudi mawinguni kama umeme.

Hatari ya kurudi nyuma wakati huo itakuwa kubwa sana, maana mateso dhidi ya waamini yatakuwa makali mno na makristo wa uongo na manabii wa uongo watashawishi watu sana kutokana na miujiza yao. Hii ndiyo sababu Yesu anarudia tena na tena kuwaonya wanafunzi Wake kuhusu yatakayotokea muda mfupi tu kabla ya kurudi Kwake. Hakutaka wao wapotoshwe kama itakavyokuwa kwa wengi. Waamini wa kweli na walio thabiti watamngoja Yesu arudi mawinguni kama umeme, ambapo wale wasiokuwa wafuasi Wake kweli watavutwa kwa makristo hao wa uongo kama tai wanavyovutiwa na mzoga nyikani.

Ishara Mawinguni

Yesu akaendelea hivi:

Lakini mara baada ya dhiki ya siku zile, jua litatiwa giza, na mwezi hautatoa mwanga wake, na nyota zitaanguka mbinguni, na nguvu za mbinguni zitatikisika, ndipo itakapoonekana ishara yake Mwana wa Adamu mbinguni; ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza, nao watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi. Naye atawatuma malaika zake pamoja na sauti kuu ya parapanda, nao watawakusanya wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho huu (Mathayo 24:29-31).

Mifano au picha katika sehemu hii ya mafundisho ya Yesu pale Mlima wa Mizeituni bila shaka ingekuwa inafahamika na Wayahudi wa siku Zake, maana inatoka katika Isaya na Yoeli, na inazungumzia hukumu ya mwisho ya Mungu, mwisho wa dunia. Mara nyingi huitwa “siku ya Bwana”, wakati jua na mwzi vitatiwa giza (ona Isaya 13:10, 11; Yoeli 2:31). Ndipo wakazi wote wa dunia watakapomwona Yesu akirudi mawinguni katika utukufu Wake, nao wataomboleza. Kisha malaika wa Yesu “watawakusanya wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho huu,” kuonyesha kwamba waamini watanyakuliwa na kukusanywa ili kumlaki Yesu mawinguni, na hayo yote yatatokea baada ya mlio wa “baragumu”.

Hapa tena, kama ungemwuliza Petro, Yakobo au Yohana ikiwa Yesu angewarudia kabla au baada ya wakati wa mpingakristo na dhiki kuu, bila shaka wangesema, “Baada.”

Kurudi Kwake, Na Unyakuo

Hii sehemu ya Mafundisho ya pale Mlima wa Mizeituni inaeleweka sana, kulingana na tukio ambalo Paulo aliandika juu yake, ambalo bila shaka ni Unyakuo wa kanisa, ingawa waandishi wengi wa vitabu vya kufafanua Biblia wanasema linatokea kabla ya kipindi cha Dhiki kuanza. Hebu tazama andiko lifuatalo, tulilotazama mwanzoni mwa sura hii.

Lakini ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini. Maana, ikiwa twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika yesu, Mungu atawaleta pamoja naye. Kwa kuwa twawaambieni haya kwa neno la Bwana, kwamba sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti. Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko,na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tuli hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele. Basi, farijianeni kwa maneno hayo. Lakini ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie. Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku. Wakati wasemapo, Kuna amani n salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa (1Wathes. 4:13 – 5:3. Maneno mepesi kukazia).

Paulo aliandika juu ya Yesu kuja kutoka mbinguni kwa parapanda ya Mungu na kwamba waamini watanyakuliwa “mawinguni ili kumlaki Bwana hewani.” Ni sawa kabisa na yale Yesu aliyokuwa akieleza katika Mathayo 24:30, 31 – yanayotokea baada ya kutokea kwa mpingakristo na dhiki.

Tena, Paulo alipoendelea kuandika kuhusu kurudi kwa Kristo, anataja kwamba ingetokea lini – “majira na nyakati” – na kuwakumbusha wasomaji wake kwamba walikuwa wanafahamu vizuri sana kwmaba “siku ya Bwana ingekuja kama mwivi anavyokuja usiku.” Paulo aliamini kwamba kurudi kwa Kristo na Unyakuo wa waaminio ungetokea “siku ya Bwana,” siku ambapo hasira kali na maangamizi vingewapata wale waliokuwa wanatazamia “amani na salama.” Kristo anaporudi kulinyakua kanisa Lake, hasira Yake itashuka juu ya dunia.

Hili linakubaliana vizuri sana na kile ambacho Paulo aliandika katika barua kwa Wathesalonike baadaye, kuhusu kurudi kwa Kristo na hasira Yake.

Kwa kuwa ni haki mbele za Mungu kuwalipa mateso wale wawatesao ninyi; na kuwalipa ninyi mteswao raha pamoja na sisi; wakati wa kufunuliwa kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake katika mwali wa moto; huku akiwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu,na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu; watakaoadhibiwa kwa maagamizi ya milele, kutengwa na uso wa Bwana na utukufu wa nguvu zake; yeye atakapokuja ili kutukuzwa katika watakaifu wake, na kustaajabiwa katika wote waliosadiki katika siku ile, (kwa sababu ushuhuda wetu ulisadikiwa kwenu). (2Wathes. 1:6-10. Maneno mepesi kukazia)

Paulo alisema kwamba wakati ambao Yesu angerudi kuwapa nafuu Wathesalonike waliokuwa wanateswa (ona 1Wathes. 1:4, 5), angetokea “pamoja na malaika wake katika mwali wa moto” ili kuwaadhibu wale waliokuwa wanawatesa wao, kutoa hukumu ya haki, inayostahili. Hii haifanani na kile kinachosemwa na wengi, kwamba Unyakuo utatokea kabla ya dhiki, na kanisa kunyakuliwa na Kristo kabla ya kile kipindi cha dhiki cha miaka saba kuanza. Hii pia huitwa kuja kwa siri kwa Yesu ili kunyakua kanisa Lake. Hapana kabisa! Maelezo haya yanafanana na kile ambacho Yesu alieleza katika Mathayo 24:30, 31 – kurudi Kwake karibu au mwishoni mwa kipindi cha dhiki kuu – anapowanyakua waaminio na kumimina hasira Yake juu ya wasoiamini.

Siku Ya Bwana

Baadaye, katika barua hiyo hiyo, Paulo aliandika hivi:

Basi ndugu, tunakusihini, kwa habari ya kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo, na kukusanyika kwetu mbele zake, kwamba msifadhaishwe upesi hata kuiacha nia yenu, wala msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno, wala kwa waraka unaodhaniwa kuwa ni wetu, kana kwamba siku ya Bwana imekwisha kuwapo (2Wathes. 2:1, 2).

Kwanza: Ona kwamba mada ya Paulo ni kurudi kwa Kristo na Unyakuo. Aliandika kuhusu “kukusanyika kwetu mbele zake,” akitumia maneno yale yale ambayo Yesu alitumia katika Mathayo 24:31, alipozungumza juu ya malaika ambao “wangekusanya” wateule Wake “kutoka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho ule.”

Pili: Ona kwamba Paulo anayaita matukio hayo kuwa ni “siku ya Bwana,” sawa na alivyofanya katika 1Wathesalonike 4:13 hadi 5:2. Hilo liko wazi kabisa.

Kisha anaendelea hivi:

Mtu awaye yote asiwadanganye kwa njia yoyote; maana haiji, usipokuja kwanza ule ukengeufu; akafunuliwa yule mtu wa kuasi, mwana wa uharibifu; yule mpingamizi, ajiinuaye nafsi yake juu ya kila kiitwacho Mungu ama kuabudiwa; hata yeye mwenyewe kuketi katika hekalu la Mungu, akijionyesha nafsi yake kana kwamba yeye ndiye Mungu (2Wathes. 2:3, 4. Maneno mepesi kukazia).

Wakristo Wathesalonike walikuwa wanadanganywa kwa namna fulani kwamba siku ya bwana – ambayo kulingana na Paulo lazima ianze kwa Unyakuo na kurudi kwa Kristo – ilikuwa imekwisha fika. Akatamka wazi wazi kwamba haiji mpaka baada ya ule ukengeufu (labda ndiyo kule kurudi nyuma ambako Yesu alizungumzia katika Mathayo 24:10) na baada ya mpingakristo kujitangaza kwamba ni Mungu kutoka hekalu la Yerusalemu. Basi, Paulo anawaambia waamini Wathesalonike wazi wazi kwamba wasitazamie kurudi kwa Kristo – au Unyakuo – wala siku ya Bwana, mpaka baada ya tamko la mpingakristo kwamba ni Mungu.[6]

Kisha, Paulo anaelezea kuhusu kurudi kwa Kristo na jinsi anavyomwangamiza kabisa mpingakristo.

Je, hamkumbuki ya kuwa wakati nilipokuwapo pamoja nanyi naliwaambieni hayo? Na sasa lizuialo mwalijua, yule apate kufunuliwa wakati wake. Maana ile siri ya kuasi hivi sasa inatenda kazi; lakini yuko azuiaye sasa, hata atakapoondolewa. Hapo ndipo atakapofunuliwa yule asi, ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, na kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake; yule ambaye kuja kwake ni kwa mfano wa kutenda kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za uongo; na katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa (2Wathes. 2:5-10).

Paulo alitamka kwamba mpingakristo atakomeshwa “kwa ufunuo wa kuja Kwake” Kristo. Kama “ufunuo” Wake ni sawa na ule unaotajwa wakati wa Unyakuo – kiasi cha mistari tisa nyuma (ktk 2:1), basi mpingakristo atauawa wakati huo huo ambapo Kanisa litakusanywa ili kumlaki Bwana hewani. Hii inalingana na taarifa itolewayo katika Ufunuo sura ya 19 na 20. Hapo tunasoma juu ya kurudi kwa Kristo (ona Ufunuo 19:11-16), kuangamizwa kwa mpingakristo na majeshi yake (ona 19:17-21), kufungwa kwa Shetani (ona 20:1-3) na “ufufuo wa kwanza” (ona 20:4-6), ambapo waamini waliouawa katika kipindi cha Dhiki yamiaka saba watafufuliwa. Kama huu ndiyo ufufuo wa kwanza kweli kweli kwa maana ya jumla kwamba ni kwa ajili ya wenye haki, basi hakuna mashaka kwamba Unyakuo na kurudi kwa Kristo katika hasira Yake kunatokea wakati huo huo ambapo mpingakristo anaharibiwa, maana, Maandiko yanatuambia wazi kabisa kwamba wote waliokufa katika Kristo watafufuliwa wakati wa Unyakuo (ona 1Wathes. 4:15-17).[7]

Kuwa Tayari

Hebu turudi tena kwenye Mafundisho pale Mlima wa Mizeituni.

Basi kwa mtini jifunzeni mfano. Tawi lake likiisha kuchipuka na kuchanua majani, mwatambua ya kuwa wakati wa mavuno u karibu. Nanyi kadhalika, myaonapo hayo yote, tambueni ya kuwa yu karibu, milangoni. Amin nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.[8] Mbingu na nchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe (Mathayo 24:32-35).

Yesu hakutaka wanafunzi Wake wanaswe bila kufahamu – na hilo ndilo jambo la msingi katika Mafundisho ya pale Mlima wa Mizeituni. Wangejua kwamba “yuko malangoni” baada ya kuona “mambo hayo yote” – dhiki duniani kote, kurudi nyuma kwa watu, kutokea kwa manabii na makristo wa uongo, tangazo la mpingakristo kwamba ni Mungu, na kutiwa giza jua na mwezi pamoja na kuanguka kwa nyota, wakati karibu na kurudi Kwake.

Ila, baada tu ya kuwaambia kuhusu ishara zitakazotangulia kuja Kwake kwa miaka michache, au miezi au siku, aliwaambia sasa wakati hasa wa kurudi Kwake ungebakia kuwa siri.

Walakini kwa habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake (Mathayo 24:36).

Mara nyingi andiko hili linatajwa kinyume cha mantiki yake! Kwa kawaida linatajwa ili kuunga mkono dhana kwamba hatuna habari Yesu atarudi lini, kwa sababu anaweza kurudi wakati wowote na kunyakua kanisa. Lakini katika mantiki yake, Yesu hakumaanisha hicho. Alikuwa ndiyo kamaliza kuhakikisha kwamba wanafunzi Wake wangekuwa tayari kwa ajili ya kurudi Kwake kwa kuwaambia ishara nyingi ambazo zingetokea muda mfupi tu kabla ya kurudi Kwake. Sasa anachowaambia ni kwamba, siku hasa na saa havitafunuliwa kwao. Tena, Yesu hasemi juu ya kuja Kwake mara ya kwanza kabla ya kipindi cha Dhiki ya miaka saba kuanza, wakati ambapo kanisa lingenyakuliwa, bali kuhusu kurudi Kwake wakati wa mwisho au karibia mwisho wa Dhiki. Hilo halina matatizo ukitazama mantiki vizuri.

Je, Kurudi Kwake Hakujulikani Kabisa?

Hoja ambayo mara nyingi hutumika dhidi ya Unyakuo kutokea karibu au wakati wa mwisho wa Dhiki ni kwamba kurudi kwa namna hiyo kusingekuwa kitu kisichojulikana kama Yesu alivyodaiwa kusema, kwa sababu kurudi kwa namna hiyo kungetazamiwa kwa matukio ya Dhiki. Lazima kuwe na Unyakuo kabla ya dhiki, la sivyo waamini wasingehitaji kuwa tayari na kukaa macho kama Maandiko yasemavyo wanapaswa kuwa, maana watajua ni miaka saba au zaidi kabla ya Yesu kurudi.

Ila, hoja hii inapingwa na ukweli kwamba lengo kuu la Mafundisho ya Yesu pale Mlima wa Mizeituni lilikuwa ni kuhakikisha kwamba wanafunzi Wake wawe tayari kwa ajili ya kurudi Kwake wakati au karibu na mwisho wa Dhiki, naye aliwafunulia ishara nyingi tu ambazo zingetangulia kuja Kwake. Mbona Mafundisho ya Mlimani yamejaa mashauri mengi sana kwamba watu wawe tayari na kuwa macho, ingawa Yesu alijua kwamba kurudi Kwake kuko mbele miaka mingi sana baada ya kusema maneno hayo? Bila shaka ni kwa sababu Yesu aliamini kwamba Wakristo wanahitaji kuwa tayari na kuwa macho hata ingawa kurudi Kwake bado kuko miaka mingi mbele. Mitume ambao katika barua zao waliwashauri waamini kuwa macho na kuwa tayari kwa ajili ya kurudi kwa Yesu walikuwa wanamwiga Yesu Mwenyewe.

Tena, wale wanaoamini kwamba Unyakuo kabla ya dhiki ndiyo wenye kuhalalisha mashauri yoyote ya kuwa tayari, wana tatizo lingine. Kulingana na mawazo yao, kurudi kwa Yesu mara ya kwanza hutangulia dhiki kwa miaka saba. Kwa hiyo, kurudi kwa Yesu mara ya kwanza kulingana na hoja zao hakuwezi kutokea wakati wowote – lazima itakuwa ni miaka saba kabla ya Dhiki kuanza. Basi, hakuna haja ya kutazamia kwamba Yesu atarudi mpaka matukio duniani yakamilike na kuwa tayari kuanza miaka saba ya Dhiki. Matukio hayo yanaweza kutazamiwa na kuhakikishwa kabisa.

Wengi wenye kuamini Unyakuo kabla ya dhiki – kama ni wakweli – watasema kwamba wanajua Yesu hatarudi leo wala kesho kwa sababu ya hali ya kisiasa duniani. Bado yapo matukio yaliyotabiriwa ambayo hayana budi kutimizwa kabla ya ile miaka saba ya Dhiki kuanza. Kwa mfano: Kama tutakavyoona katika kitabu cha Danieli, mpingakristo atafanya agano na Israeli kwa miaka saba, na huo utakuwa ndiyo mwanzo wa kipindi cha Dhiki. Hivyo basi, kama Unyakuo unatokea miaka saba kabla ya dhiki kuanza, lazima utokee wakati mpingakristo atakapofanya agano lake la miaka saba na Israeli. Basi, hakuna haja ya wale wanaoshikilia kwamba Unyakuo utafanyika kabla ya Dhiki kutazamia Yesu atarudi kabla ya kuona kitu katika siasa kinachofanya hayo yawezekane.

Zaidi ya hayo – kwa wale wanaoamini kwamba Unyakuo utatokea kabla ya dhiki, na kuamini kwamba Yesu atarudi mwishoni mwa Dhiki pia, maana yake ni kwamba siku kamili ya kurudi kwa Yesu mara ya pili inaweza kujulikana kimahesabu. Mara tu Unyakuo utokeapo, mtu yeyote angeweza kukadiria na kujua kile ambacho Yesu alisema ni Baba tu akijuacho. Unachofanya ni kuhesabu mbele miaka saba tu.

Tuseme tena hivi – Kutokana na yale ambayo Yesu alisema, Yeye hakutaka kurudi Kwake kuwe kitu cha kuwashtua watu. Ukweli ni kwamba alitaka kurudi Kwake kutazamiwe, na hivyo akataja matukio kadhaa ya Dhiki. Yesu hakutaka wanafunzi Wake wakutwe hawako tayari, kama ambavyo dunia itakutwa. Basi anaendelea kusema hivi katika Mafundisho Yake pale Mlima wa Mizeituni:

Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. Kwa kuwa kama vile siku zile ziliozkuwa kabla ya gharika watu walivyokuwa wakila na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. Wakati ule watu wawili watakuwako kondeni; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa. Wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa.[9] Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu. Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa. Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja (Mathayo 24:37-44).

Hapa tena, kitu ambacho Yesu anajali ni kwamba wanafunzi Wake wawe tayari kwa ajili ya kurudi Kwake. Hicho ndicho kilisababisha yote aliyosema kabla ya hapa na baada ya hapa, katika mafundisho Yake. Maonyo Yake mwengi kwamba wawe tayari na wakeshe si kwamba ni kwa kuwa kurudi Kwake kutakuwa kwa kushtukiza, bali ni ishara ya jinsi ambavyo itakuwa vigumu kwa sababu ya upinzani wa wakati wenyewe, kuendelea kuwa macho na kuwa tayari. Basi, wale wanaotarajia Unyakuo kabla ya Dhiki, wakati wowote, wanaodhani kwamba wako tayari kuliko Wakristo wengine, wanaweza wasiwe tayari kwa uhalisi kabisa, kwa kile kinachokuja. Kama hawatazamii dhiki yoyote na wajikute katikati ya mateso ya dunia nzima, wakati wa utawala wa mpingakristo, jaribu la kuanguka linaweza kuwazidi nguvu. Afadhali kuwa tayari kwa kile kinachofundishwa na Maandiko kwamba kitatokea.

Halafu tena – kama ungemwuliza Petro, Yakobo au Yohana kwamba walitazamia kumwona lini Yesu akirudi, wangekwambia kuhusu ishara hizo zote ambzo Yesu aliwaambia zingetokea, kabla ya kurudi Kwake. Wasingetazamia kumwona kabla ya kipindi cha dhiki, au kutokea kwa mpingakristo.

Mwivi Usiku

Ona kwamba hata mfano wa Yesu wa “mwivi usiku” uko katika mantiki ya Yeye kudhihirisha ishara nyingi ambazo zingewasaidia wanafunzi Wake wasinaswe ghafula kwa kurudi Kwake. Basi, mfano huo hauwezi kutumiwa kisahihi kuonyesha kwamba hakuna mtu anayeweza kuwa na wazo lolote kuhusu Yesu anarudi lini.

Paulo na Petro walitumia mfano wa Yesu wa “mwivi usiku” walipokuwa wanaandika kuhusu “siku ya Bwana” (ona 1Wathes. 5:2-4; 2Petro 3:10). Waliamini huo mfano ulikuwa na maana kwa habari ya Yesu kurudi kwa ghadhabu wakati wa au mwisho wa Dhiki ya miaka saba. Ila, Paulo aliwaambia hivi wasomaji wake: “Bali ninyi, ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi” (1Wathes. 5:4). Yeye alitafsiri kwa usahihi mfano wa Yesu, akitambua kwamba wale walio macho na makini kuona zile ishara, na wenye kumfuata Yesu kwa utiifu, hawakuwa gizani mpaka kuja kwa Kristo kuwapate kwa ghafula. Kwa watu namna hiyo, Yesu asingekuja kama mwivi usiku. Ni wale walio gizani tu ndiyo wangeshtushwa – na ndivyo Yesu alivyofundisha. (Ona vile vile matumizi ya Yesu ya maneno “mwivi usiku” katika Ufunuo 3:3 na 16:15. Hapo anatumia maneno hayo kusema juu ya kuja Kwake kwenye vita ya Har-magedoni.)

Kuanzia hapa na kuendelea katika Mafundisho Yake ya pale Mlima wa Mizeituni, Yesu alirudia kuwaonya wanafunzi Wake kuwa tayari kwa ajili ya kurudi Kwake. Hapo hapo akawaambia pia jinsi ya kuwa tayari, aliposema mifano kuhusu mtumwa asiyekuwa mwaminifu, kuhusu wanawali kumi, na kuhusu talanta, na baadaye akatabiri hukumu ya kondoo na mbuzi (yote inafaa kusomwa). Katika hiyo mifano yote, aliwaonya kwamba jehanamu ilikuwa inawasubiri wale wote wasiokuwa tayari kwa ajili ya kurudi Kwake (ona Mathayo 24:50, 51; 25:30, 41-46). Njia ya kuwa tayari ni kupatikana ukifanya mapenzi ya Mungu, wakati Yesu atakaporudi.[10]

Hoja Nyingine

Kuna wanaopinga Unyakuo unaotokea karibu na, au mwisho wa Dhiki kwa msingi kwamba, kulingana na Biblia, wenye haki hawaadhibiwi pamoja na wasio haki. Ushahidi ni mifano ya watu kama Nuhu, Lutu na Waisraeli kule Misri.

Kweli, tunazo sababu nzuri tu za kuamini kwamba wenye haki hawatakutwa na ghadhabu ya Mungu wakati wa dhiki ya miaka saba, maana hilo litakuwa kinyume na ahadi nyingi na mifano mingi ya Biblia. (Ona mfano: 1Wathes. 1:9, 10; 5:8).

Lakini, Yesu alitabiri juu ya dhiki kuu ambayo ndani yake wenye haki watateseka. Mateso hayo hayatatoka mikononi mwa Mungu, bali mikononi mwa wasioamini. Wakristo hawaepushwi na mateso – wameahidiwa mateso. Katika kipindi cha Dhiki ya miaka saba, waamini wengi watapoteza maisha yao (ona Mathayo 24:9; Ufunuo 6:9-11; 13:15; 16:5-6; 17:6; 18:24; 19:2). Wengi watakatwa vichwa (ona Ufunuo 20:4).

Basi, kama kila mwamini katika taifa fulani atauawa, hakutakuwa na chochote cha kuzuia ghadhabu ya Mungu isimwangukie kila mmoja katika taifa hilo. Na kwa hakika – kama kuna waamini katika taifa, Mungu aweza kuwalinda kutokana na huku Zake zitakapokuwa zinawaangukia waovu. Wakati wa hukumu Zake kule Misri katika siku za Musa, alithibitisha hilo. Mungu alizuia hata mbwa asibweke kinyume cha Mwisraeli, huku hukumu baada ya nyingine kushuka juu ya Wamisri jirani (ona Kutoka 11:7). Vivyo hivyo tunasoma katika kitabu cha Ufunuo kuhusu nzige wenye kuuma watu, watakaoachiliwa ili kuwatesa waovu wa dunia kwa miezi mitano, lakini wanaambiwa na hawaruhusiwi kuwatesa Wayahudi mia na arobaini na nne elfu (144,000) watakaokuwa wametiwa muhuru maalum kwenye vipaji vya nyuso zao (ona Ufunuo 9:1-11).

Unyakuo Katika Kitabu Cha Ufunuo

Hakuna popote katika Kitabu cha Ufunuo tunaposoma juu ya Unyakuo wa kanisa, wala hatusomi juu ya kutokea kwa Kristo kwingine, isipokuwa katika Ufunuo 19, anapokuja ili kumwua mpingakristo na majeshi yake katika vita ya Har-magedoni. Hakuna lolote linalosemwa kuhusu Unyakuo kutokea hata hapo. Ila, ufufuo wa wafia dini wa Dhiki unatajwa kutokea wakati huo (ona 20:4). Kwa kuwa Paulo aliandika kwamba wafu katika Kristo watafufuliwa wakati wa kurudi kwa Kristo, ambapo pia kanisa litanyakuliwa, mstari huu pamoja na mingine tuliyokwisha tazama, hutuongoza kuamini kwamba Unyakuo hautatokea mpaka mwisho wa Dhiki ya miaka saba, kama inavyoonekana katika Ufunuo 19 na 20. Lakini, yapo mawazo mengine tofauti.

Kuna wanaopata Unyakuo katika Ufunuo sura ya 6 na 7. Katika Ufunuo 6:12 na 13, tunasoma juu ya jua kuwa “jeusi kama gunia la singa” na nyota kuanguka kutoka mbinguni – ishara mbili ambazo Yesu alisema zingetokea muda mfupi tu kabla ya kuonekana Kwake na kuwakusanya wateule (ona Mathayo 24:29-31). Kisha baadaye katika sura ya 7, tunasoma juu ya kundi kubwa la watu wakiwa mbinguni, kutoka kila taifa, kabila na lugha, ambao “wametoka katika dhiki ile kuu” (7:14). Hawatajwi kwamba ni wafia dini kama wanavyotajwa wengine katika sura iliyotangulia (ona 6:9-11), na hilo linatufanya tuseme kwamba wamenyakuliwa, hawajauawa – ni waaminio waliokombolewa kutoka katika dhiki ile kuu.

Ni sahihi kudhani kwamba Unyakuo utatokea wakati fulani mara tu baada ya matukio hayo ya mbinguni yanayotajwa katika Ufunuo 6:12 na 13, kwa sababu yanafanana na yale aliyosema Yesu katika Mathayo 24:29-31. Ila, hatuna ishara iliyo dhahiri kuhusu wakati wa kutokea hayo mambo yanayotajwa katika Ufunuo 6:12 na 13, katika kipindi cha dhiki ya miaka saba. Kama matukio yanayotajwa katika Ufunuo 6:1-13 yanafuatana, na kama Unyakuo unatokea mara tu baada ya 6:13, hilo linatuongoza kuamini kwamba Unyakuo hautatokea mpaka baada ya kufunuliwa kwa mpingakristo (ona 6:1, 2), na vita ya dunia nzima (ona 6:3-4), njaa (ona 6:5, 6), kufa kwa robo ya watu wa duniani kwa vita, njaa, magonjwa na wanyama wakali (ona Ufunuo 6:7-8), na wafia dini wengi kupatikana (ona Ufunuo 6:9-11). Hakika matukio hayo yote yanayotajwa yanaweza kutokea kabla ya kumalizika kipindi cha Dhiki cha miaka saba, lakini pia yanaweza kuwa ndiyo yatakayotokea katika kipindi chote cha miaka saba cha dhiki, na Unyakuo kuwa mwisho kabisa.

Wazo la Unyakuo kutokea kabla ya mwisho wa miaka saba ya dhiki linaongezewa uzito na kweli kwamba Kitabu cha Ufunuo kinaeleza juu ya makundi mawili ya hukumu saba, baada ya Ufunuo sura ya 8, kama ifuatavyo: “hukumu za baragumu” na “hukumu za vitasa”. Hizi za vitasa zinasemekana ndiyo mwisho wa ghadhabu ya Mungu (ona 15:1). Lakini, kabla ya hukumu hizo za vitasa kuanza, Yohana anawaona “wale wenye kushinda, watokao kwa yule mnyama na sanamu yake, na kwa hesabu ya jina lake, wamesimama kandokando ya hiyo bahari ya kioo” (15:2). Hawa watakatifu washindi yawezekana walinyakuliwa. Lakini tena, yawezekana walifia imani yao. Maandiko hayaelezi. Tena, hatujui kama mambo ya 15:2 yana uhusiano wowote na maelezo ya mambo yanayotajwa hapo.

Kweli nyingine inayopatikana katika Ufunuo, yenye kuweza kuongezea uzito kwenye wazo la Unyakuo kutokea kabla ya mwisho wa miaka saba, ni hili: Wakati wa “hukumu ya baragumu” ya tano katika Ufunuo 9:1-12, tunaambiwa kwamba nzige wenye kuuma wataruhusiwa kuwadhuru wale tu “wasiokuwa na muhuri ya Mungu kwenye vipaji vya nyuso zao” (9:4). Watu pekee tunaoambiwa watakuwa na muhuri ni Waisraeli mia na arobaini na nne elfu (144,000) tu (ona Ufunuo 7:3-8). Basi inaonekana kwamba waamini wengine wote itabidi wanyakuliwe kabla ya baragumu hiyo ya tano ya hukumu; vinginevyo, hawataepuka nguvu za hao nzige waumao. Tena, kwa sababu nzige hao watawaumiza watu kwa miezi mitano (9:5, 10), inadhaniwa kwamba ni lazima Unyakuo utokee miezi mitano kabla ya kumalizika kwa miaka ile saba ya Dhiki.

Kuna jinsi ya kufafanua hoja hizo. Pengine kuna wengine waliotiwa muhuru ambao hawatajwi katika kitabu cha Ufunuo. Vyovyote vile, kama hili linathibitisha kwamba Unyakuo utatokea kabla ya hukumu yabaragumu ya tano, pia linaonyesha kwamba kuna kundi moja la waamini ambao hawatanyakuliwa kabla ya kuachiwa kwa hao nzige waumao – wale Waisraeli mia na arobaini na nne elfu (144,000) waliotiwa muhuri. Ila, watakuwa na alama ya kuwalinda wasipatikane na ghadhabu ya Mungu, itakayokuwa inatolewa kwa njia ya nzige hao waumao.

Tuhitimishe. Cha kusema ni kwamba bila shaka Unyakuo utatokea karibu na mwisho au mwishoni kabisa mwa ile miaka saba ya Dhiki. Waamini wasihofu kuhusu ghadhabu ya Mungu, lakini pia wawe tayari kwa ajili ya mateso makali na hata kufa kwa ajili ya imani yao.

Kipindi Cha Dhiki

Hebu tutazame kwa karibu zaidi kile ambacho Maandiko yanafundisha kuhusu ile miaka saba ya Dhiki. Tunapataje saba kwamba ndiyo urefu wa Dhiki? Ni lazima tujifunze kitabu cha Danieli, ambacho kinatoa ufunuo mpana zaidi kuhusu nyakati za mwisho, pamoja na kitabu cha Ufunuo.

Katika sura ya tisa ya kitabu chake, tunagundua kwamba Danieli ni mtumwa huko Babeli, na Wayahudi wenzake. Akiwa katika kujifunza kitabu cha Yeremia, Danieli aligundua kwamba muda wa utumwa wa Wayahudi huko Babeli ungekuwa miaka sabini (ona Danieli 9:2; Yeremia 25:11, 12). Baada ya kutambua kwamba kipindi cha miaka ile sabini kinakaribia kumaliziika, alianza kuomba, akitubu dhambi za watu wake na kuomba rehema. Malaika Gabrieli alimtokea kama jibu la maombi yake, na kumfunulia wakati ujao wa taifa la Israeli, mpaka wakati wa Dhiki na kurudi kwa Kristo. Unabii ulio katika Danieli 9:24-27 ni wa kushangaza sana katika Maandiko. Unabii wenyewe ni kama ifuatavyo, pamoja na maelezo zaidi katika mabano.

Muda wa majuma sabini [bila shaka ni majuma yanayowakilisha miaka kama tutakavyoona – jumla ya miaka 490] umeamriwa juu ya watu wako [Israeli], na juu ya mji wako mtakatifu [Yerusalemu], ili kukomesha makosa [labda maana yake ni tendo kuu la dhambi kwa Israeli – kumsulubisha Masiya wao], na kuishiliza dhambi [pengine maana yake ni kazi ya ukombozi ya Kristo pale msalabani], na kufanya upatanisho kwa ajili ya uovu [maana yake ni ile kazi ya Kristo ya ukombozi pale msalabani], na kuleta haki ya milele [mwanzo wa utawala wa Yesu duniani], na kutia muhuri maono na unabii [pengine kuonyesha mwisho wa kuandikwa kwa Maandiko Matakatifu, au kutimizwa kwa unabii wote unaohusiana na utawala wa Miaka elfu], na kumtia mafuta yeye aliye mtakatifu [pengine kusimamishwa kwa hekalu la kipindi cha utawala wa Kristo miaka elfu moja hapa duniani]. Basi ujue na kufahamu ya kuwa tangu kuwekwa amri ya kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu [amri hii ilitolewa na Mfalme Artashasta mwaka wa 445 K.K.] hata zamani zake masihi aliye mkuu [Bwana Yesu Kristo]; kutakuwa na majuma saba; na katika majuma sitini na mawili [yaani, jumla ya majuma 69 au miaka 483] utajengwa tena pamoja na njia kuu zake na handaki, naam, katika nyakati za taabu [hii inahusu kujengwa upya kwa Yerusalemu, uliokuwa umeharibiwa na WaBabeli]. Na baada ya yale majuma sitini na mawili [yaani, miaka 483 baada ya amri ya mwaka wa 445 K.K.], masihi atakatiliwa mbali, naye atakuwa hana kitu [Yesu angesulubiwa mwaka wa 32B.K., tukihesabu mwaka kulingana na kalenda ya Kiyahudi yenye siku 360 kwa mwaka]; na watu [Warumi] wa mkuu atakayekuja [mpingakristo] watauangamiza mji na patakatifu [maelezo kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 70 B.K. na majeshi ya Kirumi chini ya uongozi wa Tito]; na mwisho wake utakuwa pamoja na gharika, na hata mwisho ule vita vitakuwapo; ukiwa umekwisha kukusudiwa. Naye [huyo ‘mkuu atakayekuja’ – mpingakristo] atafanya agano thabiti na watu wengi [Israeli] kwa muda wa juma moja [au miaka saba – hiki ni kipindi cha Dhiki]; na kwa nusu ya juma hiyo [yaani, miaka mitatu na nusu] ataikomesha sadaka na dhabihu; na mahali pake litasimama chukizo la uharibifu [wakati mpingakristo atakapojisimamisha mwenyewe katika hekalu la Kiyahudi huko Yerusalemu na kujiita Mungu – ona 2Wathes. 2:1-4]; na hivyo, hata ukomo, na ghadhabu iliyokusudiwa imemwagwa juu yake mwenye kuharibu [Yesu atakuja, na kumshinda mpingakristo] (Danieli 9:24-27. Maneno mepesi kukazia).

Miaka 490 Maalum

Baada ya amri ya mwaka wa 445 K.K. iliyotolewa na Mfalme Artashasta kwamba Yerusalemu ujengwe tena, Mungu alitoa miaka 490 maalum sana katika historia ya wakati ujao. Lakini hiyo miaka haikuwa yenye kufuatana – iligawanywa katika sehemu mbili – moja yenye miaka 483 na nyingine yenye miaka saba. Wakati ile miaka 483 ya kwanza ilipokamilika (mwaka ule Yesu aliposulubiwa), saa ilisimama. Danieli asingeweza kudhani kwamba saa ingesimama kwa muda unaozidi miaka elfu mbili! Wakati fulani huko baadaye, saa itaanza tena kutembea, na itatembea kwa miaka saba ya mwisho. Hiyo miaka saba ya mwisho haiitwi tu “Dhiki”, bali pia inajulikana kama “juma la sabini la Danieli.”

Hiyo miaka saba imegawanywa katika vipindi viwili vya miaka mitatu na nusu. Kama tulivyojifunza katika unabii wa Danieli, itakapofikia katikati, mpingakristo atavunja agano lake na Israeli na “kukomesha sadaka na dhabihu.” Kisha, kama alivyotuambia Paulo, ataketi katika hekalu la Yerusalemu na kujitangaza kuwa ni Mungu.[11] Hilo ndilo “chukizo la uharibifu” alilotaja Yesu (ona Mathayo 24:15). Ndiyo sababu waamini wa Uyahudi wanapaswa “kukimbilia milimani” (Mathayo 24:16), maana huo ndiyo mwanzo wa dhiki mbaya zaidi iliyowahi kuowepo duniani (ona Mathayo 24:21).

Yawezekana “kukimbia kwa Wayahudi” kulionekana na Yohana kwa jinsi ya mfano katika maono yake, katika sura ya 12 ya kitabu cha Ufunuo. Kama ndivyo, waamini wa Kiyahudi watakuta mahali maalum pa usalama pameandaliwa kwa ajili yao huko nyikani, watakapo”tunzwa na kulishwa” kwa miaka mitatu na nusu, ambao ndiyo muda utakaokuwa umebaki wa kipindi cha Dhiki ya miaka saba (ona Ufunuo 12:6, 13-17). Yohana aliona Shtani akikasirishwa na kutoroka kwao, na vita iliyofuata aliyoifanya kwa wale wengine “wazishikao amri za Mungu na ushuhuda wa Yesu” (Ufunuo 12:17). Ndiyo sababu ni vizuri waamini duniani kote wakimbilie usalama katika maeneo yaliyofichika, wakati mpingakristo atakapotangaza ‘uungu’ wake huko Yerusalemu.

Ufunuo Wa Mwisho Wa Danieli

Fungu lingine la maandiko lenye kuvutia kutoka Danieli ambalo hatujalitazama, ni ile mistari 13 ya mwisho ya kitabu chake cha kushangaza sana. Ni maneno yaliyotamkwa na malaika. Yanafuata sasa, pamoja na maelezo zaidi katika mabano.

Wakati huo Mikaeli [malaika] atasimama, jemadari mkuu asimamaye upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo [bila shaka hii ni ile dhiki ambayo Yesu alisema juu yake katika Mathayo 24:21]; na wakati huo watu wako wataokolewa [pengine ndiyo kule kukimbia kwa Wayahudi, au kuokolewa kwa waamini wakati wa Unyakuo]; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile. Tena, wengi wa hao walalao katika mavumbi ya nchi wataamka, wengine wapate uzima wa milele, wengine aibu na kudharauliwa milele [huu ni ufufuo wa wenye haki na waovu]. Na walio na hekima watang’aa kama mwangaza wa anga; na hao waongozao wengi kutenda haki watang’aa kama nyota milele na milele. [Baada ya ufufuo wao, wenye hai watapokea miili mipya itakayong’aa kwa utukufu wa Mungu.] Lakini wewe, Ee Danieli, yafunge maneno haya, ukakitie muhuri kitabu hata wakati wa mwisho; wengi wataenda mbio huko na huko, na maarifa yataongezeka. [Maendeleo ya kushangaza sana katika usafirishaji na maarifa katika karne iliyopita yanaonekana kutimiza unabii huu.]

Ndipo mimi, Danieli, nikatazama, na kumbe, wamesimama wengine wawili, mmoja ukingoni mwa mto upande huu, na mmoja ukingoni mwa mto upande wa pili. Na mmoja akamwuliza yule mtu aliyevikwa nguo za kitani, aliyekuwa juu ya maji ya mto; ‘Je! Itakuwa muda wa miaka mingapi hata mwisho wa mambo haya ya ajabu?’ Nami nikamsikia yule mtu aliyevikwa nguo za kitani, aliyekuwa juu ya maji yam to, hapo alipoinua mkono wake wa kuume na mkono wake wa kushoto kueloekea mbinguni; akaapa kwa yeye aliye hai milele na milele, ya kwamba itakuwa wakati, na nyakati mbili, na nusu wakati [sawa na miaka mitatu na nusu, kulingana na ufunuo wenye kufumbua katika Ufunuo 12:6 na 12:14); tena watakapokuwa wamekwisha kuvunja nguvu za hao watu watakatifu, ndipo mambo hayo yote yatakapotimizwa. [Sawa tu na jinsi Danieli 7:25 ilivyotueleza kwamba watakatifu watatiwa mikononi mwa mpingakristo kwa miaka mitatu na nusu. Inaonekana dhahiri kwamba ni ile miaka mitatu na nusu ya mwisho katika ile miaka saba ya Dhiki. Mwisho wa matukio hayo yote yaliyotajwa na malaika utakuja wakati “nguvu za watakatifu” zitakapokwisha “kuvunjwa.”] Nami nikasikia, lakini sikuelewa; ndipo nikasema, ‘Ee Bwana wangu, mwisho wa mambo haya utakuwaje?’ Akasema, ‘Enenda zako, Danieli; maana maneno haya yamefungwa na kutiwa muhuri, hata wakati wa mwisho. Wengi watajitakasa, na kujifanya weupe, na kusafika [kwa njia ya dhiki bila shaka]; bali wabaya watatenda mabaya; wala hataelewa mtu mbaya awaye yote; bali wao walio na hekima ndiyo watakaoelewa. Na tangu wakati ule ambapo sadaka ya kuteketezwa ya daima itaondolewa, na hilo chukizo la uharibifu litakaposimamishwa, itapata siku elfu na mia mbili na tisini. [Hizo siku zisitafsiriwe kumaanisha muda utakaopita katikati ya hayo matukio mawili, kwa sababu yote yanatokea katikati ya ile miaka saba. Inatakiwa kueleweka hivi: tangu wakati wa matukio hayo mawili, siku 1,290 zitapita mpaka kitu kingine kikubwa kitakapotokea mwishoni. Siku 1290 ni zaidi ya miaka mitatu na nusu kwa siku 30, kwa hesabu ya miaka yenye siku 360. Muda huu hutajwa mara kwa mara katika maandiko ya kinabii ya Danieli na Ufunuo. Sababu ya kuongezwa hizo siku thelathini haitajwi na haijulikani. Tena, malaika akamwambia Danieli hivi:] Heri angojaye, na kuzifikilia siku hizo elfu na mia tatu na thelathini na tano. [Sasa tena tuna siku zingine arobaini na tano zisizojulikana ni za nini.] Lakini enenda zako hata utakapokuwa mwisho ule; maana wewe utastarehe, nawe utasimama [kufufuka kwa Danieli mwenyewe] katika kura yako mwisho wa siku hizo. (Danieli 12:1-13).

Ni dhahiri kwamba kitu kizuri sana kitatokea mwisho wa hizo siku 75 za ziada! Itabidi tusubiri ili tuone.

Kutokana na kusoma sura za mwisho za kitabu cha Ufunuo, tunajua kuna matukio mengi ambayo yatakuwepo mara tu baada ya Kristo kurudi – moja likiwa Karamu ya Arusi ya Mwana Kondoo. Malaika alimwambia Yohana hivi juu ya jambo hilo, “Heri walioalikwa kwenye karamu ya arusi ya Mwanakondoo” (Ufunuo 19:9). Pengine hii ndiyo baraka hiyo hiyo inayotajwa na malaika aliyesema na Danieli. Kama ni hivyo, karamu hiyo ya utukufu mwingi itatokea kama miezi miwilina nusu hivi baada ya kurudi kwa Yesu.

Labda zile siku sabini na tano zimejaa vitu vingine ambavyo tunajua vitatokea, kulingana na ilivyoandikwa katika sura za mwisho za kitabu cha Ufunuo, kama vile kutupwa kwa mpingakristo na nabii wa uongo katika ziwa la moto; kufungwa kwa Shetani; na kuanzishwa kwa utawala wa ufalme wa Kristo duniani kote (ona Ufunuo 19:20 hadi 20:4).

Kipindi Cha Miaka Elfu

Utawala wa Miaka Elfu ni jina linaloeleza wakati ambapo Yesu Mwenyewe atatawala dunia nzima kwa kipindi cha miaka elfu moja (ona Ufunuo 20:3, 5, 7). Hii inatokea baada ya ile Dhiki ya miaka saba. Isaya aliona utawala wa Kristo juu ya dunia, miaka elfu tatu na zaidi iliyopita. Anaeleza hivi:

Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; naye ataitwa … Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe, katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake, kuuthibitisha na kuutegemeza kwa hukumu na kwa haki, tangu sasa na hata milele (Isaya 9:6, 7. Maneno mepesi kukazia).

Vivyo hivyo, malaika Gabrieli alimtangazia Mariamu kwamba Mtoto wake angetawala ufalme usio na mwisho. Alimwambia hivi:

Malaika akamwambia, ‘Usiogope Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu. Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho’ (Luka 1:30-33. Maneno mepesi kukazia).[12]

Wakati wa Miaka Elfu, Yesu binafsi atatawala kutoka Yerusalemu, pale Mlima Sayuni, na mlima huo utainuliwa na kuwa mrefu kuliko sasa. Utaala Wake utakuwa wa haki kabisa kwa mataifa yote, na itakuwepo amani kamili na halisi duniani kote.

Na itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya BWANA utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, ‘Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake. Maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la BWANA katika Yerusalemu. Naye atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upana juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe (Isaya 2:2-4).

Hata Zekaria naye alitabiri hayo hayo, kama ifuatavyo:

BWANA wa majeshi asema hivi, ‘Mimi nina wivu kwa ajili ya Sayuni, wivu mkuu, nami nina wivu kwa ajili yake kwa ghadhabu kuu.’ BWANA asema hivi, ‘Mimi nimerudi Sayuni, nami nitakaa katikati ya Yerusalemu; na Yerusalemu utaitwa, Mji wa kweli; na Mlima wa BWANA wa majeshi utaitwa, Mlima Mtakatifu.’ … BWANA wa majeshi asema hivi, ‘Itatokea halafu ya kwamba watakuja mataifa na wenyeji wa miji mingi; wenyeji wa mji huu watauendea mji huu, wakisema, ‘Haya! Twendeni zetu kwa haraka tuombe fadhili za BWANA, na kumtafuta BWANA wa majeshi; mimi nami nitakwenda.’ Naam, watu wa kabila nyingi na mataifa hodari watakuja Yerusalemu kumtafuta BWANA wa majeshi, na kuomba fadhili za BWANA. BWANA wa majeshi asema hivi, ‘Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naama, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi’. (Zekaria 8:2-3; 20-23).

Biblia inafundisha kwamba waamini watatawala pamoja na Kristo katika kipindi hicho cha miaka elfu moja. Viwango vya majukumu na wajibu zao katika ufalme Wake vitategemeana na uaminifu wao kwa sasa (ona Danieli 7:27; Luka 19:12-27; 1Wakor. 6:1-3; Ufunuo 2:26, 27; 5:9, 10 na 22:3-5).

Tutakuwa katika miili yetu ya ufufuo, lakini watakuwepo watu wengine wakiishi katika miili yao ya kawaida tu duniani. Tena, inaonekana urefu wa maisha utarudishwa, na wanyama wakali watakoma kuwa hivyo.

Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza. Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa. … Mbwa-mwitu na mwana-kondoo watalisha pamoja, na simba atakula majani kama ng’ombe; na mavumbi yatakuwa chakula cha nyoka. Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu mtakatifu wote, asema BWANA (Isaya 65:19, 20, 25. Ona pia Isaya 11:6-9).

Biblia imetaja sana habari za Miaka Elfu inayokuja – hasa katika Agano la Kale. Ukitaka kujifunza zaidi, soma Isaya 11:6-16; 25:1-12; 35:1-10; Yeremia 23:1-5; Yoeli 2:30 hadi 3:21; Amosi 9:11-15; Mika 4:1-7; Sefania 3:14-20; Zekaria 14:9-21 na Ufunuo 20:1-6.

Vile vile, Zaburi nyingi za kinabii zinahusiana na kipindi cha Miaka Elfu. Kwa mfano: Soma fungu hili katika Zaburi ya 48.

Bwana ndiye aliye mkuu, na mwenye kusifiwa sana. Katika mji wa Mungu wetu, katika mlima wake mtakatifu. Kuinuka kwake ni mzuri sana, ni furaha ya dunia yote. Mlima Sayuni pande za kaskazini, Mji wa Mfalme mkuu. Mungu katika majumba yake amejijulisha kuwa ngome. Maana, tazama, wafalme walikusanyika; walipita wote pamoja. Waliona, mara wakashangaa; wakafadhaika na kukimbia. Papo hapo tetemeko liliwashika, utungu kama wa mwanamke azaaye (Zaburi 48:1-6. Maneno mepesi kukazia).

Wakati Yesu atakaposimamisha utawala Wake huko Yerusalemu wakati wa kuanza kwa kipindi cha Miaka Elfu Moja, inaonekana kwamba watawala wengi wa dunia watakaopona Dhiki watapata taarifa ya utawala wa Yesu na kusafiri kwenda huko ili kujionea wenyewe! Watakachokiona kitawashangaza.[13]

Ukitaka Zaburi zingine zenye kusimulia habari za utawala wa Kristo katika Miaka Elfu, angalia Zaburi 2:1-12; 24:1-10; 47:1-9; 66:1-7; 68:15-17; 99:1-9 na 100:1-5.

Umilele

Mwisho wa kipindi cha Miaka Elfu ni mwanzo wa kitu kinachoita na wasomi wa Biblia “umilele”, muda unaoanza kwa mbingu mpya na nchi mpya. Kisha, Yesu atamrudishia Baba kila kitu, kulingana na 1Wakorintho 15:24-28.

Hapo ndipo mwisho, [Yesu] atakapompa Mungu Baba ufalme wake; atakapobatilisha utawala wote, na mamlaka yote, na nguvu. Maana sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti. Kwa kuwa, ‘Alivitiisha vitu vyote chini ya miguu yake’ [Zaburi 8:6]. Lakini atakaposema, ‘Vyote vimetiishwa,’ ni dhahiri ya kuwa yeye [Baba] aliyemtiishia vitu vyote hayumo. Basi, vitu vyote vikiisha kutiishwa chini yake [Baba], ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote, ili kwamba Mungu awe yote katika wote.

Shetani ambaye atakuwa amefungwa kwa kipindi chote hicho cha miaka elfu, atafunguliwa mwisho wake. Ndipo atawadanganya wale ambao ndani yao wanamwasi Yesu, waliokuwa wanajifanya kumtii wakati wa kipindi hicho chote (ona Zaburi 66:3).

Mungu atamruhusu Shetani kuwadanganya ili kudhihirisha hali halisi yamiyo yao, waweze kuhukumiwa kihalali. Katika kudanganywa kwao, watajikusanya ili kuushambulia mji mtakatifu – Yerusalemu – lengo lao likiwa kuipindua serikali ya Yesu. Vita haitadumu sana kwa sababu moto utashuka kutoka mbinguni na kuteketeza majeshi yaliyouzunguka mji, na Shetani atatupwa milele katika ziwa la moto na kiberiti (ona Ufunuo 20:7-10).

Kujikusanya huko kwa ajili ya vita kunatabiriwa katika Zaburi ya 2, kama ifuatavyo:

Mbona mataifa wanafanya ghasia, na makabila wanatafakari ubatili? Wafalme wa dunia wanajipanga, na wakuu wanafanya shauri pamoja, juu ya BWANA, na juu ya masihi wake [Kristo], ‘Na tuvipasue vifungo vyao, na kuzitupia mbali nasi kamba zao!’ Yeye aketiye mbinguni anacheka, Bwana anawafanyia dhihaka. Ndipo atakaposema nao kwa hasira yake, na kuwafadhaisha kwa ghadhabu yake. ‘Nami nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu.’ [Yesu sasa anazungumza na kusema hivi:] ‘Nitaihubiri amri. BWANA aliniambia, Ndiwe mwanangu, mimi leo nimekuzaa. Uniombe, nami nitakupa mataifa kuwa urithi wako, na miisho ya dunia kuwa milki yako. Utawaponda kwa fimbo ya chuma, na kuwavunja kama chombo cha mfinyanzi.’ Na sasa, enyi wafalme, fanyeni akili, enyi waamuzi wa dunia, mwadibiwe. Mtumikieni BWANA kwa kicho, shangilieni kwa kutetemeka. Shikeni yaliyo bora, asije akafanya hasira nanyi mkapotea njiani, kwa kuwa hasira yake itawaka upesi. Heri wote wanaomkimbilia!

Hukumu Ya Mwisho

Kabla ya kuanza Umilele, hukumu moja itatolewa. Wasio haki wote wa nyakati zote watafufuliwa kutoka wafu ili wasimame mbele ya kiti cha enzi cha Mungu na kuhukumiwa kulingana na matendo yao (ona Ufunuo 20:5; 11-15). Kila mtu ambaye kwa sasa yuko Hades (kuzimu) atafikishwa hukumuni hapo. Hukumu hii inajulikana kama “Hukumu ya Kiti Kikubwa cha Enzi, Cheupe”. Kisha, atatupwa Jehanamu – katika ziwa la moto. Hiyo inaitwa “mauti ya pili” (Ufunuo 20:14).

Umilele unaanza kwa kupita kwa mbingu na nchi za kwanza, na hivyo kutimiza ahadi ya Yesu ya zaidi ya miaka elfu mbili iliyopita: “Mbingu na nchi zitapita, bali maneno yangu hayatapita kamwe” (Mathayo 24:35).

Kisha, Mungu ataumba mbingu na nchi mpya, sawa na Petro alivyotabiri katika barua yake ya pili, hivi:

Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi. Katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea. Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa, mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka? Lakini, kama ilivyo ahadi yake, mnatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake (2Petro 3:10-14. Ona pia Isaya 65:17, 18).

Hatimaye – Yerusalemu mpya utashuka kutoka mbinguni mpaka chini duniani (ona Ufunuo 21:1, 2). Mawazo yetu hayawezi hata kuanza kuelewa utukufu wa mji huo, wenye eneo kubwa sana – karibu nusu ya bara la Afrika (ona Ufunuo 21:16), au maajabu ya miaka hiyo isiyo na mwisho. Tutaishi katika jamii kamilifu milele, chini ya utawala wa Mungu, kwa utukufu wa Yesu Kristo!


[1] Maandiko mengine yenye kuonyesha imani ya Paulo kwamba Yesu angeweza kurudi katika wakati wa uhai wake ni Wafilipi 3:20; 1Wathes. 3:13; 5:23; 2Wathes. 2:1-5; 1Timo. 6:14, 15; Tito 2:11-13; Waebrania 9:28.

[2] Maandiko mengine yenye kuonyesha imani ya Petro kwamba Yesu angeweza kurudi wakati wa uhai wake ni 2Petro 1:15-19; 3:3-15.

[3] Katika Marko 13:3 wanatajwa wale wanne waliokuwepo: Petro, Yakobo, Yohana na Andrea. Mafundisho ya pale Mlima wa Mizeituni yanapatikanapia katika Marko 13:1-37 na Luka 21:5-36. Utapata habari kama hizo katika Luka 17:22-37 pia.

[4] Mara nyingi ahadi hii huondolewa mahali pake. Watu husema mara kwa mara kwamba kabla Yesu hajarudi, imetupasa kukamilisha kazi ya kuufikia ulimwengu kwa Injili. Lakini, katika mantiki hii, ahadi hii inazungumzia kutangazwa kwa mwisho wa Injili duniani kote kabla ya mwisho wa dunia.

[5] Kama Unyakuo wa kanisa unatokea wakati huo katika ile Dhiki ya miaka saba kama wengine wanavyosema, maagizo ya Yesu kamba waamini wakimbie kuokoa maisha yao yasingekuwa na maana kwa sababu si watanyakuliwa wote?

[6] Hii inapinga hoja kwamba maneno ya Yesu katika Mafundisho pale Mlima wa Mizeituni yanawahusu waamini wa Kiyahudi tu ambao wataokolewa wakati wa Dhiki, maana wengine wote walio-okoka kabla ya Dhiki watakuwa wamekwisha nyakuliwa. Paulo anawaambia waamini Wathesalonike – mataifa – kwamba Unyakuo wao na kurudi kwa Kristo visingetokea mpaka baada ya mpingakristo kujitangaza kwamba ni Mungu, kitu kinachotokea katikati ya Dhiki ya miaka saba.

[7] Kuna wanaosema kwamba huu ufufuo unaotajwa katika Ufunuo 20:4-6 ni sehemu ya pili ya ufufuo wa kwanza, ufufuo uliotokea wakati wa kurudi mara ya kwanza kwa Kristo wakati wa Unyakuo. Nini sababu ya tafsiri hiyo? Kama ufufuo wa Ufunuo 20:4-6 ni wa pili, mbona usiitwe “ufufuo wa pili”?

[8] Ingawa waliomsikia Yesu siku hiyo wanaweza kuwa walidhani kwamba kizazi chao ndicho kingeyaona hayo yote, tunajua sivyo. Basi, lazima tutafsiri maneno ya Yesu katika 24:34 kumaanisha kwamba mambo hayo yote yatafanyika katika kizazi kimoja, au pengine kwamba taifa la Wakristo (au Wayahudi basi) lisingepita mpaka mambo hayo yote yatimie.

[9] Hakuna tofauti yoyote ikiwa mwenye kupatikana na hukumu katika mifano hii ni mwenye kutwaliwa au mwenye kubaki, kama ambavyo watu wengi hubishana. Hoja ni kwamba, kuna watakaokuwa tayari kwa ajili ya kurudi kwa Kristo, na kuna ambao hawatakuwa tayari. Utayari wao utaamua umilele wao.

[10] Ni dhahiri kwamba uwezekano wa wanafunzi wa Yesu kutokuwa tayari wakati wa kurudi Kwake ulikuwepo, maana aliwaonya sana kuhusu hilo. Kama aliwaambia kwamba adhabu ni hukumu ya milele kwa kutokuwa tayari kwa sababu ya dhambi, basi ilikuwa inawezekana kwao kupoteza wokovu kwa sababu ya dhambi. Hili linapaswa kutupa angalizo juu ya umuhimu wa utakatifu, na tutambue kwamba ni upuuzi kusema kwamba waamini hawawezi kupoteza wokovu wao, kama wengine wanavyosema na kufundisha.

[11] Hii inatuonyesha kwamba lazima hekalu la Yerusalemu lijengwe tena maana kwa sasa hakuna hekalu lolote huko Yerusalemu (mwaka 2005 kitabu hiki kinapoandaliwa).

[12] Andiko hili linaonyesha jinsi ilivyo rahisi kukosea kuhusu matukio ya kinabii kwa kusoma isivyo. Mariamu angeweza kudhani kihalali kabisa kwamba Mtoto wake maalum sana angekalia kiti cha enzi cha Daudi baada ya miaka kadhaa. Gabrieli alimwambia angezaa mwana ambaye angetawala juu ya nyumba ya Yakobo, kana kwamba kuzaliwa kwa Yesu na kutawala vingekuwa vitu vinavyofuatana. Mariamu asingeweza kudhani kwamba kuna zaidi ya miaka elfu mbili kati ya kuzaliwa na kutawala. Sisi pia tunapaswa kuwa makini – tusije tukatafsiri unabii vibaya.

[13] Kutokana na maandiko mengine, inaonekana kwamba kipindi cha Miaka Elfu kitaanza kwa wasioamini kujaza dunia, si waamini tu. (Ona Isaya 2:1-5; 60:1-5; Danieli 7:13, 14).

To subscribe to David Servant's periodic e-teachings, click here.


Mchungaji Afanyaye Watu Kuwa Wanafunzi » Unyakuo Wa Kanisa Na Nyakati Za Mwisho

Mpango Wa Mungu Wa Milele

Sura Ya Ishirini Na Nane

 

Kwa nini Mungu alituumba? Je, amekuwa na lengo fulani katika akili Zake tangu mwanzo? Je, hakujua kwamba kila mtu angemwasi? Je, hakuona matokeo ya uasi wetu – mateso yote na huzuni ambavyo vimewapata binadamu tokea hapo? Kama ndivyo, alimwumba mwanadamu wa nini basi?

Biblia inatujibu maswali hayo. Inatuambia kwamba, kabla ya Mungu kumwumba Adamu na Hawa alijua kwamba wao na wengine baada yao wangetenda dhambi. Cha ajabu ni kwamba alikwisha panga mpango wa kuwakomboa binadamu walioanguka, kwa njia ya Yesu. Paulo ameandika hivi kuhusu huo mpango wa Mungu kabla ya uumbaji wa vyote:

Kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele (2Timo. 1:8b, 9. Maneno mepesi kukazia).

Sisi tulipewa neema ya Mungu katika Kristo tangu milele, sio kwa milele tu. Hiyo inaonyesha kwamba kifo cha Yesu cha kujitoa sadaka ni kitua mbacho Mungu alipanga tokea milele iliyopita.

Pia, Paulo ameandika hivi katika barua yake kwa Waefeso:

Kwa kadiri ya kusudi la milele alilolikusudia katika Kristo Yesu Bwana wetu (Waefeso 3:11. Maneno mepesi kukazia).

Kifo cha Yesu msalabani hakikuwa wazo la haraka au mpango ulioandaliwa upesi-upesi ili kutengeneza kitu ambacho Mungu hakuwa amekiona.

Si kwamba Mungu alikuwa na kusudi la milele kutupa sisi neema Yake tangu milele, bali pia alifahamu tangu milele iliyopita, nani wangechagua kupokea neema Yake, naye akaandika hata majina yao katika kitabu.

Na watu wote wakaao juu ya nchi watamsujudu, kila ambaye jina lake halikuandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo [Yesu], aliyechinjwa tangu kuwekwa misingi ya dunia (Ufunuo 13:8. Maneno mepesi kukazia).

Anguko la Adamu halikumshtua Mungu. Hata wewe unapoanguka au mimi ninapoanguka, Mungu hashangazwi. Mungu alijua tutatenda dhambi, naye pia alijua atakayetubu na kumwamini Bwana Yesu.

Swali Linalofuata

Ikiwa Mungu alijua kwamba wengine wangemwamini Yesu na wengine wangemkataa, kwa nini aliumba watu ambao alijua wangemkataa? Mbona asirahisishe tu mambo kwa kuwaumba wale aliojua kwamba watatubu na kumwamini Yesu?

Jibu la swali hilo ni gumu kidogo kuelewa, lakini linaweza kueleweka.

Cha kwanza tunachopaswa kuelewa ni kwamba Mungu alituumba tukiwa na hiari. Yaani, sisi sote tuna fursa ya kujiamulia wenyewe ikiwa tutamfuata Mungu au hapana. Maamuzi yetu ya kutii au kutotii, kutubu au kutotubu, Mungu hajatupangia. Ni uchaguzi wetu wenyewe.

Kwa kuwa ni hivyo, lazima wote tupimwe. Ni kweli kwamba Mungu alijua tutakachofanya kabla hatujakifanya, lakini ilitubidi sisi tufanye kitu hicho wakati fulani ili Yeye akijue kabla.

Tutazame mfano. Mungu anajua matokeo ya kila mchezo wa mpira kabla haujachezwa, lakini lazima kuwe na michezo ya mpira na matokeo yake kama Mungu atajua. Ni kwamba Mungu hawezi kujua kabla matokeo ya michezo ya mpira ambayo haichezwi kwa sababu hakuna matokeo ya kujulikana.

Vivyo hivyo, Mungu anaweza kujua kabla matokeo ya watu wenye hiari, kama hao watu watapewa nafasi ya kufanya maamuzi hayo, na kuyafanya. Lazima wapimwe. Na hiyo ndiyo sababu Mungu hakuumba watu ambao Yeye alijua kabla kwamba watatubu na kumwamini Yesu peke yao.

Swali Lingine

Tunaweza pia kuuliza hivi: “Kama Mungu wanataka watu watiifu tu, kwa nini alituumba tukiwa na hiari? Mbona hakuumba mashine za robot ambazo ni tiifu zinazoishi milele?”

Jibu ni hili: Ni kwa sababu Mungu ni Baba. Anataka kuwa na uhusiano wa baba na mtoto pamoja nasi, na haiwezekani ukawepo kama tutakuwa mashine. Shauku ya Mungu ni kuwa na familia ya milele ya watoto ambao wamechagua, kwa hiari yao wenyewe, kumpenda. Huo ndiyo uliokuwa mpango Wake kulingana na Maandiko.

Kwa kuwa alitangulia kutuchagua, ili tufanywe wanawe kwa njia ya Yesu Kristo, sawasawa na uradhi wa mapenzi yake (Waefeso 1:4b, 5. Maneno mepesi kukazia).

Ukitaka kujua raha ambayo Mungu angepata kutoka kwa mashine za robot, hebu chukua mwanasesere mkononi, umwambie akwambie kwamba anakupenda! Ukweli ni kwamba hutasikia raha moyoni mwako! Maana, huyo mwanasesere atakwambia kile unachomfanya aseme. Hakupendi kwa kweli.

Kinachofanya upendo kuwa maalum sana ni kwa sababu umejengwa kwenye uchaguzi wa mtu mwenye hiari. Wanasesere na mashine za robot hawajui chochote kuhusu upendo kwa sababu hawawezi kuamua chochote wao wenyewe.

Kwa kuwa Mungu alitaka familia ya watoto ambao wangechagua kumpenda na kumfuata kutoka mioyoni mwao, ilibidi aumbe watu wenye hiari. Uamuzi huo ulihusisha Yeye kukubali kwamba kuna uwezekano wa baadhi ya hao watu wenye hiari kuamua hawatampenda au kumfuata. Na hao, baada ya kuishi maisha ya kumpinga Mungu anayejidhihirisha na kuwavuta watu wote kwa njia ya uumbaji Wake, na dhamiri zao na wito wa Injili, wangekabiliwa na hukumu yao halali kabisa, baada ya kujithibitisha kwamba wanastahili hasira ya Mungu.

 

Hakuna mtu kuzimu atakayeweza kumnyooshea Mungu kidole cha lawama kwa haki, kwa sababu Mungu alitoa njia ya kila mtu kuepukana na adhabu ya dhambi zake. Mungu anataka kila mtu aokolewe (ona 1Timo. 2:4; 2Petro 3:9) lakini kila mtu lazima ajiamulie mwenyewe.

Kuchaguliwa Kabla KiBiblia

Lakini, vipi kuhusu maandiko katika Agano Jipya yanayosema kwamba Mungu alituchagua sisi kabla ya kuwekwa misingi ya dunia?

Kwa bahati mbaya, kuna wengine wanaodhani kwamba Mungu amewachagua watu fulani kuokoka, na wengine kulaaniwa, na msingi wa kuamua Kwake si chochote ambacho watu hao wamefanya. Yaani, Mungu amekwisha chagua wale watakao-okoka au kupotea. Wazo hili linaondoa dhana ya hiari ya mtu, na wala halifundishwi na Maandiko. Hebu tutazame Biblia inafundisha nini kuhusu kuchaguliwa kabla.

Ni kweli Biblia inafundisha kwamba Mungu ametuchagua, lakini lazima kutolewa maelezo. Tangu dunia ilipowekwa misingi, Mungu amechagua kuwakomboa watu ambao aliwajua kabla kwamba wangetubu na kuiamini Injili kutokana na ushawishi Wake, lakini kwa hiari yao wewenyewe. Hebu angalia maneno ya mtume Paulo kuhusu watu ambao Mungu huwachagua.

Mungu hakuwasukumia mbali watu wake waliowajua tokea awali. Au hamjui yale yaliyonenwa na maandiko juu ya Eliya? Jinsi anavyowashitaki Waisraeli mbele za Mungu, ‘Bwana! Wamewaua manabii wako, wamezibomoa madhabahu zako, nami nimesalia peke yangu, nao wananitafuta roho yangu. Lakini ile jawabu ya Mungu yamwambiaje? ‘Nimejisazia watu elfu saba wasiopiga goti mbele ya Baali’. Basi ni vivi hivi wakati huu wa sasa, yako mabaki waliochaguliwa kwa neema (Warumi 11:2-5. Maneno mepesi kukazia).

Ona kwamba Mungu alimwambia Eliya “amejisazia watu elfu saba,” lakini hao watu elfu saba kwanza walikuwa wamekwisha fanya uchaguzi “kutompigia Baali goti”. Paulo akasema, vivyo hivyo, walikuwepo pia mabaki ya Wayahudi waaminio waliochaguliwa na Mungu. Basi, tunaweza kusema hivi: Ndiyo, Mungu ametuchagua, lakini amewachagua wale ambao kwanza wamefanya uchaguzi sahihi wao wenyewe. Mungu amechagua kuwaokoa wote wenye kumwamini Yesu, na huo ulikuwa mpango Wake hata kabla ya kuumba dunia.

Mungu Kujua Mambo Kabla

Kwa hali hiyo hiyo, Maandiko pia yanafundisha kwamba Mungu aliwajua kabla wale wote ambao wangechagua kufanya uchaguzi sahihi. Kwa mfano: Petro aliandika hivi:

Wakaao hali ya ugeni … kama vile Mungu Baba alivyotangulia kuwajua (1Petro 1:1-2a. Maneno mepesi kukazia).

Tumechaguliwa kulingana na uwezo wa Mungu kujua mambo kabla. Hata Paulo naye aliandika kuhusu waamini waliojulikana na Mungu kabla.

Maana wale aliowajua tangu asili [sisi], aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye [Yesu] awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza (Warumi 8:29-30).

Mungu alitujua kabla sisi sote ambao tungechagua kumwamini Yesu, Naye akatuchagua tufananishwe na mfano wa Mwna Wake, yaani, tuzaliwe na kuwa watoto wa Mungu katika familia Yake kubwa. Kulingana na mpango huo wa milele, alituita kwa njia ya Injili, akatuhesabia haki na hatimaye atatutukuza katika ufalme Wake wa milele.

Katika barua nyingine, Paulo aliandika hivi:

Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu yesu Kristo, aliyetubarikmi kwa baraka zote za rohoni katika ulimwengu wa roho ndani yake Kristo; kama vile alivyotuchagua katika yeye kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu, ili tuwe watakatifu, watu wasio na hatia mbele zake katika pendo. Kwa kuwa alitangulia kutuchagua, ili tufanywe wanawe kwa njia ya Yesu Kristo, sawasawa na uradhi wa mapenzi yake. Na usifiwe utukufu wa neema yake, ambayo ametuneemesha katika huyo Mpendwa (Waefeso 1:3-6. Maneno mepesi kukazia).

Kweli hiyo hiyo inatajwa hapa – Mungu alituchagua sisi (ambao alijua kabla kwamba tungetubu na kuamini) kabla ya misingi ya ulimwengu ili tuwe watoto Wake watakatifu kwa njia ya Yesu Kristo.

Kama tulivyokwisha sema, kuna wanaopotosha maana ya mistari kama hiyo kwa kupuuzia mengine yote yanayofundishwa na Biblia, na kudai kwamba sisi hatukuwa na uchaguzi wowote kwa habari ya wokovu wetu – Mungu ndiye mwenye neno la mwisho. Fundisho hili wanaliita “kuchaguliwa pasipo masharti”. Lakini, nani amewahi kusikia juu ya kitu cha aina hiyo – yaani, uchaguzi usiokuwa na masharti fulani? Katika nchi huru, tunachagua wagombea wanasiasa kulingana na wao kutosheleza masharti tuliyo nayo akilini mwetu. Tunawachagua wenzi kulingana na masharti watakayotimiza, sifa zao zinazowafanya wakubalike kwetu. Lakini wanatheolojia wengine wanataka tuamini kwamba uchaguzi wa Mungu kwamba nani aokoke na nani asiokoke “hauna masharti” – hautegemeani na masharti fulani ambayo hao watu wameyatimiza! Kwa hali hiyo, wokovu wa watu ni kwa bahati tu, ni atakavyoamua anayeitwa Mungu, ambaye ni mkatili, asiye na haki, mnafiki na asiyekuwa na akili – kwa mawazo yao! Neno lenyewe – “kuchaguliwa pasipo masharti” linapingana, maana uchaguzi unaonyesha masharti. Kama ni “kuchaguliwa pasipo masharti” hakuna uchaguzi hapo; huko ni kubahatisha.

Picha Kubwa

Sasa tunaiona picha yote kwa ukamilifu. Mungu alijua sisi sote tungetenda dhambi, lakini alifanya mpango wa kutukomboa kabla yeyote kati yetu hajazaliwa. Mpango huo ungedhihirisha upendo Wake wa ajabu sana na haki, maana ingebidi Mwana Wake asiye na dhambi afe kwa ajili ya dhambi zetu, kwa niaba yetu. Tena, Mungu hakutupangia sisi tutakaotubu na kuamini tu msamaha, bali pia kwamba tungekuwa kama Mwana Wake, Yesu. Ndiyo sababu Paulo akasema, “Si mimi ninayeishi, bali Kristo ndani yangu” (Wagal. 2:20).

Sisi ambao ni wana wa Mungu tuliozaliwa mara ya pili tutapewa miili isiyoharibika siku moja, nasi tutaishi katika jamii kamilifu, tukimtumikia, na kumpenda na kushirikianana Baba yetu wa ajabu wa mbinguni! Tutaishi katika dunia mpya, katika Yerusalemu Mpya. Hayo yote yatakuwa yamefanikiwa kwa sababu ya kifo chakujitolea sadaka cha Yesu! Mungu asifiwe kwa ajili ya mpango Wake wa milele!

Maisha Ya Sasa

Tukiisha kuelewa mpango wa Mungu wa milele, tunaweza kufahamu zaidi maana ya maisha haya. Kimsingi ni kwamba, maisha ya sasa ni kama kipimo au mtihani kwa ajili ya kila mtu. Uchaguzi wa kila mtu huamua kama atafurahia fursa ya pekee ya kuwa mtoto mmojawapo wa Mungu, atakayeishi pamoja na Baba milele. Wale wanaojinyenyekeza wenyewe, wanaokubaliana na mvuto wa Mungu, na kutubu na kuamini, watatukuzwa (ona Luka 18:14). Maisha haya ni kipimo kwa ajili ya maisha ya wakati ujao.

Hii pia hutusaidia kuelewa baadhi ya mambo ya siri katika maisha haya ya sasa. Kwa mfano: Wengi wamejiuliza hivi: “Kwa nini Shetani na mapepo yake wanaruhusiwa kuendelea kuwajaribu watu?” Au, “Wakati Shetani alipotupwa kutoka mbinguni, kwa nini aliruhusiwa kufika duniani?”

Twaweza kuona kwamba hata sasa Shetani anatimiza kusudi fulani katika mpango wa Mungu. Kimsingi, Shetani ndiyo kama uchaguzi mwingine kwa ajili yabinadamu. Kama uchaguzi pekee ungekuwa ni kumfuata Yesu, basi kila mtu angemfuata Yesu apende, asipende.

Ingekuwa sawa na kuwepo na uchaguzi ambao kila mtu anatakiwa kupiga kura, lakini mgombea ni mmoja tu. Huyo mgombea bila shaka angepita bila kupingwa, lakini asingekuwa na imani kwamba anapendwa na waliomchagua! Hawakuwa na uchaguzi – ilibidi wampigie kura! Mungu Naye angekuwa katika hali kama hiyo kama kusingekuwepo na yeyote anayeshindana Naye ili kupata mioyo ya watu.

Hebu tufikiri hivi: Ingekuwaje kama Mungu angewaweka Adamu na Hawa katika bustani ambayo hakuna kilichokatazwa? Ingekuwa hivi: Adamu na Hawa wangekuwa mashine za robot kutokana na mazingira. Wasingeweza kusema, “Tumeamua kumtii Mungu” kwa sababu wasingekuwa na nafasi ya kutokumtii.

Cha muhimu zaidi ni hiki: Mungu asingeweza kusema, “Ninajua Adamu na Hawa wananipenda” kwa sababu Adamu na Hawa wasingekuwa na nafasi ya kutii na kuthibitisha upendo wao kwa Mungu. Mungu lazima atoe nafasi ya kutotii kwa watu wenye hiari ili Yeye aamue kama wanataka kumtii. Mungu hamjaribu mtu (ona Yakobo 1:13), lakini humpima kila mtu (ona Zaburi 11:5; Mithali 17:3). Njia moja ya kuwapima ni kuwaruhusu wajaribiwe na Shetani, ambaye kwa njia hiyo anatekeleza kusudi maalum katika mpango wa Mungu wa milele.

Mfano Mzuri

Tunasoma hivi katika Kumbukumbu la Torati 13:1-3:-

Kukizuka katikati yako nabii au mwotaji wa ndoto, akikutolea ishara au ajabu, ikatukia hiyo ishara au hiyo ajabu aliyokuambia akisema, ‘Na tuifuate miungu mingine usiyoijua, tuitumikie hiyo’; wewe usiyasikize maneno ya nabii yule, au yule mwotaji wa ndoto, kwa kuwa BWANA, Mungu wenu, yuawajaribu, apate kujua kwamba mwampenda BWANA, Mungu wenu, kwa mioyo yenu yote na roho zenu zote (Maneno mepesi kukazia).

Inaonekana ni halali kabisa kuamua kwamba si Mungu aliyemwezesha huyo nabii wa uongo kufanya ishara au maajabu – bila shaka ni Shetani. Lakini Mungu anaruhusu na anatumia jaribu la Shetani kama kipimo Chake mwenyewe ili kugundua kilichomo ndani ya mioyo ya watu Wake.

Kanuni hiyo hiyo inaonekana katika Waamuzi 2:21 hadi 3:8 wakati Mungu aliporuhusu Israeli kujaribiwa na mataifa yaliyowazunguka ili kuamua ikiwa wangemtii au hapana. Yesu pia aliongozwa na Roho nyikani kwa kusudi la kujaribiwa na Shetani (ona Mathayo 4:1) na kwa njia hiyo kupimwa na Mungu. Ilibidi athibitishwe kwamba hana dhambi, na njia ya pekee ya kuthibitishwa kwamba hana dhambi ilikuwa kwa kujaribiwa.

Shetani Hastahili Lawama Zote

Tayari Shetani amedanganya watu wengi sana duniani kwa kupofusha mawazo yao kwa kweli ya Injili, lakini lazima tutambue kwamba Shetani hawezi kumpofusha mtu yeyote tu. Anaweza kuwadanganya wale watakaokubali kudanganywa, yaani, watu wanaokataa ukweli.

Paulo alitangaza kwamba wasioamini “wametiwa giza katika ufahamu wao” (Waefeso 4:18) na wale wasiojua, lakini pia amedhihirisha kiini cha ufahamu wao kutiwa giza, na kutokujua kwao.

Tangu sasa msienende kama Mataifa waenendavyo, katika ubatili wa nia zao; ambao, akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa Mungu, kwa sababu ya ujinga uliomo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao; ambao wakiisha kufa ganzi wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani (Waefeso 4:17b – 19. Maneno mepesi kukazia).

Watu ambao hawajaokoka si wenye bahati mbaya ambao wamedanganywa na Shetani. Ni wenye dhambi waasi ambao kwa makusudi, hawataki kujua, na ambao wanataka kudumu katika hali hiyo kwa sababu mioyo yao ni mgumu sana.

Hakuna mtu anayetakiwa kudumu katika kudanganywa, kama maisha yako wewe yanavyothibitisha! Ulipolainisha moyo wako na kumwelekea Mungu, Shetani hakuweza kuendelea kukudanganya.

Mwishoni, Shetani atafungwa katika kipindi cha utawala wa Kristo kwa miaka elfu moja, naye hatakuwa na ushawishi kwa mtu yeyote.

[Malaika] Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; akamtupa katika kuzimu, akamfunga, akatia muhuri juu yake, asipate kuwadanganya mataifa tena, hata ile miaka elfu itimie; na baada ya hayo yapasa afunguliwe muda mchache (Ufunuo 20:2, 3).

Ona kwamba kabla ya kufungwa kwake, Shetani “alidaganya mataifa,” lakini atakapofungwa hataweza kuwadanganya tena. Ila, akifunguliwa, atawadanganya tena.

Na hiyo miaka elfu itakapokwisha, Shetani atafunguliwa, atoke kifungoni mwake; naye atatoka kuwadanganya mataifa walio katika pembe nne za nchi … kuwakusanya kwa vita … Wakapanda juu ya upana wan chi, wakaizingira kambi ya watakatifu, na mji huo uliopendwa. Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukawala (Ufunuo 20:7-9. Maneno mepesi kukazia).

Kwa nini Mungu amfungue Shetani kwa muda huo mfupi? Sababu ni kwamba wote wanaomchukia Kristo katika mioyo yao waliokuwa wanajifanya kumtii wakati wa utawala Wake, watadhihirika. Ndipo wataweza kuhukumiwa kihalali. Kitakuwa kipimo cha mwisho hicho.

Kwa sababu hiyo hiyo, Shetani anaruhusiwa kufanya kazi duniani wakati huu – ili wale wanaomchukia Kristo mioyoni mwao waweze kudhihirishwa na hatimaye kuhukumiwa. Mara tu Mungu atakapokuwa hana kazi na Shetani katika kutimiza makusudi Yake ya milele, huyo mdanganyaji atatupwa katika ziwa la moto ili ateswe huko milele (ona Ufunuo 20:10).

Kujiandaa Kwa Ajili Ya Ulimwengu Ujao

Kama umetubu na kuiamini Injili, umekwisha faulu mtihani – kipimo – wa msingi na muhimu sana katika maisha haya. Lakini, usifikiri kwamba hutaendelea kupimwa ili Mungu aweze kuendelea kuona uaminifu wako na msimamo wako unaoendelea. Ni wale tu watakao”dumu katika imani” ndiyo watakaosimama mbele za Mungu “watakatifu, na bila lawama” (Wakolosai 1:22, 23).

Zaidi ya hayo, Maandiko yanaonyesha wazi kwamba sisi sote siku moja tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu, na hapo tutapewa thawabu kibinafsi kulingana na utii wetu duniani. Basi, bado tunapimwa ili kujua kustahili kwetu kupokea thawabu maalum za baadaye katika ufalme wa Mungu. Paulo aliandika hivi:

Lakini wewe je! Mbona wamhukumu ndugu yako? Au wewe je! Mbona wamdharau ndugu yako? Kwa maana sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu. Kwa kuwa imeandikwa, ‘Kama niishivyo, anena Bwana, kila goti litapigwa mbele zangu; na kila ulimi utamkiri Mungu.’ Basi ni hivyo, kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe mbele za Mungu (Warumi 14:10-12. Maneno mepesi kukazia).

Kwa maana imetupasa sisi sote kudhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda kwa mwili, kadiri alivyotenda, kwamba ni mema au mabaya (2Wakor. 5:10).

Basi ninyi msihukumu neno kabla ya wakati wake, hata ajapo Bwana; ambaye atayamulikisha yaliyositirika ya giza, na kuyadhihirisha mashauri ya mioyo; ndipo kila mtu atakapoipata sifa yake kwa Mungu (1Wakor. 4:5. Maneno mepesi kukazia).

Thawabu Zitakuwa Nini?

Sasa – hizo thawabu zitakazotolewa kwa wale watakaothibitisha upendo wao kwa Yesu ni zipi?

Maandiko yanaonyesha aina mbili ya thawabu – kusifiwa na Mungu, na nafasi zaidi ya kumtumikia. Zote zinadhihirishwa katika mfano wa Yesu kuhusu kabaila mmoja.

Basi akasema, “Mtu mmoja, kabaila, alisafiri kwenda nchi ya mbali, ili ajipatie ufalme na kurudi. Akaita watu kumi katika watumwa wake, akawapa mafungu kumi ya fedha, akawaambia, ‘Fanyeni biashara hata nitakapokuja.’ Lakini watu wa mji wake walimchukia, wakatuma wajumbe kumfuata na kusema, ‘Hatumtai huyu atutawale.’ Ikawa aliporudi, ameupata ufalme wake, aliamuru waitwe wale watumwa aliowapa fedha, ili ajue faida aliyopata kila mtu kwa biashara yake. Akaja wa kwanza akasema, ‘Bwana! Fungu lako limeleta faida ya mafungu kumi zaidi.’ Akamwambia, ‘Vema, mtumwa mwema; kwa vile ulivyokuwa mwaminifu katika neno lililo dogo, uwe na mamlaka juu ya miji kumi.’ Akaja wa pili akasema, ‘Bwana! Fungu lako limeleta mafungu matano faida.’ Akamwambia huyu naye, ‘Wewe uwe juu ya miji mitano.’ Akaja mwingine akasema, ‘Bwana! Hili ndilo fungu lako, ambalo nililiweka akiba katika leso. Kwa maana nilikuogopa kwa kuwa u mtu mgumu; waondoa usichoweka, wavuna usichopanda.’ Akamwambia, ‘Nitakuhukumu kwa kinywa chako, mtumwa mwovu wewe. Ulinijua kuwa ni mtu mgumu, niondoaye nisichoweka na kuvuna nisichopanda. Basi, mbona hukuiweka fedha yangu kwa watoao riba, ili nijapo niipate pamoja na faida yake?’ Akawaambia waliosimama karibu, ‘Mnyang’anyeni hilo fungu, mkampe yule mwenye mafungu kumi.’ Wakamwambia, ‘Bwana! Anayo mafungu kumi.’ Nawaambia, ‘Kila aliye na kitu atapewa, bali yule asiye na kitu atanyang’anywa hata alicho nacho. Tena wale adui zangu, wasiotaka niwatawale, waleteni hapa mwachinje mbele yangu’.” (Luka 19:12 – 27).

Bila shaka Yesu anawakilishwa na yule kabaila ambaye hakuwepo, na baadaye akarudi. Wakati Yesu atakaporudi, itabidi tutoe hesabu ya yale tuliyofanya na karama, uwezo, huduma na nafasi alizotupa Yeye, ambazo zinawakilishwa na fungu ambalo kila mtumwa alipewa katika mfano tuliosoma hapo juu. Kama tumekuwa waaminifu, tutapewa thawabu kwa kusifiwa Naye na kupewa mamlaka ya kumsaidia kutawala juu ya nchi (ona 2Timo. 2:12; Ufunuo 2:26, 27; 5:10; 20:6), kama ambavyo kila mtumishi mwaminifu alivyopewa kutawala miji katika mfano tuliosoma.

Jinsi Hukumu Yetu Ya Baadaye Itakavyokuwa Ya Haki

Mfano mwingine ambao Yesu alitoa unaonyesha haki kamilifu ya hukumu yetu ya baadaye.

Kwa maana ufalme wa mbinguni umefananana mtu mwenye nyumba aliyetoka alfajiri kwenda kuajiri wakulima awapeleke katika shamba lake la mizabibu. Naye alipokwisha kupatana na wakulima kuwapa kutwa dinari, aliwapeleka katika shamba lake la mizabibu. Akatoka mnamo saa tatu, akaona wengine wamesimama sokoni wasiokuwa na kazi; na hao nao akawaambia, ‘Enendeni nanyi katika shamba langu la mizabibu, na iliyo haki nitawapa.’ Wakaenda. Akatoka tena mnamo saa sita na saa kenda, akafanya vile vile. Hata kama saa kumi na moja akatoka, akakuta wengine wamesimama. Akawaambia, ‘Mbona mmesimama hapa mchana kutwa bila kazi?’ Wakamwambia, ‘Kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri.’ Akawaambia, ‘Enendeni nanyi katika shamba la mizabibu.’ Kulipokuchwa, yule bwana wa shamba akamwambia msimamizi wake, ‘Waite wakulima uwalipe ujira wao, ukianzia wa mwisho hata wa kwanza.’ Na walipokuja wale wa saa kumi na moja, walipokea kila mtu dinari. Na wale wa kwanza walipokuja, walidhani kwamba watapokea zaidi; na hao pia wakapokea kila mtu dinari. Basi wakiisha kuipokea, wakamnung’unikia mwenye nyumba wakisema, ‘Hao wa mwisho wametenda kazi saa moja tu, nawe umewasawazisha na sisi tuliostahimili taabu na hari za mchana kutwa.’ Naye akamjibu mmoja wao akamwambia, ‘Rafiki! Sikudhulumu. Hukupatana nami kwa dinari? Chukua iliyo yako uende zako; napenda kumpa huyu wa mwisho sawa na wewe. Si halali yangu kutumia vilivyo vyangu kama nipendavyo? Au jicho lako limekuwa ovu kwa sababu ya mimi kuwa mwema?’ Vivyo hivyo wa mwisho watakuwa wa kwanza, na wa kwanza watakuwa wa mwisho (Mathayo 20:1-16).

Hapa, Yesu hakuwa anafundisha kwamba watumishi wote wa Mungu watapokea thawabu ile ile, maana hilo si haki, na pia lingekuwa kinyume cha maandiko mengine mengi (kwa mfano, Luka 19:12-27; 1Wakor. 3:8).

Hapa, Yesu alikuwa anafundisha kwamba kila mtumishi wa Mungu atapata thawabu, si kwa kutegemea alichofanya kwa ajili ya Yesu tu, bali pia kutegemeana na nafasi kiasi gani aliyopewa na Yesu. Watenda kazi kwa muda wa saa moja katika mfano wa Kristo wangefanya kazi kutwa nzima kama wangepewa nafasi ya mwenye shamba. Hivyo, wale waliotumia vizuri nafasi yao ya saa moja walipewa sawa na wale waliopewa nafasi ya kutwa nzima.

Basi – Mungu naye hutoa nafasi tofauti tofauti kwa kila mtumishi Wake. Kwa wengine anawapa nafasi kubwa sana za kutumikia na kubariki maelfu ya watu kwa kutumia karama za ajabu sana alizowapa. Kwa wengine, anatoa nafasi chache nak arama chache pia, lakini wao nao wanaweza kupokea thawabu ile ile mwishoni kama watakuwa waaminifu pia kwa kile ambacho Mungu amewapa.[1]

Hitimisho

Hakuna kitu chamaana kuliko kumtii Mungu, na siku moja kila mtu atajua hilo. Wenye hekima wanajua hilo sasa, na wanafanya kama inavyotakiwa!

Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche Mungu, nawe uzishike amri Zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu. Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya (Mhubiri 12:13, 14).

Mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi humtii Mungu kwa moyo wake wote, na anafanya kila anachoweza kuwahamasisha wanafunzi wake kufanya hivyo hivyo!

Ili kujifunza zaidi kuhusu mada hii muhimu ya hukumu yetu ya baadaye, ona maandiko yafuatayo: Mathayo 6:1-6, 16-18; 10:41, 42; 12:36, 37; 19:28, 29; 25:14-30; Luka 12:2, 3; 14:12-14; 16:10-13; 1Wakor. 3:5-15; 2Timo. 2:12; 1Petro 1:17; Ufunuo 2:26, 27; 5:10; 20:6.


[1] Vile vile huu mfano haufundishi kwamba wale wanaotubu wakiwa na umri mdogo na kuwa waaminifu kwa miaka mingi watapewa thawabu sawa na wale wanaotubu mwaka wa mwisho wa maisha yao na kumfuata Mungu kwa mwaka mmoja tu. Hiyo isingekuwa halali, na isingetegemea nafasi ambazo Mungu alimpa kila mmoja, maana Mungu alitoa kwa kila mmoja nafasi ya kutubu maishani mwao. Basi, wale wanaofanya kazi zaidi watapokea thawabu zaidi kuliko wale wanaofanya kazi kwa muda mfupi.

 

To subscribe to David Servant's periodic e-teachings, click here.


Mchungaji Afanyaye Watu Kuwa Wanafunzi » Mpango Wa Mungu Wa Milele

Maisha Baada Ya Haya

Sura Ya Ishirini Na Saba

 

Wakristo wengi wanajua kwamba watu wanapokufa wanakwenda aidha mbinguni au kuzimu. Si wote wanaotambua kwamba mbinguni si kituo cha mwisho kwa wenye haki, wala kwamba Kuzimu si kituo cha mwisho kwa wasio haki.

Wafuasi wa Yesu Kristo wanapokufa, roho na nafsi zao huenda mbinguni moja kwa moja, mahali anapokaa Mungu (ona 2Wakor. 5:6-8; Wafilipi 1:21-23; 1Wathes. 4:14). Wakati fulani baadaye, Mungu ataumba mbingu mpya na nchi mpya, na Yerusalemu Mpya utashuka kutoka mbinguni kuja duniani (ona 2Petro 3:13; Ufunuo 21:1, 2). Wenye haki wataishi humo milele.

Wakati wasio haki wanapokufa, wanakwenda moja kwa moja mpaka Kuzimu. Hapo ni mahali pa kusubiria tu mpaka miili yao ifufuliwe. Siku hiyo itakapofika, watasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu na baada ya hukumu watatupwa katika ziwa liwakalo moto na kiberiti – Jehanamu katika Biblia. Hayo yote tutayatazama kwa kinaganaga kabisa, tena na Maandiko husika.

Wasio Haki Wanapokufa

Ili tuweze kuelewa vizuri zaidi kinachotokea kwa wasio haki wanapokufa, inabidi tujifunze neno moja la Kiebrania, na maneno matatu ya Kiyunani. Jap ohayo maneno ya Kiebrania na Kiyunani yanaeleza sehemu tatu tofauti, katika Biblia nyingi yanatafsiriwa kuzimu, kitu ambacho kinaweza kuwapotosha wasomaji.

Tuanze kwa kutazama neno la Kiebrania – Sheol katika Agano la Kale.

Neno Sheol linatajwa zaidi ya mara sitini katika Agano la Kale. Linataja waziwazi makao ya wasio haki baada ya kufa. Kwa mfano: Wakati Kora na wafuasi wake walipomwasi Musa nyikani, Mungu aliwahukumu kwa kufunua ardhi, iliyowameza wote na mali zao. Maandiko yanasema waliangukia Sheol.

Basi wao, na wote waliokuwa nao, wakashukia shimoni wali hai; nayho nchi ikawafunika wakaangamia kutoka mle mkutanoni (Hesabu 16:33. Maneno mepesi kukazia).

Baadaye katika historia ya Israeli, Mungu aliwaonya kwamba hasira Yake huwasha moto katika Sheol.

Maana, moto umewashwa kwa hasira yangu, unateketea hata chini ya kuzimu, unakula dunia pamoja na mazao yake, unaunguza misingi ya milima (Kumbu. 32:22. Maneno mepesi kukazia).

Mfalme Daudi alitamka hivi:

Wadhalimu watarejea kuzimu, naam, mataifa yote wanaomsahau Mungu (Zaburi 9:17. Maneno mepesi kukazia).

Kisha aliomba kinyume cha wasio haki, hivi:

Mauti na iwapate kwa ghafula, na washuke kuzimu wangali hai, maana uovu u makaoni mwao na katikati yao (Zaburi 55:15. Maneno mepesi kukazia).

Akiwaonya vijana kuhusu ujanja wa kahaba, Sulemani mwenye hekima aliandika hivi:

Nyumba yake ni njia ya kwenda kuzimu, hushuka mpaka vyumba vya mauti … Lakini huyo hajui ya kuwa wafu wamo humo; ya kuwa wageni wake wamo chini kuzimuni (Mithali 7:27; 9:18. Maneno mepesi kukazia).

Sulemani aliandika mithali zingine zenye kutuongoza tuamini kwamba wenye haki hawatakwenda Sheol.

Kwa mtu mwenye akili njia ya uhai huenda juu, ili atoke katika kuzimu chini (Mithali 15:24. Maneno mepesi kukazia).

[Mtoto wako] Utampiga kwa fimbo, na kumwokoa nafsi yake na kuzimu (Mithali 23:14. Maneno mepesi kukazia).

Mwishowe, akiwahi kabla ya Yesu kutoa maelezo ya kuzimu, Isaya alizungumza kinabii kuhusu mfalme wa Babeli, aliyekuwa amejitukuza sana, na ambaye angetupwa chini hadi Sheol.

Kuzimu chini kumetaharuki kwa ajili yako, ili kukulaki utakapokuja; huwaamsha waliokufa kwa ajili yako, naam, walio wakuu wote wa dunia; huwainua wafalme wote wa mataifa, watoke katika viti vyao vya enzi. Hao wote watajibu na kukuambia, Je! Wewe nawe umekuwa dhaifu kama sisi! Wewe nawe umekuwa kama sisi! Fahari yako imeshushwa hata kuzimu, na sauti ya vinanda vyako; funza wametandazwa chini yako, na vidudu vinakufunika. Jinsi ulivyoanguka kutoka mbinguni, Ewe nyota ya alfajiri, mwana wa asubuhi! Jinsi ulivyokatwa kabisa, ewe uliyewaangusha mataifa! Nawe ulisema moyoni mwako, nitapanda mpaka mbinguni, nitakiinua kiti changu juu kuliko nyota za Mungu; nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano, katika pande za mwisho za kaskazini. Nitapaa kupita vimo vya mawingu, nitafanana nay eye Aliye juu. Lakini utashushwa mpaka kuzimu, mpaka pande za mwisho za shimo. Wao wakuonao watakukazia macho, watakuangalia sana, wakisema, Je! Huyu ndiye aliyeitetemesha dunia, huyu ndiye aliyetikisa falme, aliyeufanya ulimwengu ukiwa, akaipindua miji yake; asiyewafungua wafungwa wake waende kwao? (Isaya 14:9-17. Maneno mepesi kukazia).

Maandiko hayo na mengine yanatufanya tuamini kwamba tangu zamani mpaka sasa, Sheol ni mahali pa mateso ambapo wasio haki hufungiwa baada ya kufa kwao. Bado kuna ushahidi zaidi.

Hades

Ni wazi kwamba neno la Kiyunani – Hades – katika Agano Jipya husema juu ya mahali pale pale panapotajwa na neno la Kiebrania – Sheol – katika Agano la Kale. Ili tuone hili, tunachohitaji kufanya ni kulinganisha Zaburi 16:10 na Matendo 2:27, maana maneno hayo yametumiwa.

Maana hutakuachia kuzimu (Sheol) nafsi yangu, wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu (Zaburi 16:10. Maneno mepesi kukazia).

Kwa maana hutaiacha roho yangu katika kuzimu (Hades); wala hutamtoa Mtakatifu wako aone uharibifu (Matendo 2:27. Maneno mepesi kukazia).

Kama ni hivyo, ni kitu cha kuona kwamba mara zote kumi ambapo kuzimu (Hades) hutajwa katika Agano Jipya, ni mahali pabaya, na mara nyingi husemw akwamba ni mahali pa mateso ambapo waovu hufungiwa baada yakufa (ona Mathayo 11:23; 16:18; Luka 10:15; 16:23; Matendo 2:27; 2:31; Ufunuo 1:18; 6:8; 20:13, 14). Hayo yote huonyesha kwamba Sheol au Hades (kuzimu) ni makao ya wasio haki baada ya kufa – mahali pa mateso.[1]

Je, Yesu Alikwenda Kuzimu (Sheol/Hades)?

Hebu tutafakari zaidi Zaburi 16:10 na jinsi maneno yake yanavyotumiwa na Petro katika Matendo 2:27, mistari miwili yenye kuonyesha kwamba Sheol na Hades ni mahali pale pale. Kulingana na mahubiri ya Petro siku ya Pentekoste, Daudi alikuwa hasemi juu yake mwenyewe katika Zaburi 16:10, bali, kinabii alikuwa anazungumza juu ya Kristo, kwa sababu mwili wa Daudi – kinyume na mwili wa Kristo – uliharibika kabisa (ona Matendo 2:29-31). Kama ndivyo, tunatambua basi kwamba katika Zaburi 16:10, Yesu alikuwa anazungumza na Baba Yake, akitangaza imani Yake kwamba Baba Yake asingeiacha nafsi Yake huko Sheol na kuruhusu mwili Wake upatikane na uharibifu (yaani, uoze).

Kuna wanaotafsiri tamko hilo la Yesu kuwa ni uthibitisho kwamba nafsi Yake ilikwenda Sheol/Hades katika ule muda wa siku tatu kati ya kufa na kufufuka Kwake. Sivyo. Hebu tazama kwa makini maneno ya Yesu kwa Baba Yake.

Maana hutakuachia kuzimu nafsi yangu; wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu (Zaburi 16:10).

Yesu hakumwambia Baba Yake, “Najua nafsi yangu itakaa siku chache huko Sheol/Hades, lakini naamini hutanisahau huko.” Alikuwa anasema hivi, “Ninaamini nitakapokufa, sitatendwa kama wasio haki kwa nafsi yangu kuachwa huko Sheol/Hades. Sitakaa hata dakika moja huko. Ninaamini mpango wako ni kunifufua baada ya siku tatu, nawe hutaruhusu hata mwili wangu kupatikana na uharibifu.”

Hii tafsiri inaweza kuwa sahihi. Wakati Yesu aliposema, “Wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu”, hatumaanishi kwamba mwili wa Yesu uliharibika taratibu kwa siku tatu, mpaka uliporejezwa wakati wa kufufuka Kwake. Tunatafsiri kwamba maana yake ni kwamba mwili Wake haukupatikana na aina yoyote ya uharibifu tangu alipokufa hadi alipofufuka.

Vivyo hivyo, tamko Lake kwamba nafsi Yake isingesahauliwa huko Sheol/Hades halihitaji kutafsiriwa kwamba aliachwa Sheol/Hades kwa siku chache, lakini hakusahauliwa huko moja kwa moja.[2] Badala yake, tafsiri sahihi ni kwamba nafsi Yake isingetendewa kama ya mtu asiye haki, kuachwa huko Sheol/Hades. Nafsi Yake isingekaa huko hata dakika moja. Ona pia kwamba Yesu alisema hivi: “Maana hutakuachia kuzimu nafsi yangu.” Hakusema, “Hutaacha nafsi yangu Kuzimu.”

Nafsi Ya Yesu Ilikuwa Wapi Kwa Zile Siku Tatu?

Kumbuka kwamba Yesu aliwaambia wanafunzi Wake angekaa siku tatu – mchana na usiku – katika tumbo la nchi (ona Mathayo 12:40). Hii haiwezi kumaanisha mwili Wake kuwa kaburini kwa siku tatu maana kaburi haliwezi kuhesabiwa kuwa ni “tumbo la nchi”. Yesu alikuwa anazungumza juu ya roho/nafsi Yake kuwa ndani sana katika nchi. Basi, tunaweza kusema kwamba roho/nafsi Yake havikuwa mbinguni kati ya kufa na kufufuka Kwake. Yesu alithibitisha hilo wakati alipofufuka alipomwambia Mariamu kwamba hajapaa bado kwenda kwa Baba Yake (ona Yohana 20:17).

Usisahau kwamba Yesu pia alimwambia yule mwizi aliyetubu pale msalabani kwamba angekuwa pamoja naye huko Paradiso siku hiyo hiyo (ona Luka 23:43). Tukiunganisha hayo yote, twajua kwamba roho/nafsi ya Yesu ilikaa siku tatu mchana na usiku katika tumbo la nchi, na sehemu fulani ya muda huo alikuwa mahali ambapo Yeye mwenyewe alipaita Paradiso. Hilo si jina lingine la mahali pa mateso paitwapo Sheol au Hades!

Yote hayo yanatuongoza kudhani kwamba lazima kuna mahali pengine katika tumbo la nchi licha ya Sheol/Hades, paitwapo Paradiso. Wazo hili linaungwa mkono na kisa ambacho Yesu alisimulia cha watu wawili waliokufa, mmoja mwenye haki na mwingine asiye haki – tajiri na Lazaro.

Palikuwa na mtu mmoja tajiri, aliyevaa nguo za rangi ya zambarau na kitani safi, na kula sikuzote kwa anasa. Na maskini mmoja jina lake Lazaro, huwekwa mlangoni pake, ana vidonda vingi, naye alikuwa akitamani kushibishwa kwa makombo yaliyoanguka katika meza ya yule tajiri; hata mbwa wakaja wakamramba vidonda vyake. Ikawa yule maskini alikufa, akachukuliwa na malaika mpaka kifuani kwa Ibrahimu. Yule tajiri naye akafa, akazikwa. Basi, kule kuzimu aliyainua macho yake alipokuwa katika mateso, akamwona Ibrahimu kwa mbali, na Lazaro kifuani mwake. Akalia akasema, ‘Ee baba Ibrahimu, nihurumie umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake majini, auburudishe ulimi wangu; kwa sababu ninateswa katika moto huu.’ Ibrahimu akasema, ‘Mwanangu, kumbuka ya kwamba wewe uliyapokea mambo mema yako katika maisha yako, na Lazaro vivyo alipata mabaya; na sasa yeye yupo hapa anafarijiwa, na wewe unaumizwa. Na zaidi ya hayo, kati yetu sisi na ninyi kumewekwa shimo kubwa, ili wale watakao kutoka huku kwenda kwenu wasiweze; wala watu wa kwenu wasivuke kuja kwetu’ (Luka 16:19-26. Maneno mepesi kukazia).

Usisahau kwamba Lazaro na yule tajiri hawakuwa katika miili yao baada ya kufa, lakini walikuwa wamesafiri kwenda mahali pao kama roho/nafsi.

Lazaro Alikuwa Wapi?

Ona kwamba yule tajiri alijikuta yuko Kuzimu. Lakini, aliweza kumwona Lazaro mahali pengine, akiwa na Ibrahimu. Lazaro anasemekana alikuwa “kifuani pa Ibrahimu.” Hilo si jina la mahali penyewe bali pengine ni lugha ya kuonyesha faraja ambayo Lazaro alikuwa anapokea kutoka kwa Ibrahimu, baada ya yeye kufika mahali hapo.

Je, kulikuwa na umbali gani kati ya tajiri na Lazaro, baada ya kufa kwao?

Maandiko yanasema yule mtu tajiri alimwona Lazaro kwa mbali,” na tunaambiwa kwamba lilikuwepo “shimo kubwa” kati yao. Basi, umbali kati yao ni wa kukisiwa tu. Ila, inaonekana ni sawa kudhani kwamba umbali wao haukuwa mkubwa sana kama umbali wa tumbo la nchi na mbinguni. Maana ingekuwa hivyo, isingewezekana kwa tajiri kumwona Lazaro (bila ya msaada wa Mungu), na isingekuwepo haja ya kusema kwamba kuna “shimo kubwa” kati ya maeneo hayo mawili, lililoko makusudi ili kumzuia mtu asivuke kutoka upande mmoja hadi mwingine. Tena, yule mtu tajiri “alipaza sauti yake” kumwita Ibrahimu, na Ibrahimu akamjibu. Basi hii inatufanya tudhani kwamba walikuwa karibu tu kiasi cha kuzungumza.

Yote hayo yanatufanya tuamini kwamba Lazaro hakuwa mahali tunapoita mbinguni bali katika eneo tofauti ndani ya nchi.[3] Bila shaka hapo ndipo Yesu alipaita Paradiso wakati aliposema na yule mwizi aliyetubu. Hiyo paradiso katika tumbo la nchi ndipo wenye haki wa Agano la Kale walikwenda baada ya kuf akwao. Hapo ndipo Lazaro alipokwenda, na ndipo Yesu na yule mwizi aliyetubu walipokwenda.

Bila shaka nabii Samweli alikwenda huko pia baada ya kufa kwake. Tunasoma katika 1Samweli 28 kwamba, wakati Mungu aliporuhusu roho ya Samweli kutokea na kuzungumza na Sauli kinabii, yule mchawi wa Endori alimtaja Samweli kuwa “kama mungu anayepanda kutoka nchi” (1Sam. 28:13. Maneno mepesi kukazia). Samweli mwenyewe alimwambia Sauli hivi: “Mbona umenitaabisha kwa kunipandisha?” (1Sam. 28:15. Maneno mepesi kukazia). Inaonekana roho/nafsi ya Samweli ilikuwa Paradiso katika nchi.

Maandiko ni kama yanaunga mkono wazo kwamba, wakati wa kufufuka kwa Kristo, Paradiso ilifunguliwa na waliokuwemo kutoka, na wenye haki wote waliokufa katika kipindi cha Agano la Kale walipelekwa mbinguni na Yesu. Biblia inasema kwamba wakati Yesu alipopaa mbinguni kutoka pande za mwisho za nchi, “aliteka mateka” (Waefeso 4:8, 9; Zaburi 68:18). Hao mateka bila shaka ni wote waliokuwa wanakaa Paradiso. Yesu hakuwafungua watu kutoka Sheol/Hades![4]

Yesu Alihubiria Roho Zilizokuwa Gerezani

Maandiko pia yanatuambia kwamba Yesu alitangaza kitu fulani kwa kundi la watu – roho za watu – wakati fulani kati ya kufa na kufufuka Kwake. Tunasoma hivyo katika 1Petro 3.

Kwa maana Kristo naye aliteswa mara moja kwa ajili ya dhambi, mwenye haki kwa ajili yao wasio haki, ili atulete kwa Mungu; mwili wake akauawa, bali roho yake akahuishwa, ambayo kwa hiyo aliwaendea roho waliokaa kifungoni, akawahubiri; watu wasiotii hapo zamani uvumilivu wa Mungu ulipokuwa ukingoja, siku za Nuhu, safina ilipokuwa ikitengenezwa; ambamo ndani yake wachache, yaani watu wanane, waliokoka kwa maji (1Petro 3:18-20).

Fungu hili la Maandiko linazua maswali ambayo hayana majibu. Kw anini Yesu aende kutoa tangazo kwa watu wasiotii, waliokufa wakati wa gharika ya Nuhu? Aliwaambia nini?

Pamoja na hayo, andiko hilo linaunga mkono ukweli kwamba Yesu hakukaa siku zote tatu mchana na usiku kati ya kufa na kufufuka Kwake, huko Paradiso.

Jehanamu

Siku hizi, miili ya wenye haki inapokufa, roho/nafsi zao huenda mbinguni moja kwa moja (ona 2Wakor. 5:6-8; Wafilipi 1:21-23; 1Wathes. 4:14).

Wasio haki bado wanakwenda Sheol/Hades, ambapo wanateswa na kusubiri ufufuo wa miili yao, na hukumu yao ya mwisho, na wao kutupwa katika “ziwa la moto”, mahali ambapo ni tofauti na Sheol/Hades.

Hili ziwa la moto linaelezwakwa neno la tatu ambalo wakati mwingine hutafsiriwa kuzimu. Neno hilo ni la Kiyunani – Gehenna. Ni jina linalotokana na mahali pa kutupa takataka nje ya Yerusalemu katika bonde la Hinomu, maali penye uozo mkubwa, penye funza na mabuu, na mahali ambapo daima palitoka moshi na kuwaka moto.

Yesu alipozungumza kuhusu Gehenna, alipataja kama mahali ambapo watu wangetupwa kimwili. Kwa mfano: Alisema hivi katika Injili ya Mathayo:

Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanum [Gehenna]. … Msiwaogope wauuao mwili wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum [Gehenna] (Mathayo 5:30; 10:28. Maneno mepesi kukazia).

Gehenna na Hades si mahali pale pale kwa sababu Maandiko yanasema kwamba wasio haki hupelekwa Hades kama roho/nafsi bila miili. Baada ya miaka elfu moja ya utawala wa Kristo ndipo miili ya wasio haki itakapofufuliwa na kusimama mbele za hukumu ya Mungu, kisha watatupwa katika ziwa la moto, au Gehenna (ona Ufunuo 20:5, 11-15). Tena, siku moja Hades penyewe patatupwa katika hilo ziwa la moto (ona Ufunuo 20:14). Basi, ni mahali tofauti na ziwa la moto.

Tartarus

Neno la nne ambalo mara nyingi hutafsiriwa kuzimu katika Maandiko ni la Kiyunani – tartaros. Linapatikana mara moja tu katika Agano Jipya.

Kwa maana ikiwa Mungu hakuwachilia malaika waliokosa, bali aliwatupa shimoni [tartaros] akawatia katika vifungo vya giza, walindwe hata ije hukumu (2Petro 2:4).

Kikawaida, tartaros hudhaniwa kuwa ni gereza maalum kwa ajili ya malaika fulani waliotenda dhambi. Basi, si Sheol/Hades wala si Gehenna. Hata Yuda anaandika juu ya malaika walio kifungoni, hivi:

Na malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu, amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku ile kuu (Yuda ms. 6).

Ubaya Wa Kuzimu

Mwenye dhambi anapokufa pasipo kutubu, hapati nafasi nyingine ya toba. Mambo yake yanakuwa yamekwisha. Biblia inasema hivi: “Watu wamewekewa kufa mara moja, na baada ya kufa, hukumu” (Waebrania 9:27).

Kuzimu ni kwa milele, na wale waliofungiwa huko hawana matumaini ya kutoka. Yesu alisema hivi kuhusu hukumu ya baadaye ya wasio haki, “Na hao watakwenda katika adhabu ya milele, bali wenye haki watakwenda katika uzima wa milele” (Mathayo 25:46. Maneno mepesi kukazia). Adhabu ya wasio haki huko kuzimu ni ya haki, sawa ambayo uzima wa milele kwa wenye haki ulivyo haki.

Paulo naye aliandika hivi:

Kwa kuwa ni haki mbele za Mungu kuwalipa mateso wale wawatesao ninyi … wakati wa kufunuliwa kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake katika mwali wamoto; huku akiwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasiotii Injili ya Bwana wetu Yesu; watakaoadhibiwa kwa maangamizi ya milele, kutengwa na uso wa Bwana na utukufu wa nguvu zake (2Wathes. 1:6-9. Maneno mepesi kukazia).

Kuzimu ni mahali penye mateso yasiyoelezeka kwa sababu itakuwa adhabu isiyo na mwisho. Wasio haki watabeba hatia yao milele na kuteseka kwa hasira ya Mungu wakiwa wamefungiwa huko milele, katika moto usiozimika.

Yesu alipaelezea huko kama mahali penye “giza la nje,” ambapo kutakuwa na “kilio na kusaga meno,” mahali ambapo “funza wake hawafi, wala moto wake hauzimiki” (Mathayo 22:13; Marko 9:44). Tunahitaji kuwaonya watu kuhusu mahali hapo na kuwaambia juu ya wokovu upatikano katika Kristo tu!

Kuna dhehebu moja linalofundisha dhana ya purgatory – mahali pa utakaso, ambapo waamini watateseka kwa muda ili kusafishwa dhambi zao na kuweza kustahilishwa kuingia mbinguni. Wazo hilo halipatikani popote katika Biblia.

Wenye Haki Baada Ya Kufa

Wakati aaminiye anapokufa, roho yake inakwenda mbinguni mara moja, kwenda kuwa na Bwana. Paulo aliweka wazi jambo hili alipoandika kuhusu kifo chake mwenyewe.

Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo na kufa ni faida. Ila ikiwa kuishi katika mwili, kwangu mimi ni matunda ya kazi; basi nitakalolichagua silitambui. Ninasongwa katikati ya mambo mawili; ninatamani kwenda zangu nikae na Kristo maana ni vizuri zaidi sana (Wafilipi 1:21-23. Maneno mepesi kukazia).

Ona kwamba Paulo alisema anatamani kwenda, na kama akienda, angekuwa na Kristo. Roho yake isingeingia katika hali fulani ya kupoteza fahamu huku akisubiria ufufuo (kama ambavyo wengine hudhani – kwa bahati mbaya sana).

Vile vile ona kwamba Paulo alisema kwake kufa kungekuwa faida. Huo ni ukweli ikiwa angekufa na kwenda mbinguni.

Katika barua yake ya pili kwa Wakorintho, Paulo alitangaza kwamba wakati roho ya aaminiye inapotoka katika mwili, huyo mwamini alikuwa “pamoja na Bwana”.

Basi siku zote tuna moyo mkuu; tena twajua ya kuwa, wakati tuwapo hapa katika mwili, tunakaa mbali na Bwana. … Lakini tuna moyo mkuu; nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana (2Wakor. 5:6-8).

Hoja nyingine yenye kuunga mkono imo katika maneno haya aliyoandika Paulo:

Lakini ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini. Maana, ikiwa twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye (1Wathes. 4:13, 14).

Kama Yesu atakuja na wale “waliolala” kutoka mbinguni, maana yake ni kwamba wako mbinguni pamoja Naye wakati huu.

Fununu Ya Mbinguni

Je, mbinguni pakoje? Kwa akili zetu finyu hatuwezi kupokea kikamilifu utukufu wote unaotungojea huko, na Biblia inatupa fununu kidogo tu. Ukweli wa kusisimua sana kuhusu mbinguni kwa waaminio ni kwamba tutamwona Bwana na Mwokozi wetu Yesu, na Mungu Baba yetu uso kwa uso. Tutakaa “nyumbani mwa Baba”.

Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi nanyi mwepo (Yohana 14:2, 3).

Tutakapofika mbinguni, siri nyingi ambazo akili zetu haziwezi kelewa kwa sasa, zitaeleweka. Paulo aliandika hivi:

Maana wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi ninavyojuliwa sana (1Wakor. 13:12).

Kitabu cha Ufunuo kinatupa picha bora zaidi ya jinsi mbinguni palivyo. Mbinguni hapatakuwa mahali pa watu kuketi tu kwenye mawingu na kupiga vinubi kutwa kucha! Panaelezwa kuwa penye shughuli nyingi, uzuri wa ajabu, tofauti nyingi, na furaha isiyoelezeka.

Yohana ambaye alipata maono ya mbinguni, aliona kwanza kiti cha enzi cha Mungu, ambacho ni kiini cha ulimwengu wote.

Na mara nalikuwa katika Roho; na tazama, kiti cha enzi kimewekwa mbinguni na mmoja ameketi juu ya kile kiti; na yeye aliyeketi alionekana mithili ya jiwe la yaspi na akiki, na upinde wa mvua ulikizunguka kile kiti cha enzi, ukionekana mithili ya zumaridi. Na viti ishirini na vinne vilikizunguka kile kiti cha enzi, na juu ya vile viti naliona wazee ishirini na wanne, wameketi, wamevikwa mavazi meupe; na juu ya vichwa vyao walikuwa na taji za dhahabu. Na katika kile kiti cha enzi kunatoka umeme na sauti na ngurumo. Na taa saba za moto zilikuwa zinawaka mbele ya kile kiti cha enzi, ndizo Roho saba za Mungu. Na mbele ya kile kiti cha enzi kulikuwa na mfano wa bahari ya kioo kama bilauri; na katikati ya kile kiti cha enzi, na pande zote za kile kiti, walikuwako wenye uhai wanne, wamejaa macho mbele na nyuma. Na huyo mwenye uhai wa kwanza alikuwa mfano wa simba; na mwenye uhai wa pili alikuwa mfano wa ndama; na mwenye uhai wa tatu alikuwa na uso kama uso wa mwanadamu; na mwenye uhai wa nne alikuwa mfano wa tai arukaye. Na hawa wenye uhai wanne, kila mmoja alikuwa na mabawa sita; na pande zote na ndani wamejaa macho, wala hawapumziki mchana wala usiku wakisema, Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Bwana Mungu Mwenyezi, aliyekuwako na aliyeko na atakayekuja. Na hao wenye uhai wanapompa yeye aketiye juu ya kiti cha enzi utukufu na heshima na shukrani, yeye aliye hai hata milele na milele, ndipo hao wazee ishirini na wanne huanguka mbele zake yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi, nao humsujudia yeye aliye hai hata milele na milele, nao huzitupa taji zao mbele ya kile kiti cha enzi, wakisema, Umestahili wewe, Bwana wetu na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa (Ufunuo 4:2-11).

Yohana alijitahidi sana kueleza kwa lugha ya mbinguni mambo ambayo hayawezi kulinganishwa na chochote hapa duniani. Ukweli ni kwamba hatuna jinsi ya kuelewa kila kitu alichokiona mpaka tutakapojionea sisi wenyewe. Lakini, inapendeza sana kusoma.

Maelezo ya mbinguni yenye kusisimua sana yanapatikana katika Ufunuo sura ya 21 na 22, mahali ambapo Yohana alieleza kuhusu Yerusalemu Mpya, ambayo kwa sasa iko mbinguni, ila itashuka duniani baada ya kile kipindi cha utawala wa Yesu wa miaka elfu moja.

Akanichukua katika Roho mpaka mlima mkubwa mrefu, akanionyesha ule mji mtakatifu Yerusalemu, ukishuka kutoka mbinguni kwa Mwenyezi Mungu, wenye utukufu wa Mungu, na mwangaza wake ulikuwa mfano wa kito chenye thamani nyingi kama kito cha yaspi, safi kama bilauri. Ulikuwa na ukuta mkubwa, mrefu, wenye milango kumi na miwili, na katika ile milango malaika kumi na wawili. … Na yeye aliyesema nami alikuwa na mwanzi wa dhahabu, apate kuupima huo mji, na milango yake, na ukuta wake. Na ule mji ni wa mraba, na marefu yake sawasawa na mapana yake. Akaupima mji kwa ule mwanzi; ulikuwa kama maili elfu na mia tano; marefu yake na mapana yake na kwenda juu kwake ni sawasawa. … Na majenzi ya ule ukuta wake yalikuwa ya yaspi, na mji ule ulikuwa wa dhahabu safi, mfano wa kioo safi. Na misingi ya ukuta wa mji ilikuwa imepambwa kwa vito vya thamani vya kila namna. … Na ile milango kumi na miwili ni lulu kumi na mbili; kila mlango ni lulu moja. Na njia ya mji ni dhahabu safi kama kioo kiangavu. Nami sikuona hekalu ndani yake; kwa maana Bwana Mungu Mwenyezi na Mwana-Kondoo, ndio hekalu lake. Na mji ule hauhitaji jua wala mwezi kuuangaza, kwa maana utukufu wa Mungu huutia nuru, na taa yake ni Mwana-Kondoo. … Kisha akanionyesha mto wa maji ya uzima, wenye kung’aa kama bilauri, ukitoka katika kiti cha enzi cha Mungu, na cha Mwana-Kondoo, katikati ya njia kuu yake. Na upande huu na upande huu wa ule mto ulikuwapo mti wa uzima, uzaao matunda aina kumi na mbili, wenye kutoa matunda yake kila mwezi; na majani ya mti huo ni ya kuwaponya mataifa. Wala hapatakuwa na laana yoyote tena. Na kiti cha enzi cha Mungu na cha Mwana-Kondoo kitakuwamo ndani yake. Na watumwa wake watamtumikia; nao watamwona uso wake, na jina lake litakuwa katika vipaji vya nyuso zao. Wala hapatakuwa na usiku tena; wala hawana haja ya taa wala ya nuru ya jua; kwa kuwa Bwana Mungu huwatia nuru, nao watatawala hata milele na milele (Ufunuo 21:10 – 22:5).

Kila mfuasi wa Yesu atazamie maajabu hayo yote, mradi atadumu katika imani. Bila shaka tutatumia zile siku za kwanza tukiwa mbinguni kuambiana hivi: “Loo! Kumbe hiki ndicho Yohana alikuwa anajaribu kueleza katika Kitabu cha Ufunuo?”


[1] Kuna wanaojaribu kutoa hoja kwamba Sheol palikuwa mahali ambapo hata wenye haki walikwenda baada ya kufa kwao, kutokana na maandiko machache kama vile Mwanzo 37:35; Ayubu 14:13; Zaburi 89:48; Mhubiri 9:10 na Isaya 38:9, 10. Maandiko hayo hayatoi ushahidi wa kushawishi sana. Kama Sheol palikuwa mahali pa wenye haki na wasio haki kwenda baada ya kufa, basi bila shaka kulikuwa na ‘vyumba’ au maeneo mawili – eneo moja kuzimu, na eneo lingine paradise. Wanaotoa mawazo hayo hufafanua hivyo.

[2] Wale wanaoshikilia tafsiri hii wanalazimika kukubaliana na nadharia mojawapo kati ya mbili. Moja ni kwamba Sheo/Hades lilikuwa jina la makao ya wasio hai na wenye haki baada ya kufa, yaliyokuwa yamegawanywa katika maeneo mawili – mahali pa mateso na mahali pa raha, ambapo Yesu alikwenda. Nadharia ya pili ni kwamba Yesu alivumilia mateso ya wasio haki kwa siku tatu mchana na usiku huko Sheol/Hades katika moto, akipitia kikamilifu kabisa adhabu ya dhambi kama mwakilishi wetu. Nadharia hizo zote ni ngumu kuzithibitisha kutoka Maandiko, na wala si za lazima ikiwa Yesu hakukaa hata kidogo huko Sheol/Hades, ambayo ndiyo maana ya tamko Lake. Kwa habari yanadharia yapili, yesu hakupitia mateso ya wasio haki kwa muda wa siku tatu mchana na usiku kati ya kufa na kufufuka Kwake kwa sababu, ukombozi wetu ulipatikana kwa mateso Yake pale msalabani (ona Wakolosai 1:22), si kwa sababu ya mateso Yake huko Sheol/Hades.

[3] Ona vile vile kwamba Lazaro na tajiri – japo hawako katika miili yao – walikuwa na ufahamu wao kamili pamoja na uwezo wao wa kuona, kugusa na kusikia. Walikuwa wanasikia faraja na maumivu, na kukumbuka mambo yaliyopita. Hii inapingana na nadharia kwamba “nafsi hulala” – hoja kwamba watu huingia katika hali ya kutojua chochote wanapokufa, wakisubiri kuzinduka wakati wa kufufuliwa miili yao.

[4] Kuna wanaodhani – pengine ni sawa – kwamba mateka wanaotajwa katika Waefeso 4:8, 9 ni sisi wote tuliokuwa mateka kwa dhambi, ambao sasa tuko huru kwa sababu ya kufufuka kwa Kristo.

To subscribe to David Servant's periodic e-teachings, click here.


Mchungaji Afanyaye Watu Kuwa Wanafunzi » Maisha Baada Ya Haya

Kufunga

Sura Ya Ishirini Na Sita

 

Kufunga ni tendo la hiari la kuacha kula chakula na kinywaji, au kuacha kinywaji, kwa kipindi fulani.

Biblia imeandika mifano mingi ya watu waliofunga. Wengine waliacha kula vyakula vyote na wengine waliacha kula vyakula fulani tu kwa muda wa mfungo wao. Mfano wa hili la mwisho ni ule mfungo wa Danieli wa majuma matatu, ambao hakula “chakula kitamu … nyama wala divai” (Danieli 10:3).

Vile vile kuna mifano michache katika Maandiko ya watu waliofunga kula chakula na maji, lakini aina hii ya mfungo kamili si wa kawaida, na unatakiwa kuhesabiwa kuwa wa kiMungu ikiwa ulizidi siku tatu. Kwa mfano: Wakati Musa alipokaa siku arobaini bila kula wala kunywa chochote, alikuwa mbele za Mungu Mwenyewe mpaka uso wake uling’aa (ona Kutoka 34:28, 29). Alirudia mfungo wa siku arobaini tena, muda mfupi tu baada ya ule wa kwanza (ona Kumbu. 9:9, 18). Hiyo mifungo yake haikuwa ya kawaida, na si vizuri kwa yeyote kujaribu kuiga. Bila ya msaada wa Mungu, haiwezekani kwa mtu kukaa zaidi ya siku chache bila maji. Kuishiwa maji mwilini husababisha kifo.

Hatari kwa afya si kukaa bila maji kwa muda mrefu tu. Hata kuacha kula chakula kwa vipindi virefu huweza kuwa hatari pia, hasa kwa watu ambao wana matatizo ya chakula tayari. Na hata wenye afya nzuri wanapaswa kuwa makini ikiwa wanapanga kufunga kwa muda mrefu zaidi ya wiki moja.

Kwa Nini Watu Wafunge?

Kusudi la msingi la kufunga ni kujipatia muda wa ziada ili kuomba na kumtafuta Bwana. Ukisoma Biblia, hakuna mahali ambapo kufunga kunatajwa bila kuhusisha maombi. Hiyo inatufanya tuseme kwamba kufunga bila kuomba ni kazi bure. Kwa mfano: Katika kitabu cha Matendo, tunasoma sehemu mbili kuhusu kufunga, na kote maombi yanatajwa. Sehemu ya kwanza (ona Matendo 13:1-3), manabii na waalimu katika kanisa la Antiokia walikuwa “wakimfanyia Mungu ibada na kufunga.” Walipofanya hivyo, wakapokea mafunuo ya kinabii, na kwa sababu hiyo wakamtuma Paulo na Barnaba kwenda safari yao ya kwanza ya kimishenari. Katika sehemu ya pili, Paulo na Barnaba walikuwa wanaweka wazee wa kusimamia makanisa mapya huko Galatia. Tunasoma hivi:

Na walipokwisha kuwachagulia wazee katika kila kanisa na kuomba pamoja na kufunga, wakawaweka katika mikono ya Bwana waliyemwamini (Matendo 14:23).

Pengine katika mfano huu wa pili, Paulo na Barnaba walikuwa wanafuata mfano wa Yesu, maana yeye aliomba usiku kucha kabla ya kuchagua wale Thenashara (ona Luka 6:12). Maamuzi muhimu – kama kuchagua viongozi wa kiroho – yanahitaji kuombewa mpaka mtu awe na uhakika kwamba ameongozwa na Bwana. Kufunga kutatoa nafasi nzuri zaidi ya kuomba kwa habari hiyo. Ikiwa Agano Jipya linashauri wanandoa kuacha kushirikiana kimwili ili kuongeza muda wa kuomba (ona 1Wakor. 7:5), basi ni rahisi kuelewa jinsi ambavyo kuacha chakula kwa muda kutafanikisha kusudi hili hilo.[1]

Basi, tunapohitaji kuomba ili Mungu atuelekeze kwa maamuzi muhimu ya kiroho, kufunga ni kitu cha kufanya. Maombi kwa ajili ya mahitaji mengine yanaweza kufanywa kwa muda mfupi sana. (Mfano: Hatuhitaji kufunga ili kuomba sala ya Bwana.) Maombi kwa ajili ya uongozi yanachukua muda mrefu zaidi kwa sababu ya ugumu wetu wa “kusikia sauti ya Mungu.” Kupata uhakika kuhusu maongozi kunaweza kuhitaji maombi ya muda mrefu, na hapo ndipo kufunga kunapokuwa na faida.

Sababu Mbaya Za Kufunga

Kwa kuwa tumetoa sababu za kiMaandiko za kufunga katika Agano Jipya, hebu tutazame sababu zisizokuwa za Maandiko za kufunga.

Kuna watu ambao wanafunga kwa matumaini kwamba itaongeza uwezekano wa Mungu kujibu maombi yao. Sivyo, maana Yesu alituambia kwamba msingi wa kujibiwa maombi ni imani, si kufunga (ona Mathayo 21:22). Tukumbuke kwamba kufunga hakumbadilishi Mungu hata kidogo. Yeye yuko vile vile kabla hatujafunga, na tunapofunga, na baada ya kufunga. Kufunga si njia ya “kumbana Mungu” au namna ya kumwambia, “Lazima ujibu maombi yangu la sivyo nitafunga mpaka nife!” Huko si kufunga KiBiblia – huko ni kugomea chakula! Kumbuka Daudi alifunga na kuomba kwa siku kadhaa ili yule mtoto wake mgonjwa waliyezaa na Batsheba asife, lakini mtoto alikufa kwa sababu Mungu alikuwa anamwadhibu. Kufunga hakukubadilisha hali yake. Daudi hakuwa anaomba kwa imani kwa sababu hakuwa na ahadi yoyote ya kusimamia. Alikuwa anafunga na kuomba kinyume cha mapenzi ya Mungu, kama matokeo yalivyo-onyesha.

Kufunga si sharti la kupata uamsho, kama wengine wanavyofikiri. Katika Agano Jipya, hakuna mfano wa yeyote akifunga kwa ajili ya uamsho. Badala yake tunawaona mitume wakimtii Yesu kwa kuhubiri Injili. Kama mji haukupokea, walimtii Yesu tena, wakikung’uta mavumbi miguuni pao na kusafiri hadi mji uliofuata (ona Luka 9:5; Matendo 13:49-51). Hawakuketi mahali na kufunga, wakisubiri uamsho.

Vile vile kufunga si njia ya “kutiisha mwili” maana shauku ya kula chakula ni kitu halali na wala si dhambi. Angalia katika Wagalatia 5:19-21 uone orodha ya “tamaa za mwili.” Ila, kufunga ni zoezi la kujitawala – au kiasi – na hiyo ni sifa inayohitajika ili kuenenda katika Roho, si katika mwili.

Kufunga kwa kusudi la kuboresha kiroho chako au kutangaza jinsi unavyompenda Mungu ni kupoteza wakati na ni ishara ya unafiki. Hiyo ndiyo sababu iliyowafanya Mafarisayo kufunga, na Yesu aliwasema kwa hilo (ona Mathayo 6:16; 23:5).

Watu wengine hufunga ili kumshinda Shetani. Hilo nalo si Maandiko. Maandiko yanatuahidi kwamba tukimpinga Shetani kwa imani katika Neno la Mungu, atatukimbia (ona Yakobo 4:7; 1Petro 5:8, 9). Hapo kufunga hakupo.

Lakini, si Yesu alisema kwamba kuna mapepo mengine yasiyotoka “isipokuwa kwa kufunga na kuomba”?

Maneno hayo yalisemwa kwa habari ya kumweka mtu huru kutokana na pepo ililokuwa limempagaa, si kwa habari ya mwamini anayehitaji kupata ushindi juu ya mashambulizi ya Shetani kinyume chake.

Swali: Je, maneno ya Yesu hayaonyeshi kwamba tunaweza kupata mamlaka makubwa zaidi juu ya mapepo kwa kufunga?

Kumbuka kwamba wakati baadhi ya wanafunzi wa Yesu walipomwuliza kwa nini wao walishindwa kumtoa mvulana fulani pepo, kwanza alijibu kwamba ni kwa sababu ya imani yao ndogo (ona Mathayo 17:20). Pengine aliongezea, “Namna hii haiwezeani isipokuwa kwa kufunga na kuomba” (Mathayo 17:21), lakini maneno hayo huenda hayakuwepo katika Injili ya Mathayo – yaliongezwa baadaye.

Ila – hata kama Yesu alisema maneno hayo, tutakosea sana kuamua kwamba kufunga kunaweza kuongeza mamlaka ya mtu juu ya mapepo. Kama Yesu atampa mtu mamlaka juu ya mapepo kama alivyofanya kwa wanafunzi Wake kumi na mbili (ona Mathayo 10:1), basi anayo, na kufunga hakuwezi kuyaongeza. Ila, kufunga kunatoa muda zaidi wa kuomba na kutafakari, na kwa njia hiyo kumwongezea imani katika mamlaka yake aliyopewa na Mungu.

Kumbuka kwamba kama Yesu alisema maneno hayo tunayochambua, yalihusu aina moja tu ya pepo. Kufunga bado kungechukua sehemu ndogo sana katika huduma ya ukombozi kwa ujumla, kama basi kuna sehemu yoyote.

Mkazo Kupita Kiasi Kuhusu Kufunga

Kwa bahati mbaya sana, baadhi ya Wakristo wameunda dini kwa habari ya kufunga, wakitoa mahali pakubwa sana katika maisha yao ya Kikristo kwa jambo hilo. Kufungwa hakutajwi hata mara moja katika nyaraka za Agano Jipya.[2] Hakuna mafundisho yatolewayo kwa waamini kuhusu jinsi ya kufunga, au wafunge lini. Watu hawatiwi moyo kufunga. Hii inatuonysha kwamba kufunga ni sehemu ndogo sana katika kumfuata Yesu.

Inaonekana kwamba wakati wa agano la zamani kufunga kulikuwa na mahali pakubwa zaidi. Mara nyingi kufunga kulihusisha na wakati wa maombolezo – kama mtu akifa au wakati wa toba, na wakati wa maombi ya dhati katika vipindi vya matatizo kitaifa au kibinafsi (ona Waamuzi 20:24-28; 1Sam. 1:7, 8; 7:1-6; 31:11-13; 2Sam. 1:12; 12:15-23; 1Waf. 21:20-29; 2Nyakati 20:1-3; Ezra 8:21-23; 10:1-6; Nehemia 1:1-4; 9:1, 2; Esta 4:1-3, 15-17; Zaburi 35:13, 14; 69:10; Isaya 58:1-7; Dan. 6:16-18; 9:1-3; Yoeli 1:13, 14; 2:12-17; Yona 3:4-10; Zekaria 7:4-5).

Vile vile, Agano la Kale linafundisha kwamba kuheshimu sana kufunga na kupuuza kutii amri za muhimu zaidi kama vile kuwajali maskini, ni makosa (ona Isaya 58:1-12; Zekaria 7:1-14).

Bwana Yesu ambaye alifanya huduma Yake wakati wa agano la zamani hawezi kusemwa kwamba yeye alitilia mkazo kufunga kupia kiasi. Alishtakiwa na Mafarisayo kwa kutotilia mkazo wa kutosha (ona Mathayo 9:14, 15). Aliwasema wao kwa kutilia mkazo kupita kiasi (ona Luka 18:9-12).

Lakini pia, Yesu alizungumza na wafuasi Wake kuhusu kufunga, katika mahubiri Yake ya Mlimani. Aliwaagiza wafunge kwa sababu sahihi, akionyeshakwamba aliwatazamia wafuasi Wake kufunga nyakati fulani fulani. Pia aliahidi kwamba Mungu angewapa thawabu kwa sababu ya kufunga kwao. Yeye Mwenyewe alifunga kwa kiasi fulani (ona Mathayo 17:21).

Mtu Afunge Muda Gani?

Mifungo yote ya siku arobaini iliyoandikwa katika Biblia si ya kawaida. Tayari tumetazama habari za Musa na mifungo yake miwili ya siku arobaini, akiwa mbele za Mungu. Eliya vile vile alifunga siku arobaini, lakini kabla ya hapo aliletewa chakula na malaika (ona 1Waf. 19:5-8). Pia, kuna mambo yasiyokuwa ya kawaida kuhusu mfungo wa Yesu wa siku arobaini. Yeye aliongozwa na Roho Mtakatifu kiajabu sana kwenda nyikani. Alipata majaribu yasiyo ya kawaida, kutoka kwa Shetani, alipokaribia mwisho wa mfungo wake. Pia, alitembelewa na malaika alipomalizia mfungo Wake (ona Mathayo 4:1-11).

Ingawa inawezekana kwa watu wengine kufunga kwa siku arobaini pasipo msaada wa Mungu, wengi wanaweza kuwa wanahatarisha afya zao. Mifungo ya siku arobaini si kawaida ya KiBiblia.

Mtu akiacha mlo mmoja kwa hiari yake mwenyewe kwa kusudi la kupata wakati wak umtafuta Bwana, amefunga. Wazo kwamba kipimo cha mifungo ni siku husika ni kosa.

Ile mifungo miwili katika Kitabu cha Matendo tuliyokwisha taja (ona Matendo 13:1-3; 14:23) haikuwa ya muda mrefu. Yawezekana ilikuwa ni mlo mmoja tu.

Kwa kuwa kusudi la kufunga ni kupata muda wa kumtafuta Bwana katika maombi kwa habari ya uongozi Wake, ushauri unaofaa ni kwamba, funga muda wote unaohitaji, mpaka upate mwongozo unaohitaji kwa uwazi. Kumbuka: Kufunga hakumlazimishi Mungu kusema na wewe. Kufunga kunaweza kuboresha usikivu wako kwa Roho Mtakatifu. Mungu anasema na wewe ukifunga na usipofunga. Ugumu tulio nao sisi ni kupambanua maongozi Yake na shauku zetu.

Ushauri Muhimu

Kwa kawaida, kufunga huathiri mwili kwa njia mbalimbali. Mtu anaweza kujisikia udhaifu, uchovu, kichwa kuuma, hali ya kutaka kutapika, kujisikia kulewa, tumbo kuuma na kadhalika. Kama mtu amezoea kunywa kahawa, chai, au vinywaji aina hiyo, baadhi ya mambo yaliyotajwa hapo mbele yanaweza kutokana na kutotumia vitu hivyo katika muda wa mfungo. Kama ni hivyo, ni vizuri kwa watu kama hao kuanza kuacha kutumia vinywaji hivyo siku chache kabla ya mfungo wao. Mtu akizoea kufunga mara kwa mara, atagundua kwamba inakuwa rahisi kufunga kadiri anavyoendelea, japo atajisikia udhaifu fulani.

Mifungo imalizwe polepole, na kama mfungo ulikuwa mrefu, basi mtu awe makini sana kwamba anamalizaje. Kama tumbo la mtu halijasaga chakula kigumu kwa muda wa siku tatu, si vizuri kwake kufungua kwa kula vyakula vigumu. Anapaswa kuanza na vyakula rahisi kusagwa – au vyepesi. Mifungo mirefu inahitaji muda mrefu zaidi kwa tumbo kuanza kuzoea vyakula tena, lakini ukiacha mlo mmoja au miwili huna haja ya kipindi kirefu cha kumaliza mfungo.


[1] Tafsiri nyingi za zamani za 1Wakorintho 7:5 zinaruhusu waume na wake kuacha kuhusiana kimwili ili waweze kujitoa zaidi kwenye “kufunga na kuomba.” Katika tafsiri za kisasa za mstari huu, neno kufunga halipo.

[2] Mahali pekee ni pale Paulo anapotaja kuhusu kufunga kwa wenye ndoa, katika 1Wakor. 7:5, japo hata hapo inategemeana na tafsiri fulani fulani. Kufunga kwa lazima kunatajwa katika Matendo 27:21, 33, 34; 1Wakor. 4:11 na 2Wakor. 6:5; 11:27. Kufunga katika mistari hii hakukuwa kwa sababu za kiroho, bali kwa sababu hali zilikuwa ngumu au kwa sababu hakukuwa na chakula.

To subscribe to David Servant's periodic e-teachings, click here.


Mchungaji Afanyaye Watu Kuwa Wanafunzi » Kufunga

Kukabili Mtu, Msamaha Na Upatanisho

Sura Ya Ishirini Na Nne

 

Tulipojifunza Mahubiri ya Yesu pale Mlimani katika sura fulani iliyotangulia, tulijifunza jinsi ilivyo muhimu kwamba tuwasamehe wale wanaotukosea. Tusipowasamehe, Yesu alisema wazi kwamba Mungu hatatusamehe (ona Mathayo 6:14, 15).

Sasa basi – nini maana ya kumsamehe mtu? Hebu tutazame Maandiko yanavyofundisha.

Yesu alifananisha msamaha na tendo la kumfutia mtu deni lake (ona Mathayo 18:23-35). Hebu fikiri: Una mtu unayemdai, kisha unamfungua, kwamba asikulipe. Unapasua karatasi iliyokuwa imeandikwa deni lake. Hutazamii kulipwa tena, nawe umeacha hasira na mdeni wako. Unamwona kitofauti kuliko ilivyokuwa wakati bado unamdai.

Tutaelewa vizuri tena maana ya kusamehe kama tutatafakari maana ya kusamehewa na Mungu. Wakati Yeye anapotusamehe sisi dhambi fulani, hatuhesabu kuhusika tena kwa kile tulichofanya, kilichomchukiza. Haendelei kuwa na hasira nasi kwa sababu ya dhambi ile. Hatatuadhibu wala kutuhukumu kwa tulichofanya. Tunakuwa tumepatanishwa Naye.

Vivyo hivyo basi, kama kweli nitamsamehe mtu fulani, ninamweka huru mtu huyo moyoni mwangu, nikishinda shauku ya kutafuta haki au kisasi kwa kuonyesha rehema. Sina hasira tena na mtu aliyenitenda dhambi. Tunakuwa tumepatanishwa. Kama ninaweka hasira au uchungu dhidi ya mtu fulani, ni kwamba sijamsamehe.

Mara nyingi Wakristo hujidanganya wenyewe katika swala hili. Wanasema wamemsamehe mtu, wakijua kwamba hivyo ndivyo wanavyotakiwa kufanya, lakini bado wana kitu ndani yao kuhusu aliyewakosea. Wanamkwepa mkosaji kwa sababu inasababisha ile hasira iliyofunikwa kutokea tena. Ninajua hayo maana ha ta mimi nimewahi kufanya hivyo. Tusijidanganye. Kumbuka kwamba Yesu anatukataza hata kumkasirikia mwamini mwenzetu (ona Mathayo 5:22).

Sasa – Tujiulize swali hili: Ni yupi aliye rahisi kusamehe – ni mkosaji anayeomba msamaha au ni mkosaji asiyeomba msamaha? Bila shaka sote tutakubaliana kwamba ni rahisi zaidi kumsamehe mkosaji anayekiri kosa lake na kuomba msamaha. Ni ukweli kwamba ni rahisi zaidi sana kumsamehe mtu anayeomba msamaha kuliko mtu ambaye haombi. Kumsamehe mtu asiyetaka kusamehewa huonekana kama kitu kisichowezekana.

Hebu tulitazame kwa upande mwingine. Kama kukataa kumsamehe mkosaji anayetubu na kama kukataa kumsamehe mkosaji asiyetubu ni makosa, dhambi kuu zaidi hapo ni ipi? Nadhani tutakubaliana kwamba kama vyote viwili ni kosa, basi kukataa kumsamehe mkosaji anayetubu ni uovu mkubwa zaidi.

Cha Kushangaza Kutoka Maandiko

Hayo yaliyotangulia yanasababisha swali lingine – Je, Munguanatazamia tumsamehe kila mtua nayetukosea, hata wale wasiojinyenyekeza na kukiri dhambi yao na kuomba msamaha?

Tukitazama Maandiko kwa karibu tutagundua kwamba jibu ni “Hapana.” Wakristo wengi watashangaa kujua kwamba, Maandiko yanaweka wazi kuwa ingawa tunaagizwa kumpenda kila mtu, hatutakiwi kumsamehe kila mtu.

Kwa mfano: Je, Yesu anatazamia sisi tumsamehe mwamini mwenzetu anayetukosea? Hapana. Vinginevyo, asingetuambia kufuata zile hatua nne za upatanisho zilizo katika Mathayo 18:15-17, ambazo mwisho wake ni kutengwa, kama mkosaji hatatubu.

Na ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye wewe na yeye peke yenu. Akikusikia, umempata nduguyo. La kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja au wawili, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike. Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa, na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru.

Ni kwamba, ikiwa hatua ya nne itafikiwa (ya kutengwa), msamaha hautolewi kwa mkosaji, maana msamaha na kutengwa ni vitu visivyoambatana. Ingekuwa kitu cha ajabu kumsikia mtu akisema hivi: “Tulimsamehe, kisha tukamtenga.” Maana, kusamehe huishia kwenye upatanisho, sio kutengana. (Jiulize: Ungefikiriaje kama Mungu angesema, “Ninakusamehe, lakini hatuna mahusiano na wewe kuanzia leo”?) Yesu alituambia huyo aliyetengwa awe kama “mtu wa Mataifa na mtoza ushuru,” aina mbili za watu ambao Wayahudi hawakushirikiana nao kabisa, tena waliwakwepa.

Katika zile hatua nne ambazo Yesu alitaja, msamaha hautolewi katika hatua ya kwanza, ya pili au ya tatu mpaka mkosaji atubu. Asipotubu baada ya kila hatua, anapelekwa hatua inayofuata, akiwa bado anahesabiwa kama mkosaji asiyetubu. Tunaambiwa kwamba “akikusikia” (yaani, akitubu), ndipo “umempata nduguyo” (yaani, mmepatanishwa tena).

Kusudi la kukabiliana na mtu ni ili msamaha utolewe. Ila, msamaha unategemeana na toba ya mkosaji. Basi, (1) tunamkabili mtu kwa matumini kwamba kama mkosaji, yeye ata (2) tubu ili sisi tuweze (3) kumsamehe.

Pamoja na hayo yote, tunaweza kusema kwa hakika kwamba Mungu hatutazamii sisi kuwasamehe waamini wenzetu kirahisi tu ambao wametukosea, na ambao hawana toba, hata baada ya kukabiliwa. Lakini pia, hii haitupi sisi haki ya kumchukia mwamini aliyekosea. Kinyume ni kwmaba tunamkabili kwa sababu tunampenda mkosaji, na tungetaka kumsamehe na kupatanishwa naye.

Ila, baada ya kila juhudi kufanyika kufuata zile hatua tatu ambazo Yesu alitaja, hat ua ya nne inakomesha mahusiano yetu, kama tutatii maneno ya Kristo.[1] Kama ambavyo hatupaswi kushirikiana na wanaojiita Wakristo ambao ni wazinzi, walevi, walawiti na kadhalika (ona 1Wakor. 5:11), hatupaswi kushirikiana na wanaojiita Wakristo ambao wanakataa kutubu kulingana na makubaliano ya kusanyiko lote. Watu kama hao wanathibitisha kwamba si wafuasi wa kweli wa Kristo, nao wanaleta aibu kwa kanisa Lake.

Mfano Wa Mungu

Tunapoendelea kutafakari wajibu wetu wa kuwasamehe wengine, tunaweza pia kujiuliza hivi: Kwa nini Mungu atazamie sisi tufanye kitu ambacho Yeye Mwenyewe hafanyi? Hakika Mungu anawapenda wakosaji, na anawanyooshea mikono Yake ya rehema katika toleo la kuwasamehe. Anazuia hasira Yake na kuwapa muda wa kutubu. Lakini kusamehewa kwao hutegemeana na kutubu kwao. Mungu hasamehi wenye hatia wasipotubu kwanza. Basi, mbona sisi tudhanie kwamba ana matazamio makubwa zaidi kwetu?

Pamoja na hayo – hivi haiwezekani kwamba dhambi ya kutosamehe ambayo ni mbaya sana machoni pa Mungu ni ile dhambi ya kutowasamehe wale wanaotuomba msamaha? Mara tu baada ya Yesu kutaja zile hatua nne za kutoa adhabu kanisani, Petro aliuliza hivi:

Bwana! Ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba? (Mathayo 18:21, 22).

Je, Petro alifikiri kwamba Yesu alikuwa anamtazamia kumsamehe ndugu asiyetubu mara mia nyingi kwa ajili ya dhambi mia nyingi, wakati Yesu alikuwa amemwambia tu muda mfupi uliopita kwamba amhesabu ndugu asiyetubu kama mtu wa Mataifa au mtoza ushuru kwa sababu ya dhambi moja tu? Haiwezi kuwa hivyo. Tunarudia tena: huwezi kumtenga mtu au kumhesabu asiyefaa kushirikiana naye kama umemsamehe.

Swali lingine la kutufanya tufikiri ni hili: Kama Yesu anatutazamia kumsamehe mwamini mara mia nyingi kwa sababu ya dhambi mia nyingi ambazo hatubu, ili kudumisha uhusiano wetu, mbona anaturuhusu kuvunja ndoa kwa sababu ya dhambi moja tu kinyume chetu – dhambi ya uasherati – kama mwenzetu katika ndoa hatatubu (ona Mathayo 5:32)?[2] Hili halionekani kuwa na mantiki.

Ufafanuzi Zaidi

Mara tu baada ya Yesu kumwambia Petro amsamehe ndugu mara mia arobaini na tisa, alisimulia mfano ili kumsaidia Petro aelewe maana yake.

Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake. Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi. [Kiwango hicho ni sawa na mshahara wa zaidi ya miaka elfu tano kwa kibarua katika siku za Yesu.] Naye alipokosa cha kulipa, Bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, ikalipwe ile deni. Basi yule mtumwa akaanguka akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni. Mtumwa hule akatoka, akamwona mmoja wa wajoli wake aliyemwia dinari mia [sawa na mshahara wa siku mia moja]. Akamkamata, akamshika koo akisema, Nilipe uwiwacho. Basi mjoli wake akaanguka miguuni pake, akamsihi akisema, Nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Lakini hakutaka. Akaenda, akamtupa kifungoni hata atakapoilipa ile deni. Basi wajoli wake walipoyaona yaliyotendeka, walisikitika sana, wakaenda wakamweleza bwana wao yote yaliyotendeka. Ndipo bwana wake akamwita, akamwambia, Ewe mtumwa mwovu! Nalikusamehe wewe deni ile yote uliponisihi. Nawe je! Haikukupasa kumrehemu mjoli wako kama mimi nilivyokurehemu wewe? Bwana wake akaghadhibika, akampeleka kwa watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote. Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake (Mathayo 18:23-35).

Ona kwamba yule mtumwa wa kwanza alisamehewa kwa sababu alimwomba bwana wake msamaha. Kisha, ona kwamba yule wa pili naye alimwomba msamaha yule mtumwa wa kwanza kwa unyenyekevu sana. Yule wa kwanza hakumpa yule wa pili kile alichokuwa amepewa yeye, na hicho ndicho kilichomkasirisha sana bwana wake. Kama ni hivyo, kweli Petro angedhani kwamba Yesu anamtazamia amsamehe ndugu asiyetubu, ambaye hakuomba msamaha? Kitu hicho hakionekani katika mfano wa Yesu. Basi, haiwezekani, na zaidi sana, kwa sababu Yesu alikuwa amekwisha tangulia kumwambia jinsi ya kufanya na ndugu asiyetubu baada ya kukabiliwa ipasavyo – awe kwake kama mtu wa Mataifa, na mtoza ushuru.

Haiwezekani kwamba Petro alidhani alitazamia kumsamehe ndugu asiyetubu kwa sababu ya hukumu ambayo Yesu alituabudi kama ha tutawsamehe ndugu zetu kutoka mioyoni mwetu. Yesu aliahidi kurudisha deni lote tulilokuwa tumesamehewa kwanza, na kutukabidhi kwa watesaji mpaka tulipe kile tusichoweza kulipa. Je, hiyo ingekuwa ni adhabu halali kwa ndugu Mkristo asiyemsamehe ndugu, ndugu ambaye hata Mungu hatamsamehe? Kama ndugu akinikosea, anamkosea Mungu, na Mungu hatamsamehe mpaka atubu. Je, Mungu ataniadhibu mimi kwa haki kwa kutomsamehe mtu ambaye hata Yeye hamsamehi?

Ufupisho

Matarajio ya Yesu kwetu kumsamehe mwamini mwenzetu yanatajwa katika maneno Yake yanayopatikana katika Luka 17:3-4.

Jilindeni! Kama ndugu yako akikosa, mwonye. Akitubu msamehe. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe (Maneno mepesi kukazia).

Tunataka iwe wazi kuliko hivyo? Yesu anatutazamia kuwasamehe waamini wenzetu, wakati wanapotubu. TUnapoomba na kusema, “Utusamehe deni zetu kama nasi tunavyowasamehe wadeni wetu” tunamwomba Mungu atutendee kama ambavyo na sisi tumewatendea wengine. Hatutazamii Yeye atusamehe kama hatutaomba. Basi, mbona sisi tudhani kwamba anatutazamia kuwasamehe wale wasio-omba?

Hapo tena, hayo yote hayatupi sisi kibali cha kuwa na chuki kinyume cha ndugu au dada katika Kristo aliyetukosea. Tunaagizwa kupendana. Hiyo ndiyo sababu tunaagizwa kumkabili mwamini anayetenda dhambi kinyume chetu, ili kuwepo na upatanisho kati yetu, na ili naye aweze kupatanishwa na Mungu, ambaye anakuwa amemkosea pia. Upendo ungefanya hivyo. Lakini mara nyingi, Wakristo watasema wamemsamehe mwamini mwanzao aliyekosea, lakini utagundua kwamba ni njia tu ya kuepuka kukabiliana naye. Ukweli ni kwamba hawasamehi, na inaonekana kwa matendo yao. Wanamkwepa mkosaji kwa gharama yoyote, na mara nyingi wanasema jinsi walivyoumizwa. Hakuna upatanisho hapo.

Tunapofanya dhambi, Mungu hutukabili kwa Roho Wake Mtakatifu ndani yetu kwa sababu anatupenda na anataka kutusamehe. Tunapaswa kumwiga Yeye, tukiwakabili kwa upendo waamini wenzetu wanaotenda dhambi kinyume chetu ili kuwepo toba, msamaha na kupatana.

Mungu kila mara amewatazamia watu Wake kupendana kwa upendo wa kweli – upendo unaoruhusu kukemea, lakini usioruhusu kuwa na kinyongo. Katika Torati ya Musa utakuta sheria ifuatayo:

Usimchukie ndugu yako moyoni mwako; ni lazima kumkemea jirani yako, wala usichukue dhambi kwa ajili yake. Usifanye kisasi, wala kuwa na kinyongo juu ya wana wa watu wako, bali umpende jirani yako kama nafsi yako. Mimi ndimi BWANA (Walawi 19:17, 18. Maneno mepesi kukazia).

Pingamizi

Lakini – vipi kuhusu maneno ya Yesu katika Marko 11:25, 26? Je, hayaonyeshi kwamba lazima tuwasamehe wote kwa kila kitu, bila kujali kwamba ameomba msamaha au hapana?

Nanyi kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu, ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. [Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu.]

Huu mstari mmoja haukanushi mistari ile mingine yote ambayo tumemkwisha tazama kuhusu mada hii. Tunajua tayari kwamba, kilicho kibaya zaidi sana kwa Mungu ni sisi kukataa kumsamehe mtu anayetuomba msamaha. Basi, tunaweza kutafsiri mstari huu kulingana na kweli hiyo thabiti. Yesu hapa anatilia mkazo tu kwmaba lazima tuwasamehe wengine kama tunataka msamaha wa Mungu. Hatuambii utaratibu ili tusamehewe, na kitu ambacho mtu anapaswa kufanya ili kuupokea kutoka kwa mwingine.

Ona pia kwamba Yesu hasemi hapa kwamba lazima tumwombe Mungu msamaha ili tuweze kuupokea kutoka kwake. Kama ni hivyo, ina maana tupuuze kila kitu kingine ambacho Maandiko yanafundisha juu ya msamaha wa Mungu kutegemea sisi kumwomba (ona Mathayo 6:12; 1Yohana 1:9)? Je, tudhanie tu kwamba hatuhitaji kuomba Mungu atusamehe tunapotend adhambi kwa sababu Yesu hasemi hilo hapa? Hapo ni kutokuwa na busara, kulingana na tunachojifunza katika Maandiko. Pia, si busara kupuuza kila kitu kingine ambacho Maandiko yanafundisha kuhusu sisi kuwsamehe wengine kuwa kumejengwa juu ya wao kuomba msamaha.

Pingamizi Nyingine

Je, Yesu hakuwaombea wale askari waliokuwa wanagawana mavazi yao kwamba, “Baba! Uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo” (ktk Luka 23:34)? Je, hiyo haionyeshi kwamba Mungu huwasamehe watu bila wao kumwomba?

Ndiyo, kwa kiwango fulani tu. Inaonyesha kwamba Mungu huwahurumia watu wasiojua – ni kiwango fulani cha msamaha. Kwa kuwa Mungu ni mwenye haki kabisa, anawawajibisha watu wakati wanapojua kwamba wanatenda dhambi.

Sala ya Yesu kwa ajili ya wale askari haikuwahakikishia kuingia mbinguni. Iliwalinda tu wasiwajibishwe kwa ajili ya kugawana mavazi ya Mwana wa Mungu, na ni kwa sababu wao hawakumjua Yeye ni nani. Walimhesabu kuwa ni mhalifu mwingine tu anayestahili kuuawa. Basi, Mungu aliwahurumia kwa tendo ambalo lingestahili hukumu ya hakika, kama wangejua walichokuwa wanafanya.

Vivyo hivyo, sisi tunapaswa kuwaonea huruma watu wasiojua kile walichotutendea, kama wale askari wasioamini na wasiojua, waliogawana mavazi ya Yesu. Yesu anatutazamia kuwaonyesha wasioamini rehema ya ajabu sana, na kuwapenda adui zetu, na kuwatendea mema wale wanaotuchukia, na kuwabariki wale wanaotulaani na kuwaombea wale wanaotutendea mabaya (ona Luka 6:27, 28). Tunapaswa kujaribu kuyeyusha chuki yao kwa upendo wetu, na kushinda ubaya kwa wema. Jambo hili lilielezwa hata katika Torati ya Musa, kama ifuatavyo:

Ukimwona ng’ombe wa adui wako au punda wake amepotea, sharti umrudishie mwenyewe tena. Ukimwona punda wake huyu akuchukiaye hali ameanguka chini yamzigo wake, nawe untejizuia usimsaidie, lazima umsaidie (Kutoka 23:4, 5).

Adui yako akiwa ana njaa, mpe chakula. Tena akiwa ana kiu, mpe maji ya kunywa. Maana utatia makaa ya moto kichwani pake; na BWANA atakupa thawabu (Mithali 25:21, 22).

Inashangaza kwamba, ingawa Yesu alituamuru tuwapende adui zetu, tuwatendee mema wanaotuchukia, tuwabariki wanaotulaani, na tuwaombee wanaotuonea (ona Luka 6:27, 28), hakutuambia tuwasamehe. Tunaweza kuwapenda watu bila kuwasamehe – sawa tu na ambavyo Mungu anawapenda watu bila kuwasamehe. Si tu kwamba tunaweza kuwapenda, tunapaswa kuwapenda, maana ni amri ya Mungu kwamba tufanye hivyo. Na upendo wetu kwao unapaswa kuonekana kwa matendo yetu.

Kwa kuwa Yesu alimwomba Baba Yake awasamehe wale askari waliokuwa wanagawana nguo zake, si uthibitisho kwamba tunapaswa kupuzia kila kitu kingine tulichojifunza kutoka Maandiko kwa habari ya mada hii, na kumsamehe kila mtu aliyetukosea. Tunachojifunza hapo ni kwamba tunapaswa kuwasamehe bila kusita wale wasiojua dhambi yao dhidi yetu, na kuonyesha rehema na huruma ya ajabu sana kwa wasioamini.

Kutenda Mathayo 18:15-17

Ingawa zile hatua nne za upatanisho zilizotajwa na Yesu ni rahisi kueleweka, zinaweza kuwa ngumu kutekeleza. Wakati Yesu alipozitaja hizo hatua nne, alifanya hivyo kutokana na mtazamo wa ndugu A kuwamini – sawasawa kabisa – kwamba ndugu B amemkosea. Ila, kihalisi, Ndugu A anaweza kuwa amekosea. Hebu basi tubuni hali ambayo kila uwezekano unatazamwa.

Kama ndugu A anaamini kwamba ndugu B amemkosea, anatakiwa kwanza ahakikishe kwamba haingii kwenye kulaumu sana, akitafuta kibanzi katika jicho la ndugu B. Makosa mengine madogo yanapaswa kupuuzwa tu na huruma kuonyeshwa (ona Mathayo 7:3-5). Ila, kama ndugu A akijisikia kuudhika na ndugu B kwa sababu ya kosa kubwa la maana, basi amkabili.

Anapaswa kufanya hivyo kibinafsi, akitii agizo la Yesu, na kuonyesha upendo wake kwa ndugu B. Kusudi lake liwe upendo na lengo lake upatanisho. Hapaswi kumwambia mtu mwingine yeyote juu ya kosa hilo. “Upendo husitiri wingi wa dhambi” (1Petro 4:8). Tukimpenda mtu hatufunui dhambi zake; tunazisitiri.

Sasa – anapomkabili mwenzake, awe mpole, akionyesha pendo lake. Atumie maneno kama haya: “Ndugu B. Kweli nathamini sana uhusiano wetu. Lakini kuna kitu kimetokea ambacho kimejenga ukuta moyoni mwangu juu yako. Sitaki ukuta huo uwepo, na ndiyo maana nimeona ni vizuri nikwambia kwamba umenikosea, ili tuone tutafanyaje kupatana. Na kama mimi nimefanya chochote kilichochangia tatizo hilo kuwepo, naomba uniambie.” Kisha, amwambie ndugu B kwa upole kabisa kosa ni nini.

Mara nyingi utakuta kwamba ndugu B wala hakujua kwamba aalimkosea ndugu A, na mara baada ya kufahamu kwamba amemkosea, atamwomba msamaha. Kama itakuwa hivyo, ndugu A anapaswa kumsamehe ndugu B hapo hapo. Upatanisho umetokea.

Mfano mwingine ni kwamba ndugu B anaweza kujaribu kutetea dhambi yake dhidi ya ndugu A kwa kumwambia kwamba yeye alikuwa anaitikia kosa lililokuwa limekwisha tendwa na ndugu A. kama ni hivyo, ndugu B alitakiwa kuwa amekwisha mkabili ndugu A. Pamoja na hayo, tayari kuna mazungumzo na matumaini hapo ya kupatana.

Katika hali kama hiyo, wahusika wanapaswa kuzungumza yaliyotokea, wakubali makosa kila mmoja kulingana na hali halisi, kisha wapeane na kupokea msamaha kila mmoja toka kwa mwenzake. Tayari wamekwisha patana.

Mfano wa tatu ni A na B wameshindwa kupatana. Hapo wanahitaji msaada, na ni wakati wa kupiga hatua ya pili.

Hatua ya Pili

Itakuwa vizuri ndugu A na B wakubaliane juu ya nani aongezeke ili kuwasaidia kupatana. Inafaa ndugu C na D wawe wanaowajua na kuwapenda ndugu A na B, maana hiyo itahakikisha kwamba hakuna upendeleo. Tena, ndugu C na D waambiwe juu ya kutoelewana huko kwa sababu ya ndugu A na B kupendwa na kuheshimiwa tu.

Kama ndugu B hatatoa ushirikiano hapa, ni juu ya ndugu A kutafuta mtu mmoja au wawili wanaoweza kusaidia.

Kama ndugu C na D wana busara, hawatatoa uamuzi mpaka wasikie kutoka kwa A na B. Baada ya ndugu C na D kutoa uamuzi wao, A na B wanapaswa kukubaliana na uamuzi wao na kuomba msamaha na kufanya chochote kitakachopendekezwa kwa mmoja wao, au kwa wote.

Ndugu C na D hawapaswi kujionyesha kwamba hawapendelei upande wowote na kwamba hawataki kujihusisha kwa kutoa ushauri kwamba ndugu A na B wote wanahitaji kutubu, huku ni mmoja tu anayehitaji kutubu. Wanapaswa kujua kwamba kama ndugu A au B watakataa uamuzi wao, mambo yatafika mbele ya kanisa lote, na uamuzi wao wa uoga utadhihirika kwa kila mtu. Hili jaribu linalowakabili ndugu C na D kutaka kutunza urafiki na ndugu A na B kwa kukataa kusimamia ukweli ni sababu nzuri ya waamuzi wawili kuwa bora kuliko mmoja, maana watatiana nguvu katika ukweli. Tena, uamuzi wao utakuwa na uzito zaidi kwa ndugu A na B.

Hatua Ya Tatu

Ikiwa yeyote kati ya ndugu A na B atakataa uamuzi wa ndugu C na D, jambo hilo lifikishwe mbele ya kanisa zima. Hii hatua ya tatu haifanywi katika makanisa jengo – na ni kwa sababu nzuri tu – maana ingesababisha kanisa kugawanyika kutokana na watu kujiunga upande mmoja au mwingine. Yesu hakukusudia makanisa yawe makubwa kuliko nyumba za watu. Katika kusanyiko dogo kama familia ambapo kila mmoja anajua na kujali juu ya ndugu A na B ndipo hatua ya tatu inapokusudiwa. Katika kanisa kubwa lenye watu wengi, hatua ya tatu inatakiwa kuchukuliwa katika kundi dogo la watu wanaowajua ndugu A na B na kuwapenda. Kama ndugu A na B ni washirika wa makundi tofauti, basi kiasi fulani cha washirika wanaofaa kutoka makundi yote mawili wahusike kama baraza litakalofanya maamuzi.

Baada ya kanisa kutoa uamuzi wake, ndugu A na B wanapaswa kuukubali, wakijua matokeo ya kukataa. Samahani zitolewe, misamaha itolewe na upatanisho ufanywe.

Kama ndugu A au B atakataa kufanya inavyotakiwa, atengwe na kanisa, na mtu yeyote katika kanisa asishirikiane naye tena. Mara nyingi ikifikia hapo, mtu asiyetubu anakuwa amekwisha jiondoa mwenyewe kwa hiari yake, na labda anakuwa amefanya hivyo muda mrefu tu kabla, ikitokea kwamba hakupata alichotaka katika hatua yoyote. Hii huonyesha kutokuwa tayari kwake kujitoa kwa dhati kuipenda familia yake ya kiroho.

Tatizo La Kawaida

Katika makanisa makubwa, mara nyingi watu hutatua matatizo yao kwa kuhama kutoka kanisa moja hadi lingine – mahali ambapo mchungaji, anayetaka kujenga ufalme wake kwa gharama yoyote, na ambaye hana mahusiano halisi na wachungaji wengine, huwakaribisha watu kama hao na kuungana nao wanapomweleza hadithi zao za kusikitisha. Jambo hili huua kabisa nguvu za hatua za Yesu kuhusu upatanisho. Na kwa kawaida, baada ya miezi michache tu au miaka, yule mtu aliyekosewa ambaye hukaribishwa katika makanisa ya wachungaji aina hiyo, anahama tena, kwenda kutafuta kanisa lingine, maana huku nako amekosewa.

Yesu alitazamia kwamba makanisa yangekuwa madogo kiasi cha kutosha katika nyumba, na kwamba wachungaji wa mahali/wazee/waangalizi wangekuwa wanafanya kazi pamoja kwa ushirika katika mwili mmoja. Hivyo, kutengwa kwa mshirika mmoja katika kanisa moja kungekuwa ni kutengwa kwake katika makanisa yote. Ni wajibu wa kila mchungaji/mzee/mwangalizi kuwaomba Wakristo wote wahamiaji habari kuhusu makanisa waliyotoka, kisha kuwasiliana na uongozi wa makanisa hayo ili kuamua kama watu aina hiyo wakaribishwe au hapana.

Kusudi La Mungu – Kuwa Na Kanisa Takatifu

Tatizo lingine la kawaida la makanisa jengo ni kwamba washirika wao wengi ni watu wanaohudhuria tu kwa ajili ya mambo yanayofanywa hapo. Hawataki sana kuwajibika kwa yeyote kwa sababu mahusiano yao ni ya kijamii san asana. Basi, hakuna yeyote – hata wachungaji – anayejua jinsi wanavyoishi maisha yao – na watu wasiokuwa wataka tifu wanaendelea kuleta doa kwa makanisa wanayohudhuria. Watu wa nje huwapima watu wanaowaona kuwa Wakristo kuwa si tofauti na wasioamini kwa lolote.

Hili peke yake inapaswa kuwa uthibitisho wa kutosha kwa yeyote kwamba, mfumo wa makanisa kama shirika si kusudi la Mungu kwa ajili ya kanisa Lake takatifu. Watu wasiokuwa watakatifu na wanafiki hujificha daima katika makanisa makubwa, wakisababisha jina la Kristo kutukanwa. Lakini, kutokana na tuliyosoma katika Mathayo 18:15-17, Yesu alikusudia kanisa Lake kuwa lenye watu watakatifu, viungo waliojitolea kabisa wa mwili wenye kujitakasa. Dunia ingetazama kanisa na kumwona bibi arusi wa Kristo akiwa safi. Lakini siku hizi, tunaona kahaba mkuu, mke asiyekuwa mwaminifu kwa Mume wake.

Hii hali ya kujisafisha iliyokusudiwa na Mungu kwa ajili ya kanisa inaonyeshwa wazi wakati Paulo anaposhughulika na swala fulani zito katika kanisa la Korintho. Mshirika aliyekubaliwa katika kanisa hilo alikuwa anaishi na mke wa baba yake katika mahusiano ya uzinzi.

Habari imeenea ya kuwa kwenu kuna zinaa, na zinaa ya namna isiyokuwako hata katika Mataifa, kwamba mtu awe na mke wa babaye. Nanyi mwajivuna, wala hamkusikitika, ili kwamba aondolewe miongoni mwenu huyo aliyetenda jambo hilo. Kwa maana kweli nisipokuwako kwa mwili, lakini nikiwapo kwa roho, mimi mwenyewe nimekwisha kumhukumu yeye aliyetenda jambo hilo, kana kwamba nikiwapo. Katika jina la Bwana wetu Yesu, ninyi mkiwa mmekusanyika pamoja na roho yangu, pamoja na uweza wa Bwana wetu Yesu; kumtolea Shetani mtu huyo, ili mwili uadhibiwe, ili na roho iokolewe katika siku ya Bwana Yesu. … Naliwaandikia katika waka wangu kwamba msichangamane na wazinzi. Sisemi msichangamane kabisa na wazinzi wa dunia hii, au na wenye kutamani, au na wanyang’anyi, au na wenye kuabudu sanamu; maana hapo ingewalazimu kutoka katika dunia. Lakini mambo yalivyo, naliwaandikia kwamba msichangamane na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye. Maana yanihusu nini kuwahukumu wale walio nje? Ninyi hamwahukumu hao walio ndani? Lakini hao walio nje Mungu atawahukumu. Ninyi mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu (1Wakor. 5:1-5; 9-13).

Hapakuwepo na haja ya kumpitisha mtu huyu katika zile hatua za upatanisho kwa sababu hakuwa mwamini wa kweli. Paulo anamwita “mtu aitwaye ndugu”, na “mbaya yule”. Halafu katika mistari michache baadaye aliandika hivi:

Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi (1Wakor. 6:9-10).

Ni wazi kwamba Paulo aliamini – na ni sahihi kabisa – kwamba wale wasiokuwa safi, kama yule mtu katika kanisa la Korintho, huonyesha jinsi wasivyokuwa watu wa imani. Watu kama hao wasitendewe kama ndugu na kupitishwa katika zile hatua nne za kupatanishwa. Wanapaswa kutengwa, “kukabidhiwa kwa Shetani,” ili kanisa lisije likakuza kujidanganya kwao, na wawe na tumaini la kuona haja yao ya kutubu ili kuweza “kuokolewa katika siku ya Bwana Yesu” (1Wakor. 5:5).

Katika makanisa makubwa duniani siku hizi, utakuwa watu mia kadhaa wanaojifanya kuwa Wakristo ambao, kwa viwango vya Manadiko si waamini, na wanapaswa kutengwa. Maandiko yanatuonyesha wazi wazi kabisa kwamba kanis alina wajibu wa kuwaondoa miongoni mwake wale ambao ni waasherati, wazinzi, walawiti, walevi na kadhalika. Lakini watu kama hao, chini ya bendera ya “neema” siku hizi wanakumbatia kwamba ni “waamini wanaojikongoja”, na kuwekwa katika makundi ya usaidizi, ambamo wanaweza kutiwa moyo na “waamini” wenzao wenye matatizo kama hayo. Hili ni tusi na kejeli kwa uwezo wa Injili ya Yesu Kristo, inayobadilisha maisha.

Viongozi Walioanguka

Mwisho: Je, kiongozi aliyetubu arudishwe mara moja kwenye nafasi yake, kama alikuwa katika dhambi kubwa sana (kama uasherati)? Ingawa Bwana atamsamehe mara moja huyo kiongozi mwenye kutubu (na kanisa linapaswa kufanya vivyo hivyo), kiongozi huyo anakuwa amekwisha poteza imani kwa wale anaowahudumia. Kuaminika ni kitu ambacho lazima kukifanyia kazi. Basi, viongozi walioanguka wajiondoe wenyewe kwenye nafasi zao za uongozi na kukaa chini ya uangalizi kiroho mpaka wathibitishe kuaminika kwao. Lazima waanze tena. Wale ambao hawako tayari kujinyenyekeza na kufanya shughuli ndogo ndogo ili kuweza kuaminika tena, wasikubalike kama viongozi na mtu yeyote katika kusanyiko.

Hitimisho

Kama watumishi wanaofanya wengine kuwa wanafunzi, walioitwa “kukaripia, kukemea na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho” (2Timo. 4:2), hebu tusiogope kutekeleza wito wetu. Hebu tufundishe wanafunzi wetu kupendana kweli kweli kwa kuvumiliana na kuchukuliana kwa huruma siku zote, kwa kukabiliana kwa upole ikibidi, na kukabiliana zaidi kwa msaada wa wengine inapobidi, na kwa kusamehe kila inapohitajika. Hivi ni vizuri zaidi kuliko msamaha wa uongo ambao hauleti uponyaji wa kweli katika mahusiano yaliyoharibika. Tena, tujitahidi sana kumtii Bwana katika kila eneo, ili kutunza kanisa Lake katika hali ya usafi na ut akatifu, ili liwe sifa kwa jina Lake!

Ukitaka kujifunza zaidi kuhusu makabiliano na nidhamu kanisani, soma maandiko yafuatayo: Warumi 16:17, 18; 2Wakor. 13:1-3; Wagalatia 2:11-14; 2Wathes. 3:6, 14, 15; 1Timo. 1:19, 20; 5:19, 20; Tito 3:10, 11; Yakobo 5:19, 20; 2Yohana ms. 10 na 11.


[1] Ni halali kusema kwamba, kama yule aliyetengwa atatubu baadaye, Yesu anatazamia msamaha utolewe kwake.

[2] Kama mwenzi mwasherati ni Mkristo, tunapaswa kumpitisha katika zile hatua tatu ambazo Yesu alizitoa kwa ajili ya upatanisho, kabla ya kufikia kwenye kuachana. Huyo mwenzi akitubu, tunatazamiwa kusamehe, kulingana na agizo la Yesu.

To subscribe to David Servant's periodic e-teachings, click here.


Mchungaji Afanyaye Watu Kuwa Wanafunzi » Kukabili Mtu, Msamaha Na Upatanisho

Nidhamu Itolewayo Na Bwana

Sura Ya Ishirini Na Tano

 

Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu. Hamjafanya vita hata kumwagika damu, mkishindana na dhambi. Tena, mmeyasahau yale maonyo yasemayo nanyi kama kusema na wana, ‘Mwanangu! Usiyadharau marudia ya Bwana, wala usizimie moyo ukikemewa naye. Maana yeye ambaye Bwana ampenda, humrudi, naye humpiga kila mwana amkubaliye. ‘ Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili, Mungu awatendea kama wana. Maana, ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? Basi kama mkiwa hamna kurudiwa, ambako ni fungu la wote, ndipo mmekuwa wana wa haramu ninyi, wala si wana wa halali. Na pamoja na hayo, tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi. Basi, si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi? Maana ni hakika, hao kwa siku cahche waliturudi kama walivyoona vema wenyewe; bali yeye kwa faida yetu, ili tuushiriki utakatifu wake. Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani. Kwa hiyo inyosheni mikono iliyolegea na magoti yaliyopooza, mkaifanyie miguu yenu njia za kunyoka, ili kitu kilicho kiwete kisipotoshwe, bali afadhali kipone (Waebrania 12:3-13).

Kulingana na mwandishi aliyevuviwa wa Kitabu cha Webrania, Baba yetu wa mbinguni huwaadhibu watoto Wake wote. Tusipoadhibiwa Naye, maana yake ni kwamba sisi si watoto Wake. Basi tunahitaji kuwa makini na kujua kuhusu adhabu Zake. Kuna Wakristo wengine ambao mtazamo wao wa peke ni baraka za Mungu na wema Wake tu, wanaotafsiri mazingira yote ambayo ni kinyume kuwa ni mashambulizi toka kwa Shetani, yasiyokuwa na mpango wowote wa kiMungu. Hili linaweza kuwa kosa kubwa sana, kama Mungu anajaribu kuwafikisha kwenye toba kwa kutumia adhabu Zake.

Wazazi wazuri wa kidunia hutoa adhabu kwa watoto wao kwa matumaini kwamba hao watajifunza, watakomaa na kuwa tayari kuwa watu wazima wenye kuwajibika maishani. Mungu pia hutuadhibu ili tukue kiroho, tufae katika huduma Yake zaidi, na tuwe tayari kusimama mbele ya kiti Chake cha hukumu. Anatuadhibu kwa sababu anatupenda, na kwa sababu anatamani tushiriki utakatifu Wake. Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anataka sana tukue kiroho. Maandiko yanasema hivi: “Nami niliaminilo ndilo hili, ya kwamba yeye aliyeanza kazi njema mioyoni mwenu ataimaliza hata siku ya KristoYesu” (Wafilipi 1:6).

Hakuna mtoto anayefurahia viboko vya wazazi wake. Na sisi, tunapoadhibiwa na Mungu, jambo hilo “si la furaha bali la huzuni” kama tulivyosoma. Ila mwishowe, mambo yanakuwa mazuri kwa sababu nidhamu (au adhabu hiyo) “husababisha tunda la amani la haki”.

Je, Mungu Hutuadhibu Lini, Kwa Njia Gani?

Kama baba mzuri, Mungu huwaadhibu watoto Wake wakati wanapoacha kutii. Wakati wowote tunapoacha kumtii, tuko hatarini kuadhibiwa. Ila, Bwana ni mwenye rehema sana, naye mara nyingi hutupa muda mrefu wa kutubu. Adhabu yake mara nyingi huja baada ya sisi kurudia kutokutii, na Yeye kutuonya mara nyingi.

Je, Mungu anatuadhibu namna gani? Kama tulivyojifunza katika sura mojawapo huko nyuma, adhabu ya Mungu inaweza kuja kama udhaifu fulani, ugonjwa au hata kufa kabla ya wakati.

Kwa sababu hiyo wako wengi kwenu walio hawawezi na dhaifu, na watu kadha wa kadha wamelala. Lakini kama tungejipambanua nafsi zetu, tusingehukumiwa. Ila tuhukumiwapo, twarudiwa na Bwana, isije ikatupasa adhabu pamoja na dunia (1Wakor. 11:30-32).

Hatupaswi kuamua kwamba kila ugonjwa ni matokao ya adhabu ya Mungu (hapa kumbuka swala la Ayubu). Lakini, ugonjwa ukija, ni vizuri kufanya ukaguzi kiroho ili kuona kama labda tumefungua mlango wa adhabu ya Mungu kwa kutokutii.

Twaweza kuepukana na hukumu ya Mungu kama tutajihukumu wenyewe – yaani, tukiri dhambi yetu na kuitubu. Ni dhahiri kwamba tutajikuta tunaponywa mara tu baada ya kutubu, ikiwa ugonjwa wetu ni matokeo ya adhabu ya Mungu.

Paulo anasema kwamba tunapohukumiwa na Mungu, tunaepuka kuhukumiwa pamoja na dunia. Je, alimaanisha nini? Bila shaka alimaanisha kwamba adhabu ya Mungu hutuongoza sisi kutubu ili hatimaye tusitupwe jehanamu pamoja na watu wa dunia. Hili ni gumu kukubalika na wale wanaofikiri kwamba utakatifu ni kitu cha hiari kwa wale wanaokwenda mbinguni. Lakini, kwa wale waliosoma Mahubiri ya Yesu Mlimani, wanajua kwamba wale tu wanaomtii Mungu ndiyo watakaoingia katika ufalme Wake (ona Mathayo 7:21). Basi, tukidumu katika dhambi na tusitubu, tuko hatarini kukosa uzima wa milele. Bwana asifiwe kwa adhabu Yake, inayotuongoza kutubu, na kutuokoa na jehanamu!

Shetani Kama Chombo Kwa Ajili Ya Hukumu Ya Mungu

Ni dhahiri kutokana na maandiko mengi kwamba Mungu anaweza kumtumia Shetani kwa ajili ya kutimiza adhabu Zake. Kwa mfano: Katika mfano wa mtumwa asiyesamehe upatikanao katika Mathayo 18, Yesu anasema kwamba bwana wa mtumwa yule “akaghadhabika sana” baada ya kufahamu kwamba mtumwa wake aliyemsamehe hakumsamehe mwenzake. Basi, akamtoa kwa “watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote” (Mathayo 18:34). Yesu alimalizia mfano huu kwa maneno haya mazito:

Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake (Mathayo 18:35).

Sasa – hao “watesaji” ni akina nani? Inaonekana ni Shetani na mapepo yake. Mungu anaweza kumtoa mmoja wa watoto Wake wasiokuwa watiifu kwa Shetani, ili kumfikisha mahali pa kutubu. Magumu na majanga yana njia ya kuwafikisha watu kutubu – kama alivyojifunza mwana mpotevu (ona Luka 15:14-19).

Katika Agano la Kale tunapata mifano ya Mungu akimtumia Shetani au pepo wabaya ili kutimiza adhabu Yake au hukumu katika maisha ya watu waliostahili hayo. Mfano mmoja unapatikana katika Waamuzi sura ya tisa, tunaposoma kwamba, “Kisha Mungu akapeleka roho mbaya kati ya Abimeleki na watu wa Shekemu” (Waamuzi 9:23) ili kuleta hukumu juu yao kwa sababu ya matendo yao maovu juu ya wana wa Gidioni.

Biblia pia inasema, “roho mbaya kutoka kwa Bwana” ilimsumbua mfalme Sauli ili kumfikisha kwenye toba (1Sam. 16:14). Ila, Sauli hakutubu, na mwishoni alikufa vitani kwa sababu ya uasi wake.

Katika mifano hiyo miwili ya Agano la Kale, Manadiko yanasema hizo roho mbaya (au pepo) “zilitumwa na Mungu.” Hii haimaanishi kwamba Mungu ana pepo mbinguni wanaosubiri kumtumikia. Pengine ni kwamba Mungu anaruhusu mapepo wa Shetani kufanya kazi yao mbaya kwa watu, kwa mipaka, kwa matumaini kwamba wenye dhambi watatubu kwa sababu ya mateso yao.

Njia Zingine Za Adhabu Ya Mungu

Katika Agano la Kale pia tunakuta kwamba Mungu aliwaadhibu watu Wake mara kwa mara kwa kuruhusu matatizo kama njaa au majeshi ya kigeni kutawala. Hatimaye wangetubu, Naye angewakomboa na adui zao. Walipokataa kutubu baada ya miaka mingi ya mateso na maonyo, Mungu alikuwa anaruhusu utawala wa kigeni kuwashinda kabisa na kuwahamisha kutoka nchi yao kama mateka.

Katika agano jipya, inawezekana kabisa Mungu kuwaadhibu watoto Wake wasiotii kwa kuruhusu matatizo kuingia maishani mwao. Au anaweza kuruhusu maadui zao kuwatesa. Kwa mfano: Maandiko tuliyoanza nayo sura hii kuhusu adhabu ya Mungu (Waebrania 12:3-13), yanapatikana katika mantiki ya waamini wa Kiebrania waliokuwa wanateswa kwa ajili ya imani yao. Ila, si mateso yote yanayoruhusiwa kwa sababu ya kutokutii. Kila jambo lipimwe peke yake.

Kuitikia Vizuri Adhabu Ya Mungu

Kulingana na ushauri uliotajwa mwanzoni mwa sura hii, tunaweza kuitikia vibaya adhabu ya Mungu kwa namna mojawapo kati ya hizi mbili. Tunaweza “kudharau marudia ya Bwana” au tunaweza “kuzimia moyo tukikemewa naye” (Waebrania 12:5). Kama tuta”dharau” marudia ya Bwana, maana yake ni kwamba hatuitambua adhabu yake, au ni kwamba tunapuuzia maonyo yake. Kuzimia moyo kutokana na adhabu ya Mungu ni kukata tamaa au kuacha kumpendeza kwa sababu tunaona adhabu Yake ni kali sana. Itikio lolote katika hayo ni kosa. Tunapaswa kutambua kwamba Mungu anatupenda, naye hutuadhibu kwa faida yetu. Tukitambua mkono Wake wa upendo katika adhabu, tunapaswa kutubu na kupokea msamaha Wake.

Baada ya kutubu, tutazamie nafuu kutoka kwa adhabu ya Mungu. Lakini, tusitazamie nafuu kutokana na matokeo mabaya na yasiyoepukika ya dhambi yetu, ingawa tunaweza kumwomba Bwana rehema na msaada Wake. Mungu huitikia moyo mnyenyekevu na uliopondeka (ona Isaya 66:2). Biblia inaahidi hivi, “Maana ghadhabu zake ni za kitambo kidogo, katika radhi yake mna uhai. Huenda kilio huja kukaa usiku, lakini asubuhi huwa furaha” (Zaburi 30:5).

Baada ya hukumu Yake kuwashukia Israeli, Mungu aliahidi hivi:

Kwa kitambo kidogo nimekuacha; lakini kwa rehema nyingi nitakukusanya. Kwa ghadhabu ifurikayo nalikuficha uso wangu dakika moja; lakini kwa fadhili za milele nitakurehemu (Isaya 54:7, 8).

Mungu ni mwema, na mwenye rehema!

Kwa kujifunza zaidi kuhusu adhabu ya Mungu, ona maandiko yafuatayo: 2Nyakati 6:24-31, 36-39; 7:13, 14; Zaburi 73:14; 94:12, 13; 106:40-46; 118:18; 119:67, 71; Yeremia 2:29, 30; 5:23-25; 14:12; 30:11; Hagai 1:2-13; 2:17; Matendo 5:1-11; Ufunuo 3:19.

To subscribe to David Servant's periodic e-teachings, click here.


Mchungaji Afanyaye Watu Kuwa Wanafunzi » Nidhamu Itolewayo Na Bwana

Ibada Maalum

Sura Ya Ishirini Na Tatu

Yesu alitoa ibada maalum mbili tu kwa kanisa: ubatizo wa maji (ona Mathayo 28:19) na Meza ya Bwana (ona 1Wakor. 11:23-26). Tujifunze kuhusu ubatizo wa maji kwanza.

Katika agano jipya, kila aaminiye anapaswa kubatizwa mara tatu tofauti, kama ifuatavyo: ubatizo wa kuingia katika mwili wa Kristo; ubatizo wa maji, na ubatizo wa Roho Mtakatifu.

Mtu anapozaliwa mara ya pili, anabatizwa ili kuingia katika mwili wa Kristo. Yaani, anafanyika kiungo katika mwili wa Kristo ambao ni kanisa.

Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja (1Wakor. 12:13. Ona pia Warumi 6:3; Waefeso 1:22, 23; Wakolosai 1:18, 24).

Kubatizwa katika Roho Mtakatifu ni kitu kinachofuata wokovu, na ubatizo huu ni kwa ajili ya kila aaminiye.

Mwisho – kila mwamini anapaswa kubatizwa katika maji mara tu inapowezekana, baada ya kutubu na kumwamini Bwana Yesu. Ubatizo unapaswa kuwa tendo la kwanza la utii katika maisha ya mwamini mpya.

[Yesu] Akawaambia, Enendeni ulimwengu mwote mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa (Marko 16:15, 16. Maneno mepesi kukazia).

 

Kanisa la kwanza lilihesabu amri ya Yesu kuhusu kubatiza kuwa ya muhimu sana. Karibu kila mara, waamini wapya walibatizwa mara moja baada ya kuokoka kwao (ona Matendo 2:37-41; 8:12-16; 36-39; 9:17-19; 10:44-48; 16:31-33; 18:5-8; 19:1-5).

Mawazo Kinyume Cha Biblia Kuhusu Ubatizo

Kuna wanaobatiza kwa kumnyunyuzia mwongofu mpya matone kidogo tu ya maji. Je, ni sahihi? Neno batiza katika Agano Jipya linatokana na neno la Kiyunani baptize, ambalo maana yake halisi ni “kufunika kwa maji, kuzamisha.” Basi, wale wanaobatizwa kw amaji wanatakiwa kuzamishwa ndani ya mani, si kudondoshewa matone machache tu. Maana ya ubatizo wa Kikristo ambayo tutajifunza punde tu, inaunga mkono pia wazo la kuzamishwa katika maji.

Kuna wengine wanaobatiza watoto wachanga. Hakuna mifano ya maandiko kuhusu kubatizwa kwa watoto katika Biblia. Desturi hiyo inatokana na mafundisho ya uongo kuhusu “ubatizo kuokoa” – wazo kwamba mtu huzaliwa mara ya pili anapobatizwa. Maandiko yanafundisha wazi kabisa kwamba watu wanapaswa kumwamini Yesu kwanza kabla ya kubatizwa. Hivyo, watoto wakubwa kidogo, na wenye uwezo wa kutubu na kumfuata Yesu wanastahili kubatizwa – si watoto wachanga au hata wadogo.

Kuna wanaofundisha kwamba, ingawa mtu anaweza kumwamini Yesu, hajaokoka mpaka abatizwe. Kulingana na Maandiko, hiyo si kweli. Katika Matendo 10:44-48 na 11:17, tunasoma kwamba watu wa nyumbani mwake Kornelio waliokolewa na kubatizwa kwa Roho Mtakatifu kabla hawajabatizwa katika maji. Ni kwamba haiwezekani yeyote abatizwe kwa Roho Mtakatifu kama hajaokoka kwanza (ona Yohana 14:17).

Kuna wanaofundisha kwamba kama mtu asipobatizwa kulingana na utaratibu wao, hajaokoka. Maandiko hayatoi utaratibu fulani kiibada ambao unapaswa kufuatwa, ili uwe ubatizo sahihi au halali. Kwa mfano: Kuna wanaosema mwamini anatakiwa kubatizwa “katika jina la Yesu” (Matendo 8:16). Wanadai kwamba mtu akibatizwa “kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu” (Mathayo 28:19) hajaokoka. Watu hao wanaonyesha roho ile ile ambayo iliwatawala Mafarisayo – wanachuja mbu na kumeza ngamia. Ni huzuni ilioje kwamba Wakristo wanahojiana kuhusu maneno yanayofaa kusemwa wakati wa ubatizo, huku dunia inasubiri kusikiliza Injili.

Maana Ya Ubatizo Kimaandiko

Ubatizo wa maji ni mfano wa vitu vingi ambavyo vinakuwa vimekwisha tokea katika maisha ya mwamini. Kimsingi, ni mfano kwamba tumesafishwa dhambi zetu, na sasa tunasimama mbele za Mungu tukiwa safi. Wakati Anania alipotumwa kwa Sauli (au Paulo) mara tu alipo-okoka, alimwambia hivi:

Basi sasa, unakawilia nini? Simama ubatizwe, ukaoshwe dhambi zako, ukiliitia jina lake (Matendo 22:16. Maneno mepesi kukazia).

Pili – Ubatizo wa maji ni mfano wa sisi kujitambulisha na Kristo katika kufa Kwake, kuzikwa na kufufuka. Tukiisha zaliwa mara ya pili na kuwekwa katika mwili wa Kristo, tunaanza kuhesabiwa kuwa “katika Kristo” tangu wakati huo na kuendelea. Kwa sababu Yesu alituwakilisha, Mungu anatuhesabia yote aliyofanya Yesu. Basi, “katika Kristo” tumekufa, tumezikwa na tumefufuliwa ili kuishi kama watu wapya kabisa.

Hamfahamu ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika mauti Yake? Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi tuenende katika upya wa uzima (Warumi 6:3, 4).

Mkazikwa pamoja naye katika ubatizo; na katika huo mkafufuliwa pamoja naye kwa kuziamini nguvu za Mungu aliyemfufua katika wafu (Wakolosai 2:12).

Kila mwamini mpya anapaswa kufundishwa kweli hizi muhimu sana wakati anapobatizwa kwa maji, naye anapaswa kubatizwa mara moja baada ya kumwamini Yesu.

Meza Ya Bwana

Meza ya Bwana asili yake ni katika Sikukuu ya Pasaka ya Agano la Kale. Usiku ule Mungu alipowakomboa Israeli kutoka utumwani Misri, aliagiza kila nyumba kuchinja mwana-kondoo wa umri wa mwaka mmoja na kuinyunyiza damu yake kwenye miimo ya milango ya nyumba zao. Wakati “malaika wa kifo” alipopita katika taifa hilo usiku ule, akiua wazaliwa wa kwanza wote katika Misri, angeiona damu kwenye nyumba za Waisraeli, na “kupita juu yake.”

Tena, Waisraeli walitakiwa kusherehekea sikukuu usiku huo kwa kumla mwanakondoo wao wa Pasaka na pia kwa kula mkate usiotiwa chachu kwa siku saba. Hili lilikuwa agizo la kudumu kwa Waisraeli, na ni kitu cha kufanyika kila mwaka wakati huo huo (ona Kutoka 12:1-28). Ni dhahiri kwamba mwana-kondoo wa Pasaka alikuwa mfano wa Kristo, anayeitwa “Pasaka wetu” katika 1Wakoirntho 5:7.

Wakati Yesu alipoanzisha Meza ya Bwana, Yeye na wanafunzi Wake walikuwa kwenye Sherehe ya Pasaka. Yesu alisulubiwa wakati wa Pasaka, na kwa njia hiyo kutimiza kikamilifu wito Wake kama “Mwanakondoo wa Mungu, azichukuaye dhambi za dunia” (Yohana 1:29).

Ule mkate tunaokula na maji ya matunda tunayokunywa ni mfano wa mwili wa Yesu, uliovunjwa kwa ajili yetu, na damu yake, iliyomwagika kwa ajili ya ondoleo la dhambi zetu.

Nao walipokuwa wakila Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake akasema, Twaeni mle, huu ndio mwili wangu. Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa akisema, Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi. Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu (Mathayo 26:26-29).

Mtume Paulo anasimulia kisa hicho hicho kwa njia tofauti, kama ifuatavyo:

Kwa maana mimi nalipokea kwa Bwana niliyowapa nanyi, ya kuwa, Bwana Yesu usiku ule aliotolewa alitwaa mkate, naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu. Na vivi hivi baada ya kula akakitwaa kikombe akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu; fanyeni hivi kila mnywapo, kwa ukumbusho wangu. Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo (1Wakor. 11:23-26).

Lini, Namna Gani?

Maandiko hayasemi tushiriki Meza ya Bwana mara kwa mara kiasi gani, lakini ni dhahiri kwamba katika Kanisa la Kwanza ilifanyika mara kwa mara katika mikutano ya makanisa ya nyumbani, kama mlo kamili (ona 1Wakor. 11:20-34). Kuwa kuwa Meza ya Bwana asili yake ni katika Mlo wa Pasaka, ilikuwa ni mlo kamili ilipoanzishwa na Kristo, na ilikuwa sehemu ya chakula kamili katika kanisa la kwanza. Hivyo ndivyo inavyotakiwa kuwa hata siku hizi. Kwa sehemu kubwa, makanisa mengi yanafuata “mapokeo ya wanadamu.”

Tunapaswa kuikaribia Meza ya Bwana kwa kicho na heshima. Mtume Paulo alifundisha kwamba ilikuwa kosa kubwa kushiriki Meza ya Bwana kwa jinsi isivyostahili.

Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana. Lakini mtu ajihoji mwenyewe, na hivyo aule mkate na kukinywea kikombe. Maana alaye na kunywa hula na kunywa hukumu ya nafsi yake, kwa kutokuupambanua ule mwili. Kwa sababu hiyo wako wengi kwenu walio hawawezi na dhaifu, na watu kadha wa kadha wamelala. Lakini kama tungejipambanua nafsi zetu, tusingehukumiwa. Ila tuhukumiwapo, twarudiwa na Bwana, isije ikatupasa adhabu pamoja na dunia (1Wakor. 11:27-32).

Tunashauriwa kujichunguza na kujihukumu wenyewe kabla ya kushiriki Meza ya Bwana, na tukigundua dhambi yoyote ile, tunahitaji kuungama na kuitubu. Vinginevyo, tunaweza kuwa “na hatia ya mwili na damu ya Bwana.”

Kwa sababu Yesu alikufa na kumwaga damu yake ili kutuweka huru kutokana na dhambi, kwa kweli hatutaki kushiriki Meza yenye vitu vinavyowakilisha mwili na damu Yake, tukiwa na dhambi yoyote ile tunayoijua, isiyotubiwa. Tukifanya hivyo, tunaweza kula na kunywa hukumu juu yetu wenyewe katika ugonjwa na hata kifo kabla ya wakati, kama ilivyokuwa kwa Wakristo Wakorintho. Njia ya kuepukana na adhabu ya Mungu ni “kujihukumu wenyewe” – yaani, kukiri na kutubu dhambi zetu.

Dhambi kuu ya Wakristo Wakorintho ilikuwa kutokuwa na upendo. Walikuwa wanagombana wao kwa wao. Ukweli ni kwamba, kutokujaliana kwao kulijidhihirisha hata wakati wa Meza ya Bwana, wakati wengine walikula chakula na wengine wanakaa na njaa, na wengine hata walikuwa wanalewa (1Wakor. 11:20-22).

Mkate tunaokula ni mfano wa mwili wa Kristo, ambao sasa ndiyo kanisa. Tunashiriki mkate mmoja, ambao ni mfano wa umoja wetu kama mwili mmoja (ona 1Wakor. 10:17). Ni kosa kubwa sana kushiriki kinachowakilisha mwili mmoja wa Kristo huku tuko katika mapigano na ugomvi na kutokuwa na ushirikiano na viungo wengine wa mwili huo! Kabla hatujashiriki Meza ya Bwana, tunahitaji kuhakikisha kwamba tuko katika mahusiano yaliyo sawa na ndugu zetu na dada zetu katika Kristo.

To subscribe to David Servant's periodic e-teachings, click here.


Mchungaji Afanyaye Watu Kuwa Wanafunzi » Ibada Maalum

Jinsi Ya Kuongozwa Na Roho Mtakatifu

Sura Ya Ishirini Na Mbili

Injili ya Yohana ina idadi kubwa tu ya ahadi za Yesu kuhusu nafasi ya Roho Mtakatifu katika maisha ya waaminio. Hebu tusome baadhi yake.

Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele. Ndiye Roho wa kweli, ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui. Bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu (Yohana 14:16, 17).

Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote na kuwakumbusha yote niliyowaambia (Yohana 14:26).

Lakini mimi nawaambia iliyo kweli – yawafaa ninyi mimi niondoke. Kwa maana, mimi nisipo-ondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu, bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu. … Hata bado nikali ninayo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa. Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote. Kwa maana, hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake. Yeye atanitukuza mimi, kwa kuwa atatwaa katika yaliyo yangu na kuwapasha habari. Na yote aliyo nayo Baba ni yangu, kwa hiyo nalisema ya kwamba atatwaa katika yaliyo yangu na kuwapasheni habari (Yohana 16:7; 12 – 15).

Yesu aliwaahidi wanafunzi Wake kwamba Roho Mtakatifu angekaa ndani yao. Pia angewasaidia, angewafundisha, angewaongoza na kuwaonyesha mambo yajayo. Sisi kama wanafunzi wa Kristo siku hizi tusidhani kwamba Roho Mtakatifu atafanya pungufu ya hayo.

Cha kushangaza ni kwamba, Yesu aliwaambia wanafunzi Wake kuwa ni kwa faida yao Yeye aondoke, la sivyo Roho Mtakatifu asingekuja! Hiyo ilionyesha kwao kwamba ushirika wao na Roho Mtakatifu ungekuwa wa karibu na wa ndani sana, sawa na jinsi ambavyo ingekuwa kama Yesu angekuwepo nao katika mwili wakati wote. Vinginevyo, isingekuwa faida kwao kuwa na Roho Mtakatifu badala ya kuwa na Yesu. Kwa njia ya Roho Mtakatifu, Yesu siku zote yuko pamoja nasi, na ndani yetu. Sasa – tumtazamie Roho Mtakatifu kutuongoza kwa njia gani?

Jina Lake tu – Roho Mtakatifu – linaonyesha kwamba nafasi Yake ya msingi katika kutuongoza itakuwa ni kuelekea kwenye utakatifu na kumtii Mungu. Basi, kila kitu kinachohusiana na utakatifu na kutimiz amapenzi ya Mungu hapa duniani kiko katika maongozi ya Roho Mtakatifu. Yeye atatuongoza kutii amri zote za jumla za Kristo, pamoja na zile moja moja za kipekee, zinazohusu mwito maalum sana ambao Mungu ametuitia. Hivyo, ukitaka kuongozwa na Roho kwa habari ya huduma yako maalum, lazima pia uongozwe na Roho Mtakatifu katika utakatifu kwa ujumla. Huwezi kupata kimoja bila kingine. Watumishi wengi sana wanataka kuongozwa na Roho Mtakatifu katika matendo ya huduma kuu na miujiza, lakini hawataki kushughulikia yale mambo “madogo” kuhusu utakatifu wa jumla. Hilo ni kosa kubwa. Je, Yesu aliwaongozaje wanafunzi Wake? Kimsingi ni kwa kuwapa wao mafundisho ya jumla kuhusu utakatifu. Maongozi Yake maalum kwa habari za majukumu yao kihuduma hayakuwa mara kwa mara. Ndivyo ilivyo na Roho Mtakatifu, anayekaa ndani yetu. Basi, ukitaka kuongozwa na Roho, lazima kwanza kabisa ufuate maongozi Yake juu ya kuwa mtakatifu.

Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa kuwa wote wanao-ongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu” (Warumi 8:14). Kuongozwa kwetu na Roho ndiyo alama kwamba tu miongoni mwa watoto wa Mungu. Hivyo, watoto wote wa Mungu wanaongozwa na Roho. Ni juu yetu sasa kama watu wenye uamuzi kutii maongozi ya Roho.

Pamoja na hayo, hakuna Mkristo anayehitaji kufundishwa jinsi ya kuongozwa na Roho Mtakatifu, kwa sababu Roho Mtakatifu anamwongoza kila Mkristo tayari. Ila, kwa upande wa pili, Shetani anajaribu kupotosha watoto wa Mungu, nasi bado tuna ile asili ya kale ya mwili ndani yetu, yenye kutuongoza kinyume na mapenzi ya Mungu. Hivyo, waamini wanahitaji kujifunza jinsi ya kutambua maongozi ya Roho na yale mengine. Hizo ni hatua kuelekea ukomavu. Lakini kweli ya msingi ni hii: Siku zote Roho atatuongoza kulingana na Neno la Mungu lililoandikwa, Naye atatuongoza siku zote kufanya kilicho sawa na chenye kumpendeza Mungu, na kitakachomletea Mungu utukufu (ona Yohana 16:14).

Sauti Ya Roho Mtakatifu

Ingawa Maandiko yanatuambia kwamba Roho Mtakatifu wakati mwingine anaweza kutuongoza kwa njia za kushangaza kama vile maono, unabii au sauti inayosikika ya Mungu, njia ya kawaida kabisa anayowasiliana nasi ni kuweka “dhana” ndani ya roho zetu. Yaani – kama Roho Mtakatifu anataka tufanye kitu fulani, “atatuvuta” ndani ya roho zetu – nasi tutajisikia “kuongozwa” kuelekea upande fulani au kufuata mwelekeo fulani.

Tunaweza kuita sauti ya roho zetu “dhamiri” yetu. Wakristo wote wanajua jinsi dhamiri yao inavyosema. Tunapojaribiwa kutenda dhambi, si kwamba tunasikia sauti ndani yetu inayosema, “Usikubali jaribu hilo.” Badala yake, tunajisikia kitu ndani yetu kikipinga jaribu hilo. Na tukikubaliana na jaribu, baada ya kutenda dhambi, hatusikii sauti ikisema, “Umetenda dhambi! Umetenda dhambi!” Tunahisi tu hukumu ndani yetu ambayo wakati huo inatuongoza kutubu na kuungama dhambi yetu.

Kwa hali hiyo hiyo, Roho Mtakatifu atatufundisha na kutuongoza katika kweli za jumla na ufahamu. Atatufundisha kwa kutupa mafunuo ya ghafula (yenye kukubaliana na Biblia kila mara) ndani yetu. Mafunuo hayo yanaweza kuhitaji dakika kumi kumweleza mtu, lakini huja kwa nukta chache tu kwa njia ya Roho Mtakatifu.

Vivyo hivyo, Roho Mtakatifu atatuongoza katika maswala ya huduma. Lazima tufanye juhudi za makusudi kuwa wasikivu kwa maongozi yale ya ndani na dhana, na tutajifunza polepole (kwa kujaribu na kukosea) kumfuata Roho kwa habari ya mambo yanayohusu huduma. Tunajikuta tukifanya makosa kwa habari ya mapenzi ya Mungu tunaporuhusu akili zetu (mawazo yetu sahihi au ya makosa) kufika kwenye nafasi ya mioyo yetu (mahali ambapo Roho anatuongoza).

Jinsi Roho Alivyomwongoza Yesu

Yesu aliongozwa na Roho Mtakatifu kwa dhana za ndani. Kwa mfano: Injili ya Marko inaeleza kilichotokea mara tu baada ya Yesu kubatizwa na Roho Mtakatifu, baada ya kubatizwa Kwake na Yohana.

Mara Roho akamtoa aende nyikani (Marko 1:12. Maneno mepesi kukazia).

Yesu hakusikia sauti au kuona maono yaliyomwongoza kwenda nyikani – alitolewa (au alisukumwa) aende. Ndivyo Roho Mtakatifu anavyotuongoza sisi kwa kawaida. Tutajisikia kuvutwa, kuongozwa, kushawishika ndani yetu kufanya kitu fulani.

Yesu alipomwambia yule mtu aliyepooza, aliyetelemshwa na wenzake kupitia darini kwamba dhambi zake zimesamehewa, Yesu alijua kwamba waandishi waliokuwepo walifikiri anakufuru. Alijuaje mawazo yao? Tunasoma hivi katika Injili ya Marko:

Mara Yesu, akifahamu rohoni mwake kwamba wanafikiri hivyo nafsini mwao, akawaambia, Mbona mnafikiri hivi mioyoni mwenu? (Marko 2:8. Maneno mepesi kukazia).

Yesu alitambua (au kufahamu) rohoni Mwake walichokuwa wanafikiria. Kama tutakuwa wasikivu ndani ya roho zetu, sisi pia tunaweza kujua jinsi ya kuwajibu wale wanaopinga kazi ya Mungu.

Uongozi Wa Roho Katika Huduma Ya Paulo

Baada ya kutumika katika huduma kwa miaka kama ishirini hivi, mtume Paulo alikuwa amejifunza vizuri jinsi ya kufuata maongozi ya Roho Mtakatifu. Roho alimwonyesha “mambo yajayo” kuhusiana na huduma kwa kiwango fulani. Kwa mfano: Wakati Paulo alipokuwa anamalizia huduma yake kule Efeso, alipewa mtazamo wa mwelekeo wa maisha yake na huduma, kwa kipindi cha miaka mitatu iliyokuwa mbele yake.

Mambo hayo yalipokwisha kumalizika, Paulo akaazimu rohoni mwake, akiisha kupita katika Makedonia na Akaya, aende Yerusalemu, akisema, Baada ya kuwako huko, yanipasa kuuona na Rumi pia (Matendo 19:21).

Ona kwamba Paulo hakukusudia mwelekeo huo katika akili zake bali katika roho yake. Hiyo inaonyesha kwamba Roho Mtakatifu alikuwa anamwongoza rohoni mwake aende Makedonia kwanza na Akaya (katika Ugiriki siku hizi), kisha aende Yerusalemu, na hatimaye aende Rumi. Na hivyo ndivyo alivyofanya. Kama Biblia yako ina ramani ya safari ya utume ya tatu ya Paulo na safari yake kwenda Rumi, unawea kufuatilia mwendo wake kutoka Efeso (alikopangia safari yake katika roho yake) kupitia Makedonia na Akaya, mpaka Yerusalemu, na miaka kadhaa baadaye, akafika Rumi.

Paulo alisafiri kuptia Makedonia na Akaya, kisha akarudi nyuma na kupita Makedonia tena, akizunguka pwani ya Bahari ya Uyunani. Kisha, alisafiri pwani ya Bahari ya Uyunani katika Asia Ndogo. Katika safari hiyo alisimama mjini Mileto, akawaita wazee wa kanisa la Efeso, akawaaga kwa kusema hivi:

Basi sasa angalieni, nashika njia kwenda Yerusalemu hali nimefungwa rohoni, nisiyajue mambo yatakayonikuta huko; isipokuwa Roho Mtakatifu mji kwa mji hunishuhudia akisema ya kwamba vifungo na dhiki vyaningoja (Matendo 20:22, 23. Maneno mepesi kukazia).

Paulo alisema alikuwa “amefungwa rohoni”. Maana yake ni kwamba alikuwa na msukumo rohoni mwake uliokuwa unamwongoza kwenda Yerusalemu. Hakuwa na picha kamili juu ya kitakachotokea atakapofika Yerusalemu, lakini alisema kwamba katika kila mji aliosimama akisafiri, Roho Mtakatifu alishuhudia kwamba vifungo na mateso vinamsubiri huko Yerusalemu. Je, Roho Mtakatifu “alishuhudiaje” kuhusu vifungo na mateso hayo yaliyokuwa yanamngojea Yerusalemu?

Mifano Mwili

Katika sura ya 21 ya Kitabu cha Matendo, tuna habari mbili zenye kujibu hilo swali. Mfano wa kwanza ni wakati Paulo alipofika katika mji wa Tiro, uliokuwa bandari katika Bahari ya Mediteranea.

Tukiisha kuwaona wanafunzi tukakaa huko siku saba, nao wakamwambia Paulo kwa uweza wa Roho, asipande kwenda Yerusalemu (Matendo 21:4).

Mstari huu umewafanya waandishi wengine wa vitabu vya kufafanua Biblia kusema kwamba Paulo aliacha kumtii Mungu kwa kuendelea na safari yake kwenda Yerusalemu. Lakini, kutokana na habari zaidi tupatazo katika kitabu cha Matendo, hatuwezi kusema hivyo. Hii itaonekana tunapoendelea kufuatilia kisa hiki.

Inaonekana kwamba wanafunzi wa Tiro walikuwa wasikivu, na walihisi kwamba dhiki ilikuwa inamsubiri Paulo huko Yerusalemu. Wakajaribu sana kumzuia asiende. Tafsiri moja ya Kiingereza ya Agano Jipya inatoa mwanga zaidi, maana mstari huo unasomeka hivi: “Kwa sababu ya dhana zilizotolea na Roho, walizidi kumwonya Paulo asikanyage Yerusalemu.”

Wale wanafunzi huko Tiro hawakufanikiwa, kwa sababu Paulo aliendelea na safari yake kwenda Yerusalemu, licha ya maonyo yote hayo.

Hii inatufundisha kwamba tunapaswa kuwa makini tusiongeze tafsiri yetu wenyewe kwa mafunuo tunayopokea katika roho zetu. Paulo alifahamu vizuri kabisa kwamba taabu ilikuwa inamsubiri huko Yerusalemu, lakini pia alijua kwamba ni mapenzi ya Mungu yeye kwenda huko. Kama Mungu atatufunulia kitu kwa Roho Mtakatifu, haimaanishi kwamba tunapaswa kukisema. Pia, tuwe makini tusije tukaongeza tafsiri yetu wenyewe katika yale ambayo Roho Mtakatifu amefunua.

Mapumziko Mafupi Kaisaria

Mji uliofuata katika safari ya Paulo kwenda Yerusalemu ni bandari ya Kaisaria.

Basi, tulipokuwa tukikaa huko siku nyingi, nabii mmoja jina lake Agabo akashuka kutoka Uyahudi. Alipotufikia, akautwaa mshipi wa Paulo, akajifunga miguu na mikono, akasema, Roho Mtakatifu asema hivi, Hivyo ndivyo Wayahudi wa Yerusalemu watakavyomfunga mtu mwenye mshipi huu, nao watamtia katika mikono ya watu wa Mataifa (Matendo 21:10, 11).

Hapo tena ni mfano mwingine wa Roho Mtakatifu akimshuhudia Paulo kwamba “vifungo na dhiki” vilikuwa vinamngojea Yerusalemu. Lakini, ona kwamba Agabo hakusema, “Kwa hiyo, Bwana asema hivi: Usiende Yerusalemu!” Hapana. Mungu alikuwa anamwongoza Paulo aende Yerusalemu, na kwa unabii wa Agabo alikuwa anamwandaa tu kwa ajili ya matatizo yaliyokuwa yanamsubiri huko. Pia, ona kwamba unabii wa Agabo ulithibitisha tu kitu ambacho Paulo alijua tayari katika roho yake, miezi mingi kabla. Hatupaswi kuongozwa na unabii kamwe. Kama unabii hauthibitishi tunachofahamu tayari, tusiufuate.

Unabii wa Agapo unaweza kuangukia katika fungu la “maongozi yenye kusisimua” kwa sababu ulizidi dhana ya ndani ya roho ya Paulo. Wakati Mungu anaporuhusu “maongozi ya kusisimua” kama vile maono au kusikia sauti kabisa, ni kwa sababu anajua kwamba njia haitakuwa rahisi. Tutahitaji uhakikisho wa ziada unaoletwa na maongozi aina hiyo. Kwa habari ya Paulo ni kwamba, alikuwa anaelekea kwenye kupokea chupuchupu kuuawa na kundi la watu wenye hasira, na angekaa gerezani miaka kadhaa kabla hajasafiri kwenda Rumi kama mfungwa. Ila, kwa sababu ya maongozi hayo ya kusisimua aliyopata, aliweza kuwa na amani kamilifu kabisa katika hayo yote, kwa sababu alijua kwamba hatima yake ingekuwa nzuri.

Katika Minyororo, Katika Mapenzi Ya Mungu

Paulo alipofika Yerusalemu alikamatwa na kufungwa. Hapo tena alipokea maongozi ya kusisimua. Safari hii, ni maono ya Yesu Mwenyewe.

Usiku ule Bwana akasimama karibu naye [Paulo], akasema, Uwe na moyo mkuu; kwa sababu, kama ulivyonishuhudia habari zangu Yerusalemu, imekupasa kunishuhudia vivyo hivyo Rumi nako (Matendo 23:11).

Angalia kwamba Yesu hakusema hivi: “Unaona sasa Paulo! Unafanya nini hapa? Nilijaribu kukuonya usije Yerusalemu!” Yesu alithibitisha tu maongozi ambayo Paulo alikuwa ametambua rohoni mwake miezi kadhaa kabla. Paulo alikuwa katika mapenzi ya Mungu kabisa huko Yerusalemu, ili kushuhudia habari za Yesu. Hatimaye angemtangaza Kristo hata Rumi kwenyewe.

Tusisahau kwamba sehemu ya wito wa Paulo hasa ilikuwa kuwashuhudia Wayahudi na Mataifa, pamoja na wafalme pia (ona Matendo 9:15). Paulo alipokaa kifungoni huko Yerusalemu na baadaye Kaisaria, alipata nafasi ya kushuhudia mbele za Feliksi aliyekuwa Mkuu wa Mkoa, pamoja na Porkio Festo, na Mfalme Agripa, aliyekaribia “kushawishiwa” kumwamini Yesu (Matendo 26:28). Mwishowe, Paulo alipelekwa Rumi kushuhudia mbele za Nero, aliyekuwa mfalme wa dola ya Rumi.

Kuelekea Kwa Nero

Paulo alipokea tena maongozi ya Mungu kwa kusikiliza roho yake akiwa safarini kwenda Italia. Nahodha wa merikebu pamoja na kiongozi wa safari walipokuwa wanajaribu kuamua bandari ipi ya Krete watie nanga ili kusubiri majira ya baridi, Paulo alipata ufunuo.

Na wakati mwingi ulipokwisha kupita na safari ikiwa ina hatari sasa kwa sababu siku za kufunga zilikuwa zimekwisha kupita, Paulo akawaonya, akawaambia, Wanaume, naona kwamba safari hii itakuwa na madhara na hasara nyingi, si ya shehena na merikebu tu, ila na maisha yetu pia (Matendo 27:9, 10. Maneno mepesi kukazia).

Paulo alitambua mambo ambayo yangetokea. Bila shaka kutambua huko kulitokana na dhana iliyotolewa na Roho.

Kwa bahati mbaya, yule nahodha wa merikebu hakumsikiliza Paulo, naye alijaribu kufikia bandari nyingine. Matokeo ni kwamba merikebu ilinaswa katika dhoruba kali kwa majuma mawili. Hali ikawa hatari kiasi kwamba mabaharia wa ile merikebu walitupa mizigo yote siku ya pili, na siku ya tatu wakatupa mpaka vyombo vya merikebu. Baadaye, Paulo akapokea tena maongozi mengine. Tunasoma hivi:

Jua wala nyota hazikuonekana kwa muda wa siku nyingi, na tufani kuu ikatushika, basi tukakata tamaa ya kuokoka. Na walipokuwa wamekaa wakati mwingi bila kula chakula, Paulo akasimama katikati yao akasema, Wanaume, ilinipasa kunisikiliza mimi na kutokung’oa nanga huko Krete, na kupata madhara haya na hasara hii. Sasa nawapeni shauri, iweni na moyo mkuu, kwa maana hapana hata nafsi moja miongoni mwenu atakayepotea, ila merikebu tu. Kwa maana usiku huu wa leo malaika wa Mungu yule ambaye mimi ni wake, naye ndiye nimwabuduye, alisimama karibu nami akaniambia, Usiogope Paulo. Huna budi kusimama mbele ya Kaisari; tena tazama, Mungu amekupa watu wote wanaosafiri pamoja nawe. Basi wanaume, changamkeni; kwa sababu namwamini Mungu ya kwamba yatakuwa vile vile kama nilivyoambiwa. Lakini hatuna hudi kupwelewa katika kisiwa kimoja (Matendo 27:20-26).

Bila shaka sababu ya Mungu kumpa Paulo “maongozi ya kusisimua” ya ziada iko wazi, ukizingatia hali halisi. Baada ya tukio hili, Paulo angekabiliwa na kuvunjikiwa merikebu. Baadaye kidogo angeumwa na nyoka wa sumu (ona Matendo 27:41 hadi 28:5). Ni vizuri kuwa na malaika atakayekwambia kwamba mambo yote yatakuwa mazuri kabla hayajatokea!

Mawaidha Muhimu

Anza kutafuta rohoni mwako zile dhana na hisia ambazo ni maongozi ya Roho Mtakatifu. Pengine mwanzoni utakosea kidogo, ukidhani kwamba Roho Mtakatifu anakuongoza na kumbe sivyo, lakini hiyo ni kawaida. Usivunjike moyo; endelea tu.

Pia inakusaidia kupata muda wa utulivu mbele za Mungu, ukiomba kwa lugha na kusoma Biblia. Tuombapo kwa lugha, iombayo ni roho yetu, nasi kwa kawaida tunakuwa wasikivu wakati huo. Kwa kusoma na kutafakari Neno la Mungu, tunakuwa wasikivu zaidi kwa roho zetu kwa sababu Neno la Mungu ni chakula chetu cha kiroho.

Mungu anapokuongoza mwelekeo fulani, uongozi huo haupungui. Yaani, unapaswa kuendelea kuombea maamuzi fulani makubwa kwa kitambo, ili kuwa na uhakika kwamba ni Mungu ndiye anayekuongoza, wala si mawazo yako au hisia zako. Kama huna amani moyoni wakati unapoomba juu ya mwelekeo fulani, usielekee huko mpaka upate amani.

Ukipata maongozi ya kusisimua, vizuri, ila, usijaribu “kuamini” ili uone maono au usikie sauti. Mungu hajatuahidi kutuongoza hivyo (japo wakati mwingine Yeye hufanya hivyo kulingana na mapenzi Yake kama Mwenyezi). Ila, tunaweza kuamini wakati wote kwamba atatuongoza kwa ushuhuda wa kutoka ndani.

Mwisho: Usiongeze chochote katika yale ambayo Mungu anakwambia. Mungu anaweza kukufunulia huduma fulani ambayo amekuandalia kwa wakati ujao, lakini wewe unaweza kudhani kwamba wakati wa kutimia kwa hilo ni juma lijalo kumbe ni miaka mingi baadaye. Mimi najua hayo kwa uzoefu nilio nao. Usifikiri tu. Paulo alijua kidogo juu ya wakati wake wa baadaye. Hakujua yote, na ni kwa sababu Mungu hakufunua kila kitu. Mungu anataka tuendelee kutembea kwa imani wakati wote.

To subscribe to David Servant's periodic e-teachings, click here.


Mchungaji Afanyaye Watu Kuwa Wanafunzi » Jinsi Ya Kuongozwa Na Roho Mtakatifu

Familia Ya Kikristo

Sura Ya Ishirini Na Moja

 

Ni dhahiri kwamba Mungu ndiye aliyeleta wazo la familia. Basi, ni halali kutazamia kwamba atatupa maelekezo jinsi familia zinavyotakiwa kuishi na kutuonya juu ya matatizo yanayoweza kuangamiza au kuharibu familia. Bwana ametupa kanuni nyingi sana katika Neno Lake kuhusu jinsi familia inavyotakiwa kuwa, na wajibu wa kila mshirika katika familia. Maagizo hayo ya KiBiblia yanapofuatwa, familia zitapata baraka zote ambazo Mungu alikusudia wazifurahie. Zinapovunjwa, matokeo yake ni maumivu makali moyoni, na vurugu.

Nafasi Ya Mume Na Mke

Mungu amepanga kwamba familia ya Kikristo iwe katika mfumo fulani. Kwa sababu mfumo huo unaleta uthabiti katika maisha ya familia, Shetani hufanya kazi sana kupotosha mpango aliokusudia Mungu.

Kwanza kabisa ni kwamba, Mungu amepanga mume awe kichwa cha familia. Hii haimpi mume ruhusa ya kutawala mke wake na watoto katika ubinafsi. Mungu amewaita waume kupenda, kulinda, kutimiza mahitaji na kuongoza familia zao kama kichwa. Pia, Mungu alikusudia wake wawe watiifu kwa uongozi wa waume zao. Hili ni wazi, kama Maandiko yanavyosema.

Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili. Lakini kama vile Kanisa limtiivyo Kristo, vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo (Waefeso 5:22-24).

Mume si kichwa wa mkewe kiroho – Yesu ndiye mwenye nafasi hiyo. Yesu ni kichwa wa kanisa kiroho, na mke wa Kikristo ni mshirika wa kanisa sawa na mume wake ambaye ni Mkristo pia. Ila, katika familia, mume Mkristo ndiye kichwa wa mke wake na watoto, nao wanapaswa kutii na kunyenyekea mamlaka yake hayo aliyopewa na Mungu.

Je, mke anapaswa kumtii mumewe kwa kiwango gani? Kama Paulo anavyosema, ni katika kila jambo. Wakati pekee anaporuhusiwa kuvunja sheria hiyo ni kama mume wake anamtaka kuvunja Neno la Mungu au kufanya kitu ambacho kinapinganana dhamiri yake. Ni wazi kwamba hakuna mume Mkristo atakayemtaka mke wake kufanya chochote kinachovunja Neno la Mungu au kwenda kinyume na dhamiri yake. Mume si Bwana kwa mkewe – Yesu tu ndiye mwenye nafasi hiyo maishani mwake. Kama itafikia uchaguzi kuhusu nani wa kumtii, anapaswa kuchagua kumtii Yesu.

Waume wanapaswa kukumbuka kwamba Mungu hayuko upande wao mara zote. Kuna wakati ambapo Mungu alimwambia Ibrahimu afanye kama alivyoambiwa na Sara mkewe (ona Mwanzo 21:10-12). Maandiko pia yanataja jinsi Abigaili alivyoacha kumtii Nabali mumewe, aliyekuwa mpumbavu, na kwa kufanya hivyo aliepusha tatizo (ona 1Samweli 25:2 – 38).

Neno La Mungu Kwa Waume

Mungu anawaambia hivi waume:

Enyi waume, wapendeni wake zetu kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake… Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe, maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake popote; bali huulisha na kuutunza kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa. Kwa kuwa tu viungo vya mwili wake. … Lakini kila mtu ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe; wala mke asikose kumstahi mumewe (Waefeso 5:25, 28-30, 33).

Waume wanaagizwa kuwapenda wake zao kama Kristo anavyolipenda Kanisa. Si wajibu mdogo huo! Mke yeyote atajinyenyekeza kwa furaha kabisa kwa mtu anayempenda kama Yesu – aliyetoa uhai Wake kwa sababu ya upendo wa kujitoa. Sawa na jinsi Kristo anavyoupenda mwili Wake – yaani Kanisa – ndivyo na waume wanavyotakiwa kumpenda mwanamke ambaye ni “mwili mmoja” nao (Waefeso 5:31). Kama mume Mkristo anampenda mkewe kama anavyopaswa, atamtimizia mahitaji yake, atamtunza, atamheshimu, atamsaidia, atamtia moyo, na atatumia muda kuwa naye. Akishindwa katika wajibu wake kumpenda mkewe, mume huyo yuko hatarini kuzuia majibu ya maombi yake mwenyewe.

Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima kama chombo kisicho na nguvu na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe (1Petro 3:7. Maneno mepesi kukazia).

Kihalisi ni kwamba hapajawahi kuwepo na ndoa isiyokuwa na kutokuelewana na shida mbalimbali. Ila, kwa kujitoa na kukuza tunda la Roho katika maisha yetu, waume na wake wanaweza kujifunza kuishi kwa maelewano na amani, na kufikia mahali pa kutambua baraka zinazozidi kuongezeka za ndoa ya Kikristo. Kila mwenzi anaweza kukua na kufikia ukomavu mkubwa katika kufanana na Kristo kutokana na matatizo yasiyoepukika yanayotokea katika ndoa zote.

Kwa maelezo zaidi juu ya wajibu na majukumu ya waume na wake, tazama Mwanzo 2:15-25; Mithali 19:13; 21:9, 19; 27:15, 16; 31:10-31; 1Wakor. 11:3; 13:1-8; Wakolosai 3:18, 19; 1Timo. 3:4, 5; Tito 2:3-5; 1Petro 3:1-7.

Tendo La Ndoa

Mungu ndiye mwanzilishi wa tendo la ndoa, na ni dhahiri kwamba aliliumba ili kustarehesha na kusaidia katika uumbaji. Pamoja na hayo, Biblia inatamka wazi kwamba tendo la ndoa ni la kufurahiwa na wale walioungana pamoja katika agano la ndoa, la kudumu.

Kukutana kimwili nje ya mipaka ya ndoa huitwa zinaa au uasherati. Mtume Paulo alisema kwamba wale watendao mambo kama hayo hawataurithi ufalme wa Mungu (ona 1Wakor. 6:9-11). Ingawa Mkristo anaweza kujaribiwa na pengine kufikia kuanguka katika tendo la uzinzi au uasherati, atajisikia hatia kubwa sana rohoni mwake, itakayompelekea kutubu.

Paulo pia alitoa mafundisho wazi kabisa kuhusu majukumu ya mume na mke kwa mwenzake, kuhusu tendo la ndoa.

Lakini kwa sababu ya zinaa, kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe, na kila mwanamke na awe na mume wake mwenyewe. Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe. Vivyo hivyo, mume hana amari juu ya mwili wake, bali mkewe. Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda, ili mpate faragha kwa kusali; mkajiane tena, Shetani asije akawajaribu kwa kutokuwa na kiasi kwenu (1Wakor. 7:2-5).

Mistari hii inaweka wazi kabisa kwamba tendo la ndoa lisitumiwe kama “zawadi” na mume au mke, maana hakuna mwenye mamlaka juuya mwili wake mwenyewe.

Tena, tendo la ndoa ni zawadi kutoka kwa Mungu. Si dhambi wala najisi inapokuwa katika ndoa. Paulo aliwatia moyo Wakristo wenye ndoa kushirikiana kimwili. Tena, tunapata ushauri huu kwa waume Wakristo katika kitabu cha Mithali:

Chemchemi yako ibarikiwe; nawe umfurahie mke wa ujana wako. Ni ayala apendaye na paa apendezaye; maziwa yake ytakutoshe siku zote; na kwa upendo wake ushangilie daima (Mithali 5:18, 19).[1]

Kama wanandoa Wakristo wanataka kufurahia mahusiano kimwili yenye kutosheleza, waume na wake wanahitaji kuelewa kwamba kuna tofauti kubwa sana kati ya wanaume na wanawake kwa habari ya kushirikiana kimwili. Kiasili, mwanamume ni mtu wa kimwili sana kwa habari ya kukutana kimwili. Asili ya mwanamke kwa habari ya kukutana kimwili ni kitu cha hisia. Wanaume husisimka na kuwa tayari kukutana kimwili na mwanamke kwa kuona tu (ona Mathayo 5:28). Wanawake wao husisimka na kuwa tayari kukutana kimwili kwa mahusiano ya karibu sana, na kwa kuguswa na kushikwa-shikwa (ona 1Wakor. 7:1). Wanaume huvutiwa na wanawake wanaowapendeza macho; ila wanawake huvutiwa na wanaume wanaowapendeza kwa sababu zaidi ya kuvutia kimwili. Hivyo, wanawake wenye busara hupendeza ili kuwavutia waume zao wakati wote. Na waume wenye hekima huonyesha upendo wao kwa wake zao kutwa nzima kwa kuwakumbatia na kuwatendea mambo ya ukarimu, badala ya kuwatazamia wake zao “kuwa tayari” kwa ghafula wakati wa usiku.

Kiwango cha ashiki ya mwanamume kukutana kimwili na mwenzake huongezeka kulingana na kuongezeka kwa mbegu za uzazi katika mwili wake. Kiwango cha ashiki ya mwanamke huongezeka au kupungua kutegemeana na siku zake za mwezi. Wanaume wana uwezo wa kusisimka na kuwa tayari kukutana kimwili na mwanamke, na kufikia kilele cha tendo la ndoa baada ya muda mfupi sana – nukta chache tu au dakika, ila wanawake huchukua muda mrefu. Ingawa mwanamume yuko tayari kimwili kukutana na mwanamke upesi sana, mwili wa mwanamke unaweza usiwe tayari, mpaka baada ya nusu saa au zaidi. Basi, waume wenye hekima huchukua muda katika kuanza kuwasisimua wenzao kwa kuwapapasa, kuwabusu na kuwashika-shika sehemu za mwili ambazo zinasisimua, ili kumsababisha mwanamke kuwa tayari kukutana kimwili. Ikiwa hajui sehemu zinazohusika, amwulize. Tena, anapaswa kujua kwamba, japo yeye anaweza kufikia kilele cha tendo la ndoa mara moja tu, mwenzake anaweza kufikia kilele cha tendo la ndoa mara nyingi. Mume anapaswa kuhakikisha kwamba mwenzake anapokea anachotaka.

Ni muhimu sana kwa waume Wakristo na wake zao kuzungumza kuhusu mahitaji yao kwa uwazi, na kujifunza juu ya tofauti zao kiasi wanachoweza. Mahusiano kimwili kati ya waume na wake yanaweza kuwa baraka inayozidi kuongezeka kutokana na mawasiliano ya miezi mingi na miaka, na kugunduana na kuzoeana.

Watoto Wa Familia Ya Kikristo

Watoto wanapaswa kufundishwa jinsi ya kunyenyekea na kutii kabisa wazazi wao Wakristo. Wakifanya hivyo, wameahidiwa maisha marefu na baraka zao.

Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki. Waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi, Upate heri, ukae siku nyingi katika dunia (Waefeso 6:1-3).

Akina baba Wakristo kama vichwa wa familia zao, wanapewa wajibu wa msingi kabisa kwa ajili ya kuwafundisha watoto wao, hivi:

Nanyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana (Waefeso 6:4).

Ona kwamba wajibu wa baba ni wa namna mbili: kuwalea watoto wake katika adabu na maonyo ya Bwana. Hebu tuanze kwa kutazama haja ya kuwafundisha watoto adabu.

Nidhamu Ya Watoto

Mtoto asiyetiwa nidhamu atakapokuwa mtu mzima atakuwa mbinafsi na muasi kwa mamlaka. Watoto wanapaswa kutiwa nidhamu wakati wowote wanapoacha kwa makusudi kutii sheria halali zilizowekwa na wazazi wao. Watoto wasiadhibiwe kwa makosa au kutowajibika kwa sababu ya utoto. Lakini, watakiwe kukabiliana na matokeo ya makosa yao na kutowajibika kwao, na kwa njia hiyo kuwasaidia kujiandaa kwa ajili ya uhalisi wa maisha ya utu uzima.

Watoto wadogo wanapaswa kuadhibiwa kwa kiboko, kama Neno la Mungu linavyofundisha. Lakini watoto wachanga wasipigwe viboko. Hii haina maana kwamba watoto wachanga waruhusiwe kufanya wanachotaka. Inatakiwa tangu wanapozaliwa wajue kwamba mama na baba ndiyo wenye mamlaka. Wanaweza kufundishwa wakiwa wadogo sana maana ya neno “hapana” kuwakuwakataza tu kufanya kitu wanachofanya, au wanachotaka kufanya. Wakianza kuelewa maana ya neno “hapana”, wanaweza kuchapwa kofi dogo tu matakoni ili kuwasaidia kuelewa vizuri zaidi wanapoendelea kufanya kile ambacho wazazi wanasema kisifanywe. Kama hayo yatafanyika kwa utaratibu na mara kwa mara, watoto watajifunza kuwa watiifu tangu umri mdogo sana.

Pia, wazazi wanaweza kuonyesha mamlaka yao kwa kutounga mkono tabia zisizotakiwa za watoto wao. Mfano ni kuwapa mara moja kitu wanachotaka, wakilia. Kufanya hivyo ni kuwafundisha watoto walie ili wapate matakwa yao. Au, kama wazazi watakubaliana na madai ya watoto wao kila mara wanaponuna au kukasirika ni kwamba wanawatia moyo kuendelea na tabia hiyo isiyotakiwa. Wazazi wenye hekima huunga mkono tabia nzuri tu katika watoto wao.

Kuchapa kiboko kusilete madhara kimwili, ila kusababishe maumivu ya kutosha kumfanya mtoto yule asiyetii kulia kwa muda kidogo. Kwa njia hiyo, mtoto atajifunza kuunganisha uchungu na kutokutii. Hata Biblia inaunga mkono hilo.

Yeye asiyetumia fimbo yake humchukia mwanawe; bali yeye ampendaye humrudi mapema. … Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali. … Usimnyime mtoto wako mapigo; maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa. Utampiga kwa fimbo, na kumwokoa nafasi yake na Kuzimu. … Fimbo na maonyo hutia hekima; bali mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye (Mithali 13:24; 22:15; 23:13-14; 29:15).

Wazazi wanaposimamia sheria zao, hawana haja ya kuwatisha watoto ili kuwafanya watii Mtoto anapoacha kutii kwa makusudi, achapwe fimbo. Ikiwa mzazi atatishia tu kumchapa mtoto wake ambaye si mtii, anachofanya ni kuunga mkono uasi wa mtoto wake. Matokeo ni kwamba mtoto anajifunza kutokujali utii mpaka vitisho vya wazazi wake vya maneno vinapofikia kiwango fulani cha sauti.

Baada ya kiboko, mtoto anapaswa kukumbatiwa na kuhakikishiwa upendo wa mzazi aliyemchapa.

Mlee Mtoto

Wazazi Wakristo wanapaswa kutambua kwamba wana wajibu wa kuwafundisha na kuwalea watoto wao, kama tunavyosoma katika Mithali 22:6, kwamba: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee” (maneno mepesi kukazia).

Kulea (au kufundisha) si kuadhibu tu mtoto anapoacha kutii, bali ni kumpongeza pia wakati anapofanya vizuri. Watoto kila wakati wanahitaji kusifiwa na wazazi wao ili kuunga mkono tabia zao njema, na mambo mazuri wanayofanya. Watoto wanahitaji kuhakikishiwa mara kwa mara kwamba wanapenda, wanakubalika na kufurahiwa na wazazi wao. Wazazi wanaweza kuonyesha upendo wao kwa kusifu, kuwakumbatia na kuwabusu watoto, na kwa kutumia muda mwingi nao.

“Kulea” maana yake “kufanya atii.” Basi, wazazi Wakristo wasiwape watoto wao uchaguzi kama watakwenda kanisani au kuomba kila siku au hapana. Watoto hawana ufahamu wa kutosha kujua kinachowafaa, au kilicho bora. Ndiyo sababu Mungu aliwapa wazazi. Wazazi watakaofanya bidii na kuweka juhudi na nguvu zao kuhakikisha kwamba watoto wao wanalelewa vizuri, wana ahadi kutoka kwa Mungu kwamba watoto wao hawataacha njia iliyo sawa hata wakiwa wakubwa, kama tulivyosoma katika Mithali 22:6.

Pia, watoto wanapaswa kuongezewa majukumu wanavyozidi kukua. Lengo la mzazi mwenye kufanikiwa ni kumwandaa mtoto hatua kwa hatua ili kuwajibika kabisa akiwa mtu mzima. Mtoto anapozidi kukua, apewe uhuru zaidi wa kujiamulia mambo yake mwenyewe. Tena, yule kijana mkubwa anapaswa kuelewa kwamba daima akubali wajibu utokanao na maamuzi yake, na kwamba wazazi wake hawatakuwepo siku zote “kumwokoa” katika matatizo.

Wajibu Wa Wazazi Kufundisha

Kama tusomavyo katika Waefeso 6:4, akina baba si tu kwamba wanawajibika kuwafundisha adabu watoto wao, bali pia wanatazamiwa kuwafundisha katika Bwana. Si wajibu wa kanisa kumpa mtoto mafundisho kuhusu maadili ya KiBiblia, tabia za Kikristo au theolojia – ni kazi ya baba. Wazazi wanaoachia wajibu wote kwa mwalimu wa Shule ya Jumapili awafundishe watoto wao kuhusu Mungu wanakosea sana. Mungu aliwaamuru Waisraeli hivi, kwa njia ya Musa:

Na maneno haya ninayokuamuru leo yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo (Kumbu. 6:6, 7. Maneno mepesi kukazia).

Wazazi Wakristo wawafundishe watoto wao kuhusu Mungu tangu wakiwa wadogo, wakiwaambia Yeye ni nani na anawapenda kiasi gani. Watoto wadogo wafundishe habari za kuzaliwa kwa Yesu, maisha Yake, kifo na kufufuka Kwake. Watoto wengi wanaweza kuelewa ujumbe wa Injili wanapokuwa na umri wa miaka mitano au sita, na wanaweza kufanya uamuzi wa kumfuata Kristo. Baada ya hivyo (wakiwa na miaka sita au saba, na wakati mwingine hata wakiwa wadogo zaidi), wanaweza kupokea ubatizo wa Roho Mtakatifu na kunena kwa lugha kama ishara kwamba wamejazwa. Pamoja na hayo, hatuwezi kuweka sheria kuhusu jambo hili kwa sababu kila mtoto yuko tofauti. Ila hoja ni kwamba, wazazi Wakristo wanapaswa kutoa nafasi ya kwanza kwenye kuwafundisha watoto wao mambo ya kiroho.

Amri Kumi Za Kuwapenda Watoto Wako

1). Usiwatie watoto wako mahali pagumu (ona Waefeso 6:4). Watoto wasitazamiwe kutenda kama watu wazima. Ukitazamia mengi kupita kiasi kutoka kwa watoto wako, wataacha kujitahidi kukupendeza maana wanajua haiwezekani.

2). Usilinganishe watoto wako na watoto wengine. Wajulishe jinsi unavyofurahia sifa zao za kipekee na karama au vipaji vyao kutoka kwa Mungu. Wakubali wao kama wao.

3). Wape majukumu nyumbani, ili wajue kwamba wao ni sehemu muhimu sana ya familia hiyo. Kufanikiwa ni matofali yanayojenga kujiamini katika maisha ya mtu.

4). Tumia muda kuwa na watoto wako. Hiyo inawajulisha kwamba wao ni wa maana kwako. Kuwapa vitu haichukui nafasi ya wewe kujitoa kwao. Tena, watoto hushawishiwa zaidi na wale wanaokaa nao muda mwingi.

5). Ikibidi useme kitu kibaya, jaribu kukisema kwa uzuri. Mimi sikuwahi kuwaambia watoto wangu kwamba ni “wabaya” walipoacha kunitii. Badala yake, nilikuwa namwambia hivi kijana wangu, “Wewe ni mtoto mzuri, na watoto wazuri hawafanyi ulichofanya!” (Kisha nilikuwa namchapa kiboko.)

6). Tambua kwamba, neno “hapana” linamaanisha “ninakujali”. Watoto wanaporuhusiwa mambo yao kila wakati wanatambua kwama hujali kiasi cha kutosha kuwakataza chochote wakati wowote.

7). Tazamia watoto wako kukuiga wewe. Watoto hujifunza kwa mifano ya wazazi wao. Mzazi mwenye busara hawezi kumwambia mtoto wake, “Fanya ninavyokwambia. Usifanye kama ninavyofanya mimi.”

8). Usiwaokoe watoto wako na matatizo yao yote. Ondoa mawe yanayoweza kuwakwaza tu; acha mawe ya kukanyagia yabakie mbele yao.

9). Mtumikie (na kumfuata) Mungu kwa moyo wako wote. Nimeona kwamba watoto wa wazazi waliopoa kiroho huwa hawamfuati Mungu wakiwa watu wazima. Watoto Wakristo wa wazazi ambao hawajaokoka, na watoto wa wazazi Wakristo waliojitoa kabisa kwa Mungu huendelea na wokovu hata “wakiondoka kwenye kiota” – nyumbani.

10). Wafundishe watoto wako Neno la Mungu. Mara nyingi wazazi hutoa nafasi ya kwanza kwa elimu ya watoto wao, na kushindwa kuwapa elimu ya muhimu zaidi wanayoweza kupata – elimu ya Biblia.

Nafasi Ya Huduma, Ndoa Na Familia

Pengine kosa kubwa la kawaida kabisa lifanywalo na viongozi wa Kikristo ni kutokujali ndoa zao na familia zao kwa sababu ya kujitoa kwenye huduma. Wanajihesabia haki kwa kusema kwamba kujitoa kwao “ni kwa ajili ya kazi ya Bwana.”

Kosa hili hurekebika wakati mtumishi anayefanya wengine kuwa wanafunzi anapotambua kwamba utii wake halisi na kujitoa kwake kwa Mungu huonekana kwa mahusiano yake na mke wake na watoto. Mtumishi hawezi kudai kwamba amejitoa kwa Mungu ikiwa hampendi mke wake kama Kristo anavyolipenda kanisa, au kama atapuuzia kutumia muda unaotakiwa na watoto wake, ili kuwalea na kuwakuza katika kicho na kumcha Bwana.

Tena, kumpuuza mwenzi na watoto kwa sababu ya “huduma” ni ishara ya huduma ya kimwili kabisa, inayofanywa kwa nguvu za mtu binafsi. Wachungaji wengi wenye makanisa wanaobeba mizigo mizito ni mfano wa hili, maana wanajichosha ili kuhakikisha kwamba kila utaratibu wa kanisa unakwenda vizuri.

Yesu aliahidi kwamba mzigo Wake ni mwepesi na nira Yake ni laini (ona Mathayo 11:30). Hamwiti mtumishi yeyote kuonyesha anavyopenda dunia au anavyolipenda kanisa kwa kutowapenda watu wa familia yake. Sifa mojawapo ya mzee ni kwamba, “awe mwenye kuisimamia nyumba yake vema” (1Timo. 3:4). Mahusiano yake na familia yake ni kipimo cha uwezo wake kufanya huduma.

Wale walioitwa kufanya huduma za kusafiri na ambao inawabidi kuwa nje ya nyumbani mara kwa mara lazima watumie muda wa ziada kufikiri kuhusu familia zao wanapokuwa nyumbani. Washirika wengine katika mwili wa Kristo wafanye kinachowezekana ili kufanikisha hilo. Mtumishi anayefanya wengine kuwa wanafunzi anatambua kwamba watoto wake mwenyewe ndiyo wanafunzi wake wa kwanza. Akishindwa hapo, hana haki ya kujaribu kuwafundisha wengine walio nje ya nyumbani mwake kuwa wanafunzi.


[1] Mungu anazungumzia mambo waziwazi. Hebu tazama Wimbo Ulio Bora 7:1-9 na Walawi 18:1-23.

To subscribe to David Servant's periodic e-teachings, click here.


Mchungaji Afanyaye Watu Kuwa Wanafunzi » Familia Ya Kikristo