“Mkristo” Ambaye Hajajitoa

SURA YA NNE

 

Hivi karibuni mfuasi kijana wa Ukomunisti alimwandikia mchumba wake barua ya kuvunja uchumba, baada ya kufunguliwa kutoka gerezani. Aliandika hivi:

“Sisi Wakomunisti tunakufa sana. Sisi ndiyo hupigwa risasi au kunyongwa au kudhihakiwa au kufukuzwa kazi na kufanyiwa maudhi mengi tu ili maisha yetu yasiwe mazuri. Asilimia fulani yetu huuawa au kufungwa. Tunaishi katika umaskini kabisa. Kila senti tunayopata ambayo ni zaidi ya mahitaji tuliyo nayo tunatakiwa kuitoa kwa chama. Sisi Wakomunisti hatuna muda wala fedha kwa ajili ya kwenda sinema sana, au kwenye matamasha ya muziki, au kula nyama, au kukaa nyumba nzuri, au magari mapya. Tunaitwa waliobobea. Sisi tumebobea katika ukomunisti. Maisha yetu yanatawaliwa na jambo moja kubwa: Kuufanya ulimwengu mzima kuwa wa Kikomunisti. Sisi tuna mtazamo katika maisha ambao hakuna kiasi chochote cha fedha kinachoweza kuununua. Tuna jambo tunalopigania, tuna kusudi dhahiri maishani mwetu. Tunaweka makusudi yetu na nia zetu kwenye nafasi ya pili maana nafasi ya kwanza ni kuteka ulimwengu. Basi, japo maisha yetu binafsi yanaonekana kuwa magumu au ubinafsi wetu unaonekana kuteseka kwa sababu ya kujiweka nafasi ya pili chini ya chama, tunafidiwa sana kwa wazo kwamba kila mmoja wetu kwa njia yake ndogo tu anachangia kuleta kitu kipya na cha kweli na kilicho bora kwa ajili ya mwanadamu.

Kuna kitu kimoja tu ambacho nina shauku nacho sana maishani, nacho ni Ukomunisti. Ni maisha yangu, ndiyo biashara yangu, ndiyo dini yangu, ndiyo kazi yangu, ndiyo mpenzi wangu, ndiyo mke wangu, ndiyo pumzi yangu na chakula changu. Ninautumikia mchana na kuota juu yake usiku. Ukomunisti umenishika sana, na nguvu yake inazidi badala ya kupungua kadiri muda unavyopita. Basi, siwezi kuingia kwenye urafiki, wala kujiingiza kwenye mapenzi wala mazungumzo bila ya kuvihusisha hivyo na hiki kitu changu ambacho ndicho kinasukuma maisha yangu na kuyapa nguvu. Ninawatazama watu, vitabu, hoja na matendo kulingana na jinsi vyote hivyo vinavyoathiri Ukomunisti, na jinsi wao wanavyoutazama. Tayari nimekwisha fungwa kwa ajili ya msimamo wangu, na kama ni lazima, niko tayari kupigwa risasi kwa ajili hiyo hiyo.”

Japo amedanganywa na kupotoshwa, huyu mfuasi kijana wa Ukomunisti ana kitu ambacho wengi wanaojiita Wakristo hawana: kujitoa. Tunaweza kutikisa vichwa kwa kumhurumia kwamba ameamini kitu potofu, lakini imani yake imethibitishwa kuwa ya kweli kwa matendo yake. Hatuwezi kusema hivyo kuhusu wote wanaodai kwamba ni wafuasi wa Kristo.

Imani ya kweli daima hujidhihirisha kwa matendo. Kuna mlingano usiotenganishwa kati ya imani na tabia au mwenendo. Kama alivyoandika Martin Luther katika utangulizi wa kitabu chake cha kufafanua Waraka kwa Warumi, “Kweli kweli haiwezekani kutenganisha matendo na imani, kama ambavyo haiwezekani kutenganisha joto na mwanga kutoka katika moto.”

Utajuaje kwamba mtu anaamini unachomwambia? Utajua kama atatenda kama anayekuamini. Ukimwambia kwamba kuna mdudu hatari anayempandia mguuni, naye acheke tu na kuendelea kuzungumza nawe, jua kwamba hakuamini. Vivyo hivyo mtu anayemwamini Yesu hutenda kulingana na imani yake. Imani yake inaonyeshwa kwa kutii kwake.

Japo wengi wanaokiri kwamba ni Wakristo hudai kwamba wanamwamini Yesu kuwa ni Mwana wa Mungu, inaonekana kutokana na matendo yao kwamba hawaamini hata kidogo. Juu ya hao Paulo aliandika hivi: “Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana …” (Tito 1:16).

Yesu, Afisa Mkuu Mtendaji

Hebu fikiri kwamba unafanya kazi kwenye kampuni kubwa sana. Siku moja ukiwa kazini, mtu aliyevalia vizuri sana na ambaye hujawahi kumwona anaingia kwa mlango wa pembeni. Anakuja mezani pako na kusema, “Isaka, mimi ndiye Afisa Mkuu Mtendaji wa shirika hili. Tengeneza vizuri meza yako mara moja!” Utafanyaje? Ukweli ni kwamba itategemeana na kuamini kwako au kutokuamini kwamba yeye ndiye Afisa Mkuu Mtendaji kama alivyosema. Ni hivi: Afisa Mkuu Mtendaji ndiye mwenye mamlaka makubwa kuliko mwingine yeyote katika shirika. Yeye ndiye ambaye usingependa achukizwe na wewe. Kwa hiyo, ikiwa unaamini alichosema, mara moja utamtii. Usipomtii ni kwamba huamini yeye ndiye Afisa Mkuu Mtendaji.

Bila shaka unaelewa mfano huo. Kumwamini Yesu husababisha kujitoa kwake. Tunaokolewa kwa kumwamini Yesu, lakini imani yetu lazima iwe imani tiifu, la sivyo si imani. Hicho ndicho kinachosemwa mara mbili na Paulo katika waraka wake kwa Warumi, kwamba ni “utii utokanao na imani” (ona Warumi 1:5; 16:26). Lengo kuu la huduma yake yote lilikuwa ni kusababisha “utii wa imani” kwa watu wote wa Mataifa (ona Warumi 1:5).

Mtu anaweza kusema hivi: “Mfano wako si sawa kwa sababu Yesu si Afisa Mkuu Mtendaji wa kuogopwa.”

Hoja hiyo inaonyesha kiini cha tatizo tulilo nalo. Ikiwa mfano huo si sawa, ni kwenye ukweli kwamba Yesu ni zaidi ya Afisa Mkuu Mtendaji. Yeye ndiye muumbaji wa watu wote, ndiye hakimu wa walio hai na waliokufa; Yeye ana jina kuu lipitalo majina yote.

Lakini, katika mawazo ya wengi wanaojiita Wakristo, Yesu ni Mwokozi tu, siyo Bwana. Yeye ni jirani rafiki, si Kichwa cha Kanisa. Yeye ana upendo wote lakini hana mamlaka yote mbinguni na duniani. Yeye ni “ndugu mpendwa”, si Mfalme wa wafalme. Ni muungwana, lakini si ambaye mbele Zake kila goti litapigwa. Ni mzuri lakini si Mungu. Kibaya ni hiki: Yesu wa aina hiyo hayupo, na wale wanaodhani hivyo ni waabudu sanamu wabaya mno – wamemtengeneza mungu anayelingana na mawazo yao.

Mtume Yakobo anasema tena na tena juu ya kutodanganywa kuhusu imani isiyokuwa na matendo yanayotokana na kutii. Anasema hivi:

Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu… Mtu akidhani ya kuwa anayo dini, wala hauzuii ulimi wake kwa hatamu, hali akijidanganya moyo wake dini yake mtu huyo haifai … Ndugu zangu, yafaa nini mtu akisema ya kwamba anayo imani, lakini hana matendo? Je! Ile imani yaweza kumwokoa? (Yakobo 1:22, 26; 2:14 – Maneno mepesi ni kwa ajili ya kutilia mkazo).

Yakobo ameweka hoja yake wazi kabisa na kwa uzuri kabisa. Imani pasipo matendo haiwezi kutuokoa. Tunachokiamini hudhirishwa kwa maneno yetu na matendo yetu. Tena, inawezekana kabisa kujidanganya nafsini mwetu katika jambo hili na kuwa na dini isiyo na faida.

Yakobo anaendelea na kusema hivi:

Lakini mtu atasema, Wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu. Wewe waamini ya kuwa Mungu ni mmoja; watenda vema. Mashetani nao waamini na kutetemeka. Lakini wataka kujua, wewe mwanadamu usiye kitu, kwamba imani pasipo matendo haizai?… Mwaona kwamba mwanadamu huhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo yake, si kwa imani peke yake…. Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa (Yakobo 2:18-20, 24, 26 — Maneno mepesi ni kwa ajili ya kutilia mkazo).

Yakobo anaonyesha kwamba hata mapepo wana imani kiasi fulani, na imani yao huonyeshwa kwa matendo – wanatetemeka kwa hofu. Lakini, ni wangapi wanaojiita waamini wanao-onyesha imani ndogo kuliko hata ya mapepo, kwa maana ya kwamba hawaonyeshi kumwogopa Mungu?

Yesu Alitaka Wasioamini Waamini Kwa Kutii

Ona pia kwamba Yakobo anamhimiza yeyote athibitishe imani yake bila ya matendo (ona Yakobo 2:18). Matendo hayawezi kutenganishwa na imani ya kweli. Hiyo ndiyo sababu imani ya kweli ya kuokoa huanza na toba kila mara. Na hiyo ndiyo sababu kila mara Yesu alipowaita watu waokolewe aliwataka wajitoe kabisa na kutii. Yesu aliwaita watu waingie kwenye imani tiifu, na kwa wengi waliokuwa wanaitenganisha imani na matendo, Yesu aliwakwaza maana hakusema chochote kuhusu imani wakati alipowaita watu kuokoka. Wafuasi Wake wa kweli wangeonyesha imani yao kwa matendo yao.

Cha kushangaza ni kwamba, mwito wa Yesu kwamba watu wajitoe kabisa mara nyingi hupuuzwa na watu wanaojiita Wakristo. Au kama wanakubali, wanajaribu kufafanua kwamba ni mwito wa kuingia katika mahusiano ya ndani zaidi, tena kwa wale ambao wamekwisha pokea neema ya Mungu tayari, sio wale ambao hawajaokoka. Lakini inasikitisha kwamba, wengi katika wale “waamini” wanaodai kwamba mwito wa Yesu kujitoa ni kwa ajili yao na si kwa wasioamini hawasikilizi mwito Wake kwa jinsi wanavyotafsiri. Wao wanafikiri kwamba wana uchaguzi wa kutotii mwito huo, na kwa kawaida hawafanyi hivyo.

Hatua Za Kwanza Au Kuingia Ndani Zaidi?

Hebu tutafakari mwaliko mmoja wa wokovu ambao Yesu aliutoa, unaotafsiriwa kwa makosa mara nyingi na kudhaniwa na wengi wanaokiri Ukristo kwamba ni mwito wa kuingia katika kutembea na Mungu kwa undani zaidi. Mwaliko wenyewe ni huu:

“Akawaita mkutano pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, ‘Mtu yeyote akitaka kunifuata na ajikane mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha. Kwa kuwa itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake? Ama mtu atoe nini badala ya nafsi yake? Maana kila mtu atakayenionea haya mimi na maneno yangu katika kizazi hiki cha uzinzi na dhambi, Mwana wa Adamu atamwonea haya mtu huyo, atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu’.” (Marko 8:34-38)

Je, huo ni mwaliko wa wokovu unaotolewa kwa wasioamini au ni mwaliko wa kuingia katika mahusiano ya undani zaidi unaotolewa kwa waamini? Tukisoma kwa ukweli, jibu ni wazi kabisa.

Kwanza: Ona kwamba watu waliokuwa wanaambiwa maneno hayo na Yesu ni “mkutano” pamoja na wanafunzi Wake (ms. 34). Basi, “mkutano” hawakuwa wanafunzi Wake. Wao “waliitwa” Naye ili kusikiliza kitu alichokuwa anataka kusema. Yesu alikuwa anamtaka kila mmoja – wafuasi Wake, na waliokuwa wanatafuta kumjua – waelewe ukweli aliokuwa anataka kufundisha. Ona pia kwamba alipoanza kufundisha alianza kwa kusema, “Mtu yeyote…” (ms. 34 — Maneno mepesi ni ili kutilia mkazo). Yaani, maneno Yake ni kwa yeyote na kila mmoja.

Tunapoendelea kusoma inakuwa wazi zaidi kwamba Yesu alikuwa anazungumza na nani. Maneno Yake hasa yalikuwa yanaelekezwa kwa kila mtu aliyetamani “kumfuata” Yeye, “kuiponya nafsi yake” badala ya “kupata hasara ya nafsi yake” na kuwa miongoni mwa wale ambao Yeye hatawaonea aibu wakati “atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu”. Maneno hayo yote yanaonyesha kwamba Yesu alikuwa anaeleza juu ya watu waliokuwa na shauku ya kuokoka. Je, ni sawa kwetu kufikiri kwamba kuna mtu anayetaka kwenda mbinguni ambaye hataki “kumfuata” Yesu na “kuiponya nafsi yake”? Je, ni sawa kwetu kuamini kwamba wapo waamini wa kweli watakaopata “hasara ya nafsi” zao, na wenye kumwonea Yesu na maneno Yake aibu, na ambao Yesu Mwenyewe atawaonea aibu atakaporudi? Basi, ni dhahiri kwamba Yesu alikuwa anazungumza juu ya wokovu wa milele.

Ona kwamba kila sentensi katika zile nne zilizo katika fungu hili lenye sentensi tano inasema kweli muhimu kwa kuanza na maneno “Kwa kuwa”. Ni kwamba kila moja inasaidia kufafanua zaidi ile iliyopita. Hakuna sentensi katika fungu hili inayopaswa kufafanuliwa pasipo kutazama jinsi hizo nyingine zinavyoipa mwanga. Hebu tuangalie maneno ya Yesu sentensi kwa sentensi kwa mtazamo huo.

Sentensi Ya Kwanza

“Mtu yeyote akitaka kunifuata na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate” Marko 8:34).

Ona tena hapa kwamba maneno ya Yesu yalikuwa yanaelekezwa kwa yeyote aliyetaka kumfuata, yeyote aliyetaka kuwa mfuasi Wake. Huu ndiyo uhusiano wa pekee ambao Yesu anautoa mwanzoni kabisa.

Wengi wanatamani kuwa rafiki bila kuwa wafuasi Wake, lakini hakuna uchaguzi aina hiyo. Yesu hakumhesabu yeyote kuwa rafiki Yake kama hakumtii. “Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo” (Yohana 15:14).

Wengi wangependa kuwa ndugu Zake bila kuwa wafuasi Wake. Lakini hapo tena Yesu hakutoa nafasi kama hiyo. Hakuna aliyemhesabu kuwa ndugu Yake kama hakuwa mtii. “Yeyote atendaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyo ndiye ndugu yangu …” (Mathayo 12:58 – Maneno mepesi kwa ajili ya kutilia mkazo).

Wengi wanapenda kujiunga na Yesu mbinguni bila ya kuwa wafuasi Wake, lakini Yesu aliweka wazi kwamba jambo hilo haliwezi kutokea. Ni wale watiifu tu ndiyo wanaokwenda mbinguni. “Si kila mtu aniambiaye, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni” (Mathayo 7:21).

Katika sentensi yetu tunayoitazama, Yesu aliwajulisha wale waliotaka kumfuata kwamba wasingeweza kufanya hivyo bila ya kujikana wenyewe. Lazima wawe tayari kuweka shauku zao pembeni, na kuzitia chini ya mamlaka ya mapenzi Yake. Kujikana na kunyenyekea ndicho kiini katika kumfuata Yesu.

Lakini, Yesu anategemea kujikana mpaka wapi? Je, alikuwa anazungumzia juu ya kuacha kula vitu fulani tu wakati wa Pasaka? Katika hiyo sentensi ya kwanza, Yesu alitumia maneno yaliyofanya isiwe vigumu kuelewa anachosema. “Ajitwike msalaba wake.” Pengine si Yeye aliyeanzisha kusema hivyo – labda ilikuwa lugha ya kawaida katika siku Zake. Je, nini maana yake?

Katika siku za Yesu, watu waliojitwika misalaba walikuwa wale waliohukumiwa kufa. Hicho hakikuwa kitu ambacho mtu alipenda kufanya, kwa sababu kilikuwa cha mwisho ambacho angefanya. Wakati mhalifu alipobeba msalaba wake, aliinua kile kipande cha mbao ambacho baada ya muda mfupi angetundikwa juu yake ii afe kifo kibaya, cha taratibu. Ulikuwa ni wakati wa kutisha, wa kukabiliana na kitu kisichoepukika.

Kwa hiyo maneno: “mtu ajitwike msalaba wake” yanafanana na mtu kueleza juu ya kitu ambacho kwa kawaida kisingefanyika. Huo ni mfano wa kujikana kwa hali ya juu sana, kufanya kitu ambacho mtu alikuwa hataki kufanya. Kama ulikuwa msemo wa kawaida katika siku za Yesu, basi tunaweza kufikiri kwamba akina baba walikuwa wanawaambia watoto wao wa kiume wasiopenda kabisa: “Mwanangu! Unajua ni wajibu wako kuchimba choo wakati kimejaa. Sasa, jitwike msalaba wako na uendelee na kazi.” Au wake za watu wakiwaambia waume zao waliokunja uso, “Mume wangu! Najua hupendi kusikia hiki, lakini leo kodi zetu zinatakiwa na serikali ya Kirumi, na tunayo ile fedha inayotakiwa na yule mtoza ushuru tapeli. Hatuna uchaguzi katika jambo hili. Si ujitwike msalaba wako na uende kwenye ofisi yake asubuhi hii mkamalize mambo?”

Sentensi Ya Pili

Sentensi ya pili anayotamka Yesu inafanya maana ya ile ya kwanza kuwa dhahiri zaidi. “Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha” (Marko 8:35).

Hapa tena ona kwamba sentensi inaanza kwa neno “kwa kuwa”, lenye kuiunganisha na ile ya kwanza, na kuifafanua zaidi. Hapa Yesu anatofautisha watu wawili, wale wale waliokuwa wametajwa katika sentensi ya kwanza – yule ambaye angekuwa tayari kujikana na kujitwika msalaba wake ili kumfuata, na yule ambaye asingekuwa tayari kufanya hivyo. Yule ambaye asingekuwa tayari kujikana anataka kuokoa nafsi yake, lakini ataipoteza. Yule ambaye angekuwa tayari kujikana atapoteza nafsi yake lakini mwishoni anaiokoa.

Kweli, Yesu hakuwa anazungumza juu ya mtu mmoja kupoteza au kuokoa maisha yake kimwili. Wafuasi Wake wengi walipoteza maisha yao kimwili haraka sana, kwa sababu walimfuata. Walikufa kwa ajili ya imani yao. Tena, sentensi zinazofuata katika fungu hili zinaonyesha kwamba mawazo ya Yesu yalikuwa kwenye mambo ya milele – faida na hasara za milele.

Mtu anayetajwa katika sentensi ya kwanza ambaye asingejikana ni yule yule anayetajwa katika sentensi ya pili ambaye alitaka kuyaokoa maisha yake. Basi, tunaweza kufikia hitimisho kwamba “kuokoa nafsi” maana yake “kuokoa mipango ya mtu kwa ajili ya maisha yake.” Hii inadhihirika zaidi wakati tunapotazama yule mtu anayelinganishwa katika kisa hicho, ambaye “anapoteza nafsi yake kwa ajili ya Kristo na Injili”. Ni huyo anayejikana mwenyewe, anayejitwika msalaba wake na kuachana na mipango yake binafsi, na kuanza kuishi kwa ajili ya kusudi la kuendeleza mipango ya Kristo na kueneza Injili. Huyo ndiye atakaye”okoa nafsi yake” mwisho wa siku, wakati ambapo yule mwingine ataipoteza. Anayetafuta kumpendeza Kristo badala ya kujipendeza mwenyewe atajikuta mbinguni akiwa na furaha, huku yule anayeendelea kujipendeza mwenyewe atajikuta jehanamu akiwa na huzuni, na huko kupoteza kila nafasi ya uhuru wa kufuata mambo yake mwenyewe maishani.

Sentensi Ya 3 Na Ya 4

Sasa tugeukie sentensi ya tatu na ya nne. “Kwa kuwa, itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake? Au mtu atoe nini badala ya nafsi yake?” (Marko 8:36, 37). Katika sentensi hizi, huyo mtu ambaye hatajikana anawekwa bayana. Ndiye anayetamani kuyaokoa maisha yake, lakini ndiye anayeyapoteza mwishoni. Sasa anazungumzwa kwamba ni mwenye kutaka kufuata kile kitolewacho na dunia na ambaye mwishoni “anapata hasara ya nafsi yake”. Yesu anaonyesha hasara ya mtu wa aina hiyo kwa kufananisha thamani ya dunia nzima na thamani ya hiyo roho moja. Ni kwamba hakuna mlinganisho. Mtu anaweza kupata vitu vyote ambavyo dunia inatoa, lakini, kama matokeo ya mwisho wa maisha yake ni kuwa jehanamu milele, amefanya kosa kubwa sana sana.

Kutokana na sentensi hizo mbili tunapata kuona sababu zinazowavuta watu wasijikane na kuwa wafuasi wa Kristo. Ni ile shauku waliyo nayo ya kujitosheleza, itolewayo na dunia. Wakisukumwa na kujipenda wenyewe, wale wanaokataa kumfuata Kristo wanatafuta starehe za dhambi, ambazo wafuasi wa Kristo wa kweli huziepuka kwa sababu ya kumpenda na kumtii Yeye. Wale wenye nia ya “kupata kila kinachowezekana kwa juhudi zote” hufukuzia mali, mamlaka na sifa, wakati ambapo wale wafuasi wa Kristo wa kweli hutafuta kwanza ufalme Wake na haki Yake. Mali yoyote, mamlaka au sifa vinavyopatikana nao huhesabiwa kama fursa ya uwakili kutoka kwa Mungu, na hutumiwa kwa ajili ya utukufu Wake bila ubinafsi wowote.

Sentensi Ya Tano

Hatimaye tunafikia sentensi ya tano katika fungu tunalotazama. Ona tena jinsi ilivyounganishwa na zile nyingine kwa maneno yale ya kwanza – Kwa maana. “Maana kila mtu atakayenionea haya mimi na maneno yangu katika kizazi hiki cha uzinzi na dhambi, mwana wa Adamu atamwonea haya mtu huyo, atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu” (Marko 8:38).

Hapa tena, anayehusika ni yule ambaye hakujikana mwenyewe. Badala yake, alitaka kufuata mpango wake mwenyewe, akifukuzia vile vitolewavyo na dunia, na ambaye alipoteza maisha yake na mwishowe kupata hasara ya nafsi yake. Sasa anaonyeshwa kwamba ni mtu mwenye kumwonea aibu Kristo na maneno Yake. Aibu yake inatokana na kutokuamini kwake. Kama kweli aliamini kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu, asingemwonea Yeye wala maneno Yake aibu. Lakini ni mmoja kati ya “kizazi cha uzinzi na dhambi” na Yesu atamwonea aibu wakati atakaporudi. Hapa ni wazi kwamba Yesu hakuwa anazungumza juu ya mtu ambaye ameokoka.

Hitimisho ni nini? Ni hili: Fungu hili zima haliwezi kuhesabiwa kuwa mwito wa kuingia katika maisha ya kujitoa zaidi, unaotolewa kwa wale ambao tayari wanakwenda mbinguni. Ni onyesho la wazi kuhusu njia ya wokovu kwa kuwalinganisha wale waliookoka kweli na wale ambao bado. Hakuna hata mara moja ambapo Yesu anataja juu ya imani au kuamini, japo sababu nzima ya mtu kukataa kujikana mwenyewe na kuendelea kufuata vishawishi vya dunia ni uasi wa dhambi dhidi ya Kristo. Na hiyo ni kwa sababu hamwamini Kristo. Tunda la kutokuamini ni kutokutii. Yesu hakuwa anatangaza wokovu upatikanao kwa matendo bali wokovu ambao matokeo yake ni matendo, utokanao na imani ya dhati. Basi, hakuna “Mkristo ambaye hajajitoa kikamilifu” kulingana na tafsiri Yake.

Ubatizo Kama Wanavyofanya Nepali

Mwito wa kuokoka ni mwito wa kujitoa kabisa kwa Kristo. Katika mataifa mengi duniani ambako mateso ni kawaida, jambo hilo linaeleweka vizuri sana na waamini wapya. Wao wanajua kwamba kumfuata Kristo kuna gharama ya kulipa.

Sundar Thapa, Mkristo wa KiNepali ambaye ameanzisha makanisa zaidi ya mia moja katika taifa lake la KiBuddha, alinishirikisha maswali nane ambayo anamwuliza kila mwamini mpya kabla ya kumbatiza. Ni haya:

Je, uko tayari kulazimika kuondoka nyumbani kwenu na kuwaacha wazazi wako?

Je, uko tayari kupoteza haki yako ya kurithi mali ya baba yako?

Je, uko tayari kupoteza kazi yako kama watu wakijua kwamba wewe ni Mkristo?

Je, uko tayari kwenda gerezani?

Je, uko tayari kupigwa na kuteswa na polisi?

Je, uko tayari kufa kwa ajili ya Kristo ikibidi?

Je, uko tayari kuwaambia wengine habari za Yesu?

Je, uko tayari kuleta zaka yako yote na sadaka katika nyumba ya Bwana?

Kama huyo mwamini mpya anajibu ndiyo kwa yote nane, basi lazima atie sahihi karatasi yenye tamko la majibu yake. Ndipo baada ya hapo anabatizwa. Je, ni wangapi kati yetu ambao wangehesabiwa kuwa wameokoka wakiwa Nepal? Au swali muhimu zaidi: Ni wangapi kati yetu watakaohesabiwa kuwa ni Wakristo tutakaposimama mbele za Yesu?

“Waamini” Wasiokuwa Wanafunzi

Pengine mfano mzuri sana wa tafsiri isiyo sahihi ya maneno ya Yesu kuhusu wokovu na kudhaniwa kwamba ni mwito kwa watu “kutembea kwa karibu zaidi Naye” ni yale makundi yanayoundwa siku hizi na wanatheolojia wa kisasa. Wanasema kwamba kuna waamini Wakristo na wanafunzi. Watu wengi sana kanisani wanaamini kwamba mtu anaweza kuwa mwamini wa Kristo anayekwenda mbinguni bila ya kuwa mwanafunzi Wake. Kiwango cha kujitoa ambacho Yesu alitaka kwa mtu kuhesabiwa kuwa mfuasi wake ni cha juu sana kiasi cha kwamba wengi wanaojiita Wakristo lazima wakiri haraka kwamba hawawezi kukifikia. Lakini, hakuna shida maana katika akili zao hatua ya uanafunzi ni ya hiari. Kwa kuwa hawaelewi asili ya imani yenye kuokoa, wao wanaamua kwamba kufanyika mwanafunzi si sawa na kuokoka, kwa sababu ipo gharama ya kuwa mwanafunzi, ila wokovu ni bure.

Lakini kuelewa hivyo ni makosa makubwa. Uchunguzi wa kweli wa Agano Jipya unadhihirisha kwamba wanafunzi si waamini waliojitoa zaidi – wao ni waamini wa kweli tu. Katika kanisa la kwanza havikuwepo vikundi hivyo vya kisasa – “waaminio” na “wanafunzi”. Kila aliyemwamini Yesu alikuwa mwanafunzi Wake. Ukweli ni huu: “Na wanafunzi waliitwa Wakristo kwanza hapo Antiokia” (Matendo 11:26 – Maneno mepesi kwa ajili ya kutilia mkazo).

Kumwamini Yesu ni kumfuata kwa utii, na ndivyo ilivyo mpaka leo. Wokovu kweli ni zawadi ipatikanayo pasipo kuifanyia kazi, lakini ni zawadi inayopokelewa kwa kuwa na imani hai tu. Kule kujitoa kutokanako na imani kama hiyo si kazi; bali ni kitu kinachothibitisha imani hiyo. Neema inayotusamehe pia inatubadilisha.

Masharti Ya Yesu Kuhusu Uanafunzi

Hebu tutazame masharti ambayo Yesu aliorodhesha kwa mtu kuwa mwanafunzi Wake huku tukitazama kama Maandiko yanafundisha ikiwa waamini wote wa kweli ni wanafunzi.

Tunasoma katika Luka 14:25 kwamba “makundi makubwa” yalimfuata Yesu. Lakini Yeye hakuridhika. Makundi makubwa ya mashabiki wakati mambo ni mazuri hayakumgusa. Alitaka kujitoa kwa moyo wote, bila ya kubakiza chochote. Alitazamia kupendwa na kuaminika kwa hali ya juu kabisa. Basi akawaambia hivi:

“Kama mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu” (Luka 14;26).

Hakuna mfasiri wa Maandiko mwenye akili timamu atakayesema kwamba Yesu alimaanisha mtu lazima awachukie kweli wale anaowapenda sana maishani mwake ili kuwa mfuasi Wake. Ni dhahiri kwamba Yesu alikuwa anatumia lugha ya mfano. Bila shaka alichokuwa anamaanisha ni kwamba upendo wetu kwa tunaowapenda uonekane kama chuki unapolinganishwa na upendo wetu Kwake Yeye. Alimaanisha kwamba Yeye ndiye awe wa kwanza katika kupendwa maishani mwetu. Wanafunzi Wake wanapaswa kumpenda Yeye zaidi sana kuliko mtu mwingine yeyote, na hata wao wenyewe.

Yesu akaendelea na kusema hivi: “Mtu yeyote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu” (Luka 14:27).

Hapa tena si kwamba maneno Yake yachukuliwe kama yalivyo. Hatazamii wanafunzi Wake kubeba misalaba ya mbao kila waendapo. Kuubeba msalaba wa mtu lazima iwe ni ishara ya kitu fulani, na vyovyote vile, nani atafikia mahali pa kudhani kwamba Yesu alikuwa anazungumzia kitu kizuri cha kupendeza au rahisi? Sasa sana alikuwa anazungumzia kujitoa kwa kujikana.

Ona pia kwamba hili sharti la pili la mtu kuubeba msalaba wake ni sawa na lile ambalo Yesu aliwataka wote waliotaka kumfuata wafanye, kama tulivyoona katika mafunzo yetu mapema katika sura hii, kutoka Marko 8:34 hadi 38. Yesu katika fungu hilo bila shaka alikuwa anataja masharti ya wokovu, akionyesha ushahidi dhahiri kwamba masharti ya kuokoka na kuwa mfuasi ni sawa – ni yale yale.

Alipoendelea na fundisho Lake juu ya uanafunzi, ndipo alipowashauri wasikilizaji Wake kuhesabu gharama kabla ya kuanza kuwa wafuasi Wake. Anasema hivi:

“Maana ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumalizia? Asije akashindwa kuumaliza baada ya kuupiga msingi, watu wote waonao wakaanza kumdhihaki wakisema, ‘Mtu huyu alianza kujenga, akawa hana nguvu za kumaliza.’ Au kuna mfalme gani, akitaka kwenda kupigana na mfalme mwingine, asiyeketi kwanza na kufanya shauri, kwamba yeye pamoja na watu elfu kumi ataweza kukutana na yule anayekuja juu yake na watu elfu ishirini? Na kama akiona hawezi, hutuma ujumbe kutaka sharti za amani, mtu yule akali mbali” (Luka 14:28-32).

Nani awezaye kupinga kwa usahihi kwamba hakuna gharama ya kuwa mwanafunzi wa Kristo kutokana na maneno hayo?

Akamalizia hivi: “Basi, kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu” (Luka 14:33). Ili kuwa mwanafunzi wa Yesu hatuna budi kuacha umiliki wa vitu vyetu vyote, avimiliki Yeye. Tunafanyika mawakili tu wa vitu vile ambavyo vimekuwa Vyake kuanzia hapo, na mali yetu inatumiwa kwa makusudi Yake. Vinginevyo, sisi si wanafunzi Wake.

Ni wazi Yesu alitaka kuonyesha kwamba kuwa mwanafunzi Wake ni kujitoa kwenye gharama kubwa. Lazima Yeye awe wa kwanza katika maisha yetu, nasi lazima tumpende kuliko maisha yetu, watu tunaowapenda na mali zozote.

Sharti Lingine

Wakati mwingine tena Yesu alieleza maana ya kuwa mwanafunzi Wake. Yohana anataarifu kwamba wakati Yesu alipokuwa anazungumza Hekaluni,

Wengi walimwamini. Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, ‘Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru’.” (Yohana 8:30-32)

Ona kwamba Yohana mara mbili anatuambia kwamba maneno ya Yesu katika 8:31-32 yalitolewa kwa waliokuwa wanamwamini. Kwa hao waamini wapya, Yesu hakuwaambia hivi: “Huko baadaye mtahitaji kufikiri kujitoa kabisa kama wanafunzi.” Hapana. Yeye alisema nao moja kwa moja kama wanafunzi. Kwa Yesu, kumwamini Yeye ilikuwa ni sawa na kuwa mwanafunzi.

Vile vile angalia kwamba Yesu hakuwahakikishia mara moja hao waamini kwamba wameokoka kama inavyofanyika leo. Badala yake, Yeye aliwapa changamoto wajihoji ikiwa imani yao ilikuwa ya kweli. Je, walikuwa wanafunzi Wake kweli kweli? Ingefanyika hivyo kama wangedumu katika neno Lake.

Kudumu katika neno la Yesu maana yake ni kukaa ndani yake, kupafanya kuwa nyumbani kwako au makao yako. Huonyesha shauku ya kutaka kujua na kulitii neno Lake, kama tu alivyosema: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru” (Yohana 8:32 — Maneno mepesi ni ili kutilia mkazo). Yesu hasa alikuwa anazungumza juu ya uhuru kutokana na dhambi (ona Yohana 8:34-36). Hili tena linatwambia kwamba wanafunzi wa kweli wa Yesu, wale ambao wamemwamini Yeye kweli kweli na kuzaliwa mara ya pili, wanaonekana kwa utakatifu wao unaozidi kukua.

Ubatizo Wa Wanafunzi

Katika Agizo Kuu lipatikanalo katika mistari ya mwisho ya Injili ya Mathayo, Yesu alitumia neno mwanafunzi kwa njia isiyoleta mashaka yoyote kuhusu maana yake. Alisema hivi: “Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari” (Mathayo 28:19, 20 – Maneno mepesi ni kwa ajili ya kutilia mkazo).

Cha kwanza tunachoona hapa ni kwamba Yesu anataka wanafunzi, naye anawataka hao wabatizwe. Lakini tunajua pia kwamba Yesu na waandishi wa Agano Jipya wanakubaliana kwamba kila anayemwamini Yesu anatakiwa kubatizwa mara tu anapokiri imani yake kwa Kristo. Hii inaonyesha tena kwamba waamini wote wa kweli ni wanafunzi. Yesu hakuwa anasema katika Agizo Lake Kuu kwamba tusiwabatize wale wanaomwamini Kristo, bali kwamba tuwabatize wale wote wanaochukua hatua ya kuwa wanafunzi waliojitoa kikamilifu.

Kutokana na kusoma juu ya Agizo Kuu, ni wazi pia kwamba Yesu alimhesabu mtu aliyekuwa anataka kujifunza maagizo Yake yote na kuyashika kuwa ndiye mwanafunzi (Mathayo 28:20). Ni wazi kwamba kujifunza ni kitu kinachoendelea, kwa hiyo hakuna mwanafunzi ambaye anakuwa mtii mara moja katika kila kitu. Lakini kila mwanafunzi wa kweli anakubali kuwa chini ya Kristo, anakubali kujitia katika kujifunza na kufanya mapenzi Yake, na kwa njia hiyo anakuwa mwamini wa kweli kwa sababu waamini wote wa kweli ndiyo wanafunzi.

Ushuhuda Wa Yohana

Ushahidi mwingine kwamba waamini na wanafunzi ni kitu kimoja unapatikana katika Injili ya Yohana, na waraka wake wa kwanza. Hebu linganisha mistari ifuatayo:

“Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi> wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi” (Yohana 13:34, 35 – Maneno mepesi kwa ajili ya kutilia mkazo).

Sisi tunajua ya kuwa tumepita toka mautini kuingia uzimani, kwa maana twawapenda ndugu. Yeye asiyependa, akaa katika mauti (1Yohana 3:14).

Upendo usio na ubinafsi kwa ndugu ndiyo unaonyesha wanafunzi wa Kristo wa kweli, na pia unawaonyesha wote waliopita kutoka mautini kwenda uzimani, yaani, wale ambao wamezaliwa mara ya pili. Sababu rahisi ni kwamba, wanafunzi wa Kristo ni wale tu ambao wamezaliwa mara ya pili.

Matawi Yadumuyo Katika Mzabibu

Mwaliko mmoja wa mwisho kuhusu wokovu ambao mara nyingi hutafsiriwa kwamba ni mwito wa kuingia katika “undani wa mwenendo” unapatikana katika Yohana 15. Hapa tena Yesu anafafanua maana ya kuwa mwanafunzi Wake. Anasema hivi:

“Mimi ndimi mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima. Kila tawi ndani yangu lisilozaa huliondoa; na kila tawi lizaalo hulisafisha, ili lizidi kuzaa. Ninyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya lile neno nililowaambia. Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lolote. Mtu asipokaa ndani yangu hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu huyakusanya na kuyatupa motoni yakateketea. Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa. Hivyo hutukuzwa Baba yangu, kwa vile mzaavyo sana; nanyi mtakuwa wanafunzi wangu” (Yohana 15:1-8 – Maneno mepesi ni kwa ajili ya kutilia mkazo).

Mahubiri mengi sana yamehubiriwa kwa Wakristo waamini kutoka mistari hii, yakiwashauri “kusogea karibu na Yesu” na kukaa ndani Yake ili waweze kuzaa matunda mengi! Lakini, Yesu hataki tufikiri kwamba kukaa ndani Yake ni kitu ambacho waamini waendao mbinguni wanahitaji kuamua kuwa nacho au hapana. Kukaa ndani Yake ni sawa na kuokoka – kama maneno ya Yesu yanavyoweka bayana kabisa: “Mtu asipokaa ndani yangu, hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu huyakusanya na kuyatupa motoni yakateketea” (Yohana 15:6). Wale wasiokaa ndani ya Kristo wamelaaniwa. Wale wanaokaa ndani ya Kristo huzaa matunda, wakijithibitisha kwamba ni wanafunzi Wake kama Yesu alivyosema (Yohana 15:8). Hapa tena tunaona kwamba watu waliookoka kweli ni wanafunzi wanaozaa matunda.

Mizabibu inaweza kuzaliwa kwenye tawi ambalo limeunganika na mzabibu tu. Tawi hupokea uzima kutoka kwa mzabibu, ambacho ndicho muhimu kwa ajili ya kuzaa matunda. Huo ni mfano unaofaa kabisa wa mahusiano yetu na Kristo. Tunapomwamini Kristo, tunafanyika tawi lililo hai, lenye kuzaa matunda ndani Yake. Sawa na jinsi ambavyo maji ya uzima yanavyopita katika mzabibu na kupeleka uhai kwa tawi ili liweze kuzaa matunda, ndivyo na Roho Mtakatifu anayekaa ndani yetu alivyo chanzo cha matunda ya mwamini.

Je, ni matunda ya aina gani yanayozalishwa kwa nguvu za Roho Mtakatifu? Bila shaka Roho Mtakatifu anazaa tunda la utakatifu. Orodha ya Paulo ya tunda la Roho inayopatikana katika sura ya tano ya Wagalatia inaanza kwa tunda la upendo, ambalo, kama tulivyokwisha ona hapo nyuma, ndiyo alama ya wanafunzi wa kweli wa Yesu. Orodha hiyo inaendelea kwa kutaja tunda la furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole na kiasi (ona Wgalatia 5:22). Hayo ndiyo Roho Mtakatifu akaaye ndani yetu anayozalisha, na hayo ndiyo alama ya kila mwamini wa kweli kwa kiasi fulani. Kwa mfano: Tunasoma kwamba wanafunzi wa kwanza mara zote “walijaa furaha na Roho Mtakatifu” (Matendo 13:52).

Matunda huiva na kukomaa, na ndivyo ilivyo hata kwa tunda la Roho. Wakristo wasiokomaa mara nyingi wana matunda ambayo bado ni mabichi. Lakini, kama Roho anakaa ndani ya mtu (na ndivyo ilivyo kwa kila aaminiye kweli – Warumi 8:9), haiwezekani Yeye Roho asizae matunda Yake.

Vipi Kuhusu Tawi Lisilozaa Katika Kristo?

Lakini, Yesu si alizungumzia kuhusu uwezekano wa tawi “ndani Yake” lisilozaa matunda? Ndiyo. Ila, tamko Lake lazima litafsiriwe katika maelezo Yake kuhusu mzabibu na matawi. Ona kwanza kwamba tawi “ndani Yake” lisilo na matunda “linaondolewa” (Yohana 15:2). Maana yake ni kwamba hilo tawi lililokuwa kwenye mzabibu halipo tena. Kilichotokea kwa tawi hilo baada ya “kuondolewa” ni kitu cha kufikiri. Lakini, baada ya tawi hilo “kuondolewa” na kutokuwepo tena, bila shaka haliwi “linalokaa kwenye mzabibu.” Basi, ni kitu gani kinachotokea kwa matawi yasiyokaa katika mabibu? Yesu alisema hivi katika mistari ya mbele kidogo: “Mtu asipokaa ndani yangu hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu huyakusanya na kuyatupa motoni yakateketea” (Yohana 15:6).

Inabidi tuwe makini sana tunapofasiri mfano wa aina yoyote. Mfano ni mlinganisho wa vitu viwili ambavyo havifanani kimsingi, japo vina mambo kidogo yanayofanana. Ninapomwambia mke wangu kwamba macho yake ni kama vidimbwi vya maji, maana yake ni kwamba yana kina, ni meusi na yenye kuvutia. Lakini hapo ndipo mwisho wa kufanana. Sina maana kwamba samaki huogelea ndani yake au kwamba bata maji hutua hapo au kwamba yanaganda wakati kuna baridi!

Na mifano ya Yesu ni vivyo hivyo. Tunaweza kutafuta kwa makosa maana ya kiroho katika maelezo ambayo yamekwisha kwa habari ya kufanana kwake. Kwa mfano: Siwezi kutumia mfano wa Yesu kuhusu “mzabibu na matawi” ili kuthibitisha kwamba Wakristo wanazaa matunda zaidi wakati wa miezi ya joto, kama ambavyo ni kweli kwa mizabibu. Hapo ni kuongezea mambo yasiyofaa katika mfano.

Vivyo hivyo siwezi kufikia uamuzi kwamba Yesu alikuwa anajaribu kusema kwamba mwamini wa kweli ndani Yake anaweza asizae matunda kabisa, hasa tunapotambua kwamba hoja kuu ya mfano Wake huo inakwenda kinyume na wazo hilo. Hitimisho linalofaa basi ni kwamba lile tawi lisilozaa lililokuwa “ndani Yake” linamwakilisha mwamini anayerudi nyuma na kuanguka (linganisha na Luka 8:12, 13). Anafanyika mtu asiye na matunda na mwishowe anakatiliwa mbali kutoka kwa Kristo. Licha ya kuwepo mawazo mengi kinyume cha hilo, Maandiko yanaonyesha kwamba ni kitu kinachowezekana. Tutajaribu kuthibitisha hicho katika sura nyingine huko mbele. Uwezekano mwingine wa pekee ni kwamba tunda hilo lisilozaa ni mfano wa mwamini bandia, anayedhani yuko ndani ya Kristo lakini kumbe amekufa na hapati nguvu za uzima kutoka Kwake, kama inavyo-onekana kwa kutokuwa na matunda. Lakini, Yesu hakufafanua matawi kuwa ni wale wanaokiri tu kwamba wamo ndani Yake na kumbe hawamo. Yeye alifafanua matawi kwamba ni wale walio ndani Yake.

Wale wazaao matunda wameahidiwa kusafishwa na Mungu Mwenyewe. Pengine Yesu alikuwa anazungumza juu ya kusafishwa kwa hali ya juu ambako hutokea wakati wa kuzaliwa upya, mtu anapoonyesha matunda yale ya mwanzo kabisa ya toba na imani. Au labda alikuwa anaeleza juu ya kuendelea kwa mpango wa utakaso ambao Mungu huutekeleza katika maisha ya kila mwamini anayekubaliana Naye (ona Wafilipi 2:13). Vyovyote vile, mfano wa Mungu kwamba ni mkulima (au mtunza mizabibu) unazungumzia juu Yake Yeye akikata kitu kisichompendeza katika maisha yetu. Chochote kinachozuia matunda yasizalishwe na Roho anayekaa ndani yetu kitakutana na makasi Yake ya kukatia.

Upinzani Mdogo

Mara nyingi swali hutokea kuhusu Yusufu wa Arimathea, ambaye Biblia inasema alikuwa “mwanafunzi wa siri” wa Yesu (ona Yohana 19:38). Je, anawezaje kusemekana ni mwanafunzi kama imani yake ilikuwa ya siri? Je, hayo hayapingani na yote niliyoandika juu ya hali ya kujitoa inayoonyeshwa na wanafunzi wa kweli?

Hebu nianze kwa kusema kwamba jambo hilo hunisumbua mara nyingi sana kwamba, baada ya kutoa andiko baada ya andiko lenye kuthibitisha kweli fulani, mtu atatafuta mstari mmoja mdogo, uliofichika, ambao unaonekana ni kana kwamba unapinga yote niliyofundisha. Kisha anautaja kwa kiburi, kana kwamba huo mstari mmoja tu unabatilisha ile mingine yote tuliyokwisha itazama. Hoja hii ya sasa ni mfano. Kila kitu nilichoandika juu ya gharama ya kujitoa kuhusu uanafunzi kimejengwa kwenye Maandiko. Nimesema kinachosemwa na Biblia. Kwa hiyo, swala la kuunganisha uanafunzi wa siri wa Yusufu wa Arimathaya na yale yote yaliyofundishwa na Yesu kuhusu gharama ya kujitoa ya uanafunzi wa kweli ni letu wote, si langu peke yangu.

Sasa tujibu hoja: Yusufu wa Arimathaya alimpenda Yesu sana. Kulingana na taarifa ya Biblia, alikuwa “mtu mwema na mwenye haki” (Luka 23:50). Lakini, kama mwanachama maarufu wa Baraza la Wazee wa Kiyahudi (Sanhedrin), alificha upendo wake “kwa kuwaogopa Wayahudi” (Yohana 19:38). Wayahudi aliowaogopa bila shaka walikuwa wale wanachama wengine wa Baraza la Wazee wa Kiyahudi.

Ni wazi kwamba Yusufu wa Arimathaya alijua kwamba yalikuwepo matokeo mabaya kwake kama angefunua jinsi alivyojisikia kuhusu Yesu. Inawezekana kwamba alichokuwa anaogopa ni kuondolewa kwenye Baraza lile, kitu ambacho kingempunguzia nafasi ya kuwashawishi vizuri kuhusu Kristo. Tunajifunza kutoka Luka 23:51 kwamba Yusufu “hakukubaliana” na “mipango” ya Baraza kuhusu kukamatwa, mashtaka na hukumu iliyotolewa kwa Yesu. Na baada ya kifo cha Yesu, alifanya kitu kilichoweka hatarini hadhi yake, maana tunaambiwa kwamba “akafanya ujasiri, akaingia mbele ya Pilato akauomba mwili wake Yesu” (Marko 15:43). Kisha, yeye mwenyewe binafsi akautayarisha mwili wa Yesu na kuuzika katika kaburi lake mwenyewe. Hakika uwezekano wa kugunduliwa kwa mambo aliyofanya na Baraza ulikuwa mkubwa! Lakini baada ya kusulubiwa kwa Yesu, inaonekana hakujali tena kwamba wenzake katika Baraza wanafikiri nini.

Kujitoa kwa Yusufu kwa Kristo kilikuwa kitu wazi, na usiri wake kuhusu upendo wake ulikuwa ni wa muda tu. Zaidi ya hayo, inawezekana kuwa mwanafunzi halisi wa Kristo na kuogopa matokeo mabaya yanayoweza kutokana na jambo hilo. Yusufu wa Arimathaya alikuwa na matunda mengine katika maisha yake yaliyothibitisha kujitoa kwake kwa Kristo kuwa ni halisi.

Vipi Kuhusu Wakristo “Wa Kimwili”?

Kuna upinzani mwingine unaotolewa mara kwa mara. Siku hizi kuna wanaoitwa “Wakristo wa kimwili”. Wao ni kundi la kisasa la waamini wanaodaiwa kuwa wa kweli, ambao mara kwa mara wanakubaliana na mwili, na ambao matendo yao ya kimwili huwafanya kuwa kama wasiokuwa waamini. Japo “wamempokea Kristo”, hawaonyeshi kujitoa kwao Kwake. Wengi wao hawahudhurii hata kanisani, na wanafanya dhambi nyingi tu, lakini inasemekana wao ni salama katika neema ya Mungu, na wanakwenda mbinguni.

Je, hilo wazo kwamba kuna Wakristo wa kimwili lilitokea wapi? Chanzo chake ni tafsiri potofu inayoshikiliwa na wengi ya kile ambacho Paulo aliandika katika sura ya tatu ya Wakorintho wa Kwanza. Aliandika hivi:

“Lakini ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo. Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi, kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina; je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?” (1Wakor. 3:1-3)

Swali: Je, Paulo alikuwa anazungumza juu ya kundi fulani la Wakristo ambao hawana tofauti na wasioamini kwa sababu ya kufuata asili au tabia zao za kimwili? Wengi wanasema ndiyo, japo ni kinyume kabisa cha mafundisho mengi ya Agano Jipya. Wanadai hivi: “Paulo si aliwaambia Wakristo hao kwamba ‘mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu’ (3:3) na kuonyesha kwamba walikuwa wanatenda kama watu ambao hawajaamini?”

Jibu litapatikana katika kutazama kila kitu ambacho Paulo alisema kuhusu Wakorintho. Tukifanya hivyo, tutagundua kwamba “Wakorintho wa kimwili” kweli hawakuwa na tofauti na watu wasiookoka, kwa sababu imani yao halisi ilionekana kwa matendo mengi ya nje yaliyoonyesha upendo wao kwa Kristo. Naam: na kwa kuwa walikuwa na asili mbili – kama ilivyo kwa Wakristo wote – walikabiliana na ile vita kati ya Roho na mwili. Wengi wao kwa kuwa hawakuwa wamekomaa kiroho walifikia mahali pa kukubaliana na kuenenda katika asili yao ya kale (yaani, kuenenda katika mwili), na kutoenenda katika upendo kati yao. Walikuwa wanashindana juu ya waalimu waliokuwa wanawapenda na kuonyesha hali ya kupuuza Meza ya Bwana. Wengine walikuwa wanashtakiana mahakamani. Walihitaji kukua katika tunda la upendo, na Paulo aliandika mengi sana kuwasaidia katika jambo hilo.

Sababu ya msingi ya tatizo lao ni wao kutokujua kile ambacho Mungu alitazamia kutoka kwao. Kwa kuwa walikuwa watoto katika Kristo ambao Paulo alikuwa amewalisha tu maziwa ya Neno la Mungu badala ya nyama au chakula kigumu (3:2), maarifa yao (au walichojua) yalikuwa madogo na yenye mipaka. Ndiyo sababu Paulo aliwaandikia na kushughulikia makosa yao mbalimbali. Baada ya kuwaambia kile ambacho Mungu alitazamia kutoka kwao, aliwatazamia wafikie kiwango kinachotakiwa.

Wakorintho Wa Kiroho, Waliokuwa “Kimwili”

Nini baadhi ya kazi za Wakristo Wakorintho zilizowatamblisha kwamba wana imani ya kweli? Ni nini kilichowatofautisha na wasiokuwa Wakristo? Yafuatayo ni mambo yaliyodhihirishwa na Maandiko.

Kwanza: Wakati Paulo alipohubiri Injili mara ya kwanza huko Korintho, alifanikiwa sana. Mungu Mwenyewe alimwambia kwamba walikuwepo wengi huko Korintho ambao wangeokoka (tazama Matendo 18:0), na Paulo alikaa huko mwaka mmoja na nusu. Wengi “walikuwa wakiamini na kubatizwa” (Matendo 18:8). Ubatizo ndilo lilikuwa tendo lao la utii la kwanza kwa Kristo.

Paulo, akiwaelezea baadhi ya Wakristo Wakorintho anaandika kwamba zamani walikuwa wazinzi, waabudu sanamu, waasherati, walawiti, wezi, wenye kutamani, walevi na wadanganyifu (ona 1Wakor. 6:9-10). Lakini kwa sasa walikuwa wamesafishwa na kutakaswa; walikuwa wamebadilishwa. Hilo peke yake linavunjilia mbali hoja ya kijinga kwamba Wakorintho walikuwa hawana tofauti na wasioamini.

Tena, Paulo aliwafundisha Wakristo Wakorintho kwamba “msichangamane na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi – mtu wa namna hii msikubali hata kula naye” (1Wakor. 5:11). Bila shaka Wakristo Wakorintho wenyewe hawakuwa na hatia ya kufanya hayo, maana kama ndivyo, Paulo alikuwa anawaambia wasishirikiane wao kwa wao, wala wasile pamoja!

Barua ya Paulo ya kwanza kwa Wakorintho ilikuwa ni jibu la barua aliyokuwa amepokea kutoka kwao juu ya maswala fulani. Walikuwa wameuliza kuhusu kilichokuwa sawa na kisichokuwa sawa, wakionyesha shauku yao wenyewe ya kutaka kutenda yaliyo sawa. Je, ilikuwa ni kosa kwa watu wasio na ndoa kuoana? Vipi kuhusu wale ambao waliwahi kuwa na ndoa? Vipi kuhusu kula nyama zilizokuwa zimetolewa sadaka kwa sanamu? Wengi katika Wakristo Wakorintho, kwa sababu ya kumpenda Kristo, walikataa kula nyama za aina hiyo wasije wakamchukiza Bwana – onyesho kwamba walikuwa na imani hai.

Paulo akawaandikia hivi katika 1Wakor. 11:2 – “Basi nawasifu, kwa sababu mmenikumbuka katika mambo yote, nanyi mmeyashika yale mapokeo vile vile kama nilivyowatolea.” Je, hao ni watu wasio na tofauti yoyote na wasioamini?

Wakristo Wakorintho walishiriki Meza ya Bwana mara kwa mara (japo sivyo kama ilivyotakiwa), wakitii agizo la Yesu (ona 1Wakor. 11:20-22). Pia walikusanyika mara nyingi ili kuabudu Kikristo (ona 1Wakor. Sura ya 12 na 14), kitu ambacho wasioamini hawakufanya katika siku zile.

Walikuwa na shauku sana ya kupata karama za kiroho (ona 1Wakor. 14:12).

Ukweli kwamba barua zote mbili za Paulo kwa Wakorintho zimejaa mashauri kuhusu utakatifu huonyesha kwamba Paulo aliamini kwamba watajali alichoandika. Aliwaagiza wamtenge mtu mnafiki (ona 1Wakor. 5:13) na kufanya changizo kwa ajili ya Wakristo maskini waliokuwa Yerusalemu (ona 1Wakor. 16:1-4), kitu ambacho walikuwa wamekwisha anza kukifanya, tena kwa shauku kubwa (ona 2Wakor. 8:10; 9:1-2). Kwa njia hiyo, walionyesha upendo wao kwa ndugu, kile kile kitu ambacho Yesu alisema kingekuwa alama ya wanafunzi Wake wa kweli (Yohana 13:35).

Barua ya pili ya Paulo inaonyesha kwamba wengi wao – kama si wote – walikuwa wameitikia vizuri maagizo ya barua yake ya kwanza (ona 2Wakor. 7:6-12). Baada ya barua ya kwanza na kabla ya barua ya pili, Tito alisafiri kwenda Korintho na akarudi na taarifa nzuri sana juu ya utii wao (ona 2Wakor. 7:13-16). Wale watoto wachanga katika Kristo walikuwa wanakua. Ndiyo – yalikuwepo bado matatizo kidogo huko Korintho, na Paulo alipanga kuwatembelea ili kutengeneza yaliyobaki.

Hitimisho ni hili: Wakati Paulo alipoandika kwamba Wakristo Wakorintho walikuwa wanaenenda “kwa tabia ya kibinadamu” hakumaanisha kwamba hawakuwa tofauti na wasioamini kwa kila hali. Walikuwa wanatenda kama wasioamini kwa njia moja, lakini kwa njia nyingine nyingi walikuwa wanatenda kama wanafunzi wanaompenda Kristo sana.

Vipi Kuhusu Kazi Zitakazoteketea?

Hoja nyingine ambayo mara nyingi inatumiwa kuunga mkono wazo la kundi maalum la Wakristo wa kimwili hujengwa juu ya maneno ya Paulo katika 1Wakor. 3:12-15. Inakwenda hivi: Je, Paulo hakuwahakikishia Wakorintho katika maandiko hayo kwamba wangeokolewa hata kama kazi zao zote zingeteketea wakati wa hukumu? Je, hiyo haionyeshi kwamba mtu anaweza akawa hana matunda kabisa na bado awe ameokoka?

Mantiki ya maandiko hayo inadhihirisha kosa la hoja hiyo. NI wazi kwamba Paulo alikuwa anaandika juu ya thawabu ambazo watumishi binafsi watapokea au kupoteza, kwa sababu ya ubora wa kazi zao. Akifananisha kanisa na “jengo la Mungu” (3:9), na akitaja kwamba yeye aliuweka msingi “ambao ni Yesu Kristo” (3:11), Paulo aliandika kwamba kila mtumishi “aangalie jinsi anavyojenga juu ya msingi” (3:10). Inawezekana kabisa kujenga kwa makosa. Kisha, Paulo, kwa njia ya mfano, anataja vifaa vya aina sita vya ujenzi ambavyo vingeweza kutumiwa: “dhahabu, fedha, mawe ya thamani, miti, majani [na] manyasi” (3:12). Vile vitatu ni vya thamani kubwa sana, na haviwezi kuteketea au kuungua, ila vile vya mwisho vitatu si vya thamani kubwa na ni rahisi sana kuungua na kuteketea.

Kulingana na Paulo, aina ya vifaa vinavyotumiwa na mtumishi binafsi kujenga jengo la Mungu haviwezi kuonekana wakati huu. Lakini siku moja vitakuwa dhahiri kabisa, kwa sababu “kazi ya kila mmoja … itafunuliwa kwa moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu” (3:13). Kisha anaendelea hivi:

Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu. Kazi ya mtu ikiteketea, atapata hasara; ila yeye mwenyewe ataokolewa; lakini ni kama kwa moto” (1Wakor. 3:14-15).

Yamekuwepo majadiliano mengi kuhusu ni kazi zipi zinazoweza kuwa “dhahabu, fedha na mawe ya thamani,” na ni zipi zinazoweza kuwa “miti, majani na manyasi”. Hata hivyo ni kweli kabisa kwamba watumishi “wanaojenga” jengo la Mungu kwa kutumia matofali ambayo ni Wakristo bandia na sementi ya injili ya uongo watapata maandiko hayo kuwa yanayofaa sana wakati Bwana atakapopima kazi yao. Watu wengi wasiokuwa watakatifu ambao wamo kanisani sasa hivi mwishoni watajikuta katika moto wa jehanamu, na yule mtumishi “aliyewaleta kwa Kristo” au aliyewahakikishia kwamba wameokoka kwa kutangaza neema ya uongo atatambua kwamba juhudi zake zote hazikuwa kitu katika kujenga “hekalu la kweli la Mungu” (3:16). Alichojenga kitaungua, naye “atapata hasara” (3:15), na hatapokea thawabu yoyote. Lakini, yeye mwenyewe, kama ni mwamini wa kweli, “ataokolewa; lakini ni kama kwa moto” (3:15).

Ni dhahiri kwamba kusudi la Paulo katika maandiko haya halikuwa kuwahakikishia wale wanaoitwa “Wakristo wa kimwili” kwamba wanaweza kuwa bila matunda na bado wawe na uhakika wa wokovu wao. Yeye alikuwa anaandika juu ya thawabu ambazo watumishi watapokea au kupoteza kulingana na hali ya kazi yao, itakayofunuliwa wakati wa hukumu.

Ndiyo – Wakristo wa kweli wakati mwingine hutenda mambo ya kimwili. Kila wanapokubaliana na mwili ni sawa kusema kwamba wanatenda kama “watu wa tabia ya mwilini”. Lakini, hakuna kundi maalum la “Wakristo wa kimwili” katika mwili wa Kristo, ambao wanakwenda mbinguni lakini wanakubaliana kabisa na tabia na asili zao za kimwili. Paulo anasema hivi katika Warumi, kuhusu jambo hilo:

Kwa maana kama tukiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi. Kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao> ndio wana wa Mungu (Warumi 8:13, 14 – Maneno mepesi ni kutilia mkazo).

Tena, kama anavyowaandikia Wakristo Wagalatia: “Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulubisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake” (Wagalatia 5:24).

Je, Ungefanya Nini Kama …

Kuna kisa – pengine si cha kweli – ambacho kimesimuliwa juu ya kanisa dogo katika kijiji kilichojificha sana huko Marekani ya Kati. Jumapili moja asubuhi wakati ibada inakaribia kuanza, milango ya kanisa ilifunguka na wanaume wawili wakaingia. Hawakuwa wasafi sana, tena walikuwa wamevalia mavazi ya kijeshi na wameshika bunduki. Mabegani walikuwa wamefunga mikanda yenye kujaa risasi.

Hofu ikawapata washirika. Wapiganaji Wakomunisti walikuwa na tabia ya kuwaua Wakristo katika eneo hili. Je, wakati wao ulikuwa umefika?

Mmoja akadai kuwe kimya kisha akasema: “Ninyi Wakristo sikuzote mnazungumza kuhusu kwenda kumwona Mwokozi wenu, yule mnayemwita Mwana wa Mungu. Basi leo mmebahatika kwa sababu muda si mrefu ujao mtakwenda kujua ikiwa Mungu wenu kweli yupo! Haya! Jipangeni mistari kwenye kuta za kanisa!”

Haraka haraka washirika wakaondoka kwenye viti na kwenda kujipanga ukutani pande zote.

Akasema, “Sasa, kabla ya kuwaua, tungependa kuhakikisha kwamba ni waamini tu ndiyo watakufa. Yeyote hapa ambaye haamini kweli kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu atoke upesi akipitia hapa kwetu. Harakisha!”

Wengi hawakusita. Kwa dakika moja, nusu ya washirika wakawa wametoka.

Mtu wa mwisho alipotoka, milango ikafungwa. Mmoja wa wale askari akatazama kupitia dirishani na kuwaona wale waliotoka wakikimbia mbio kutoka eneo la kanisani. Kisha, alipoweka chini bunduki yake, alisema huku akitabasamu: “Ndugu zetu! Mtusamehe tafadhali. Tulitaka kumwabudu Bwana nanyi asubuhi ya leo, lakini tulitaka kuabudu na Wakristo wa kweli tu. Sasa hebu tumwabudu Bwana pamoja!” Ikawa ibada ya kipekee sana asubuhi hiyo!

Kisa hiki husimuliwa ili kuwalazimisha watu wanaokiri Ukristo wafikiri kitu ambacho wangefanya kama wangekuwepo asubuhi hiyo. Lakini, kuamini hadithi hii kwamba ni ya kweli inabidi tupuuze ukweli kwamba Wakristo wawili wenye bunduki walijifanya, wakatoa vitisho na wakamkana Kristo, ili waweze kumwabudu Mungu katikati ya waamini wa kweli! Je, kwa walichofanya, hawakumkana Kristo sawa na wale waliokimbia kutoka kanisani?

Basi, ningependa kuigeuza hadithi hiyo kidogo tu, hasa kwenye kumalizia. Ingawa kipengele changu pia sijawahi kukishuhudia, ndivyo matukio mengi yanayofanana na hicho kisa yalivyomalizika, mara nyingi sana.

Baada ya dakika moja, nusu ya washirika wakawa wametoka nje.

Mtu wa mwisho alipotoka, milango ikafungwa. Askari mmoja akatazama kwenye dirisha na kuona wale waliotoka wakikimbia kutoka eneo la kanisa. Kisha akiwa amekunja uso kikatili, aliwaelekezea wale wanafunzi wachache waliobaki bunduki yake na kusema: “Jitayarisheni kukutana na Mungu wenu.” Baada ya kusema hivyo, alianza kupiga risasi. Ikawa ibada ya ajabu sana kwao, mbele za Bwana wao!