Kushindana Na Dhambi

SURA YA TISA

“Dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde” (Mwanzo 4:7).

KAMA tulivyoona katika sura iliyopita, utakaso wetu ni juhudi za pamoja kati ya Mungu na sisi wenyewe. Tunaendelea kuwa kama Yesu zaidi tunapozidisha ushirikiano na Baba. Yeye anatupa uwezo na hamasa ya kuwa watakatifu. “Kwa kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa” (2Petro 1:3 – Maneno mepesi kutilia mkazo). Yeye hutupa sisi asili mpya na kutuongoza kwa Roho Wake anayekaa ndani yetu. Lakini, anatuachia na sisi kitu cha kufanya. Bado tuna hiari yetu. Ni lazima tumfuate Roho anayekaa ndani yetu, na hili linafanywa na kila Mkristo wa kweli kwa kiwango fulani. Vinginevyo anajionyesha kuwa ni mwamini bandia (ona Warumi 8:5-14).

Vile vile ni wajibu wetu kufanya upya nia zetu kwa Neno la Mungu, maana lazima tujue mapenzi Yake kabla ya kuyatenda. Hata katika hilo pia Mungu hutusaidia kwa njia ya huduma ya kufundisha ya Roho Mtakatifu na kwa kupitia wanadamu waliotiwa mafuta kuwa waalimu. Nia zetu zinapofanywa upya na kweli Yake, tunabadilishwa (ona Yohana 8:31-36; Warumi 12:2). Kisha, tuna wajibu wa kutokuwa wasikilizaji tu wa neno bali watendaji pia (Yakobo 1:22).

Lazima mlingano huo utunzwe. Japo Maandiko yanafundisha juu ya wajibu wa Mungu na wa binadamu, watu wengi hukazia kimoja na kuacha kingine. Yamekuwepo makundi mawili kihistoria – wanaojaribu kuwa watakatifu kwa nguvu zao wenyewe, na wanaopinga juhudi zozote za kibinadamu kwa habari ya utakatifu, wakimwachia Mungu kila kitu. Pande zote mbili zina orodha ndefu ya maandiko, na kama wangetazama orodha zao wote wangetambua kwamba wote wako sawa na wote wamekosea. Ukweli uko katikati, mahali ambapo orodha zote mbili zinaheshimiwa. Hakuna mstari mmoja unaoeleza vizuri mlingano huo kuliko Wafilipi 2:12 na 13. Unasema hivi:

Basi wapendwa wangu, kama vile mlivyotii sikuzote, si wakati mimi nilipokuwapo tu bali sasa zaidi sana mimi nisipokuwapo, utimizeni wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka. Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema (Maneno mepesi kutilia mkazo).

Tunda ambalo Roho huzaa ndani yetu ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole na kiasi, lakini, matunda hayo yataonekana maishani mwetu kwa ushirikiano wetu tu. Ni lazima tufanye kitu fulani kwa sababu, kulingana na Maandiko, zipo nguvu kama tatu hivi zinazopinga matunda hayo.

(1) Mungu ameturuhusu sisi kubakia “duniani”, dunia ambayo inatujaribu tusiwe na upendo au kupendeka, tuwe na huzuni, tuwe na wasiwasi, tusivumilie, tusiwe wema, tuwe waovu, tusiwe waaminifu, tuwe wakali na wenye kujitosheleza.

(2) Ingawa Mungu ametujaza kwa Roho Wake, na kutupa asili mpya na kuvunja nguvu za dhambi juu yetu, Yeye pia ameruhusu mabaki ya asili yetu ya kale ya dhambi kubakia ndani yetu. Kitu hicho Paulo anakiita “mwili”.

(3) Ingawa tumekombolewa kutoka ufalme wa Shetani na sisi si watoto wake tena kiroho, tunajikuta kama wale Wakristo wa zamani tukiwa katika uwanja mkubwa uliojaa simba wanaounguruma, wenye lengo la kutumeza (ona 1Petro 5:8). Shetani na mapepo yake hutusumbua na kutunyanyasa na kutujaribu ili tufanye yale ambayo Mungu amekataza.

Hao watatu ndiyo adui zetu: dunia, mwili na shetani.

Kwa Nini Mungu Ametuacha Kwenye Eneo La Adui?

Kama Mungu anatamani tuwe watakatifu, mbona amewaruhusu adui hawa kuishi miongoni mwetu? Kwani wanatimiza kusudi gani la kimungu?

Adui zetu wanaruhusiwa kukaa miongoni mwetu ili Mungu atupime, kama alivyoruhusu mataifa maovu yabakie katika ardhi ya Israeli baada ya kufa kwa Yoshua (ona Waamuzi 2:20 hadi 3:1). Wao wanapima upendo wetu, utii wetu – yaani, imani yetu. Imani inaweza kupimwa wakati kunapokuwepo uwezekano wa kutokuamini. Upendo unaweza kupimwa wakati kuna uwezekano wa chuki. Utii unaweza kupimwa wakati kuna uwezekano wa kutokutii.

Mungu aliwaambia hivi Waisraeli wa zamani:

Kukizuka katikati yako nabii au mwotaji wa ndoto, akikutolea ishara au ajabu, ikatukia hiyo ishara au hiyo ajabu aliyokuambia akisema, ‘Na tuifuate miungu mingine usiyoijua, tuitumikie hiyo;’ wewe usiyasikilize maneno ya nabii yule au yule mwotaji wa ndoto, kwa kuwa BWANA Mungu wenu yuawajaribu, apate kujua kwamba mnampenda BWANA Mungu wenu kwa mioyo yenu yote na roho zenu zote. Tembeeni kwa kumfuata BWANA Mungu wenu; mcheni na kushika maagizo yake na kuisikia sauti yake, nanyi mtumikieni na kushikamana naye (Kumbu. 13:1-4).

Cha ajabu ni kwamba Mungu aliwapima watu Wake kwa kutumia nabii wa uongo! Lakini je! Hana maarifa yote pamoja na uwezo wa kujua mambo kabla? Mbona kuwe na haja ya kupimwa tena?

Sababu ni hii: Ili Mungu ajue matokeo ya kipimo cha mtu mwenye hiari, lazima huyo apimwe wakati fulani. Kinachoweza kujulikana kabla ni kitu kinachoweza kujulikana wakati fulani. Basi, majaribu yetu na dhiki na vipimo, ambavyo vina mipaka katika muda fulani, hutekeleza kusudi katika mpango wa Yule aishiye nje ya majira na nyakati. Hutoa njia ambayo kwayo imani yetu inathibitishwa kuwa ya kweli. Petro aliwaandikia hivi Wakristo waliokuwa wanapitia mambo magumu:

Mnafurahi sana wakati huo, ijapokuwa sasa kwa kitambo kidogo ikiwa ni lazima, mmehuzunishwa kwa majaribu ya namna mbalimbali; ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo … Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio kati yenu unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho. Lakini kama mnavyoyashiriki mateso ya Kristo, furahini; ili na katika ufunuo wa utukufu wake mfurahi kwa shangwe. (1Petro 1:6-7; 4:12-13. Maneno mepesi kutilia mkazo).

Hata kama hakuna sababu nyingine, tunapaswa kufurahi katika mateso kwa sababu yanaturuhusu nafasi ya kuonyesha imani yetu thabiti. Imani yenye kuokoa hudumu, lakini imani inaweza kuvumilia tu wakati kuna upinzani na majaribu ili isivumilie.

Wajibu Wetu Ni Nini?

Siku hizi wengi wanaojiita Wakristo wanamwachia Mungu wajibu wao ambao wamepewa na Biblia. Hii ni kwa sababu mafundisho ya kisasa ya kiinjili yamechafuliwa sana na mawazo ya kupinga kushika sheria, yenye kupotosha neema ya Mungu na kubatilisha wajibu wa mwanadamu. Kwa sababu wamedanganyika na mafundisho ya uongo kuhusu neema, ukiwatajia tu juhudi za kibinadamu unaonekana umekufuru, na huku wakidai kwamba wanatetea utukufu wa Mungu, wanasema fundisho lolote kuhusu utakatifu ni kuwafanya watu waishi kwa kufuata sheria. Matendo ni neno chafu ambalo halifai katika msamiati wa Kikristo. Hakika hatutaki liwepo wazo lolote kwamba sisi inatupasa kutenda chochote sasa kwa kuwa kazi ya Kristo imemalizika. Hiyo ni sawa na kuongezea matendo kwenye wokovu wetu (na Mungu apishe mbali!).

Kwa matazamio ya kujaribu kutibu shida hiyo ambayo haitokani na Maandiko, nimeorodhesha mambo ambayo sehemu kubwa ya Agano Jipya inasema tunapaswa kufanya. Sehemu muhimu ya wajibu wa mwanadamu katika mpango wa utakaso inaeleweka kirahisi kutokana na mistari mingi yenye maagizo na mashauri. Tunapoisoma, hatuwezi kuwa na mashaka tena kwamba Wakristo ni watu wenye hiari wanaoweza kuamua kuwa watakatifu. Pia, ule udanganyifu kwamba Mungu anaibiwa utukufu wakati tunapoongeza juudi zetu kwa habari ya utakaso unadhihirishwa wazi. Ni hivi: Mungu anawatazamia wale walio na Roho Wake Mtakatifu kufanya mambo fulani kwa nguvu za Roho. Kwa kifupi ni kwamba, sisi tunapaswa kushindana na dhambi katika hali zake zote. Sisi lazima tutafute utakatifu, ambao “hakuna mtu atakayemwona Mungu asipokuwa nao” (Webrania 12:14).

Orodha ifuatayo inafunua matazamio ya Mungu juu ya tabia yetu. Orodha imetolewa katika Injili zote nne na kitabu cha Warumi. Kama Agano Jipya linasema tabia fulani ni mbaya au ni kosa au ni dhambi, basi Mungu bila shaka anawawajibisha watu kwa tabia hiyo, kuonyesha kwamba wajibu wa mwanadamu ni kitu kinachohusika katika tabia hiyo mbaya.

Japo unaweza kujaribiwa kuiruka orodha hii ifuatayo, ningekushauri uisome pole pole kwa manufaa yako mwenyewe. Inaweza kukugusa kwa njia itakayobadili maisha yako.

Je, Mungu anatutazamia tufanye nini? Ifuatayo ni orodha. Ni dhahiri kwamba hakuna chochote katika haya yafuatayo kitakachotokea maishani mwetu bila sisi kufanya Mungu anavyosema.

Mungu anatutazamia:

Tusimjaribu (Mathayo 4:7).

Tumwabudu Bwana Mungu wetu na kumtumikia Yeye tu (Mathayo 4:10).

Tutubu ili tuokolewe (Mathayo 4:17).

Tufurahi na kushangilia wakati tunapoteswa (Mathayo 5:12).

Tuache nuru yetu iangaze mbele za watu ili wayaone matendo yetu mema (Mathayo 5:16).

Tushike amri za Mungu na kuzifundisha, hata zile zilizo ndogo kabisa (Mathayo 5:19).

Tusiue, kumchukia wala kumdhuru mtu yeyote kwa njia yoyote ile (Mathayo 5:21-22).

Tujishughulishe kupatana na wale ambao tumewakosea (Mathayo 5:24-25).

Tusizini wala kuwa na tamaa mbaya (Mathayo 5:27-28).

Tuondoe chochote kinachotufanya tuangukie dhambini (Mathayo 5:29-30).

Tusivunje ndoa isipokuwa kwa uasherati (Mathayo 5:32).

Tusiape na tusidanganye. Kila mara tutimize maneno yetu (Mathayo 5:33-37).

Tusijilipize kisasi bali tuwavumilie sana wengine, hata kuwatendea mema wanaotutendea mabaya (Mathayo 5:38-42).

Tuwapende adui zetu na kuwaombea wanaotutesa (Mathayo 5:44-47).

Tujaribu kuwa wakamilifu (Mathayo 5:48).

Tusifanye mema ili tupokee sifa za watu (Mathayo 6:1).

Tutoe sadaka (Mathayo 6:2-4).

Tuombe (Mathayo 6:5-6).

Tusirudie-rudie maneno yasiyo na maana tunapoomba (Mathayo 6:7).

Tuombe kwa kufuata mfano wa “Sala ya Bwana” (Mathayo 6:9-13).

Tuwasamehe wengine (Mathayo 6:14).

Tufunge, yaani tusile chakula (Mathayo 6:16).

Tusijiwekee hazina duniani, bali mbinguni (Mathayo 6:19-21).

Tumtumikie Mungu, siyo fedha (Mathayo 6:24).

Tusiwe na wasiwasi kuhusu mahitaji yetu (Mathayo 6:25-32).

Tutafute kwanza ufalme wa Mungu na haki Yake (Mathayo 6:33).

Tusiwahukumu wengine (Mathayo 7:1-5).

Tusiwape mbwa kilicho kitakatifu (7:6).

Tuombe, tutafute, tubishe (Mathayo 7:7-11).

Tuwatendee wengine tunavyotaka kutendewa (Mathayo 7:12).

Tuingie kwa kupitia mlango mwembamba (Mathayo 7:13).

Tujihadhari na manabii wa uongo (Mathayo 7:15-20).

Tufanye aliyosema Yesu au tuangamie (Mathayo 7:24-27).

Tumwombe Bwana awatume watenda kazi katika shamba Lake (Mathayo 9:38).

Tumkiri Yesu mbele ya wengine. Tusimkane (Mathayo 10:32-33).

Tumpende Yesu kuliko watu walio karibu nasi (Mathayo 10:37).

Tujitwike msalaba na kumfuata Yesu (Mathayo 10:38).

Tupoteze maisha yetu kwa ajili ya Yesu (Mathayo 10:39).

Tujitie nira ya Yesu (Mathayo 11:28-30).

Tuwe “pamoja” na Yesu kukusanya (Mathayo 12:30).

Tusimkufuru Roho Mtakatifu (Mathayo 12:31).

Tufanye mapenzi ya Baba (Mathayo 12:50).

Tuwaheshimu wazazi wetu (Mathayo 15:4-6).

Tusinajisike kwa mawazo machafu, mauaji, uasherati, uzinzi, wizi, udanganyifu na hila (Mathayo 15:19-20).

Tujikane (Mathayo 16:24).

Tuongoke na kuwa kama watoto. Tujinyenyekeze (Mathayo 18:3-4).

Tusimfanye mtoto yeyote anayemwamini Yesu ajikwae (Mathayo 18:6).

Tusimfanye yoyote ajikwae (Mathayo 18:7).

Tusiwadharau watoto (Mathayo 18:10).

Tumkemee kibinafsi ndugu yeyote anayetukosea (Mathayo 18:15).

Tutii agizo la Yesu kuhusu adhabu kikanisa (Mathayo 18:16-17).

Tuwasamehe ndugu zetu kutoka moyoni (Mathayo 18:35).

Tumpende jirani yetu kama tunavyojipenda wenyewe (Mathayo 19:19).

Tuwe watumishi wa wengine (Mathayo 20:26-28).

Tulipe kodi halali kwa serikali na kumpa Mungu sehemu Yake (Mathayo 22:21).

Tumpende Bwana Mungu kwa moyo wote, roho yote na akili (Mathayo 22:37).

Tusikubali yeyote kutuita ‘mwalimu’ au ‘bwana’ na tusimwite yeyote baba isipokuwa Baba yetu wa mbinguni (Mathayo 23:8-10).

Tusijiinue bali tujishushe (Mathayo 23:12).

Tusimzuie yeyote kuingia katika ufalme wa Mungu (Mathayo 23:13).

Tusiwaonee wajane (Mathayo 23:14).

Tusiwashawishi wengine kuwa wanafiki (Mathayo 23:15).

Tusipuuzie mambo makuu katika Torati kama vile haki, rehema na uaminifu (Mathayo 23:23).

Tusiwe wanafiki kwa njia yoyote ile (Mathayo 23:25-28).

Tusiogope kuhusu vita au matetesi ya vita kabla ya kurudi kwa Yesu (Mathayo 24:6).

Tusianguke, au kusaliti au kumchukia ndugu (Mathayo 24:10).

Tusikubali kupotoshwa na manabii wa uongo (Mathayo 24:11).

Tusiruhusu pendo letu kupoa kwa sababu maasi yameongezeka (Mathayo 24:12).

Tuvumilie mpaka mwisho (Mathayo 24:13).

Tusiamini taarifa za uongo kuhusu kurudi kwa Kristo (Mathayo 24:23-26).

Tutambue ishara za kurudi kwake Kristo (Mathayo 24:32-33).

Tuwe macho kwa ajili ya kurudi kwa Kristo (Mathayo 24:42).

Kila mara tuwe watumwa waaminifu, tukitazamia kurudi kwa Bwana wetu upesi. Tusirudi nyuma bali kila wakati tumtii (Mathayo 24:45-51).

Tutumie muda, vipawa na hazina ambavyo Mungu ametupa kwa ajili ya utumishi Wake (Mathayo 25:14-30).

Tuwape Wakristo maskini chakula, cha kunywa na mavazi. Tuwatembelee Wakristo waliofungwa na walio wagonjwa (Mathayo 25:34-40). Tushiriki Meza ya Bwana (Mathayo 26:26-27).

Tufanye wanafunzi katika mataifa yote, tukiwabatiza katika jina la Baba, Mwana na Roho Mtakatifu na kuwafundisha kuyashika yote aliyoamuru Yesu (Mathayo 28:19-20).

Tujihadhari tunasikia nini (Marko 4:24).

Tusipuuze amri za Mungu kwa ajili ya kushika mapokeo (Marko 7:9).

Tusimwonee Yesu aibu, wala maneno Yake (Marko 8:38).

Tuwe na amani sisi kwa sisi (Marko 9:50).

Tusiwazuie watoto kwenda kwa Yesu (Marko 10:14).

Tuwe na imani kwa Mungu (Marko 11:22).

Tuamini kwamba tumepokea yote tuyaombayo (Marko 11:24).

Tujihadhari na waalimu wa uongo waliovaa mavazi yanayowafanya waonekane, wanaopenda kusalimiwa kwa heshima, viti vya mbele na mahali pa heshima, wanaowaonea wajane na kuomba sala ndefu ili waonekane tu (Marko 12:38-40).

Tusiogope tutasema nini tukifikishwa mahakamani kwa ajili ya imani yetu bali tuseme kile ambacho Roho Mtakatifu atatwambia wakati huo (Marko 13:11).

Tubatizwe (Marko 16:16).

Tuwabariki wanaotulaani (Luka 6:28).

Tumpe kila atuombaye, wala tusidai vitu tulivyonyang’anywa (Luka 6:30).

Tuwakopeshe wengine, wala tusitazamie kulipwa (Luka 6:35).

Tuwe wenye rehema (Luka 6:36).

Tusiwahukumu wengine (Luka 6:37).

Tutoe (Luka 6:38).

Tusinyoshe kidole kuhusu kibanzi katika jicho la ndugu wakati sisi tuna boriti katika jicho letu (Luka 6:41-42).

Tusimwite “Bwana” kama hatufanyi asemayo (Luka 6:46-49).

Tulipokee Neno la Mungu mioyoni mwetu na kulishika ili tuzae matunda kwa saburi (Luka 8:12-15).

Tulisikie Neno la Mungu na kulitenda (Luka 8:21).

Tuwapokee watoto katika jina la Kristo (Luka 9:48).

Tusiangalie nyuma baada ya kutia mkono kwenye jembe (Luka 9:62).

Tuombe kupewa Roho Mtakatifu (Luka 11:13).

Tujihadhari nuru ndani yetu isiwe giza (Luka 11:35).

Tusipende viti vya heshima na salaamu (Luka 11:43).

Tusiwalemee watu wengine kwa mizigo mizito ambayo sisi hatuko tayari kuibeba (Luka 11:46).

Tusiwatese manabii Wake (Luka 11:49).

Tusiondoe ufunguo wa maarifa wala kuwazuia watu wasiingie katika maarifa ya kweli ya Mungu (Luka 11:52).

Tujihadhari na viongozi wa dini walio wanafiki (Luka 12:1).

Tusiogope wale wanaoweza kutuua kimwili tu (Luka 12:4).

Tumwogope yeye ambaye, baada ya kuua ana mamlaka ya kutupa kuzimuni (Luka 12:5).

Tusinene mabaya wala kumkufuru Yesu au Roho Mtakatifu (Luka 12:10).

Tujihadhari na kujilinda na choyo (Luka 12:15).

Tusijiwekee hazina bali tuwe matajiri kwa Mungu (Luka 12:21).

Tuuze mali zetu na kuwapa maskini (Luka 12:33).

Tuzae matunda (Luka 13:6-9).

Tujitahidi kuingia kwa kupitia mlango mwembamba (Luka 13:24).

Tusichukue mahali pa heshima, tukijitukuza wenyewe. Bali tujinyenyekeze, tukikaa kiti cha nyuma (Luka 14:8-10).

Tumpende Yeye kuliko wapendwa wetu (Luka 14:26).

Kwanza tuhesabu gharama ya kuwa wanafunzi Wake (Luka 14:28-32).

Tuweke mali yetu yote chini ya mamlaka Yake (Luka 14:33).

Tufurahi wakati Mungu anapowahurumia wenye dhambi kwa kuwaokoa (Luka 15:1-32).

Tuwe waaminifu katika mambo madogo, na fedha (Luka 16:9-11).

Tuwahurumie maskini (Luka 16:19-31).

Tumkemee ndugu akikosa, na kumsamehe akitubu (Luka 17:3-4).

Tujihesabu kuwa watumwa wasiofaa hata baada ya kufanya yote tuliyoagizwa kufanya (Luka 17:7-10).

Tuombe wakati wote wala tusikate tamaa (Luka 18:1).

Tusijione kwamba ni wenye haki, wala tusiwadharau wengine (Luka 18:9).

Tuupokee ufalme kama mtoto (Luka 18:17).

Tuwe macho wakati wote na kuomba ili tuweze kuepukana na majaribu yatakayokuwepo kabla ya kurudi kwa Kristo, na tuweze kusimama mbele zake (Luka 21:36).

Tutangaze toba na msamaha wa dhambi katika Jina la Yesu kwa mataifa yote (Luka 24:47).

Tuzaliwe mara ya pili (Yohana 3:3).

Tumwamini Yesu (Yohana 3:16).

Tumwabudu katika roho na kweli (Yohana 4:23-24).

Tumheshimu Yesu (Yohana 5:23).

Tutafute utukufu kutoka kwa Mungu (Yohana 5:44).

Tuamini aliyoandika Musa (Yohana 5:46-47).

Tusikitendee kazi chakula kiharibikacho, bali kidumucho mpaka uzima wa milele kinachotolewa na Yesu (Yohana 6:53-54).

Tusihukumu kwa jinsi mtu anavyo-onekana, bali kwa haki (Yohana 7:24).

Tukae katika neno la Yesu (Yohana 8:31).

Tulishike neno la Yesu (Yohana 8:51).

Tumtumikie (na kumfuata) Yesu (Yohana 12:26).

Tupendane, kama Yesu anavyotupenda (Yohana 13:34).

Tuamini kwamba Yeye ni ndani ya Baba, na Baba ndani Yake (Yohana 14:11).

Tufanye matendo ya Yesu, na hata makubwa zaidi (Yohana 14:12).

Tumpende Yesu na kuzishika amri Zake (Yohana 14:15).

Tukae katika pendo la Yesu (Yohana 15:9).

Tuombe lolote katika Jina la Yesu (Yohana 16:24).

Tuwe na ujasiri katika dhiki (Yohana 16:33).

Huo ndiyo mwisho wa amri za Yesu zipatikanazo katika Injili. Hayo ndiyo mambo ambayo tunapaswa kuwa tunawafundisha wanafunzi wa Kristo kwamba wayatii (ona Mathayo 28:20).

Amri na maagizo kwa ajili ya waamini katika nyaraka si tofauti sana na Injili. Sasa hebu tutazame wajibu wa mwanadamu kutoka kitabu cha Warumi tu.

Mungu anatazamia tufanye haya yafuatayo:

Tusifiche au kugandamiza ukweli (Warumi 1:18).

Tusiwe na hatia ya kuabudu sanamu (Warumi 1:23).

Tusibadili kweli ya Mungu kwa uongo (Warumi 1:25).

Tusihusike katika ulawiti (Warumi 1:26, 27).

Tusiwe wachoyo, wenye wivu, wadanganyifu, wabaya, wenye dharau, wakorofi, wenye kiburi, wasiotii wazazi, wasioaminika, wasiopenda na wasio na rehema (Warumi 1:29-31).

Tusiwasengenye watu wala kuwasingizia uongo (Warumi 1:29-30).

Tusiwaunge mkono watendao dhambi (Warumi 1:32).

Tusipuuzie utajiri wa wema Wake, ustahimilivu na uvumilivu (Warumi 2:4).

Tudumu katika kutenda mema (Warumi 2:7).

Tutafute utukufu, heshima na kutokuharibika (Warumi 2:7).

Tusiwe na tamaa ya ubinafsi (Warumi 2:8).

Tusilaani au kusema maneno yenye uchungu (Warumi 3:14).

Tujihesabu wafu kwa dhambi bali hai kwa Mungu katika Kristo (Warumi 6:11).

Tusiruhusu dhambi itawale miili yetu. Tusitii tamaa yake (Warumi 6:13).

Tujitoe kwa Mungu kama walio hai kutoka kwa wafu, na viungo vyetu kama vyombo kwa ajili ya haki kwa Mungu (Warumi 6:13).

Tusitamani (Warumi 7:7).

Tusiishi kulingana na mwili, bali tuyafishe matendo ya mwili kwa njia ya Roho (Warumi 8:12-13).

Tuitoe miili yetu kama dhabihu iliyo hai na takatifu (Warumi 12:1).

Tusifananishwe na dunia hii, bali tufanywe upya kwa kugeuzwa nia zetu (Warumi 12:2).

Tusinie makuu kuliko inavyopasa (Warumi 12:3).

Tutumie vipawa vyetu kulingana na neema tuliyopewa (Warumi 12:6).

Tuwapende wengine bila unafiki (Warumi 12:9).

Tukatae lililo ovu na kushika lililo jema (Warumi 12:9).

Tupendane kindugu na kupeana heshima (Warumi 12:10).

Tusilegee (Warumi 12:11).

Tuwe na juhudi tunapomtumikia Bwana (Warumi 12:11).

Tufurahi katika tumaini (Warumi 12:12).

Tuvumilie katika dhiki (Warumi 12:12).

Tudumu katika maombi (Warumi 12:12).

Tusaidie mahitaji ya watakatifu (Warumi 12:13).

Tuwe wakarimu (Warumi 12:13).

Tuwabariki wanaotulaani, tusiwalaani sisi (Warumi 12:14).

Tufurahi na wanaofurahi, tulie na wanaolia (Warumi 12:15).

Tusiwe wenye majivuno bali tushirikiane na wa hali ya chini (Warumi 12:16).

Tusiwe wenye hekima machoni petu wenyewe (Warumi 12:16).

Kamwe tusilipe ovu kwa ovu (Warumi 12:17).

Tujali lililo jema machoni pa watu wote (Warumi 12:17).

Kadiri iwezekanavyo, tukae kwa amani na watu wote (Warumi 12:18).

Tusijilipizie kisasi (Warumi 12:19).

Adui yetu akiwa na njaa tumlishe, akiwa na kiu tumnyweshe (Warumi 12:20).

Tusishindwe na ubaya, bali tuushinde kwa wema (Warumi 12:21).

Tukubali mamlaka ya wakuu wa serikali (Warumi 13:1).

Tusidaiwe chochote na mtu isipokuwa kupendana (Warumi 13:8).

Tuweke kando matendo yote ya giza na kuvaa silaha za nuru (Warumi 13:12).

Tuenende ipasavyo mchana, sio katika vurugu na ulevi, uasherati na tamaa mbaya, wivu au fujo. Tumvae Kristo na tusitoe nafasi kwa mwili na tamaa zake mbaya (Warumi 13:13-14).

Tuwapokee walio dhaifu katika imani (Warumi 14:1).

Tusimhukumu ndugu wala kumdharau (Warumi 14:10).

Tusiweke vikwazo mbele ya ndugu (Warumi 14:13).

Tufuate mambo yaletayo amani na kujengana (Warumi 14:19).

Tuichukue mizigo ya walio dhaifu kama sisi tuna nguvu. Tusijipendeze wenyewe (Warumi 15:1).

Tupokeane na kukubaliana, kama Kristo alivyofanya kwetu (Warumi 15:7).

Tuwatazame wenye kuleta matengano na vipingamizi kinyume cha kweli za Biblia na kuachana nao (Warumi 16:17).

Sasa niulize hivi: Je, Wakristo wanawajibika kama wanadamu? Tuseme nini juu ya mtu yule anayesema kwamba yeye ameliacha jambo la utakaso wake mikononi mwa Mungu, asije akamwibia Mungu utukufu wake na kuwa na hatia ya kuongezea matendo yake kwenye wokovu?

Vita Ya Kiroho

Kila moja katika zile amri na maagizo kwenye orodha hiyo iliyopita inathibitisha wazo kwamba mwanadamu anawajibika, lakini pia kwamba sisi sote tunakabiliwa na maamuzi. Tunaweza kuchagua kufanya au kutofanya yale aliyosema Yesu. Kutoka katika roho zetu zilizozaliwa upya, Roho Mtakatifu hutuongoza kutii, lakini nguvu zingine – dunia, mwili na Shetani – hutujaribu kutotii. Basi tunajikuta katika vita.

Kuna hoja mbili za kusemwa hapa. Kwanza: Wakristo wa bandia wakati mwingine – kwa makosa – hufikiri kwamba wanapitia katika hiyo vita ya kiroho. Lakini kihalisi, wao wanapitia vita inayofanana na hiyo, kati ya dhamiri zao na asili zao za dhambi. Kulingana na Paulo, hata watu ambao hawajaokoka wana dhamiri ambayo inawashtaki au kuwatetea (ona Warumi 2:15). Kwa kuwa wameikosea mara nyingi sana, dhamiri yao imekwisha najisika (Tito 1:15), na sauti yake inaendelea kupungua kadiri wanavyopuuza maonyo yake. Lakini, Mkristo wa kweli ana dhamiri ambayo imeamka kabisa, yenye kusema naye kila wakati, na si rahisi kuipuuza. Roho wa Mungu anawaongoza wote walio watoto wa Mungu kweli (ona Warumi 8:14).

Jambo la pili ni kwamba wanaojiita Wakristo mara nyingi hutumia hiyo vita ya kiroho kama kichocheo cha kutenda dhambi. Wanasema hivi: “Tuko vitani. Kama ni hivyo, lazima tutashindwa mapigano fulani fulani.” Kujitetea huko ni sawa na kusema hivi: “Bwana wee! Hakuna aliye mkamilifu! (Kwa hiyo nitakuwa dhaifu tu.)”

Mungu ndiye aliyeruhusu vita hiyo ya kiroho iwepo kwa enzi Yake, na kusudi Lake si kwamba watoto Wake waingie dhambini. Kusudi Lake ni kwamba tujithibitishe kuwa washindaji kwa utukufu Wake. Hebu fikiri maneno ya Paulo juu ya vita kati ya mwili na Roho katika Wagalatia sura ya 5.

Basi nasema, ‘Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka. Lakini mkiongozwa na Roho hampo chini ya sheria. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo. Katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulubisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake (5:16-24).

Bila shaka Wakristo wana asili mbili, asili ya dhambi yenye kupingana na Roho Mtakatifu aliye ndani. Lakini je, hii ni njia tu ya kukubaliana na dhambi? Hapana! Paulo anaonya kwamba wale wanaotenda matendo ya mwili hawataurithi ufalme wa Mungu. Ukweli ni kwamba hakuna Mkristo wa kweli anayetoa nafasi kwa mwili, kwa sababu, kama anavyosema Paulo, “Walio wa Kristo Yesu wameusulubisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake” (5:24). Hayo yalifanyika wakati wa wokovu, imani ya moyoni ilipoonyeshwa kwa toba na kujinyenyekeza kuwa chini ya mamlaka ya Yesu Kristo kama Bwana. Wakati huo – kwa lugha ya mfano – tulimsulubisha yule mtu wa kale wa dhambi msalabani. Naye anatakiwa kubakia hapo. Bado yuko hai na anaweza kulia aruhusiwe kufanya anachotaka, lakini kwa uwezo wa Roho kilio chake hakuna anayekisikiliza.

Katika Mwili Au Katika Roho?

Katika sura ya nane ya Warumi, Paulo anaonyesha tofauti kati ya mtu ambaye hajaokoka – anayemtaja kuwa yuko “katika mwili” – na mtu aliyeokoka – anayemtaja kuwa yuko “katika Roho”. Jambo hili ni muhimu sana kwetu kulifahamu. Hebu soma kwa makini sana maneno ya Paulo tunapotafakari Maandiko haya.

Maana yale yasiyowezekana kwa sheria, kwa vile ilivyokuwa dhaifu kwa sababu ya mwili, Mungu, kwa kumtuma Mwanawe mwenyewe katika mfano wa mwili ulio wa dhambi, na kwa sababu ya dhambi, aliihukumu dhambi katika mwili; ili maagizo ya torati yatimizwe ndani yetu sisi, tusioenenda kwa kufuata mambo ya mwili bali mambo ya Roho (Warumi 8:3-4).

Ona kwamba tayari Paulo ameeleza juu ya waamini kwamba ni wale wasio “enenda kwa kufuata mambo ya mwili, bali mambo ya Roho.”

Kwa maana wale waufuatao mwili huyafikiri mambo ya mwili; bali wale waifuatao roho huyafikiri mambo ya roho. Kwa kuwa nia ya mwili ni mauti; bali nia ya roho ni uzima na amani. Kwa kuwa ile nia ya mwili ni uadui juu ya Mungu, kwa maana haitii sheria ya Mungu, wala haiwezi kuitii. Wale waufuatao mwili hawawezi kumpendeza Mungu. Lakini ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake. (Warumi 8:5-9. Maneno mepesi kutilia mkazo).

Ni dhahiri hapo kwamba Paulo haonyeshi tofauti kati ya aina mbili za Wakristo – wale wawekao nia zao kwa mwili na wale wawekao nia zao kwa Roho. Yeye anawatofautisha wale ambao ndani yao yupo Roho wa Mungu, ambao wanaweka nia zao kwa Roho, na wale ambao hawana Roho ndani yao, wenye kuweka nia zao kwenye mwili – yaani Wakristo na wasiokuwa Wakristo.

Wakristo wanaweza kutajwa kwamba wana Kristo ndani yao, kwa yule Roho Mtakatifu anayekaa ndani yao, japo bado wana asili ya dhambi ya mwili.

Na Kristo akiwa ndani yenu, mwili wenu umekufa kwa sababu ya dhambi; bali roho yenu ni hai kwa sababu ya haki. Lakini, ikiwa Roho wake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu (Warumi 8:10-11).

Mwili wetu – “utu wetu wa nje” kama anavyouita Paulo – “umekufa” au “unachakaa” kwa sababu ya dhambi (2Wakor. 4:16). Lakini roho yetu – “utu wetu wa ndani” – sasa unahuishwa na kuwa hai kwa sababu tumefanywa kuwa wenye haki. Unafanywa upya siku kwa siku (ona 2Wakor. 4:16). Lakini, tunaweza kutazamia siku ile ambapo Roho ndani yetu ataihuisha “miili yetu ya kufa,” na wakati huo miili yetu nayo itafanywa mipya. Bila shaka Mungu anakusudia kwamba Roho anayekaa ndani yetu atawale miili yetu. Imekusudiwa kwamba atawale mpaka miili yetu ibadilishwe na ile asili ya dhambi ifutiliwe mbali kabisa.

Mwishoni, Paulo anawaonya waamini ambao alikuwa anawaandikia kuhusu kujitoa kwa mwili. Kwa nguvu ya Roho aliye ndani yao, wanaweza “kuyafisha matendo ya mwili.” Hili ni jambo ambalo lazima wao walitende. Anasema hivi:

Basi kama ni hivyo ndugu, tu wadeni, si wa mwili tuishi kwa kufuata mambo ya mwili. Kwa maana kama tukiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi. Kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu (Warumi 8:12-14).

Je, wewe ni yule ambaye Paulo anasema hutakufa bali utaishi – yaani, yule ambaye “kwa Roho” unaya “fisha matendo ya mwili”? Kama ndiyo, basi wewe ni Mkristo wa kweli. Paulo aliamini kwamba Wakristo wa kweli wanatenda tofauti na wasiokuwa Wakristo. Kama alivyosema, ni wale wanaoongozwa na Roho ndiyo wana wa Mungu wa kweli (ona Warumi 8:14).

Hoja Inajibiwa

Kuna wanaoweza kupinga hivi: “Hivi, Paulo mwenyewe si alikiri kwamba hata yeye alitenda yale mabaya aliyoyachukia, mpaka akajiita ‘maskini’ mwenye ole?”

Kweli, alifanya hivyo. Ukweli ni kwamba Paulo alisema maneno hayo katika sura ya saba ya Warumi, kabla ya kile ambacho tumekuwa tukitazama katika sura ya nane. Wakristo wamejadili kuhusu jambo hilo miaka na miaka – kwamba, je, Paulo alikuwa anazungumzia ujuzi wake kabla ya kuokoka au baada? Wale wenye kufundisha kwamba kushika sheria si vizuri wanapenda kuyaweka maneno ya Paulo hayo kwamba ndiyo kawaida katika maisha ya Kikristo.

Lakini, tukisoma Warumi sura ya 7 katika mantiki ya zile sura mbili zilizotangulia, pamoja mengine yote aliyoandika Paulo na Agano Jipya, tutapata tafsiri moja tu. Bila shaka Paulo alikuwa anazungumza juu ya mambo yalivyokuwa kabla Roho Mtakatifu hajakaa ndani yake. Vinginevyo, katika sura ya 7 anapingana na yale aliyoandika mwenyewe katika sura ya 6 na ya 8 kuhusu maisha ya kawaida ya Kikristo. Kuna swali zuri sana ambalo limewahi kuulizwa: “Kama huyo anayesemwa katika sura ya 7 ni mwamini aliyeokoka, nani basi anayesemwa katika sura ya 6 na ya 8?” Bila shaka ni watu wawili tofauti!

Kwanza: Tunaona kwamba kweli kuu ya sura ya 6 ni kutokulingana kwa dhambi na uumbaji mpya. Paulo alianza kwa swali: “Tudumu katika dhambi ili neema izidi kuwa nyingi?” (6:1) Jibu lake? “Hasha!” Kisha akaandika jinsi isivyowezekana kwa mwamini kuwa katika hali hiyo, hivi: “Sisi tuliofia dhambi tutaishije tena katika dhambi?” (6:2)

Katika mistari inayofuata, Paulo aliweka wazi zaidi kwamba waamini wote wameunganishwa na Yesu katika mauti na kufufuka Kwake, ili waweze “kuenenda katika upya wa uzima” (6:4), kwa kuwa wao si “watumwa wa dhambi” tena (6:6, 17, 20). Wao sasa wamewekwa “huru na dhambi” (6:7, 18, 22), ni “watumwa wa haki” (6:18), na ni “watumwa wa Mungu” (6:22), baada ya wao kutii “kwa mioyo ile namna ya elimu ambayo mliwekwa chini yake” (6:17). Dhambi “haitatawala tena” juu yao, kwa hiyo, wasiiruhusu “itawale” katika miili yao, wala wasikubaliane na tamaa zake (6:12). Badala yake, watoe viungo vyao “vitumiwe na haki ili mpate kutakaswa” (6:19).

Sasa, huyu Mkristo wa sura ya 6 analinganaje na mtu wa sura ya 7, ambaye Paulo anamsema kwamba ni “wa mwilini, chini ya dhambi” (7:14), ambaye anatenda yale maovu asiyotaka kuyatenda (7:15, 19), “mateka wa ile sheria ya dhambi” (7:23), na mtu “maskini, tena ole” (7:24)? Je, yule mtu wa sura ya 6 ambaye amewekwa huru kutokana na dhambi ndiye huyo huyo maskini ole wa sura ya 7 ambaye ni mfungwa wa dhambi? Je, yule mtu wa sura ya 6, ambaye asili yake ya zamani imesulubiwa na Kristo ili mwili wake “wa dhambi ubatilishwe” (6:6) ndiye huyo huyo wa sura ya 7 anayetamani sana mtu amweke huru na “mwil huu wa mauti” (7:24)? Haiwezekani! Au wewe unaonaje?

Tena, ile mistari 14 ya kwanza katika sura ya 8 ambayo tumekwisha itazama inazua maswali mengi zaidi, ikiwa yule mtu wa sura ya 7 ameokoka. Katika sura ya 8, Paulo alimwelezea Mkristo wa kweli kwamba haenendi “kwa kuufuata mwili, bali kwa kuifuata Roho (8:4). Akili yake imemwelekea Roho, sio mwili, ambayo ni tofauti na nia ya wasiokuwa Wakristo (8:5-6). Mkristo wa kweli ni yule ambaye hayuko “katika mwili” bali yuko “katika Roho” kwa sababu Roho anakaa ndani yake (8:9). Paulo hata aliwaonya wale wanaoishi kwa kuufuata mwili kwamba lazima wafe, na anawaahidi wale ambao, “kwa Roho wanayafisha matendo ya mwili” (8:13) kwamba wataishi. Kama Paulo alikuwa anazungumza juu ya ujuzi wake binafsi katika sura ya 7, tunajaribiwa kumwambia asome barua yake mwenyewe ili agundue jinsi ya kuokoka na kuwekwa huru na dhambi! Na kulingana na mashauri yake mengine yote kuhusu utakatifu ambayo ametoa kwa watu, itabidi tumweke katika fungu la mnafiki aliyehubiri hivi: “Fanyeni ninavyosema, sio kama ninavyotenda.”

Kumweka Paulo Sawa

Kama Paulo alikuwa anafanya ule ule uovu aliokuwa anauchukia, basi kwa maneno yake mwenyewe ya kuelewa wasioamini katika barua hii na zingine, hata yeye hakuwa ameokoka. (Ona Warumi 2:8-9; 1Wakor. 6:9-11; Wagalatia 5:19-21; Waefeso 5:5-6). Kulingana na yale ambayo Yohana naye aliandika, Paulo hakuwa ameokoka. Anasema hivi: “Atendaye dhambi ni wa ibilisi … Kila aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi … Yeyote asiyetenda haki si wa Mungu …” (1Yohana 3:8-10, TLR).

Ikiwa Paulo katika sura ya 7 ya Warumi alizungumza juu yake mwenyewe kwamba ni mfungwa wa dhambi atendaye maovu, basi sisi wengine tuliosoma juu yake katika sehemu zingine tunashangaa kweli kweli. Ingawa alikiri kwamba hakuwa amefikia ukamilifu (ona Wafilipi 3:12), aliwaandikia Wakorintho kwamba yeye hakuwa na lawama juu yake mwenyewe (1Wakor. 4:4), na akaendelea kusema hivi:

Kwa maana kujisifu kwetu ni huku, ushuhuda wa dhamiri yetu, ya kwamba kwa utakatifu na weupe wa moyo utokao kwa Mungu; si kwa hekima ya mwili, bali kwa neema ya Mungu; tulienenda katika dunia, na hasa kwenu ninyi” (2Wakor. 1:12).

Aliwaandikia hivi Wakristo Wathesalonike:

Ninyi ni mashahidi, na Mungu pia, jinsi tulivyokaa kwenu ninyi mnaoamini, kwa utakatifu, na kwa haki, bila kulaumiwa” (1Wathes. 2:10).

Alishuhudia kwa Timotheo kwamba alimtumikia Mungu kwa dhamiri safi (ona 2timo. 1:3). Mtu anapata picha anaposoma hadithi ya Paulo na barua zake kwamba alikuwa mtu aliyefanana na Kristo. Uaminifu wake haulinganishwi na yeyote katika Agano Jipya isipokuwa Yesu. Sasa, tunawezaje basi kumdhania akitenda maovu?

Jibu la pekee tunaloweza kulipata kutokana na ushahidi huo wote ni kwamba Paulo alikuwa anazungumza juu ya ujuzi wake kabla hajaokoka.

Mtu anaweza kuuliza hivi: “Lakini si aliandika sura ya 7 akitumia maneno ya wakati uliopo? Je, huo si ushahidi kwamba alikuwa anaandika juu ya hali yake ya wakati huo?”

Hapana. Kwamba alitumia maneno ya wakati uliopo haithibitishi chochote. Mara nyingi tunatumia maneno ya wakati uliopo ili kusimulia jambo lililopita. Ninaweza kusimulia habari ya uvuvi iliyotokea miaka kumi iliyopita kwa kusema, “Basi, niko kwenye mtumbwi wangu, mahali ninapopenda sana ziwani. Mara nasikia ndoana imenasa – sina hakika kama ni samaki au ndiyo imenaswa na majani. Kisha inajigusa! Ninaanza kuvutana na samaki mkubwa kuliko wote niliowahi kushika! Ninapomfikisha karibu na mtumbwi, mshipi unakatika, na samaki mkubwa anajiendea zake huru! Ole wangu, maskini mimi! Nani atakayeniokoa na mchezo huo?”

“Sawa, lakini, Paulo si anasema katika Warumi 7 kwamba yeye hakutaka kufanya mabaya bali mema? Hakusema, ‘Kwa utu wa ndani ninaifurahia sheria ya Mungu’ (7:22)? Angewezaje kusema hayo kama hajaokoka? Watu ambao hawajaokoka si waovu kabisa kabisa, walioharibika vibaya sana?”

Kumbuka kwamba Paulo alikuwa Myahudi Farisayo mwenye juhudi sana kabla ya wokovu. Yeye hakuwa kama mtu wa kawaida ambaye hajaokoka – yeye alikuwa anafanya kila alichoweza ili kutii amri za Mungu – mpaka kufikia hata kuliudhi kanisa! Lakini aligundua kwamba kadiri alivyojitahidi sana, asingeweza kutimiza masharti ya kiwango cha Mungu. Alikuwa mtumwa wa dhambi. Mwishoni akatambua kwamba hataweza kuwa mtakatifu bila ya msaada wa Roho Mtakatifu. Kweli – hakuna mtu maskini mwenye ole kuliko yule anayejaribu kuishi kulingana na viwango vya Mungu, lakini hajazaliwa mara ya pili!

“Wakristo” Wa Warumi 7

Inasikitisha sana kwamba, licha ya yote yaliyosemwa na Yesu, Yohana, Yakobo, Petro, Yuda na Paulo mwenyewe, yanayopinga wazo kwamba yule mtu wa Warumi sura ya 7 ameokoka, wengi siku hizi wanafikiri hivyo. Wala sababu si kwamba kuna ushahidi wa maandiko – maana haupo – bali ni kwa sababu wengi katika wanaojiita Wakristo wanajiona kama yule mtu wa Warumi sura ya 7 – wakitenda wasiyotaka, wakiwa watumwa wa dhambi. Wanafasiri Maandiko kutokana na ujuzi wao kwa hoja inayosema hivi: “Mimi ninajitambulisha na yule mtu wa Warumi sura ya 7, na mimi ni Mkristo. Basi, huyo mtu wa Warumi sura ya 7 lazima awe Mkristo.”

Hii tafsiri mbaya ya Warumi sura ya 7 inatia nguvu imani dhaifu yenye kuyumba ya walio wengi, ambao bado hawajapata uhuru kutoka kwenye nguvu za dhambi, ule ambao Paulo aliahidi katika Warumi sura ya 6 na ya 8, na ambao yeye mwenyewe aliufurahia maisha yake yote ya Kikristo. Hili ni janga kubwa sana, ukizingatia ile neema ya ajabu ya Mungu ambayo inapatikana bure kabisa kwa wote kwa njia ya Yesu Kristo, kama watu watamwendea kwa masharti Yake – kwa imani hai, yenye kunyenyekea.